UKIMWI

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA RAI 2004

Suala la ukimwi: uaminifu unavunjika mara nyingi kuliko kondomu zinavyopasuka!

“Mwisho wa mwisho (katika mambo ya kutongozana) ni kukubali. (Huyo) asiyekubali leo atakubali kesho. Asipomkubali kijana mwenzake atamkubali mheshimiwa mbunge, atamkubali bosi (wake ofisini) au atamkubali kiongozi (wake) wa dini. Huu ndio ukweli wa maisha. Hivyo (lazima kijana) ajue (kwamba) siku atakapokubali ni kupima kwanza au kujikinga kwa kutumia kondomu “. (Privatus Karugendo, Rai Na. 582).

Msomaji wa RAI, ameguswa na maneno hayo hapo juu yaliyokuwa kwenye makala yangu iliyopita. Baada ya kujadiliana naye kwa kirefu na kupata maoni yake nimeamua kuandika makala hii!
Ni ukweli usiopingika kwamba maadili ya ngono yalikuwapo kabla ya ukimwi; hata hivyo maadili haya hayakutusaidia kuukwepa ukimwi, kwa kuwa watu waliyakaidi kwa sababu kadhaa. Kwa kuangalia hali halisi ilivyo sasa, inaelekea kwamba watu wataendelea kuyakaidi maadili ya ngono mpaka hapo sababu zinazowafanya kuyakaidi zitakapoondoka. Kanuni ya umachiavelli inatawala leo kuliko kanuni nyingine yoyote kadiri maadili ya ngono yanavyohusika!


Ziko sababu kadhaa zinazowafanya watu kuwa wafuasi wa Machiavelli. Kwa kuangalia mitindo maisha ya watu kingono, ziko sababu kama saba hivi zinazowasukuma kuabudu itikadi hiyo. Nitajaribu kuorodhesha kwa ufupi.

Mtindo wa kwanza unahusisha kundi la watu wanaofanya ngono kwa sababu tu ni anasa. Kila mlango wa fahamu tulio nao wanadamu unatupa anasa kwa namna fulani. Kunusa manukato, kuonja asali, kutazama sinema, kusikiliza muziki, na kufurahia mwanga wa jua la asubuhi kwa kutumia neva zilizo kwenye ngozi ya miili yetu zote ni anasa za mwili. Anasa ya ngono inapatikana kupitia neva za ngozi ya mwili, na kwa njia ya mzunguko kupitia milango mingine yote ya fahamu. Uhusiano wa kingono hapa ni wa muda tu. Kama zilivyo anasa nyinginezo. Hakuna anasa ya kudumu! Pamoja na ukimwi kuzagaa, mtindo huu wa maisha bado imeshika mizizi. Ni mtindo unaomgusa karibu kila mtu asiye kuwa na kasoro ya kimwili. Ili kuubadilisha mtindo huu wa maisha panahitajika juhudi za pekee zikiambatana na ushirikishwaji, majadiliano, elimu, uwazi, imani ya kweli na maisha ya pamoja.Ni vigumu kuubadilisha mtindo huu wa maisha kwa kuukemea kama wafanyavyo wenye nguvu za kukemea pepo wabaya!

Mtindo wa pili unahusisha kundi la watu wanaofanya ngono kwa sababu wanataka kuzaa mtoto. Hawa, mara nyingi, ni wanawake ambao hulazimika kufanya ngono pale tu wanapojisikia kupata mtoto. Ni nani atahusika katika kusababisha mimba hiyo, ni suala la kuamua tu siku hiyo. Baada ya mimba kupatikana kila mmoja anaendelea na maisha yake. Akihitajika mtoto wa pili, atatafutwa mtu mwingine kwa utaratibu huo huo. Utaratibu huu unaendelea. Hawa, japo uhusiano wao ni wa muda, hawatatumia kondomu kama kuzuia magonjwa. Hii ni kwa sababu kondomu hiyo hiyo pia ni kizuia-mimba, wakati wao wanahitaji mimba itungwe! Pamoja na janga la ukimwi, mtindo-maisha wa aina hii bado unaendelea kushamiri.Pia ni vigumu kuubadilisha mtindo huu wa maisha kwa kuukemea tu bila kufanya kazi ya ziada.

