UHAKIKI WA KITABU: FRESHI NA MAISHA 1-4 I. Rekodi za Kibibliografia Jina la vitabu vinavyohakikiwa hapa ni Freshi na Maisha, kitabu cha kwanza hadi cha nne na vimetungwa na Elieshi Lema. Mchapishaji wa vitabu hivi ni E&D Limited na amevipatia namba zifuatazo katika sekwensia ya vitabu duniani (ISBN): Freshi ya Maisha 1, 9987-622-64-x, Freshi na Maisha2, 9987-622-65-8, Freshi na Maisha 3,9987-622-66-6,Freshi na Maisha 4, 9987-622-67-4.Vitabu vyote vinne vimechapwa mwaka wa 2005.Kitabu cha kwanza kina kurasa 34, Kitabu cha pili kina kurasa 37, Kitabu cha tatu kina kurasa 52 na kitabu cha nne kina kurasa 64.Na anayevihakiki sasa hivi ni Padre Privatus Karugendo. II. Utangulizi Vitabu hivi vilivyoithinishwa na EMAC tarehe 10 mwezi wa 5 mwaka 2005 kuwa vitabu vya Ziada kwa ajili ya Darasa la Tano na la Saba katika shule za msingi nchini Tanzania, vimeandikwa kwa aina yake.Kila kitabu kina jina lilelile la Freshi na Maisha,lakini ujumbe ni tofauti lakini ulioungana katika mwendelezo. Wahusika ni wale wale. Kitabu cha kwanza kinabeba ujumbe wa “Jipende”: “ Maisha anaishi katika familia yenye upendo na amani, ana bidii ya kazi, nyumbani na shuleni. Maisha ameanza kupata dalili za kukua. Changamoto mpya zinamkabili. Anakutana na Freshi anayekuwa rafiki yake. Freshi anamfunulia Maisha uwanja wa maarifa ya stadi za maisha kuhusu kujipenda”. Kitabu cha pili kinabeba ujumbe wa “Jilinde”: “ Freshi ameendelea kuwa rafiki mkuu wa Maisha.Katika kitabu hiki Freshi anamwezesha Maisha kuona jinsi mwili wa binadamu ulivyo wa kipekee, na jinsi ambavyo ni wajibu wetu kuulinda dhidi yamagonjwa yote, na hasa UKIMWI.” Kitabu cha tatu kinabeba ujumbe wa “Jijue”: “Mojawapo ya stadi kuu za maisha ni kufahamu jinsi ya kutumia akili yako kunufaisha maisha yako, mahali popote ulipo.Uwe mtendaji,siyo mtedewa, ili ujielewe zaidi, ujiamini zaidi, ufanye mambo makubwa na udhibiti mwelekeo wa maisha yako” Kitabu cha nne kinabeba ujumbe wa “Jithamini”: “ Maisha amefika Darasa la Saba. Amekua kimwili na akili imepevuka kiasi. Ameanza kujithamini na kutambua mazingira tofauti yanayomzunguka pamoja na changamoto zake. Maisha amegundua kwamba wazazi ni wazito katika kuongea masuala ya ngono na vijana wao. Hali hii imewaweka vijana njia panda, huku jamii ikiwa inajiundia ngao ya ukimya kuhusu masuala nyeti kama haya”. Vitabu vyote vimegawanywa kwenye sura fupi fupi zikifuatwa na maswali ya majadiliano na picha mbali mbali zinazosaidia kufikisha ujumbe. Kitabu cha kwanza kina sura Saba fupi, kitabu cha pili na cha tatu vina sura nane ambazo ni vupi pia na kitabu cha nne kina sura kuminamoja. Katika aya zifuatazo nitatoa muhtasari na tathmini yake, lakini baada ya kudokeza mazingira yanayovizunguka vitabu hivi. III. Mazingira yanayovizunguka vitabu hivi. UKIMWI ni janga la kitaifa. Taifa letu lina mikakati mbali mbali ya kupambana na ugonjwa huu. Wataalam wanakubaliana kwamba kwa kiasi kikubwa ugonjwa huu unaenea kupitia tendo la ngono. Tendo hili linapendwa kwa wingi, lakini kilamtu anapenda alifanye katika uficho. Hakuna aliyetayari kuliongelea