Ingawa baadhi ya watu wanataka  kulilazimisha tamasha la Jinsia kuwa jukwaa la hoja moja tu ya Ushoga, ukweli utabaki palepale kwamba Jukwaa hili ni la watanzania wote kujadili mambo yanayohusu maisha yao. Na mwaka huu mada iliyojadiliwa ni Ardhi, Nguvu Kazi na maisha endelevu. Ushuhuda uliotolewa kwenye tamasha, visa mkasa vilivyoelezwa vinatoa tafsiri moja kwamba maisha endelevu  ni ndoto bila demokrasia na utawala bora.

Maendeleo ya haraka katika Taifa letu yatakuja pale ambapo tutafanikiwa kusimika utawala bora na demokrasia katika ngazi ya Vijiji, Vitongoji na Mitaa. Utawala bora na Demokrasia ni muhimu katika ngazi zote za utawala, lakini kwa vile asilimia kubwa ya watanzania inaishi vijijini na kumekuwepo hali ya kutowekea mkazo utawala bora na Demokrasia kule vijijini maendeleo ya taifa letu yamekuwa yakikwama mwaka hadi mwaka.

Chimbuko la misingi ya Utawala Bora na utumiaji wa madaraka na mipaka yake liko kwenye katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) na Sheria zilizotungwa na Bunge. Misingi ya utawala bora imeainishwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Sura ya kwanza, sehemu 2 na ya 3 ambayo inaeleza misingi mikuu ya malengo muhimu yanayoongoza uendeshaji wa shughuli za Serikali katika ngazi zote. Malengo haya ya utawala bora yanasema kwamba: Wananchi ndiyo chimbuko na madaraka ya serikali; katiba inashika hatamu; Kunakuwepo na utawala wa sheria; Usawa mbele ya sheria na kutokuwepo na ubaguzi; Kunakuwepo mgawanyo wa madaraka; heshima kwa haki za binadamu na utu wa mtu; uwajibikaji kwa wananchi; ushiriki wa wananchi katika vyombo vya dola; utumiaji wa utajiri na vyanzo vya utajiri vya nchi kwa faida na ustawi wa jamii; Maendeleo ya watu na uondoaji wa umaskini, ujinga na maradhi;  Ni wajibu wa dola kuhakikisha kwamba utajiri na njia muhimu za uchumi haviingii katika mikono ya watu wachache binafsi na wajibu wa vyombo vya dola na watendaji wake kuondoa ukandamizaji, vitisho, upendeleo, ubaguzi na rushwa.

Katika muundo wa sasa wa Serikali za Mitaa nchini, Vijiji, Vitongoji na Mitaa ni ngazi muhimu zilizo karibu na wananchi. Ngazi hizi ndipo mahali pa mwanzo wa Serikali na ambapo mikutano inayowajumuisha wananchi wote hufanyia kwa lengo la kuwapa wananchi nafasi ya kushiriki kikamilifu katika maamuzi yanayohusu ustawi na maendeleo yao wenyewe na ya eneo wanamoishi.

Maafisa Watendaji wa Vijiji na Mitaa ndio wasimamizi na watekelezaji wakuu wa shughuli za Serikali katika maeneo yao. Ili Watendaji hawa waweze kutoa huduma bora kwa wananchi hawana budi kuelewa maana, dhana na msingi ya Utawala Bora na Demokrasia.

Lakini pia kwa vile maendeleo ya nchi yanategemea sana ushiriki wa wananchi, ni vyema na wananchi wenyewe wakafahamu kwa undani maana, dhana na msingi wa Utawala Bora na Demokrasia. Uelewa wa Maafisa Watendaji wa Vijiji na Mitaa na uelewa wa wananchi ni muhimu sana katika kuleta maendeleo ya haraka.

Utawala bora ni utaratibu wa uongozi wa kisiasa kutokana na ridhaa ya wananchi unaolenga kuleta amani, utulivu, ushirikiano na maendeleo ya wananchi kijamii na kiuchumi bila ubaguzi kwa misingi ya jinsia, kabila, dini, mila na desturi au haiba ya mtu. Uongozi unaofuata misingi ya Utawala Bora hufanya kila jitihada kujenga heshima, kuthamini na kukuza uhuru na utu wa wananchi wote kwa namna ambayo inawezesha utumiaji wa rasilimali na nguvu kazi kwa makini na ufanisi ili kuhakikisha kuwa wananchi au raia wote wanapata mahitaji yao ya msingi. Mahitaji ya msingi ni kama vile chakula, mavazi bora, elimu, afya njema na maji safi na salama. Hivyo, kimsingi Utawala Bora ni utaratibu wa utumiaji wa madaraka ya umma katika kusimamia rasilimali za nchi katika jitihada za kuinua hali ya maisha ya wananchi. Utumiaji huo wa madaraka huambatana na ushirikishwaji wa wahusika wote katika kuhakikisha kuwa shughuli za umma zinaendeshwa kwa kuzingatia mawazo na maslahi ya wengi, utawala wa sheria, haki, usawa na uwazi na uwajibikaji.

