MTOTO WA AFRIKA NA UPORAJI WA ARDHI.


Tarehe 16.6.2011, kama kawaida ilikuwa ni siku ya Mtoto wa Afrika .Baadhi ya watu wameikumbuka, lakini inaelekea moto wake unaendelea kupunguka na kubakia ni siku ya watoto wa shule, kukutana na kuimba nyimbo, kucheza ngoma na maigizo. Watu wazima wanaanza kuikwepa siku hii. Jana kwenye taarifa za habari ilionekana asilimia kubwa ya watoto na asilimia ndogo sana ya watu wazima. Pamoja na jitihada za kuikwepa siku hii ukweli unabaki pale pale kwamba yaliyotokea Soweto miaka hiyo yanaweza kutokea tena popote kwenye nchi hizi za Kiafrika na Tanzania ikiwemo. Matendo ya ukiukwaji wa haki za watoto ikiwemo na uporaji wa ardhi yamekuwa mengi. Binafsi nimejenga utamaduni wa kuandika makala kila tunapoikumbuka siku hii ya mtoto wa Afrika. Ninaamini mchago wangu huu unaweza usiwanufaishe watanzania wa leo, lakini kama awasemavyo kwama “Kilichoandikwa kimeandikwa” ni imani yangu kwamba mchango wangu utawanufaisha hata watanzania wa kesho.

Mnamo mwaka 1976, Kule Soweto, Afrika ya kusini, maelfu ya watoto weusi wa shule waliingia mitaani na kufanya maandamano ya zaidi ya nusu kilomita, wakipinga elimu duni waliyokuwa wakiipata na kudai kufundishwa kwa lugha yao. Walifanya maandamano ya amani kwa lengo la kufikisha ujumbe kwa serikali ya makaburu. Ujumbe huu ulikuwa mchungu kwa wakubwa na hawakuwa tayari kuusikiliza. Kama kichaa anavyoweza kutumia bunduki kuua mbu, ndivyo makaburu walivyofanya kwa wanafunzi hao. Mamia ya wasichana na wavulana walipigwa risasi na kupoteza maisha yao.  Kwa vile bunduki inaua mwili, lakini fikra na roho vinaendelea kuishi, maandamano hayo hayakuzimwa kwa risasi! Machafuko yaliyofuatia tukio hili yalipoteza maisha ya mamia ya watu na kuacha majeruhi kadhaa.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoshuhudia matatizo mengi ya watoto. Tunashuhudia watoto wetu wanavyosukumwa kila siku kwenye daladala, watoto wanavyosoma kwa shida, shule za msingi wengine wanakaa chini, sekondari wanasoma bila kuwa na walimu wa kutosha, matokeo yake  wanafanya vibaya na kushindwa kuendelea na masomo ya juu. Lakini pia na wale wanaofanikiwa kuendelea na masomo ya juu, tunashuhudia wanavyonyanyaswa na Bodi ya mikopo. Tunashuhudia watoto wetu wakikoswa ajira, tunashuhudia watoto wetu wakibugia madawa ya kulevya, wakilewa pombe, wavulana wakisuka nywele na kujifananisha na wasichana, wasichana wakitembea nusu uchi na baadhi ya watoto wetu wakiikimbia nchi kwenda kuishi ughaibuni.  Kwa asilimia kubwa maisha ya mtoto wa Kitanzania, yanakuwa ni ya shida.

Binafsi, nimeamua mwaka huu niandike juu ya Mtoto wa Afrika  na uporaji wa ardhi.  Kwanini, nimeamua kuandika hivyo: chanzo cha siku ya mtoto wa Afrika, ni maasi yaliyofanywa na watoto wa Soweto, kwa kukataa kunyanyaswa. Walikuwa wakipata elimu duni ukilinganisha na ile ya Wazungu. Pia, walitaka elimu inayotolewa kwa lugha yao. Kule Soweto, watoto walianza kutambua kwamba wale waliokuwa wakifundishwa katika shule nzuri ndio waliokuwa wakipata kazi nzuri na vyeo vya juu katika serikali. Hali ya kutamani hali bora ya maisha kwa siku za mbele, hali ya kutaka kuwa na vyeo na nafasi nzuri za kazi, iliwafanya wanafunzi kukataa elimu duni waliyokuwa wakiipata. Hawakuogopa nguvu za jeshi la Makaburu. Walikuwa tayari kupambana bila silaha – na kweli wengi wao walipoteza maisha. Watoto wa Soweto, walitambua kwamba kujifunza kwa lugha za kigeni wasingepata maarifa yenyewe. Walitaka wafundishwe kwa lugha ya kwao, lugha inayofanana mazingira yao, lugha inayogusa maisha halisi, lugha inayoweza kuharakisha maendeleo. Hoja yangu ni kwamba Bila kuwa waangalifu, inawezekana na sisi hapa Tanzania, tunaandaa Tanzania ya kesho yenye maasi kama ya Soweto.

Kumetokea wimbi la uporaji wa ardhi. Watu wenye fedha wananunua ardhi kubwa kwa kisingizio cha kuwekeza. Matokeo yake vijana wengi watajikuta hawana ardhi na wataikataa hali hii. Na tunavyosikia kwenye vyombo vya habari sehemu nyingine hali hii imekataliwa mapema. Tunasikia kule Manyara jinsi watu wanavyovamia mashamba, kukata mazao na kuwashambulia wanao miliki mashamba. Tukio la Tegeta, la kukatana mapanga katika harakati za vijana kufukuzia mbali waporaji wa ardhi, ni la kusikitisha na kutafakarisha; na ni fundisho pia kwamba vijana wakiamua kudai ardhi yao, patachimbika.

Mgogoro wa ardhi wa Loliondo, tumeshuhudia jinsi ulivyovuruga amani kwenye maeneo hayo na kupanda mbegu ya maasi na chuki kwa vizazi vijavyo. Mashirika mbali mbali yasiyokuwa kiserikali yamepiga kelele juu ya swala hili la uporaji wa ardhi, lakini kelele hizi zimekuwa kama ile sauti iliayo nyikani. Mashirika haya yamekuwa yakijitahidi kutengeneza majukwaa ya majadiliano, ili watanzania tukae pamoja na kujadiliana juu ya uhai wa taifa letu. Tamasha la jinsia ni miongoni mwa majukwaa haya ya majadiliano.

Tamasha la jinsia ni nafasi ya wazi kwa ajili ya watu binafsi, mashirika na mitandao, walio katika mapambano yanayofanana, kubadilishana uzoefu, taarifa, kujengana uwezo, kusherehekea mafanikio na kutathimini changamoto zilizo mbele yao, kujenga na kuimarisha mitandao; na kupanga kwa pamoja mikakati kwa ajili ya kuleta mabadiliko ya -kijamii kwa mtazamo wa kifeminsti, kujengeana uwezo ili kuchangia katika mijadala ya wazi kuhusu maendeleo ya jamii na binafsi.

Tamasha la jinsia huandaliwa na Mtandao wa Jinsia  Binadamu na Usawa wa Jinsi (FemAct) pamoja na washirika wao. Tamasha la mwaka huu litafunguliwa kwenye viwanja vya TGNP Mabibo tarehe 13.9.2011 hadi 16.9.2011, kujadili mada kuu: Jinsia, Demokrasia na Maendeleo: Ardhi, Ajira na Maisha Endelevu. Wakimlenga mwanamke aliye pembezoni. Hii ni mada inayomguza moja kwa moja mtoto wa Tanzania na uporaji wa Ardhi. Tunajua fika kwamba ardhi inapoporwa na matajiri na mafisadi, anayeteseka kuwalea watoto ni mwanamke aliye pembezoni.

Ardhi ni muhimu sana kwa maisha yetu ya leo na vizazi vijavyo; uchumi wetu unategemea kilimo; bila ardhi hatuwezi kulima, hatuwezi kupata chakula na mazao ya kuuza na kujipatia fedha za kigeni. Hivyo ni muhimu sote kusimama pamoja kupinga wimbi hili kubwa la kupora ardhi yetu. Tuhakikishe kila Mtanzania ana ardhi yake ya kutosha na kupiga vita kwa nguvu zote ardhi kuwa mikononi mwa watu wachache.

Tunapoikumbuka siku mtoto wa Afrika, ni bora tukazingatia umuhimu wa ardhi kuwa ustawi wa mtoto wa Afrika. Tukiilinda ardhi yetu leo, tunaepusha machafuko ya ardhi kesho na keshokutwa. Lengo la makala hii pamoja na kuikumbuka siku ya mtoto wa Afrika, ni kuwakumbusha wasomaji wangu, kwamba tamasha la jinsi liko karibu. Tujiandae kushiriki na kupata jukwaa la kupaaza sauti zetu, kujadili na kupanga mbinu za kuleta maendeleo ya haraka katika taifa letu.

Na,
Padri  Privatus Karugendo.


 



1 comments:

Unknown said...

Padre. Ukigomboa (redeem)ardhi wewe mtoto wa miaka 30, je ardhi hiyo inakuwa yako au unairudisha kwenye familia? Huosi udhulumaji? KAMA jibu kuirudisha kwenye familia.

Post a Comment