Mtindo wa tatu unahusisha kundi la watu wanaofanya ngono kwa sababu wanataka usalama wa kijamii maofisini, makanisani, mashuleni, vyuoni na hata ikulu. Kwa mfano, mwanafunzi mmoja anayeyaweza mambo kidogo darasani anaweza kujenga urafiki wa kingono na mwenzake kama namna ya kumweka karibu rafiki yake ambaye anaamini anaweza kumsaidia kusoma vizuri. Jambo kama hili linafanyika katika biashara, kwenye siasa na maofisini kati ya wakubwa wa kazi na watu walio chini yao. Hata kwenye baraza letu la mawaziri tunasikia kwamba ngumi zinapigwa. (Kwa mfano, inasemekana kwamba Mawaziri wawili wa kike walipigana kwa ajili ya Kigogo wa juu katika serikali yetu). Uhusiano wa kingono hapa ni wa muda tu. Pamoja na ukimwi kushamiri, mwenendo huu unazidi kushamiri hata leo.

Mtindo wa nne unahusisha kundi la watu wanaofanya ngono kwa sababu tu wanatafuta kutambulika kwa wenzao kundini. Kundi laweza kuwa kikundi cha kusoma pamoja chuoni, au kikundi cha makuli, au kikundi cha wavuvi, au kikundi cha walimu katika shule fulani, au madaktari katika hospitali fulani, au hata kikundi cha vijana wa rika za kuchumbiana(courtship age).

Hawa wa kundi la kuchumbiana wanahangaika kutafuta kuolewa na mtu ambaye amekwisha jijenga kiuchumi. Njia pekee ambayo wamechagua ni kutoa rushwa za ngono kwa watu wengi wengi tu, mpaka hapo atakapojitokeza mwenye nia ya kuoa lakini aliyejijenga tayari!

Kitu kimoja ambacho nimegundua hapa ni kwamba, inawezekana kabisa kuna mtu anayemzimia msichana ili kumwoa, na msichana pia anatamani kuolewa na huyo bwana. Lakini, ugunduzi wangu ni kwamba, msichana huyu akishatokea kufanya ngono na mtu fulani hata kama alikuwa hampendi sana, kuliko yule wa kwanza ambaye anajifanya mwana maadili, huyu mwanamaadili anasahauliwa! Baadaye, msichana anatelekezwa. Safari hii inaendelea! Mwenendo huu unaendelea kushamiri pamoja na kwamba janga la ukimwi lipo.

Mtindo wa tano unahusisha kundi la watu wanaofanya ngono kwa sababu wanataka kuonyeshana upendo(affection) au shukrani. Kwa kawaida kama unampenda mtu unampa zawadi. Na zawadi nzuri ni kumpa mtu kile kitu anachokipenda. Kitu kitakachomfurahisha. Watu wengi wanapenda anasa, na hasa anasa ya ngono. Hivyo, kumpa mtu hiyo anasa ni namna ya kuonyesha upendo au shukrani. Mwenendo huu bado unaendelea pamoja na kwamba ukimwi umezagaa.

Mtindo wa sita unahusisha kundi la watu wanaofanya ngono kwa sababu za kimapato Hawa hujihusisha na ngono kama tendo la mabadilishano yanayohusisha vitu kama vile kama vile pesa, gari, kiatu kizuri, nguo bei mbaya, au mshahara mzuri!. Mabadilishano huweza kuhusisha pesa, mali au huduma nyingine yoyote. Kinachofanyika kati ya mhudumu wa baa na mnywaji wa pombe bar ndicho hicho hicho kinachofanyika kati ya bosi ofisini na katibu wake, tangu ofisi ndogo ndogo kama vile bucha ya nyama mpaka ikulu! Masukari baba na masukari mama ni mafundi wa kutoa zawadi za magari. Bosi ofisini huweza kumpa mtu aliye chini yake ruhusa ya kuondoka ofisini kila Ijumaa saa sita mchana, badala ya saa kumi na nusu, ili mradi tu mtu huyo awe tayari kutoa penzi kadiri bosi wake anavyotaka. Ikiwa kuna maeneo ya kupaki kwa ajili ya vigogo wa ngazi za juu kwenye kampuni, mtu wa chini, hata kama ni mfagiaji, atapata sehemu ya kuegesha gari lake ilimradi tu awe tayari kutoa anasa ya ngono kwa bosi mhusika. Yako matukio mengi ya aina hii. Na pamoja na ukimwi, bado tabia hii inashamiri. Na kibaya zaidi makuwadi wakuu wa tabia hizi ni baba na mama zetu, wajomba na shangazi zetu, na watu wengine wa rika za kati kwenda juu, kwa kuwa hawa ndio tayari wana nyenzo za udhibiti (power resources) kwenye makampuni haya.

