MWANA MAMA




Ananilea Nkya

Safu hii ya Mwana mama imekuwa ikikuletea wasifu wa Mwana Mama, ni jitihada za kuhakikisha mchango unaotolewa na wanawake walio hai na wale waliotangulia mbele ya haki unafahamika. Vyombo vyetu vya habri vinatawaliwa na mfumo dume, kiasi kwamba utafikiri wanaoishi ndani ya taifa hili ni wanaume peke yao. Hivyo tumeamua kuwafutatilia wanawake popote walipo na kuandika juu yao, ili jamii itambue mchango wao na historia ya nchi yetu iandikwe kwa usahihi!

Leo hii tunawaletea Mwana mama Ananilea Nkya. Huyu ni mama jasiri ambaye amejitokeza kupagania haki na usawa wa wanawake na watoto. Amepambana kukomesha ukeketaji, mimba za utotoni, ukatili wa kijinsia na hasa kuhakikisha vyombo vya habari vinaandika na kufichua madhambi yote ya kuwanyanyasa na kuwatesa wawanawake na watoto.

Mama huyu ameongoza maandamano kupinga aina zote za uonevu katika taifa letu. Alipotekwa nyara, kupigwa na kuumizwa Dkt Ulimboka, Mama Ananilea, alikuwa mstari wa mbele kupinga unyama huo hadi akakamtwa na kuhojiwa na polisi. Msimamo wake, kuongea kwa kujiamini bila kuogopa, vimepelekea watu wengi kuhoji kama Mama huyu ameolewa! Kana kwamba mtu aliyeolewa, hana haki ya kuwa jasiri au kuzungumza kwa ukali juu ya mausala yanayokiuka haki nausawa. Ukweli ni kwamba mama huyu ameolewa, ana ndoa yake nzuri na watoto watatu.

Ukipata bahati ya kufanya kazi na Mama huyu ndipo unapoapata kumtambua na kumfahamu; Mama anayefanya kazi kwa kujitoa bila hata kuangalia posho na malipo; Mama anayependa kufuata muda na kuhakikisha kila kazi inafanyika kwa uhakika na utimilifu. Mama Mzalendo ambaye analipenda taifa lake na kuchukia kwa nguvu zote mfumo dume na ukatili wa ina yoyote ile wa kijinsia. Ni wazi utagundua kwamba hafanyi kazi zake ili kujijengea jina; anasukumwa na uzalendo ndani ya moyo wake. Ni mama anayetaka kuunganisha nguvu katika kufanikisha mambo; amekuwa mstari wa mbele kutaka mashirika yote yanayotetea haki za binadamu, haki za wanawake na watoto kuungana na kuwa na sauti moja. Nia yake ya kutaka kuunganisha nguvu, inampambanua na mashirika mengi yanayofanya kazi kwa lengo la kutengeneza fedha; anajipambanua na watu wote wanaofanya kazi kwa lengo la kujijengea jina na kutafuta sifa. Mama huyu anapenda majadiliiano na kuheshimu maoni ya watu wengine.

Mama huyu anauchukia ufisadi kwa chukio kamili. Anapinga mfumo wa watu wachache kupora rasilimali za taifa. Daima anasema “ Tunawaandalia watoto wetu vita. Ufisadi huu, ni lazima watoto wetu wachinjane. Hivyo ni wajibu wote sote kusimama na kusema hapana, ili tusiache maafa nyumba yetu”



Mama Ananilea Nkya, alikuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa) tangia 2001 hadi mwaka huu alipomaliza kipindi chake.



Anaelezwa kama miongoni mwa watu walio mstari wa mbele kupigania haki za kijinsia Tanzania. Jina la mama huyu linasikika pia katika nchi za Sweden, Holland, Ujerumani, Italia. Amesimama kidete kupaaza sauti yake juu ya ukeketaji, ukatili wa wanawake na watoto, habari za wanawake kuandikwa kwenye vyombo vya habari na usawa wa kijinsia katika vyeo vya kisiasa.



Tarehe 2 Mwezi wa tatu 2010 Balozi wa Marekani Tanzania Alfonso E. Lenhardt alimtunukia mama huyu Tuzo ya Mwanamke Jasiri wa 2010 katika utetezi wa usawa, fursa sawa na haki za wanawake na watoto Tanzania. Wakati anatukiwa tuzo hiyo, alikuwa kwenye unaharakati zaidi ya miaka 20.