kwa uwazi. Wazazi hawataki kuliongea na watoto wao, ingawa kuna ushahidi wa kutosha kwamba vijana hadi watoto wadogo wa miaka 10 wanatenda tendo hili. Nyakati tulizomo, maadili yameporomoka, ngono kimekuwa kitu cha kawaida. Mbaya zaidi vijana wetu wameachwa kuogelea bila mwongozo wa maisha yao. Wazazi wanaogopa kuongea na kujadiliana na watoto wao juu ya mahusiano, juu ya mabadiliko katia miili yao, juu ya kupenda na kupendwa na hasa juu ya kujikinga na ugonjwa huu hatari. Kama anavyosema mwandishi: “ Lakini kwa sababu ya mabadiliko ya jamii kiuchumi na kisiasa, pamoja na mwingiliano wa hali ya juu wa tamaduni na amali za jamii tofauti, mifumo ya jadi yaliyoongoza mahusiano katika jamii yamefifia kabisa. Hivyo, katika muda mwingi, vijana wanajilea wenyewe. Vijiwe vyao vimekuwa taasisi. Wanajijengea amali zinazoongoza matendo yao katika mahusiano ya kila siku. Wanabuni lugha yao ya kujieleza katika jamii iliyojaa utenganisho. Katika kujilea huko,vijana wengine wanajiona wajanja kwa sababu ya uzoefu uliojengeka katika kufanya majaribio, hata kama ni uzoefu potofu. Wanaokuwa na ushawishi mkubwa na wanawarubuni wenzao kirahisi” Freshi ya Maisha 4, uk 31-32. Serikali nayo imeshindwa kuwa na mfumo wa wazi wa kufundisha maadili na kuwasaidia vijana kujitambua na kujithamini. Mashirika ya kidini pia yameshindwa. Hatuoni mfumo wao kuhusu malezi ya vijana na swala zima la maadili na kujingina na UKIMWI. Mwandishi wa vitabu vya Freshi na Maisha, aliandika kitabu cha hadithi ya “Parched Earth”. Kitabu hiki kina mafundisho juu ya vijana kujitambua, kuwatambua wengine na kwa pamoja kushirikiana kujenga mahusiano yaliyo bora kwa lengo la kulinda uhai na hasa kupambana na ugonjwa wa UKIMWI. Baada ya kukisoma kitabu hikili, nilimshauri mwandishi atunge vitabu kwa lugha ya kiswahili, ili viwe msaada wa kuwafundisha watoto wetu namna ya kujilinda, kujipenda na kujithamini. Jibu la mwandishi ni zawadi ya vitabu vinne, vya Freshi na Maisha, ninavyovifanyia uhakiki siku ya leo. Wakati ninampatia ushauri, kumbe yeye alishaviandika na vinatumika kwenye shule za msingi! Huu ni mchango mkubwa na wa kuingwa. Kabla ya kuviandika vitabu hivi mwandishi alifanya utafiti wa akina. Alifanya majadiliano nakuongea nawatu mbali mbali,pia alichimbua vitabu vingi.Hapa kuna baadhi ya vitabu alivyovitumia wakati akiandaa Freshi ya Maisha: Choosing Good Health 5&6,Scott, Forestman& Co.,1983; Soul City: Living Positively with HIV and AIDS; Family Medical Encyclopedia, An Illustrated Guide, Hamlyn, 1983; Prescription for Nutritional Hearing, Avery Publishing Group,1997; All About the Human Body, Random House,1958. Ingawa mwandishi ametumia vitabu mbali mbali wakati akiaandaa Freshi na Maisha,na kufanya majadiliano na watu wengi, ubunifu wote ni wake na mapungufu yote yanayojitokeza kwenye vitabu hivi ni mzigo wake mwenyewe! IV. Muhtasari wa vitabu Kitabu cha kwanza; Freshi na Maisha 1, kina ujumbe wa “Jipende”. Kitabu hiki ndicho kinachofungua safari ya maisha ya msichana Maisha, anayeishi katika familia yenye upendo na amani, ana bidii ya kazi nyumbani na shuleni. Binti huyu ameanza kupata dalili za kukua. Changamoto mpya zinamkabili. Maisha, anaanza kutafakari juu ya maisha yake: “Hivi kukua maanake nini?”, “ Hivi, watu hukua mwili tu, au sehemu nyingine nazo hubadilika?” (Uk 2). Wakati Maisha, akiwa amezama kwenye tafakuri juu ya maisha yake, anakutana na rafiki yake. Huyu rafiki jina lake ni Freshi. Huyu Freshi, anajitokeza kwa namna ya miujiza. Anajitokeza katika umbo la jiwe. Huyu ni rafiki ambaye ni mshauri wa kiroho. Watu wengine wanampatia jina la kipaji fiche ndani mwa kila binadamu. Kwenye mazingira Fulani, huyu anaweza kuitwa malaika mlinzi au roho mtakatifu. Rafiki huyu ni silika iliyomo ndani mwa kila binadamu yenye nguvu na ufahamu isiyohitaji kufundishwa. Huyo ndiye Freshi, rafiki wa maisha, anayemwongoza kujipenda, kujilinda, kujijua na kujithamini. Freshi, anamfunulia Maisha, ukweli wa maarifa kwamba kujipenda ni ufunguo wa safari ndefu ya kila kijana kuelekea kujilinda, kujijua na kujithamini. Kwamba kujipenda kunaanza na mtu kuangalia usafi wa mwili wake, usafi wa mazingira yake na kutambua kwamba mwili ni muhimu na maalumu, nivyo ni lazima kuulinda dhidi ya magonjwa. Maisha, anasikiliza ushauri wa Freshi.Anakuwa msafi yeye mwenyewe, anatunza usafi nyumbani na sehemu anakofanyia biashara mama yake. Shuleni anakuwa mfano wa kuigwa katika usafi. Kitabu kina maswali mengi ya majadiliano. Kila baada ya sura kuna maswali zaidi ya matatu. Mfano wa maswali ni kama: Taja mabadiliko matatu ambayo yanaonesha kwamba msichana au mvulana amepevuka. Halafu jadili na rafiki yako: je, kupevuka maana yake ni nini?, Mweleze rafiki yako, kujipenda maana yake ni nini? Kwa nini Freshi alimpa Maisha uwezo wa kugeuza takataka na uchafu kuwa kitisho? Taja madhara matatu unayoyajua yanayotokana na mazingira machafu. Kitabu cha pili, Freshi na Maisha 2, kina ujumbe wa “Jilinde”. Freshi, anaendelea kumpatia Maisha, maarifa. Maisha anatambua kwamba mwili wa binadamu ni wa kipekee na kwamba ni wajibu wa kila binadamu kuulinda mwili dhidi ya magonjwa, na hasa UKIMWI. “Lakini kwa kifupi, mwili wako ni kama mashine. Sehemu zake tofauti hufanya kazi kwa pamoja na kwa kutegemeana. Lakini mwili wako ni mashine hai, yenye akili asili ya kupanga, kuratibu, kutathmini na kujilinda” Freshi na Maisha 2 uk 23. Kitabu kinaelezea kwa lugha nyepesi jinsi mwili wa binadamu unavyofanya kazi: Mfumo wa mifupa na viungo, mfumo wa misuli, mfumo wa mzunguko wa damu na hewa, mfumo wa kusaga chakula, mvumo wa neva, mfumo unaoshughulikia ulinzi wa mwili na mfumo wa hisia. Kitabu hiki pia kina maswali ya majadiliano kila baada ya sura. Kitabu cha tatu, Freshi na Maisha 3, kina ujumbe wa “Jijue”. Kitabu hiki kinaelezea kwamba mojawapo ya stadi kuu za maisha ni kufahamu jinsi ya kutumia akili yako kunufaisha maisha yako, mahali popote ulipo. Yaani mtu awe mtendaji, siyo mtendewa ili mtu ajielewe zaidi, ajiamini zaidi, afanye mambo makubwa na awe na udhibiti wa mwelekeo wa maisha yake. “ Kujijua kunaanza na nafsi yako. Unajichunguza wewe mwemyewe ulivyo, kwa kujiona jinsi unavyoishi na familia yako, rafiki zako na watu kwa ujumla. Yale utakayopata kutoka kwa wengine, yanakuongezea maarifa juu yako, au yanakupa changamoto ya kubadilika, au yanakazia ukweli unaoufahamu tayari” Freshi na Maisha 3 uk 29. Katika kitabu hiki, Freshi, anamfunulia Maisha, ukweli kwamba maisha ya binadamu yanaongozwa na Ubongo. Ubongo umechorwa na kuonyesha kila sehemu ya ubongo na kazi zake: “ Kichwani mwako Maisha, kuna kitu kinachoitwa ubongo. Ubongo ni ogani ya miujiza tupu. Wasomi wameutafiti sana, lakini mpaka sasa mambo mengi yanayohusu uwezo wa ubongo wa binadamu hayajafahamika. Lakini huko ndiko kila tendo la mwili wako linakoratibiwa, tanfsiriwa na utekelezaji wake kuamrishwa.” Freshi na Miasha 3 uk 46. Kama ilivyokwa kitabu cha kwanza na chapili, kitabu cha tatu pia kina maswali mengi ya majadiliano. Kitabu cha nne, Freshi na Maisha 4, kina ujumbe wa “Jithamini”. Hapa Maisha amefika Darasa la Saba. Amekua kimwili na akili imepefuka kiasi. Ameanza kujithamini na kutambua mazingira tofauti yanayomzunguka pamoja na changamoto zake. Maisha amegundua kwamba wazazi ni wazito katika kuongea masuala ya ngono na vijana wao. Hali hii imewaweka vijana njia panda, huku jamii ikiwa inajiundia ngao ya ukimya kuhusu masuala nyeti kama haya. “Vijana wanahitaji stadi za maisha, siyo tu kwa kujikinga na UKIMWI na magonjwa mengine ya zinaa. Wanazihitaji stadi hizo kama mhimili wa maendeleo yao. Stadi za maisha zitakazowawezesha kufahamu wanachotaka maishani, jinsi ya kukipata na jinsi ya kukilinda na kukiendeleza baada ya kukipata”Freshi na maisha 4 uk 47. “ Alaa, sasa naanza kumpatapata Freshi! kumbe kujithamini ni kufanya vitu kibao.Kujithamini ni kujifanyia kila jambo zuri: kuwa msafi, kula vizuri, kuweka mazingira safi, kuwa na uelewa wa mambo muhimu kwa maendeleo yako, kujijua ili uweze kuwa chachu ya maendeleo yako na jamii yako, hapo ulipo.” Freshi na Maisha 4 uk 48. Kitabu cha nne, nacho kina maswali ya majadiliano. Swali lenye mvuto katika kitabu hiki ni hili: Taja mambo mawili abayo siyo rahisi kuyazungumza na wazazi wako. Jadili mambo hayo na rariki yako, kasha mjaribu kubuni mbinu ya kuyazungumza na wazazi. V. Tathmini ya vitabu hivi Baada ya kuona muhtasari huu sasa nifanye tathmini ya kazi hii aliyoifanya Mama Elieshi Lema. Niungame kwamba wakati mwingine ni vigumu kufanya tathmini ya mawazo ya mtu ambaye kwa kiasi Fulani mnakubaliana kwa mambo mengi. Nitajitahidi kuwa mwaminifu kwa kile kilichoandikwa katika vitabu vya Freshi na Maisha! Awali ya yote lazima niseme kwamba, kwa kuangalia hadhira anayoikusudia, vitabu hivi vinasisimua sana kutokana na mtindo alioutumia mwandishi. Ni mtindo wa sura fupi fupi, kutumia miujiza ya maisha ya kila siku, picha na maswali ya majadiliano. Pili, ni wazi kwamba mwandishi amefanikiwa kutimiza Lengo Lake, yaani kubainisha na kisha kutoa majibu kamilifu kwa changamoto zinazowakabili vijana na walezi wao katika nyakati hizi tulizomo. Tatu, mwandishi amefanikiwa kutoa mchango mkubwa katika kufundisha maadili kwa vijana wetu. Amevumbua kitu ambacho hakikuwepo. Mfumo wa kufundisha kwa kusoma vitabu, kuuliza maswali na kujadiliana. Mwandishi anasisitiza kwamba elimu inapatikana kwa njia ya kusoma vitabu. Msisitizo huu unajitokeza sana kwenye kitabu cha nne cha Jithamini. Nne, mwandishi amefanikiwa kutumia lugha nyepesi na mifano hai kuelezea mambo magumu. Ameonyesha mbinu ambazo vijana wanaweza kuzitumia kufanya majadiliano na wazazi wao. Wale wanaoshindwa kuongea na wazazi wao wanaweza kutumia mtindo wa kuandika kwenye daftari maswali, na wazazi wanajibu kwa kuandika: “kwa wanangu Robert na Richard, Hamtaweza kukimbia au kuyachenga maisha. Mazungumzo ya ana kwa ana yamewashinda. Tujaribu maandishi. Awapendaye, Mama”. Freshi na Maisha 4, uk 38. VI. Hitimisho Vitabu hivi vinasomwa kwenye shule za msingi. Hivi vinaitwa vitabu vya watoto. Inawezekana na mwandishi, aliwaandikia watoto. Lakini ukivisoma kwa makini, unagundua kwamba hivi si vitabu vya watoto, hivi ni vitabu vya watanzania wote na hasa watu wazima! Kwa maoni yangu, vitabu hivi ni muhimu kwa watu wazima. Ni muhimu kila mzazi kuwa na vitabu hivi nyumbani kwake, avisome na kuviweka kichwani, baadaye afanye kazi ya kuwasimulia watoto au asome na watoto wake na kufanya majadiliano. Ukiangalia mpangilio wa vitabu vyenyewe: Jipende, Jilinde, Jijue, na Jithamini, utaona lengo zima la kutaka familia na jamii nzima ya watanzania kuanzisha mazungumzo na majadiliano juu ya maadili. Na mazungumzo haya ni lazima yaanzishwe na watu wazima wenye uzoefu. Ni lazima yaanzishwe na akina Freshi. Freshi, rafiki wa Maisha,ni changamoto kubwa.Mwandishi, amemchora na kumwingiza katika hadidhi za miujiza.Amefanikiwa vizuri sana na ujumbe unafika. Ukweli unabaki kwamba Freshi, ni rafiki wa kila binadamu. Kila mtu ana malaika wake mlinzi, kila mtu ana kipaji fiche ndani mwake. Kazi iliyo mbele ya kila mtu ni kukikuza kipaji fiche, ni kukubali kumsikiliza malaika wake mlizi. Tunaona mambo ya Maisha, yanakwenda vizuri baada ya kukubali kumsikiliza rafiki yake Freshi. Fundisho tunalolipata ni kwamba kila mtu akikubali kumsikiliza malaika wake mlizi, mambo yanakwenda vizuri. Huu ndio ujumbe mzito tunaoupata kutoka kwenye vitabu hivi vya Freshi na Maisha. Vitabu vya Freshi na Maisha, vina maswali zaidi 150.Maswali haya yakijibiwa, vinaweza kuandikwa itabu vingine zaidi ya vinne. Huu unaweza kuwa mchango mkubwa wa kuboresha maadili katika jamii yetu. Kwa njia hii tunaweza kupambana na ugonjwa wa UKIMWI. Mama Elieshi Lema, anatutoa kwenye hatua ya kulalamika na kunyosheana vidole juu ya maadili na kutuingiza kwenye hatua ya kutenda. Wakati ni huu, timiza wajibu wako! Nunua vitabu, soma na watoto wako, fanya majadiliano na kukubali kumsikiliza malaika mlinzi! Pongezi nyingi zimwendee Mama Elieshi Lema, aliyeonyesha ubunifu mkubwa wa kuelezea mambo magumu kwa lugha nyepesi. Ni matumaini yetu kwamba mto wa hekima bado unatiririka kichwani mwake, hivyo tunategemea atuandikie tena Freshi na Maisha 5 hadi 10. Kwa mtindo wake wa kuandika vitabu hivi vinaweza kuendelea bila ya kikomo! Na, Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment