MWANA MAMA





Leo katika safu hii ya Mwana Mama tunawaletea Sista Martha Mwasu Waziri kutoka Kondoa, Huyu ni ni mshindi wa TUZO ya Mama Shujaa wa Chakula 2021-2013, ambaye aliibuka mshindi wa kwanza na kujinyakulia zawadi ya vifaa vya kilimo vyenye thamani ya shilingi milioni 10.

Sister Mwasu aliibuka kidedea kwa kuwaangusha washiriki wenzie 13 walioingia katika kinyanganyiro hicho kutokana na kuwa na juhudi na ubunifu mkubwa aliouonyesha kwa kipindi cha wiki mbili alizokuwa akiishi katika kijiji cha Maisha Plus zilizomsababisha kupata kura nyingi kutoka kwa wananchi Nafasi ya pili ilishikiliwa na Bi.Emilian Eligaisha kutoka Karagwe na kupewa zawadi ya vifaa vya ujenzi vya milioni 3, nafasi ya tatu ikichukuliwa na Bi. Tatu Abdi Kutoka Lushoto ambapo alipewa shilingi 700000

Akizungumza wakati akikabidhi zawadi kwa mshindi wa tuzo ya hiyo Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Bw. January Makamba alisema kuwa kuna kila sababu ya kuboresha mazingira rafiki kwa wakulima hususani kwa akina mama kwani shughuli zote za kilimo zinafanywa na wanawake

Alisema kuwa Fikra dume, sera dume, pamoja na mipango dume huzaa matokeo dume hii inasababishwa na kuleta utofauti wa jinsia katika utekelezaji na uwajibikaji wa maendeleo

Makamba alisema kuwa asilimia 95 ya chakula tunachokula kinazalishwa na akina mama, cha kushangaza asilimia 99 ya wasiyozalisha chakula ndio wanaomiliki ardhi, na kusababisha kuwa na unyanyasaji wa kijinsi unaomgusa moja kwa moja mwanamke

Sista Martha, ni mtawa wa kanisa Katoliki huko Kondoa. Kwa maelezo yake mwenyewe alianza kutamani maisha ya utawa akiwa na umri mdogo. Alijitahidi kujiunga na mashirika ya kitawa mara tatu akishindwa kwa sababu za afya yake mbaya. Baadaye alifanikiwa na kujiunga na utawa. Mama huyu mwenye umri wa miaka 45, leo hii ni kielelezo cha mwana mama shujaa. Ushindi wake wa Maisha Plus, haukuwa wa kubahatisha.

Huyu ni Mwana Mama asiyekata tamaa. Maisha yake ya kupigania maisha ya utawa bila ya kukata tamaa ni mfano mzuri wa kupambana na maisha. Alijaribu mara tatu kujiunga na utawa anashindwa, alikini hakukata tamaa, aliendelea mpaka akafanikiwa. Lakini pia kama tutakavyoona huko mbele, huyu ni mwana mama aliyebadilisha maisha ya wanakijiji chake kwa kuanzisha mbinu ya kilimo kwa kuikomboa ardhi iliyoonekana haina faida yoyote.

Kawaida tumezoea watawa kukaa ndani na kusali. Na kuna watu wengi hata na baadhi ya viongozi wa dini wanaoamini kwamba maisha ya watawa ni kukaa ndani na kusali. Lakini kwa Martha, maisha ni sala na kazi. Ameonyesha tofauti na kupigana hadi Taifa na dunia nzima imetambua kwamba utawa si kukaa tu ndani ya nyumba. Mtawa kushinda Maisha Plus, halikuwa jambo la kawaida. Sista huyu amekuwa akiongoza juhudi za kupata ardhi katika kijiji chake. Akiwa na umri wa miaka 17, aliona umuhimu wa kupambana kukomboa ardhi ambayo alikuwa ni ya mchanga mchanga na mto wa vipindi. Kila mtu alibeza jitihada hizo, lakini mama huyu shujaa, akukata tama. Kwa jitihada hizo na kwa kusaidiana na wanashirika wenzake amefanikiwa kupata eka 18.

Katika ardhi hii iliyokombolewa na kutengenezwa vizuri ili iweze kutumika, Sista Martha na wenzake wanaweza kuendesha kilimo cha miwa, mahindi, mihogo, ndizi na viazi. Wanazalisha miwa kiasi cha kuuza na kupata faida. Pia wanatumia sehemu ya ardhi hii kufuga mbuzi na kuku. Kilimo na ufugaji vimeinua uchumi wa shirika la masisita na wanaweza kuishi maisha bora ya kujitegemea. Pamoja na kilimo, kwa vile ardhi hiyo ina mkondo wa maji ambao unakuja wakati wa masika, waliamua kutengeneza pia na bwawa la samaki. Baada ya muda, na hasa wakati wa kiangazi bwawa hilo la samaki lilikauka. Wale waliokuwa wakimbeza sista Martha, ndo walipata nafasi nzuri ya kumcheka na kuona sasa kushindwa kwake kumefika. Kama Waswahili wasemavyo kwamba ukishikwa unashikamana. Hapo ndipo Sista Martha, alipoonyesha ubunifu wake. Alianzisha mkakati wa kuyalinda mazingira kwa kupanda miti na kuhakikisha matumizi mazuri ya maji. Ingawa mama huyu hana elimu ya juu, lakini ameweza kutoa mchango mkubwa wa matumizi ya ardhi na utunzaji wa mazingira.

Kupambana na bwawa lililo kauka, kilikuwa ni kigezo kikubwa cha watu kumkubali na kuona kwamba huyu ni mbunifu na mwenye kuona mbali. Kwa kuona mfano huo wa Sista Martha, zaidi ya wanakijiji 300, wamejiunga kwenye makundi zaidi ya matano na kushirikiana na Sista Martha, kuitumia ardhi iliyoonekana haina faida yoyote, ili kuendesha kilimo na kufuga. Wote wanasema bila kuona mfano wa Sista Martha, wasingejishughulisha na kilimo hicho ambacho siku za nyuma kilionekana kama ni mchezo tu wa kuingiza.

Mafanikio ya Sista Martha, katika kijiji chake na ndani ya shirika lake, mafanikio yake ya kushinda shindano la Maisha Plus, vinampatia mama huyu nafasi ya kuonekana ni mama shujaa katika jamii. Huyu ni miongoni mwa wanawake wengi kule vijijini wanaotoa mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa letu, lakini mama hawa hawasikiki. Na hawa watawa, wako wengi wamefanya mambo mengi makubwa, wamefanya kazi kwa hospitali, wametunza watoto wadogo kuwafundisha maadili na kuwaendeleza kwa kuwafundisha kazi za mikono na wakati mwingine hawa ndo mama wanaofundisha watoto kuanza kusoma na kuandika, lakini masisita hawa hawasikiki popote pale. Wamebaki kuwa watawa wa kanisani na kanisa linameza sifa zao zote. Viongozi wao kama mapadri na maaskofu ndo sifa zao zinachomoza kila kukicha. Ndo maana safu hii ya Mwana Mama imeamua leo kukuletea habari za mama huyu ambaye kwa nafasi yake ametoa mchango chanya kwenye taifa letu.

Na,

Padri Privatus Karugendo.



























































































0 comments:

Post a Comment