Wakati wa kumkabidhi tuzo hiyo Balozi wa Marekani alikuwa na haya ya kusema:

"Mama Nkya kupitia tuzo hii ya mwanamke jasiri wa mwaka 2010 unatambuliwa kwa jitihada zako kutumia vyombo vya habari kuhamasisha jamii kujua haki zao, kukemea kwa nguvu ukatili wa wanawake na kupigania mabadiliko ya sheria kandamizi kwa wanawake...Jitihada zako za kufundisha waandishi wa habari wanawake na kuwawezesha wanawake kujitetea wenyewe kumeleta mabadiliko makubwa kwa jamii ya Watanzania,"

Balozi huyo alisema Tanzania inaweza tu kupata mafanikio iwapo wanawake watashirikishwa kikamilifu katika shughuli za ukuaji wa uchumi na kwamba njia bora ya kufika huko ni kuhakikisha wanawake wanapata elimu ya vyuo vikuu.

Alisema kupigania haki za wanawake ni suala la msingi ambalo wanawake na wanaume kwa pamoja wanapaswa kujivunia nalo kwani si suala la wanawake tu kwani linahusu haki za binadamu.

Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Nkya aliishukuru Marekani kwa kubuni tuzo hiyo na kwamba imeonyesha namna nchi hiyo inavyounga mkono mapambano mbalimbali ya wanawake katika kupigania haki zao. Alisema wanawake wanapambana ili kuweza kushiriki katika masuala ya maendeleo ili hatimaye wanufaike na rasilimali za nchi na kwenye huduma za afya,elimu, mirathi, uchumi na uongozi wa nchi yao.

Alisema ana hakika kuwa baada ya muda, tuzo hiyo itazaa matunda ya neema hasa kwa wanawake wengi wanaotaabika kwa mambo mbalimbali mijini na vijijini ambao wanapambana ili wapate haki ya kuthaminiwa utu wao.

Alisema wanawake wengi nchini hawana amani wala furaha kwa sababu ya mifumo kandamizi imewapora haki na fursa ya kutoa maamuzi kuhusu mambo yanayohusu maisha yao na familia zao na wameporwa pia fursa ya kushiriki katika vyombo vya kutoa maamuzi.



Mmama huyu alianza kazi ya uandishi wa habari 1982 RadioTanzania na wakati anajiunga na TAMWA 2001, alikuwa amepanda hadi Naibu Mhariri ndani ya RedioTanzania na kuendesha kipindi cha kutetea haki za wanawake –MWANGAZA.



Mama huyu anaamini kwamba uandishi wa habari ni kazi ya kuheshimika duniani ambayo ikitumika vizuri inaweza kuchangia kuibadilisha dunia hii kuwa sehemu nzuri ya kuishi kwa viumbe vyote.



Mwaka 1987, yeye na wanawake wengine 11 waandishi wa habari, waliungana kuunda TAMWA kama chombo cha kupigania na kulinda haki za wanawake na watoto kupitia vyombo vya habari. Na mwaka hadi mwingine mchango wa TAMWA unaonekana na kusikika ndani na nje ya Tanzania. Na kwa uongozi wa Mama Ananilea, mchango wa TAMWA umesikika zaidi kufikia hatua ya kutomtenganisha Ananilea na TAMWA, kila ikitajwa TAMWA, kinachokuja kichwani mwa watu ni Ananilea!



TAMWA imechangia utungaji sera, mfano SOSPA 1998, ambapo kwa mara ya kwanza sheria inatambua ukeketaji kuwa ni kosa la jinai na kuongeza miaka ya wabakaji kuwa 30 hadi kifungo cha maisha.



Mama huyu anaamini kwamba hata kama nchi itapiga hatua kubwa ya maendeleo ya kiuchumi ,kama heshima na haki ya wanawake havizingatiwi, maendeleo hayo yatatiliwa mashaka.



Mama huyu ana digrii ya Uzamili ya Uandishi wa Habari kutokaCardiff, UK 1992, Digrii ya kwanza kwenye Taaluma za maendeleo kutoka Kimmege, Ireland 2008 (Daraja la kwanza), Na Diploma ya uandishi wa habari aliyoipata Dar-es-salam kutoka Tanzania School of Journalism,1986. Alitunukiwa Tuzo ya Waziri Mkuu ya Mwanamke bora mwanafunzi na tasinifu bora ya uandishi wa habari.





Aliteuliwa kwenye bodi ya wakurugenzi wa huduma ya utangazaji 2001-2003. Kamishina wa Tume ya UKIMWI2008-2011. Mbali na kazi za ofisi Mama huyu hupendelea kucheza mpira wa kikapu, kuangalia taarifa za habari na kuwezesha shughuli za maendeleo ya vijijini.



Juhudi zake za kupenda kuchochea maendeleo ya vijijini zimejionyesha kwenye mradi wa kujenga nyumba bora katika kijiji cha Mwarazi – Morogoro, ambako alienda na kuishi siku kadhaa na wanakijii na kutengeneza kamati ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa nyumba bora 60.

Kwa kifupi, huyo ndiye Mama Ananilea Nkya!

Na,

Padri Privatus Karugendo.

+255 754 633122.

www.karugendo.net





0 comments:

Post a Comment