JUKWAA LA KIMATAIFA LA WANANCHI

MAKALA HII ILICHAPWA KWENYE GAZETI LA RAI 2005


JUKWAA LA KIMATAIFA LA WANANCHI

Niungame wazi kwamba kabla ya kuhudhuria warsha juu ya Jukwaa La Kimataifa La wananchi, iliyofanyika kikanda(Mwanza, Kagera na Mara) Bukoba, tarehe 27 na 28 mwezi huu, nilikuwa sijapata kusikia lolote juu ya jukwaa hili. Nina imani si mimi peke yangu ambaye hakuwa na habari juu ya kitu hiki. Mwanzo mwa warsha, hata wanawarsha wengine walionyesha dalili za kutofahamu vizuri Jukwaa hili maana yake nini.

Nilivyokuwa nikishangaa juu ya Jukwaa hili ndivyo na warsha wengine walivyokuwa wakishangaa. Mbali na Jukwaa lenyewe kulikuwa na mambo mengine ya kushangaza kidogo katika warsha hii. Mfano, tulikuwa na wawezeshaji wawili. Mmoja kijana sana miaka 24 na mwingine mzee wa makamo miaka 54? Jinsi walivyokuwa wakishirikiana na kuendesha warsha kwa amani na utulivu ni jambo la kushangaza kidogo. Lakini pia kijana mdogo huyo kutoka Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, alionyesha ukweli kwamba na vijana wanaweza na kwamba Jukwaa la Wananchi, ni wananchi wote, vijana, wazee, wanawake, wasiojiweza nk. Labda kwa vile nimeanza kuongelea mambo ya kushangaza ni bora nidokeze na hili. Kwamba wana warsha wa kutoka Mwanza ma Mara, walishangaa sana kusikia kwamba “Mwekezaji” aliyeukarabati uwanja wa Kaitaba, uwanja ambao wananchi wa Kagera, waliamini ni mali yao na wamekuwa wakiutumia kwa shughuli mbali mbali, kama vile sherehe za Saba saba, Nane nane na maonyesho ya Kilimo, mwaka huu wamezuiwa kuutumia! Sherehe za Nane nane za mwaka huu zitafanyika nje ya uwanja katika maeneo ambayo hayaendani na shughuli kama hizo. Shida ni kwamba “Mwekezaji” amekatalia uwanja wake! Kwa vile warsha ilikuwa juu ya Jukwaa la Wananchi, wanawarsha walisema hilo ni la kushikia bango. Mwekezaji mwingine, ameamua kujenga Choo, kando kando ya Ziwa! Labda, na wawekezaji wengine wataamua kuendelea kujenga vyoo kando kando ya choo. Kama huyu hajakemewa na kushikiwa bango, basi na wengine watajifunza! Hayo ni ya Bukoba, wakati vuguvugu la uchaguzi linashika kasi. Niendelee na mada yetu: Jukwaa la Kimataifa la Wananchi. Lakini pia ni imani yangu kwamba baadhi ya watanzania wana habari juu ya Jukwaa hili, maana warsha iliyoendeshwa Bukoba, ilikuwa ya mwisho kati ya warsha zilioendeshwa kikanda nchi nzima. Warsha hizi zimeendeshwa Kanda ya Zanzibar, inayounganisha Unguja na Pemba, Kanda ya kusini, inayounganisha Lindi na Mtwara, Kanda ya Nyanda za juu, inayounganisha Ruvuma, Mbeya na Rukwa, Kanda ya mashariki, inayoziunganisha Coast, Morogoro, Iringa na Tanga, Kanda ya magharibi, inayoziunganisha, Shinyanga, Dodoma na Kigoma.

Pamoja na ukweli huu kwamba Jukwaa hili limekwisha sambaa nchi nzima, bado nina wasiwasi kwamba kuna baadhi ya watanzania ambao hawajapata kusikia kitu chochote juu ya Jukwaa hili.