Mtindo wa saba unahusisha na unapaswa kuhusisha kundi la watu wanaofanya ngono kwa utaratibu unaohusisha sababu zote nilizozitaja hapo juu. Kusudi hili liwezekane watu hawa wanaishi pamoja kama mke na mume katika ndoa. Kwao penzi linapaswa kuwa ni zawadi! Kwa kawaida ukishampa mtu zawadi, iwe kalamu au nguo, ni yake. Huwezi kumnyang’anya. Vivyo hivyo ukishajitoa kwa mwenzako kama zawadi huwezi ukajinyakua na kujitoa kwa mwingine. Kwa tafsiri ya namna hii hawa watu wanapaswa kujenga uhusiano wa kudumu kabisa. Mtindo-maisha wa aina hii ndio “unaopigiwa debe” na viongozi wengi wa dini. Watu katika kundi hili, kwa sababu za kimantiki hawatarajiwi kujihusisha na ngono za kupokezana(relay sex). Lakini, kwa masikitiko makubwa kabisa, watu katika kundi hili ndio wanakata mbuga na kujiingiza katika mitindo maisha mingine iliyotajwa hapo juu. Pamoja na ukimwi, bado ukataji mbuga unaendelea asubuhi, mchana, jioni na usiku wa manane kama kawaida!


Kwa msingi huu, nafikiri kwamba, wakati watu wanaendelea na itikadi ya umachiavelli, ni bora kuwasaidia kwa mbinu yoyote inayowezekana, kama vile kondomu mpaka hapo watakapouacha umachiavelli! Watu wakiacha umachiavelli, hata kondomu zitakosa soko! Izingatiwe kwamba jambo la msingi si kuzuia matumizi ya kondomu, la msingi ni kuwaelimisha watu wabadilishe maisha yao. Na hii si kwa kuhubiri na kutunga sheria nyingi nyingi – ni kwa kuyagusa maisha yenyewe kwa kushirikiana na jamii nzima.

Ziko mbinu nyingi za kuweza kuwafanya watu waache imani ya kimachiavelli. Lakini kwa maoni yangu, mahali pa kuanzia ni kutokomeza itikadi mbovu ya mfumo dume(patriarchy)! Kanisa Katoliki ni kinara wa mfumo dume. Limechangia kiasi kikubwa kuendeleza na kuutukuza mfumo dume. Linaishi na kutenda kana kwamba wanawake si watu! Uongozi wote, maamuzi yote ya kanisa hata na maamuzi yanayowahusu wanawake moja kwa moja, kama uzazi wa mpango, utoaji mamba yanaamuliwa na wanaume. Mfumo dume ni hatari kubwa katika vita ya kupambana na UKIMWI, kama kanisa katoliki linataka kutoa mchango wake katika vita hii ni lazima liupige vita mfumo dume Ni vigumu watu kuupiga vita mfumo dume wakati wanaoana viongozi wao wa kiroho wanaukumbatia mfumo huu wa kiunyanyasaji.
Mitindo-maisha hii yote inafanana katika jambo moja kubwa: ngono za kupokezana (relay sex) ambapo mwanamke ni kama mawimbi ya sauti ambayo huruka toka mnara mmoja hadi mwingine! Hii imekuwa ni kanuni ya maisha ya wanawake wengi leo, na hasa wale wa maofisini.

Kwa sababu ya itikadi hii mbovu, siasa za kijinsia(sexual politics) zinatawaliwa na wanaume. Hii inatokana na nguvu za kiuchumi walizo nazo kwa msaada wa mfumo dume. Kutokana na itikadi ya mfumo dume, nyenzo za udhibiti kiuchumi (economic power resources) ziko mikononi mwao. Nyenzo hizi ziko mikononi mwao kutokana na itikadi mbovu ya kutukuza mfumo dume. Kwa upande mwingine, wanawake wanazo nyenzo za udhibiti wa kingono(sexual power resources)! Hizi nyenzo wanapewa kwa msingi wa maumbile yao.

Katika mazingira haya, ambapo itikadi mbovu ya mfumo dume imemfanya mwanamme kuwa na nguvu za kiuchumi, lakini ikamwacha mwanamke akiwa ametelekezwa, japo anazo nyenzo za udhibiti kijinsia, sasa mwanamke anajikomboa kupitia nyuma ya pazia!

Kinachotokea sasa hivi ni kama kuna sumaku mbili zinazovutana: sumaku ya kiume yenye nguvu za kiuchumi, na sumaku ya kike yenye nguvu za kingono. Mwanamme anapata anasa ya ngono, mwanamke anapata anasa ya ngono na gawio la kiuchumi kidogo.

Itikadi ya mfumo dume imekuwa na athari kubwa kwa sasa, kiasi kwamba kila mwanamke anataka kuuza “huduma ya ngono” kwa sababu ni njia ya haraka ya kujikomboa. Hata wale waliobahatiwa kupata elimu nzuri kabisa, bado akili yao imenasa katika tope hili la mfumo-dume. Bado wanatumia miili yao kama ngazi, badala ya kutumia akili na maarifa yao waliyoyapata.

Na kibaya zaidi ni kwamba, mwenendo huu unazo baraka zote za wazazi wote ambao nimewatafiti kwa njia zangu , baadhi yao wakiwa ni washauri wangu. Baadhi ya wazazi hawa ni wazee wa makanisa, wenyeviti wa mabaraza ya maparokia, maprofesa, na hata mawaziri! Hawa hawa ni washauri wa karibu wa mapadre na maaskofu wetu. Ninapata shida kufikiri juu ya jambo hili! Nahisi kila mtu ni mnafiki leo!

“The World is messed up to the extent that fidelity breaks frequently than condoms! What do we do?”
Mheshimiwa sana Askofu Kilaini, amekuja na mpya anasema: Tuone Soo! Je, tuone Soo kwa ngono tu? Mbona yako mengi. Nimeelezea juu ya mfumo dume na matatizo yake. Mbona Askofu Kilaini, asiseme tuone Soo, juu ya mfumo dume? Mbona asiupige vita mfumo dume? Yeye anasema kwamba maadili mabaya juu ya ngono yalisambaratisha himaya kubwa kama ya Warumi. Lakini anasahau kwamba mfumo dume pia umeivuruga dunia na unaendelea kuivuruga. Uchu wa madaraka unaongozwa na mfumo dume umeleta vita na maafa makubwa duniani. Na kama nilivyotaja hapo juu ni kwamba na ugonjwa wa UKIMWI umeenea zaidi kwa sababu ya mfumo dume. Hivyo haitoshi kuwataka watu waone Soo, bila jitihada ya kubadilisha mifumo. Mambo si rahisi kama anavyoyachukulia Askofu Kilaini.
Kama uaminifu unavujika kuliko Kondomu zinavyopasuka si ni vyema kutengeneza kondomu zilizo imara zaidi hadi na kuhimiza matumizi yake hadi pale watu watakapo elimika na kujikomboa juu ya umaana na umuhimu wa tendo la ngono? Haitoshi kuwakataza watu kutumia kondomu bila kuliangalia swala zima kwa upana. Ugonjwa uko pale pale, namba ya watu wanaokufa kwa ugonjwa huu inaongezeka usiku na mchana, ngono inaendelea mtindo mmoja, uaminifu umekufa. Tufanye nini? Loh! Kama ni hivyo, hata wimbo wa usione soo ulikuwa unayo nafasi kubwa kabisa: mtu akikubali ajue kwamba ama atumie kondomu au akapimwe!
Na,
Padre Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment