MWANA MAMA SAIDA KAROLI




Katika safu yetu ya Mwana Mama, leo hii tunawaletea Saida Karoli, mwana mama mwimbaji aliyevuma kwa nyimbo zake za Maria Salome, Kaisiki, Ndombolo na Mimi nakupenda. Mwana mama aliyejaliwa sauti nzuri nzuri ya kuimba na ufundi wa kupiga ngoma na kucheza. Mashabiki wake walimbatiza jina la “Wanchekecha”.

Ingawa umaarufu wake ulidumu kwa muda mfupi na baadaye kuzimika kama mshumaa, hakuna ubishi kwamba Mama huyu alikuwa mwimbaji wa kwanza Tanzania kupata umaarufu mkubwa nje na ndani ya nchi. Ni bahati mbaya kwamba mama huyu hakuwa na elimu ya kutosha kuweza kupigania mafanikio yake; mapromota waliomwibua ndo hao hao walioamua kumzika baada ya kuvuna kiasi cha kutosha kutokana na jasho na msanii huyu.

Saida Karoli (amezaliwa tar. 4 Aprili, 1976, Kagera) ni mwanamuziki wa nyimbo za asili ya Kihaya nchini Tanzania.

Saida alipata elimu ya msingi mwisho darasa la tano tu ambapo ilibidi aache shule kutokana na kukosa msaada kutoka kwa baba yake ambaye hakuwa anaitazama sana elimu ya mtoto wake hivyo hakuweza kuendelezwa

Saida alikulia katika kijiji cha Rwongwe mkoani Kagera na kutokana na mila za ukoo wake wasichana walikuwa hawaruhusiwi kushiriki katika shughuli za kimuziki.

Hata hivyo kwa vile mama yake alikuwa na kipaji cha muziki alimpa moyo na kumfundisha masuala mbalimbali ya kimuziki.

Akiwa na miaka 20 mama yake mzazi alifariki dunia lakini Saida aliendelea kujijengea kipaji chake cha uimbaji na upigaji ngoma.

Kukua kwake kimuziki Kipaji cha usanii wa muziki kwa Saida kilijitokeza ghafla baada ya kujikuta akichukuliwa na kudhaminiwa na FM Productions Ltd waliokuwa mkoani Kagera wakitafuta wasanii wenye vipaji kwa ajili ya kuwaendeleza.

FM ilimchukua Karoli wiki tatu tu kurekodi nyimbo yake ya kwanza ilotoka na kuishitua Dar es Salaam mzima pamoja na nchi za jirani za Afrika Mashariki.

Albamu yake ya kwanza ilizinduliwa tarehe 2 Septemba mwaka 2001.

Albamu hiyo ilipata mafanikio makubwa na kupata umaarufu mkubwa sana kwakuwa albamu hiyo ilikuwa na vionjo vingi vya kabila la Kihaya.

Albamu hiyo ilijulikana kama Maria Salome. Japokuwa mashabiki wake waliibatiza jina la Chambua kama Karanga kutokana na maneno aliokuwa anaimba katika nyimbo ya Maria Salome nyimbo iliobeba jina la Albamu.

Albamu hiyo ilifuatiwa na ziara kubwa alizokuwa anafanya katika nchi za jirani kama vile Burundi, Rwanda, Uganda na Kenya ambapo alipata mafanikio makubwa na Saida kujikuta akibatizwa na kupewa jina la malkia wa nyimbo za asili.

Mara tu Saida kutoa albamu yake, wimbo wa Maria Salome ulipanda chati katika Kumi bora za Maredio kadha wa kadha nchini Tanzania na kufikia namba moja ikishikilia nafasi hiyo kwa wiki sita mfululizo.

Nyimbo zingine zilizotamba katika albamu hiyo ni pamoja na Kaisiki na Ndombolo.

Baada ya miezi mitatu tu tangu kutoa albamu hiyo, Karoli alipata mwaliko wa kuimba Uganda akialikwa na Kabaka wa Buganda katika sherehe ya kiutamaduni kama mmojawapo wa mwanamuziki aliyefanikiwa Afrika na kujulikana sana nchini Uganda na pia kumfanya kuwa mwanamuziki wa mwaka katika sherehe ile nchini Uganda.

Kujulikana kwake kwa kasi nchini Uganda kulisababishwa na matumizi ya lugha ya Kihaya, lugha inayofanana zaidi na lugha ya Kiganda inayotumika na Waganda wengi, sauti nyororo na ya kuvutia na vionjo kibao vya kuvutia vya kijadi katika nyimbo zake.

Mnamo mwezi Juni mwaka 2003 Saida akatoa albamu nyingine nzuri iliyokwenda kwa jina la Mapenzi Kizunguzungu na kuweza kuteka soko la muziki tena kwa mara ya pili kutokana na vionjo kama vya awali vya kijadi.

Hata hivyo Saida Karoli ametoa shukrani zake za dhati kwa Mkurugenzi Mkuu wa FM Productions LTD bwana Felician Mutta kwa kuona kipaji chake na kumpandisha chati kama mojawapo wa wanamuziki maarufu chini Tanzania.

Mutta amesema nia yake kwa msanii huyo ni kuona Saida anajulikana na kushika cha katika bara zima la Afrika na kuweza kufanya ziara za kimuziki nchi nyingi tu duniani.

Kutokana na uwezo alionao na kipaji katika masuala ya muziki ni rahisi kugundua kuwa mwanamuziki huyo ana kiwango cha kuweza kupata mashabiki wa muziki wake mbali na Tanzania na Afrika ya Mashariki tu, bali hata nje ya Afrika

1. Maria Salome

2. Kaisiki

3. Ndombolo

4. Mimi Nakupenda



0 comments:

Post a Comment