Jukwaa la Kimataifa la Wananchi “ Citizen’ Global Platform” (CGP), ni Jukwaa la Kiraia lililoanzishwa kutokana na mchakato wa Helsinki, ambao ni mchakato mwingine unaohusu masuala ya Utandawazi na Demokrasia ulioanzishwa na Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje za Tanzania na Finland ( Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania na Mheshimiwa Erkki Tuomioja wa Finland)- linalidhamiria kuboresha demokrasia na kuthamini uwazi kati ya nchi za kaskazini na zile za Kusini kwa kuongeza ushirikiano. Jukwaa hili lina agenda kuu katika Utandawazi na Demokrasia.

Mchakato wa Helsinki, una malengo mazuri ambayo bila ufuatiliaji yataozea kwenye karatasi kama mipango mingine mizuri inayoibuka na kuzama bila ya kutekelezwa. Malengo ya mchakato huu ni: - Kuongeza demokrasia na usawa katika ushirikiano wa kimataifa kwa kuwezesha kuwepo kwa uwanja mpana wa majadiliano wenye kujumuisha watu wengi, Kuendeleza ushirika uliojikita katika usawa wa makundi mbalimbali ya kijamii ya kiwemo ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali kutoka pande zote, kusini na kaskazini mwa utawala wa kidunia. Kuwawezesha washika dau kuunda nguvu za pamoja ili kuleta mabadiliko ya lazima katika utawala wa kidunia. Kusaidia ushiriki na ushirikishwaji wa mawazo ya watu wa kusini na vyama vya kiraia katika uundaji wa sera zenye mrengo wa kidunia. Kukuza na kusaidia michakato ya kidemokrasia ya watu wengi iliyojikita katika Tamko la Milenia la Umoja wa Mataifa ili kupunguza umaskini.

Hivyo basi, vyama vya kiraia vya nchi hizi mbili(Tanzania na Finland) viliamua kuansisha jukwaa hili liitwalo Jukwaa la Kimataifa la Wananchi la Tanzania, ili kuhakikisha sauti za vyama vya kiraia zinasikika kwenye masuala ya kuiendesha dunia hii au utoaji maamuzi. Jukwaa la Kimataifa la Wananchi la Tanzania lilianzishwa kutoa nafasi na njia za kupata nguvu/uwezo jamii ya karaia kuweza kutoa mawazo mbadala na kuwa na sauti juu ya demokrasia na wakati wa kutoa maamuzi hasa yale yanayofanywa kimataifa.

Kama sehemu ya uanzilishi wake, baadhi ya malengo ya kuanzisha jukwaa hili la Kimataifa la Wananchi hapa nchini yalikuwa ni kupima matarajio, matumaini na utendaji bora wa jamii ya kiraia. Kituo cha Huduma za Kimaendeleo cha Finland (KEPA) na United Nations Association (UNA Finland) kwa upande mmoja, na Umoja wa AZISE Tanzania (TANGO) na UNA Tanzania kwa upande mwingine, wanaendesha mradi huu (Jukwaa la Kimataifa la Wananchi) kwa pamoja.
Tangu kuzinduliwa kwa Jukwaa hili mnamo mwezi Juni Mwaka 2004, limetekeza masuala kadhaa yaliyosaidia kukuza uelewa wa jamii ya kiraia nchini hasa juu ya masuala ya kimataifa. Lakini ukweli ni kwamba Jukwaa hili lilikuwa halijafika kwa wananchi walio wengi. Uamuzi wa kuendesha warsha nchi nzima zinazowakutanisha washiriki kutoka mashirika yaliyo katika ngazi ya mkoa na wilaya walio wanachama wa TANGO na UNA, mashirika changamfu, viongozi wa serikali za mitaa, madiwani, na waandishi/vyombo vya habari kwa kuzingatia usawa wa kijinsia, wanawake, vijana, wanaume na wenye ulemavu, mwaka huu ulikuwa unalenga kulisogeza Jukwaa hili kwa wananchi. Lengo kuu likiwa ni kufikisha ujumbe na maamuzi yaliyomo katika ripoti ya mwisho ya mchakato wa Helsinki kwa wananchi walio wengi wa Tanzania na kujaribu kuona kama wananchi wanaweza kuanzisha majukwaa yao wenyewe madogo kwa ngazi zile walizomo ili kukuza demokrasia na kuhakikisha kunakuwa na utandawazi wenye kujali watu na haki za binadamu.

Ili kuweza kuainisha vizuri mambo ya kujifunza kutoka Kusini na Kaskazini Jukwaa la Raia la Kiulimwengu limeelekeza jitihada zake katika makundi matatu ya kimkokoto:
- Njia mbadala za utatuzi wa matatizo ya kidunia
- Ajenda ya Uchumi ya Kidunia
- Usalama wa Binadamu.

Hali ya sasa ya ulimwengu haiwavutii wengi. Matatizo mengi yaliyopo duniani hivi sasa yanavuka mipaka ya kijiografia na kisiasa. Kwa kiasi kikubwa mifumo ya kimataifa imeleta matatizo mengi hivi sasa kuliko huko nyuma. Matatizo kama: Umaskini, ukosefu wa usawa, tofauti za kiuchumi na kiteknolojia, demokrasia na utawala bora na nchi kuwa na maamuzi huru yanahitaji ufumbuzi mpya, chini ya mfumo mpya wa kiulimwengu. Kwa njia tunahitaji njia mbadala za utatuzi wa matatizo ya kidunia. Njia mbadala ni lazima iwe inazingatia Ushirikiano, ushiriki na kuzingatia mpango wa maendeleo ya Milenia.


Mashirika ya kimataifa ya uchumi kama; Benki ya dunia (WB), shirika la fedha la kimataifa (IMF), na shirika la biashara la kimataifa (WTO) yamepoteza uhalali na mvuto katika mtazamo wa watu wengi, kwa mwonekano wa wengi yanajitokeza kama kivuli cha ubabe wa mataifa tajiri na njia ya kukandamiza mataifa yanayoendelea, hali hii ikidhihirishwa na uwepo wa umaskini wa kutisha wa mataifa mengi ya kusini na huku pengo kati ya nchi tajiri na maskini likiendelea kukua siku hadi siku. Hali hii inatulazimisha kuwa na ajenda ya uchumi ya dunia. Mkokoto huu unajaribu kuibua mapendekezo katika nyanja ya uchumi wa Dunia ukiwa na lengo la kutengeneza mfumo mzuri wa uchumi wa dunia katika mtazamo wa kuwepo na utadawazi wenye kunufaisha wengi. Ni lazima kuwepo mfumo thabiti/imara wa uchumi wa kimataifa.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa kuona hatari nyingi zinazomwelekea binadamu wa kawaida kama athari za asili na zinazosababishwa na binadamu, aliamua kuunda Tume ya Usawa wa Binadamu mnamo Januari mwaka 2000. Tume, iliyoundwa na watu mashuhuri duniani, ilipewa muda wa miaka miwili yaani baina ya 2001-2003. Masuala yaliyolengwa yalijumuisha migogoro, maendeleo na kusikiliza kero za watu walio katika mazingira yasiyo salama. Shughuli kubwa katika usalama wa kibinadamu ni namna ya kupunguza mfumo usio sawa kiuchumi na kisiasa. Hivyo ajenda ya Usalama wa Binadamu ni muhimu na ni bora kujadiliwa katika ngazi za chini katika jamii kupitia mifumo kama hii ya Jukwaa la Raia la Kiulimwengu.

Maoni yaliyotoka kwenye warsha zilizofanyika nchi nzima yataunganishwa kwenye mkutano utakao fanyika mwezi wa nane katikati kule Dar-es-Salaam, ili kupata sauti ya pamoja ya wawakilishi wa Tanzania, katika mkutano wa Helsinki utakaofanyika Septemba 7-9 2005, utakao angalia ni jinsi gani wabunge wetu wanashiriki kuhakikisha taasisi za kimataifa zinawajibika, ni jinsi gani nchi wahisani zinatimiza ahadi zao za kufikia malengo ya maendeleo ya milenia na ni jinsi gani mataifa ya dunia yanakabiliana na tatizo la dunia la maswala ya afya.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment