TUWEKEZE KWENYE ELIMU, TUACHE VISINGIZIO


Nimesikia kwenye vyombo vya habari kwamba migomo inayoendelea kwenye vyuo vikuu inachochewa na vyama vya upinzani. Na wengine wanakuwa na ujasiri zaidi kiasi cha kutaja chama  husika, kwamba CHADEMA ndo kinara wa migomo ya vyuo vikuu. Nafikiri hivi ni visingizio. Nisingependa kukubali hoja hii ambayo kwa upande mkubwa inaungwa mkono na serikali. Wahaya wana msemo kwamba ukishaumwa na nyoka, hata mjusi unauogopa. Serikali yetu ina changamoto nyingi na kati ya hizi asilimia kubwa zinatoka kwenye vyama vya upinzani, hivyo kila tukio lenye harufu ya changamoto ni lazima vinyoshewe vidode vyama vya upinzani.

Kama msemo wa Kiswahili wa lisemwalo lipo na kama halipo litakuwa njiani linakuja, usemavyo, basi tuamini kwamba CHADEMA ina nguvu na ushawishi mkubwa hivyo? Vyuo vyote viendeshe mgomo kwa kushawishiwa na CHADEMA? Maana yake chama tawala hakina ushawishi tena? Mbona umoja wa vijana wa CCM umejipenyeza kila sehemu kwenye vyuo vyote?

Tukitaka kuwa wa kweli na kuachana na visingizio na porojo ni kwamba tumeshindwa kuwekeza kwenye Elimu. Tungewekeza kwenye elimu kuanzia ngazi ya chini hadi vyuo vikuu, vijana wakasoma na kupata elimu bora katika mazingira mazuri, tusingesikia migomo na maandamano. Mfumo wa mikopo ya elimu ya juu ni mbovu kabisa. Migomo karibia yote inayoendelea kwenye vyuo vikuu inahusu Mikopo ya Elimu ya juu. Vijana wanaanza vyuo vikuu na kukaa siku nyingi bila kupata mikopo. Wanahitaji fedha za kununua chakula, wanahitaji fedha za kupanga chumba, wanahitaji fedha za usafiri, wanahitaji fedha za kununua vitabu nk. Bila kuwapatia fedha hizo kwa wakati, ni wazi vijana hawawezi kutulia na kusoma. Watafanya maandamano na kuendesha migomo. Hata wale wanaoikataa migomo na kuonekana tofauti na wengine, ni wasanii tu. Rohoni wanaumia na wengine wanapata matatizo ya kisaikolojia, hawawezi kutulia na kujifunza; Bila fedha za chakula, bila fedha za kulipia chumba, mtu hawezi kutulia na kusoma.

Kama tungekuwa na mfumo mzuri wa kuwekeza kwenye elimu, kwa maana ya kuandaa mazingira mazuri ya vijana wetu kusoma, kama tungekuwa na mfumo mzuri wa kuwapatia vijana wetu mikopo kwa wakati, nina mashaka kama migomo tungeisikia vyuoni hata kama CHADEMA ina ushawishi mkubwa kupindukia.

Tanzania tumeamua kutowekeza kwenye elimu kuanzia elimu ya msingi hadi vyuo vikuu. Shule za msingi hapa Tanzania, ukitoa zile za binafsi zinazowapokea watoto wa matajiri, hazina madawati, watoto wanakaa chini, nyingine hazina hata vyoo, mishahara ya walimu inachelewa muda mrefu kiasi cha kuvunja moyo na juhudi za walimu na matokeo yake ni watoto kumaliza darasa la saba bila kufahamu kusoma na kuandika. Tumeamua kuua elimu, kama tulivyofanya kwenye kilimo. Tulikuwa tunaimba kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa taifa letu. Lakini hatukuwekeza kwenye kilimo na matokeo yake, kilimo kimekufa kabisa. Tunaamua kukifufua kwa kuwakaribisha wawekezaji wa nje wenye malengo ya kulima chakula cha nchi zao na kuendeleza uchumi wa nchi zao. Hakuna mtu atakayetoka nchi za nje na kuja  hapa kuendeleza kilimo chetu, ni lazima sisi kufanya kazi ya ziada ya kuwekeza kwenye kilimo.

Hivyo hivyo hakuna mtu atakayetoka nje kuja hapa Tanzania kuendeleza elimu yetu. Tumekuwa tukiimba kwamba vijana ni  taifa la kesho, ni taifa gani hili lenye kuandaliwa na mfumo mbaya wa elimu? Ni lazima sisi kufanya kazi ya ziada ya kuwekeza kwenye elimu, bila kufanya hivyo tutabaki watu wa mwisho katika dunia hii ya sayansi na teknolojia. Tukiwekeza kwenye elimu, tutapata nguvu na uwezo wa kufufua kilimo, kufufua uchumi wetu, kufufua viwanda vyetu na kuchimba madini yetu wenyewe.

Tumejenga sekondari za kata kwa wingi bila kuwekeza kwanza, matokeo yake, sekondari zipo, wanafunzi wapo, lakini walimu , vifaa na vitabu hakuna. Wanafunzi hawa wakianza migono na maandamano ya kudai walimu na vitabu, tutasema ni uchochezi wa CHADEMA?

Tumeanzisha vyuo vikuu vingi. Ni kiasi gani tumewekeza kuwaandaa walimu wa kufundisha kwenye  vyuo hivi vikuu. Wanafunzi hawa wanaonyimwa mikopo na kusoma kwa mashinikizo, ndio hao kesho na keshokutwa watarudi kufundisha kwenye sekondari hizi za kata. Kama hawakuandaliwa vizuri watakuwa walimu wa aina  gani? Wanafunzi hawa wakifanya maandamano na migomo ya kudai maandalizi mazuri ya elimu yao, tuseme ni uchochezi wa CHADEMA?

Hata hivyo sina imani kwamba CHADEMA, inaendesha siasa za uasi au siasa za kuwafanya vijana kuendesha migomo. Tunachokijua na kukielewa, na  tukiangalia vijana waliochomoza na kujiunga na CHADEMA na kupata nafasi ya kuingia Bungeni; wanatuonyesha moyo wa uzalendo na nia ya wazi ya kupigania rasilimali za nchi hii. Kwa wachache wanaofikiri  Tanzania ni yao peke yao, wanauchukulia mchango wa vijana wa CHADEMA kama vurugu na fujo.

Hivyo basi migomo na vurugu kwenye vyuo vikuu inasababishwa na mfumo mbovu wa kutoa mikopo kwa vijana wetu. Vigezo vinavyotumika kuwapatia baadhi mkopo na kuwanyima wengine havieleweki vizuri, tungesema labda wanaangalia uwezo wa familia, kwa mantiki kwamba familia masikini vijana watapata mkopo asilimia mia moja. Lakini si hivyo maana tumeshuhudia watoto wanaotoka kwenye familia tajiri wanapata mkopo asilimia mia moja  wakati watoto wanaotoka kwenye familia masikini hawapati mkopo kabisa, au wanapata asilimia ishirini, arobaini au sitini kwa kigezo kwamba zinazobaki watafute wenyewe. Hawa watu masikini wanaolilia nyongeza ya nauli  ya shilingi mia moja ya kivuko cha Kigamboni watapata wapi mamilioni ya kuwalipia watoto wao?

Badala ya kuilaumu CHADEMA kwa ushawishi  hasi kwa vijana wetu, ni bora tulaumu mfumo wetu wa kutoa mikopo na kuilaumu hali halisi ya Tanzania. Hoja yangu hapa ni kwamba  hali halisi ya maisha ya Tanzania ina ushawishi hasi kwa vijana kuliko kitu kingine kile. Vijana wetu wanashuhudia serikali yao ikitumia fedha nyingi kusherehekea miaka hamsini ya uhuru na baadaye kutoa visingizio kwamba haina fedha za kutosha kuwapatia mkopo wanafunzi wote.

Mfumo wa kutoa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu si watanzania peke yake. Duniani kote, wanatoa mikopo ya elimu ya juu. Hakuna mtu anayejilipia elimu ya juu. Serikali inatoa mikopo na kuandaa mvumo mzuri wa kurudisha mikopo hiyo baada ya masomo ili na wengine wanufaike na mikopo hiyo.  Nchi nyingine bajeti ya elimu inakuwa na kipaumbele kuliko wizara nyingine. Wanawekeza kwenye mikopo, utafiti, vifaa vingine vya elimu na vitabu.

Vijana wetu wanashuhudia vingozi wakijenga mahekalu na kuendesha magari ya kifahari, wanashuhudia watoto wa viongozi wakisomeshwa nje ya nchi na wakirudi, maana wengine hawarudi kabisa, wanapatiwa kazi nzuri serikalini, kwenye mashirika ya kimataifa, benki kuu na sehemu nyingine nyeti.

Vijana wetu wameshuhudia litania ya Tanzania ya EPA, DOWANS na mambo mengine kama hayo ya kutorosha twiga na kuwauza nchi za nje. Kuna orodha ndefu inayoonyesha kwamba visingizio vya serikali kutokuwa na  fedha za kuwapatia mkopo  wanafunzi ni vya  uongo. Katika hali kama hii, si lazima CHADEMA kuingia vyuoni na kushinikiza migomo, bali hali halisi ndo chanzo cha matatizo yote hayo.

Serikali yetu ikiwa makini na kupanga vipaumbele, haishindwi kuwapatia wanafunzi wote na mtu yeyote anayependa kujipatia elimu ya juu mkopo. Uwezo huo upo, tatizo ni kwamba hatuna nia ya kuwekeza kwenye elimu. Hivyo tuache visingizio na porojo, vurugu za vyuo vikuu zinasababishwa na mfumo mbaya wa kutoa mikopo  kwa wanafunzi wa elimu ya juu.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment