RWANDA, WAMETHUBUTU, WAMEWEZA NA WANAENDELEA KUSONGA MBELE.

Siku za hivi karibuni hapa kwetu Tanzania tumekuwa na kauli mbiu ya tumethubutu, tumeweza na tunaendelea kusonga mbele. Ni kauli mbiu ya kutia moyo na  yenye ushawishi mkubwa wa ndani na nje kuonyesha kwamba kama taifa huru tumepiga hatua kubwa. Ni wazi yamefanyika mengi na mengine yalikufa mapema hata kabla ya kuzaa matunda mengi; siasa ya ujamaa na kujitegemea, mashirika ya umma, viwanda, usafiri wa anga na wa reli, lugha yetu ya Kiswahili na mambo mengine mengi aliyokuwa ameyaanzisha Marehemu Mwalimu Nyerere. Hivyo kusonga kwetu mbele ni jambo linalotia shaka. Wakati mwingine ni vigumu kuangalia kwa macho na kuyaona yale tuliyoyafanya miaka hamsini ya uhuru wetu. Si lengo la makala hii kusema kwamba hatujafanya kitu, swali ni je tunaweza kutembea kifua mbele kwa kauli mbiu hii?

Tunaposema tumethubutu, tumeweza na tunaendelea kusonga mbele, hatuna viwanda vya kuonyesha kwamba hivi ni viwanda vyetu, hatuna ndege za kuonyesha kwamba hili ni shirika letu la ndege, hatuna hospitali nzuri za kuwatibu viongozi wetu, wakiugua tunawakimbiza  Uingereza na India, la kushangaza zaidi hatuna hata na lugha yetu! Miaka hamsini ya Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam hotuba zote hata na msherekeshaji walitumia lugha ya kigeni. Tunaweza vipi kusema tunasonga mbele wakati kwa miaka hamsini  wasomi wetu wameshindwa kuiendeleza na kuisimika lugha yetu ya Kiswahili kuwa na uwezo wa kuelezea mambo yote ya kimataifa, ya kisiasa, kiuchumi, kisayansi nk. Kwa nini tuendelee kuamini kwamba tunapotumia lugha ya kigeni tunaeleweka zaidi ndani na je ya nchi yetu? Kwa nini tuendelee kuamini kwamba lugha za kigeni ndio “Usomi”? Huko ni kusonga mbele? Au ni kurudi nyuma kwenye ukoloni na utumwa wa kifikira?

Katika makala iliyopita nilidokeza kwamba Rwanda, wamethubutu, wameweza na wanaendelea kusonga mbele. Wakati sisi tunaiimba kauli mbiu hii kwa mbwe mbwe zote, wenzetu wa Rwanda wanaitekeleza kauli mbiu hii kwa vitendo. Safari yetu ya kwenda Kigali, mimi na Mama Eva Kihwele Mwingizi, tulioiwakilisha TARAFA katika sherehe za kumkumbuka Marehemu Mwalimu Nyerere, tulipanda Ndege ya Shirika la Ndege la Rwanda (RwandAir). Shirika hili lenye ndege za kisasa, linafanya safari zake nchini Rwanda, Bujumbura, Dar-es-Salaam, Arusha, Nairobi, Mombasa, Johannesburg, Libreville, Brazzaville, Dubai na kwa kushirikiana na mashirika mengine linafanya safari za London, Amsterdam na Guang Zhou. Tulifurahi kusafiri na shirika hili na kukubali kwamba Rwanda, wamethubutu, wameweza na wanaendelea kusonga mbele. Wakati sisi shirika letu la Ndege haliwezi hata kufanya safari za ndani, Wanyarwanda wanakata anga kuelekea mashariki ya mbali na Ulaya.

Jambo la pili lililoyavutia macho yetu na kutusukuma kukubali kwa kauli moja kwamba Rwanda wamethubutu, wameweza na wanaendelea kusonga mbele ni usafi na mpangilio wa Jiji la Kigali. Jiji hili ni safi na limepangiliwa vizuri. Mwaka wa 2008, shirika la umoja wa mataifa la makazi, lilipatia Kigali tuzo ya kuwa miongoni mwa majiji safi Afrika. Mkuu wa wilaya ya Muleba Bi Angelina Mabula, tuliyeungana naye Kigali kusherehekea kumbukumbu ya kifo cha Mwalimu Nyerere, kwa kushangaa usafi wa jiji la Kigali alisema  “ Kigali ni safi kiasi kwamba hata na miti inaogopa kudondosha majani”. Si kwamba miti inaogopa kudondosha majani, bali kuna watu wanalisafisha Jiji la Kigali usiku na mchana. Mbali na usafi, Kigali ni jiji lenye ndoto za kutokomeza rushwa, uhalifu, utapiamlo na migogoro ya kiutawala.

Jambo la tatu la kujifunza ni Rwanda kufanikiwa kuwashirikisha vijana na wanawake kati uongozi wa nchi. Wakuu wa wilaya, wakuu wa mikoa, mawaziri, wabunge na maseneta umri wao ni kati ya miaka 30 hadi 45. Wazee wanabaki kuwa washauri, lakini uongozi wa nchi unakuwa mikononi mwa vijana wenye uwezo wa kukimbia mchakamchaka. Kufuatana na yale tuliyoyaona na kuyashuhudia, vijana  wameisaidia Rwanda kupata maendeleo ya kasi.

Jambo la nne la kujifunza ni kwamba Kiongozi wao Rais Paul Kagame, ana vision, analipenda taifa lake, anawapenda watu wake na hana uswahiba . Hana cha ndugu wala mwenzetu. Yeye anafuata utendaji wa kazi. Watumishi wote wa umma wana mkataba wa kila mwaka na rais wao. Mwaka unapoanza kila mtumishi anaorodhesha vipaumbele vyake vya mwaka huo na kufunga mkataba na rais. Mwaka unapokwisha, kuna tathimini, na nguzo kuu nne za tathimini ni uchumi, utawala bora, huduma za -kijamii na haki, yule anayepata alama chini ya hamsini basi huyo anakuwa amejifukuza kazi. Anayevuka juu ya hamsini na kufanya vizuri zaidi anapata zawadi na cheti cha ushindi na wakati mwingine anapandishwa cheo.  Kutokuwa na uswahiba kumemsaidia Rais  Kagame, kulishughulikia kwa ujasiri mkubwa suala la ardhi. Wale waliokuwa wamejilimbikizia ardhi kubwa aliwanyang’anya na kuigawa ardhi kwa Wanyarwanda waliokuwa hawana hata kipande cha ardhi. Ni wazi baadhi ya viongozi wa Rwanda, hawakupendezwa na hatua hiyo, waliamua kuikimbia Rwanda na kueneza uongo dunia nzima kwamba Rais Kagame ni dikteta. Kwa upande mwingine, kitendo hiki cha kuigawa ardhi bila kuangalia cheo cha  mtu, bila kufuata uswahiba na bila kufuata undugu kiliongeza sifa na upendo wa Wanyarwanda kwa Rais Kagame.

Leo hii Tanzania tuna migogoro mikubwa ya ardhi. Baadhi ya viongozi wameteka ardhi kubwa na wengine wanapora ardhi ya wananchi. Kuna haja ya kwenda Rwanda kujifunza jinsi walivyoitanzua migogoro ya  ardhi maana kusema kweli kwa suala hili la ardhi, wamethubutu, wameweza na wanaendelea kusonga mbele. Kwa kifupi ni kwamba sisi watanzania tuna mambo mengi ya kujifunza kutoa Rwanda:

Tulipokutana na Waziri wa Serikali za mitaa Mheshimiwa James Musoni alitwambiwa “ Kufikia Desemba mwaka huu hakuna Mnyarwanda atakayekuwa akilala kwenye nyumba ya nyasi. Wanyarwanda wote watakuwa na nyumba nzuri za kisasa zilizoezekwa kwa mabati na vigae. Hayo ndiyo malengo tuliyojiwekea na kuingia mkataba na Rais wetu. Yasipotimia, basi mimi na wote walio chini yangu ni lazima tuwajibike kwa kuacha kazi. Hata hivyo nina imani tutafanikiwa maana tumepiga hatua kubwa”. Mheshimiwa Musoni aliendelea kutuelezea kwamba “ serikali ikisaidiana na mashirika yasiyokuwa kiserikali, inahakikisha kwamba kufikia mwaka kesho, kila Mnyarwanda awe na godoro”. Na kuongezea kwamba “Familia ambazo ni masikini serikali inazipatia Ng’ombe mmoja wa maziwa ili waweze kuinua kipato na kuboresha lishe ndani ya kaya. Soko la maziwa liko mlangoni mwa kila kaya, maana gari la kusomba maziwa linazunguka kila siku kupita kwenye kaya zenye maziwa”.

Mheshimiwa James Musoni, alituelezea sheria iliyotushangaza sote ya maji ya mvua: “ tumetunga  sheria ya maji ya mvua. Hakuna mtu anayeruhusiwa kuyaachia maji ya mvua kwenye paa la nyumba yake kutiririka kwenda kwa jirani yake au barabarani. Kila mtu ni lazima kuhakikisha anayavuna maji kwenye paa lake ili kuepusha kuleta maafa kwa jirani au mafuriko. Anayeshindwa kufanya hivyo anawajibishwa kisheria”. Sheria hii ingekuja hapa Dar-es-Salaam, labda adha ya mafuriko mvua zinaponyesha ingepungua.

Mikutano tuliyoifanya na wakuu wa wilaya, wakuu wa mikoa na kuongea na watu mbali mbali, tumeambiwa na kuona wenyewe kwamba Rwanda inapiga hatua kubwa katika maendeleo. Barabara nyingi zimetengenezwa kwa kiwango cha lami, majengo yamejengwa kwa mpangilio mijini na vijijini, usafi unazingatiwa mijini, vijijini, barabarani hadi kwenye kaya. Mazingira yametunzwa kwa kupanda miti na maua. Wanyarwanda wanaweza kusimama kifua mbele na kusema: Tumethubutu, tumeweza na tunaendelea kusonga mbele:

Rwanda wameweza kuzalisha chakula cha kutosha na kubakiza ziada ya kuuza nje. Hii ina maana wameweza kupambana na janga la njaa ambalo lilikuwa likiisumbua nchi hii kwa miaka mingi. Wameweza kuwatunza na kuwalinda watoto yatima na wajane, wamefanikiwa kusimamisha utawala wa sheria na kuiletea nchi yao amani na utulivu. GDP ya Rwanda inakuwa kwa asilimia saba kila mwaka, na kufikia mwaka huu kipato cha Mnyarwanda kwa mwaka ni zaidi ya dola 500. Kwa sababu ya amani na utulivu watalii wameendelea kuja Rwanda, mwaka wa 2010 kiasi cha watalii 666,000 walikuja Rwanda na kuingizia nchi hiyo kiasi cha dola za marekani milioni 200. Kuna chanzo kingine cha mapato, ambacho sisi kwetu Tanzania hatujakirasimisha na hadi leo hii hatujui kinaingiza kiasi gani. Wanyarwanda wanaoishi nje ya Rwanda wanaingiza zaidi ya dola milioni 200 kila mwaka.

Mwaka 2003, Wanyarwanda waliokuwa wakipata huduma ya maji safi na salama walikuwa asilimia 41, mwaka huu Wanyarwanda asilimia 80 wanapata maji safi na salama. Mwaka 2000, ni kaya asilimia 4 ndio zilikuwa na huduma ya umeme, kufikia mwaka huu asilimia 13 ya kaya zinapata huduma ya umeme.

Chini ya uongozi wa Rais Kagame, Rwanda imejenga hospitali nzuri na zenye huduma bora. Tuliambiwa kwamba hata yeye Rais Kagame na viongozi wengine wa kitaifa wanatibiwa kwenye hospitali hizo. Ni tofauti kabisa na kwetu Tanzania, ambapo hata kama viongozi wetu wanaumwa mafua wanakimbizwa Uingereza na India. Mwaka 2003 asilia 7 ya Wanyarwanda ndio walikuwa na bima ya afya, lakini leo hii asilimia 96 ya Wanyarwanda wana  bima ya afya. Mwaka 2000, asilimia 40.6 ya Wanyarwanda walikufa kwa ugonjwa wa malaria, idadi hii imepungua kufikia  asilimia 16 mwaka wa 2009.

Chini ya uongozi wa Rais Kagame, Rwanda imeweza kujenga shule nyingi na kuziboresha. Tuliambiwa kwamba hata watoto wa  Rais Kagame na viongozi wengine wa kitaifa, watoto wao wanasoma kwenye shule hizo. Watoto wote wa Rwanda wanamaliza miaka tisa ya elimu ya msingi. Mpango wa kompyuta kwa kila mwanafunzi umefanikiwa kiasi kikubwa. Hadi mwanzoni mwa mwaka huu zaidi ya “laptops” 57,387 zimesambazwa kwenye shule 113 nchi nzima. Vyuo vikuu navyo vimeongezeka, leo hii Rwanda ina wanafunzi 62,734 kwenye vyuo vikuu idadi ambayo ni mara 17 ya ile ya mwaka 1993 kabla ya mauaji ya kimbali. Asilimia 44 ya wanafunzi wa vyuo vikuu ni wasichana.

Rwanda hawachangii arusi kama tunavyofanya hapa Tanzania. Wao wanachangia elimu na miradi ya maendeleo. Gharama za sherehe za arusi inabaki kuwa ni shughuli ya mtu binafsi; ndugu na jamaa wanaalikwa, lakini wanajinunulia kinywaji chao na kushiriki na ndugu yao furaha ya siku kwa gharama ndogo bila kujiingiza kuchangishana mamilioni ya fedha kama tufanyavyo sisi kwenye vikao vya arusi.  Hili nalo ni la kujifunza kutoka Rwanda, maana fedha tunazochangishana kwenye vikao vya arusi tukiziweka kwenye elimu na miradi ya maendeleo, tunaweza kusimama kifua mbele na kusema; tumethubutu tumeweza na tunaendelea kusonga mbele vinginevyo kauli mbiu hii tuwaachie wenyewe!

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment