TUMEBAKI HAI 2012 NA TUULINDE UHAI WETU!

Kufunga mwaka na kufungua mwaka ni sikukuu zinazojirudia kila mwaka. Kwa njia moja ama nyingine hakuna jinsi ya kukwepa kurudia maneno yale yale ya kila mwaka; imani yangu ni kwamba kwa kuyarudia kila mwaka inaweza kutujengea utamaduni wa kuyatafakari matukio ya mwaka mzima na kujipanga upya kwa mwaka unaoanza: Mfano kushukuru na kuomba ni mambo ambayo lazima tuyarudie kila tunapofunga na kufungua mwaka. Hivyo basi sote kwa pamoja tumshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kuuanza mwaka mpya wa 2012. Si kwa ubora wetu tumeendelea kuishi, si kwa wema wetu tumeendelea kuishi na wala si kwa umuhimu wetu tumeendelea kuishi. Tunafahamu kabisa kwamba tuna watu wakatili miongoni mwetu, lakini bado wanaendelea kuishi; kuna watu wanatenda maovu, wana chuki na roho ya kujilipiza kisasi, lakini bado wanaendelea kuishi. Tulikuwa na watu bora wenye wema  wa kupindukia na muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu, lakini hatunao tena! Hawakubarikiwa kuiona 2012! Kuendelea kuwepo, kuendelea kuishi ni neema na huruma ya Mwenyezi Mungu. Hivyo kwa wale waliobahatiwa kuendelea kuishi ni lazima kumshukuru Mwenyezi  Mungu. Mimi na wewe, kwa vile tunaishi, tumshukuru Mwenyezi Mungu na kujitahidi kulijibu swali muhimu ambalo nimekuwa nikilirudia mara kwa mara:-

Swali la msingi la kujiuliza ni Je,  kwa nini Mungu, ameturuhusu kuendelea kuishi? Tunaishi ili tufanye nini? Tunaishi ili tuendelee kula na kunywa? Tunaishi kufurahia maisha? Tunaishi ili kuonyeshana ubabe? Tunaishi ili kuwatesa wengine? Tunaishi ili kuhakikisha tunayatumia madaraka yetu kiubabe? Tunaishi kuhakikisha kwamba furaha tunayoipata sasa hivi wajaliwe kuipata na wale wa vizazi vijavyo? Kwanini tuendelee kuwepo? Pamoja na ukatili wetu na roho mabaya kwa nini Mungu anaendelea kutulinda? Je, Mungu, anataka nini kutoka kwetu? Uhai tunazawadiwa, hakuna anayeuomba ! Lakini baada ya kuzawadiwa kila mwenye uhai ana wajibu wa kuulinda . Uhai ukishapotea haurudi tena! Hivyo ni wajibu wa kila mwenye uhai, kila aliyebahatika kuumaliza mwaka 2011 na kuingia mwaka wa 2012 kuulinda uhai wake, uhai wa wengine na uhai wa viumbe vingine vyote vinavyomzunguka. Ni wajibu wa kila mwenye uhai kuulinda uhai wa mazingira yetu ili na mazingira yetu yachangie kuulinda uhai wetu!

Mwanateolojia wa theolojia ya ukombozi Boff, ameanza kuhubiri theolojia mpya kabisa. Theolojia ya mazingira. Ana wito kwa viongozi wa dini kuanza kuyaangalia mazingira yetu kwa jicho la kiimani. Mazingira yanalinda uhai wa binadamu, hivyo binadamu huyu ambaye ni mcha Mungu, ambaye anaamini kwamba maisha yake yanaongozwa na Mwenyezi Mungu, ni lazima ayatunze mazingira kwa misingi ya kiimani. Kwa maneno mengine ni kwamba kutunza mazingira ni wajibu wa kiimani na hakuna mtu wa kukwepa wajibu huu. Anasisitiza kwamba huu sasa ndo msingi wa mahubiri yanayoendana na wakati.

Boff, alikuwa padri wa Kanisa katoliki na mwanateolojia wa hali ya juu. Alikosana na Kanisa Katoliki, baada kuhubiri theolojia ya ukombozi. Baada ya mapambano ya muda mrefu, aliamua kuachana na upadri na kuendelea kuihubiri injili kwa uhuru zaidi bila vitisho vya watawala. Yeye ni mwanafunzi wa Baba Mtakatifu Benedicto wa 16, na ndiye alipandikiza ndani mwake roho ya “Uana mapinduzi”, lakini Boff, akacharuka zaidi, na Baba Mtakatifu, wakati akisimamia imani ya Kanisa Katoliki, akatumia nyundo ya utawala kumsambaratisha.

Kanisa Katoliki, nalo limesisitiza umuhimu wa Mazingira, kwa kutaja kwamba kuharibu mazingira ni dhambi. Inawezekana kabisa kwamba Ushawishi wa Theolojia ya Boff, umeanza kufanya kazi. Hii inaweza kuwa ishara nzuri kwamba hata silaha za kinyonge zinafanya kazi. Si lazima mtu kuwa na madaraka (power) na silaha nzito nzito ili kuleta ushawishi. Sasa hivi imekubarika katika kanisa katoliki kwamba, mtu anayeharibu mazingira ni lazima atubu na kusamehewa kama mtu anayetenda dhambi nyingine. Kama tunavyosema usiibe, usizini nk, sasa imeongezwa na usiharibu mazingira! Hii ni hatua nzuri na yenye changamoto hasa kwa viongozi wetu wanaopenda kutawala badala ya kuongoza. Changamoto hii inahitaji majadiliano na ushirikishwaji, kitu ambacho ni kigeni sana ndani ya Kanisa Katoliki na hasa Afrika.

Kila tarehe moja ni siku ya kupanda miti. Tumeshuhudia Rais wetu Mheshimiwa Jakaya Kikwete, akipanda miti. Je, ni viongozi wangapi wamekumbuka kupanda miti? Ni watu wangapi wamekumbuka kupanda miti katika maeneo yao? Mungu anatuweka hai ili kulinda uhai na mazingira yetu. Kwa kupanda miti tunalinda uhai wa mazingira yetu. Je, Maaskofu wetu wametuombea tu makanisani, au wamekumbuka kupanda miti? Ni wangapi wamefanya hivyo? Tumezoea kuwaona kwenye vyombo vya habari wakiilaumu serikali kwa utendaji mbovu; ingekuwa vizuri kuwaona wakipanda miti, maana matendo ni muhimu zaidi ya maneno. Tunajua kabisa kwamba  Baadhi ya Maaskofu wetu hawapendi kukosolewa; ukiwakosoa wanakuona kama adui – lakini kwa hili na mengine mengi yanayohusu uhai ni lazima tuwakosoe bila kuwaogopa. Hata wakitumia madaraka yao kiasi cha kutuumiza ni lazima tukubali kuubeba msalaba kwa faida ya vizazi vijavyo.

Huu wito wa kuyalinda mazingira yetu unakwenda sambamba na ujenzi wa Tanzania yenye amani na salama si tu kwa wakati wetu sisi ambao tumefanikiwa kuingia mwaka mpya wa 2012,bali pia na kwa vizazi vijavyo. Mungu, anaendelea kutuweka hai ili tupambane na hatari zote zinazotishia uhai wa Mtanzania. Kuna hatari nyingi za magonjwa, ujinga na umasikini na majanga mbalimbali. Mfano njaa bado ni tishio la uhai wa Mtanzania. Na njaa ni njaa kwa wote, wawe wa CCM au vyama vya upinzani. Njaa ikija ni tatizo la taifa zima la Tanzania. Mvua isiponyesha ya kutosha. Baadhi ya maeneo ya Tanzania, yanakumbwa na uhaba wa chakula na miaka mingine inakuwa mbaya kiasi cha watu kufa. Ni aibu jambo hili kutokea kwenye nchi yenye maziwa na mito na ardhi ya kutosha. Wakati mwingine ni uzembe na kutowajibika. Kuna mikoa inakuwa na chakula kingi  wakati mikoa mingine watu wanakufa kwa njaa. Tatizo kubwa likiwa usafiri wa kusafirisha chakula hicho kutoka mkoa hadi mwingine. Barabara zilikuwa mbaya! Sasa hivi barabara zinatengenezwa. Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete, kwenye  ahadi zake wakati wa uchaguzi mkuu alituhakikishia  kwamba barabara zitatengenezwa. Tunaendelea kuamini kwamba hilo litatendeka.

Umaskini na ujinga vinatishia pia uhai wa watanzania walio wengi. Pamoja na jitihada za serikali inayowajibika, kuondoa umaskini na ujinga ni mradi wa pamoja pia! Ni lazima kila Mtanzania kushiriki katika jitihada za kuutokomeza umaskini na ujinga. Hatuwezi kuutokomeza umaskini bila kufanya kazi kwa bidii. Watanzania tuna utamaduni wa uzembe. Kazi iliyofanyika wakati wa Mjerumani, aliyewalazimisha Watanganyika kufanya kazi kwa viboko, haikufanyika wakati wa utawala wa Mwingereza. Hivyo basi Mungu, amezikataa roho zetu ili tuweze kuendelea kupamba na na umasikini na ujinga.

Je, Mungu, ametuacha hai ili tushuhudie mwaka mwingine wa awamu ya nne ya uongozi wa taifa letu? Ametuacha hai ili tushiriki kuiandika historia hai ya taifa letu na kushuhudia demokrasia ikikua na kukomaa? Ametuacha wazi kushangilia tu au kushangilia na kushiriki kufanya kazi. Mheshimiwa Jakaya Kikwete,hata kama amejaliwa karama elfu na moja, hawezi kutanzua kila kitu bila ushirikiano wa watanzania wote waliojaliwa kuuona mwaka mpya wa 2012.

Hata hivyo ukweli unabaki pale pale kwamba mwanadamu ni yule yule, mwenye tamaa, uchu wa madaraka, kujipenda, chuki, kulipiza kisasi nk. Na ukweli mwingine ni kwamba pamoja na ukorofi wa mwanadamu,  Mungu, hachoki kumvumilia. Jinsi Mungu, anavyotuvumilia ndivyo tunapaswa kuvumiliana sisi kwa sisi. Viongozi wetu watuvumilie, na sisi tuwavumilie. Bila kuvumiliana, hatuwezi kuendelea kuishi. Ubabe si karama ya Kimungu, bali kishetani! Ni lazima CCM kuwavumilia wapinzani na wapinzani kuwavumilia CCM, tukiwa na imani kwamba sote tunajenga kitu kimoja. Huruma ya Mungu, ndiyo inatufanya tuendee kuishi. Kwa vile bado Mungu bado ametusimamia, tushirikiane naye kuulinda uhai wetu na uhai wa taifa letu. Lakini hasa jambo la msingi ni kuijenga Tanzania bora ya vizazi vijavyo. Heri ya mwaka mpya!

Na,
Padri Privatus Karugendo.


0 comments:

Post a Comment