Tumesema kwamba Utawala bora unazingatia Utawala wa Sheria. Tukumbuke pia kwamba sheria ni utaratibu ambao umewekwa na watu ili kuwaongoza kwa namna mbalimbali za kufikia malengo yao katika jamii au kati ya jamii fulani na nyingine. Katika utawala wa sheria kila mtu anapaswa kuzingatia na kuongozwa na Katiba ya nchi (ambayo ndiyo sheria mama na sheria nyingine zote zinapata uhalali kutoka kwenye katiba), sheria, kanuni na taratibu zilizopo katika kuendesha maisha yake mwenyewe, katika uhusiano na watu wengine na katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali. Hivyo utawala bora ni ule ambao unafuata sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa ili kuongoza shughuli za Serikali za kulinda  haki za msingi za wananchi na kudhibiti vitendo visivyotakiwa au kukubalika katika Jamii.

Utawala bora ni lazima uzingatie Uwazi na Uwajibikaji. Watendaji wa Serikali za Mitaa na Viongozi wa Kuchaguliwa katika ngazi mbalimbali wapo kwa minajili ya kuwahudumia wananchi na sio kuwatawala na kuwaburuza. Yamekuwepo malalamiko ya Maafisa watendaji wa Vijiji na Mitaa kuwaburuza wananchi. Huo si utawala bora.

Mbali na kuzingatia uwazi na Uwajibikaji, utawala bora ni pamoja na kuimarisha ulinzi na usalama wa Taifa pamoja na usalama wa raia na mali zao. Jukumu la ulinzi na usalama linategemea sana ushirikiano kati ya vyombo vya dola, watendaji wa serikali na wananchi wote kwa ujumla. Maafisa  Watendaji wa Vijiji na Mitaa wanapaswa kuhakikisha kuwa shughuli za ulinzi na usalama katika maeneo yao zinaimarishwa kwa kujadiliana na viongozi pamoja na wananchi kuhusu mbinu na mikakati ya kutekeleza jukumu hilo. Pia Utawala bora ni lazima upige vita rushwa. Tunajua kwamba rushwa ni adui wa haki na haina budi kupigwa vita na kila mpenda haki. Maafisa Watendaji wa Vijiji na Mitaa  kwa kushirikiana na wananchi ni lazima wahakikishe kuwa wanapambana na vitendo vyote vya rushwa katika maeneo yao ili kufanikisha ujenzi wa Utawala Bora nchini.

Jambo la kukumbusha hapa ni kwamba Utawala bora ni pamoja na Serikali katika ngazi zote kuwawezesha wananchi kuondokana na umaskini, ujinga na maradhi kwa kuwapatia huduma bora za kiuchumi na kijamii. Ni kazi ya Afisa Mtendaji wa Kijiji na Mtaa kusimamia uwezeshaji huu katika maeneo yao. Kama  tulivyosema hapo juu kwamba watanzania asilimia kubwa wako vijijini na kwenye mitaa, uwezeshaji huu ukifanikiwa, basi taifa letu linakuwa limepiga hatua ya haraka katika maendeleo.

Pamoja na yote niliyoyataja  hapo juu ni kwamba Demokrasia ni msingi muhimu sana katika ujenzi wa Utawala Bora. Bila Demokrasia ni ndoto kujenga Utawala bora katika ngazi zote za Utawala, kuanzia Vijijini, Mitaa hadi Serikali Kuu. Neno Demokrasia limetokana na lugha ya Kigiriki “Demos” ikiwa na maana ya watu na “Kratos” ikiwa na maana ya utawala. Ndiyo kusema, demokrasia maana yake ni Utawala wa watu walio wengi ambapo msingi wa mamlaka yote ya nchi ni wananchi wenyewe. Kwa maneno mengine, Serikali ya Kidemokrasia ni ile inayoundwa na watu wenyewe kwa ajili ya maslahi yao. Maana hii ya Demokrasia, ni muhimu kueleweka kwa Maafisa watendaji wa Vijiji na mitaa, na pia kueleweka kwa wananchi ili kusaidia kujenga Utawala bora katika ngazi ya Serikali za mitaa.

Ni imani yetu kwamba Tamasha la Jinsia, linachangia kiasi kikubwa kujenga uelewa huu( Maisha endelevu, demokrasia na utawala bora) miongoni mwa watanzania.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment