SAKATA LA POSHO NI KIPIMA JOTO KWA WABUNGE  WETU.


Inawezekana kabisa kwamba Mheshimiwa Zitto ana ajenda yake binafsi ya kuibua hoja hii  ya kufuta posho za wabunge na watumishi wengine wa serikali; Inawezekana analenga uchaguzi mkuu wa 2015; kwa mwanasiasa tena kijana kama yeye kuwa na malengo ya mbele si dhambi; na kama ajenda yenyewe si ya kuliangamiza taifa letu. Lakini pia inawezekana kabisa kwamba Mheshimiwa Zitto, ana nia njema ya kuibua hoja hii. Si kweli kwamba leo hii Zitto ameibuka kuwa tajiri kiasi cha kuzikataa posho; anazihitaji posho lakini ziwe za haki na zisiwe mzigo mkubwa kwa walipa kodi masikini wa Tanzania. Kwa vile hatuko ndani ya moyo wa Zitto Kabwe, hatuwezi kusema kwa uhakika lile analoliwaza yeye zaidi ya kuiweka hoja yenyewe kwenye mizani, kuipima, kuijadili na kuichambua kwa kina. Tuiangalie hoja yenyewe bila kujali aliyeiibua; tuiangalie hoja yenyewe bila kujali imetoka kambi gani.

Hatuwezi kusema kwamba hii ni hoja ya Zitto Kabwe na kwamba anaitumia kujitafutia umaarufu, maana tumeshuhudia sote kwamba hoja hii imeungwa mkono na wabunge wote wa CHADEMA na baadhi ya wabunge wengine kutoka vyama vingine hata ndani ya CCM. Wabunge makini wa CCM, wanajua fika kwamba wakicheza na hoja hii wanakwenda na maji; kwamba haitapitishwa Bungeni ni wazi; maana wabunge wa CCM ni wengi na kwa utamaduni wao waliojijengea wa kukitanguliza chama chao badala ya kulitanguliza taifa ni lazima waipinge hoja ya Zitto na kuipitisha bajeti ambayo haina tija kwa watanzania. Hata hivyo ukweli daima utabaki kuwa ukweli na historia ni mwamuzi mzuri.

Wengine wanataka kuipotosha hoja yenyewe. Zitto Kabwe, hajasema kwamba wabunge wasipate mshahara na posho zao za kuwawezesha kula, kunywa na kulala pale Dodoma; au posho za kumwezesha mbunge kufanya kazi zake ndani ya jimbo lake. Ugomvi wake ni posho za nyongeza ambazo mbunge anazipata wakati akitekeleza majukumu yaliyo ndani ya wajibu wake kama mbunge; majukumu ambayo  ndio yanampatia mshahara wake wa ubunge.

Ugomvi wa Zitto ni posho wanazozipata watumishi wa serikali wakiwa wanatekeleza majukumu yao. Kwa nini kwa mfano Mkuu wa Wilaya anapofungua warsha, semina kongamano au shughuli nyinginezo  ndani ya wilaya yake apokee bahasha? Hiyo posho ni ya nini wakati mkuu huyo wa wilaya anakuwa akifanya kazi yake ndani ya wilaya yake? Mkuu wa wilaya ana mshahara wake na marupurupu mengine ndani ya ofisi yake; kwa nini basi aongezewe na posho nyingine nyingi?  Au Katibu mkuu wa wizara anapoendesha mikutano, warsha au semina ndani ya wizara yake kwa nini apokee bahasha wakati kazi anazozifanya ni kati ya kazi zinazomfanya apokee mshahara wa Katibu mkuu? Ipo mifano mingi ya watumishi wa serikali kupokea posho wakati wakifanya kazi ambazo ni wajibu wao na habari za kuaminika ni kwamba baadhi ya watumishi wa serikali wanapa posho kubwa zaidi ya mishahara yao .Na baadhi ya posho hizi zinawekwa kwenye bajeti ya serikali.

Ugonjwa huu wa posho na bahasha umegeuka kuwa kansa ya taifa letu. Huwezi kuitisha mkutano, hata kama unahusu maendeleo ya watu wenyewe; ukawapata washiriki wa kutosha kama hukuandaa posho na bahasha. Inashangaza kuona hata yale mashirika (kutoka mataifa ya nchi zilizoendelea ya Ulaya na Amerika) ambayo yako mstari wa mbele kuhimiza maendeleo kuletwa na wananchi wenyewe wanaweka kifungu cha posho na bahasha kwenye bajeti zao. Serikali yenyewe inaweka bajeti ya posho na bahasha!

Hii ndiyo hoja ya Zitto, na kusisitizwa na Mheshimiwa Mbowe na watu wengine walio makini kwamba posho hizi zikishughulikiwa ipasavyo, zikapunguzwa au kufutwa kabisa, serikali itaokoa zaidi ya trilioni moja inayoweza kuelekezwa kwenye shughuli nyingine za ujenzi wa taifa letu. Kama nilivyosema mwanzoni mwa makala hii, hoja inaweza kuwa imelenga sehemu Fulani; umaarufu na mbio za urais wa 2015; vyovyote vile bado ni hoja ya msingi ambayo ni lazima watanzania wengi wenye uchungu na nchi yao wataibeba na kuikumbatia. Kama CCM walifikiri CHADEMA ni maandamano na kuzunguka nchi nzima wakitukana; wamepotea njia. Maana hoja ya posho si ya kubeza; bila wabunge wote kuchukua hatua hiki ni kitanzi kitakachowakumba wengi.

Kwenye bajeti tuliyosomewa juzi, tumesikia kwamba serikali itapunguza posho. Lakini hatukuwaambiwa posho hizo zitapungua kutoka kiasi gani hadi kiasi gani. Na wala hatukuambiwa kwamba mwaka uliopita serikali ilitumia kiasi gani cha fedha kama posho na sasa inatarajia kutumia kiasi gani. Bahati nzuri au mbaya wakati bajeti inaandaliwa hoja ya posho ilikuwa haijaibuliwa; vinginevyo mtu makini angejipanga jinsi ya kuwasilisha hoja hii ndani ya bajeti. Vinginevyo ni kusoma mambo mengi kwenye hotuba ya bajeti yasiyokuwa ya msingi na kuyaacha ya msingi.

Mheshimiwa Waziri wa Fedha, alisoma hotuba ya bajeti masaa mawili na dakika kumi na  tano. Ni kazi nzito na ya kuchosha ukizingatia na asubuhi yake alikuwa amesoma hotuba nyingine ndefu ya hali ya uchumi. Lazima tumpongeze kwa kazi hiyo ya kuchosha. Bahati mabaya ni kwamba alijichosha kwa mambo mengi yasiyokuwa na maana, ambayo watu wangeweza kujisomea. Baada ya kuvisambaza vitabu vya bajeti, kuna umuhimu gani kuisoma bajeti nzima? Muhimu ni mchango wa wabunge kwenye bajeti hiyo; na wanaweza kufanya hivyo baada ya kuisoma na kuielewa yote; hawafanyi hivyo kwa kuisikiliza ikisomwa na mheshimiwa waziri. Na tumezoa kwamba hotuba hii ya bajeti na bajeti za wizara moja moja zinawekwa kwenye magazeti yote kama tangazo ili watu wengi wazisome; ingawa kuna shinikizo la serikali kukataza matangazo haya ya bajeti kuwekwa kwenye vyombo vya binafsi bado hitaji hili ni la muhimu sana. Magazeti ya serikali ni machache na usambazaji wake ni mdogo kulinganisha na magazeti ya makampuni binafsi. Hili likitokea, la kuzuia matangazo ya bajeti kuwekwa kwenye magazeti ya makampuni ya watu binafsi, tutaamini kwamba serikali haina nia njema ya kusambaza habari kwa wananchi wake. Masaa mawili yote aliyoyatumia waziri wa fedha kusoma hotuba ya bajeti yalipotea tu kwa vitu visivyohusiana na bajeti ya wananchi! Waziri angeweza kuwasilisha bajeti hiyo kwa dakika kumi na tano tu. Wananchi wanataka kujua tumezalisha nini mwaka uliopita, tumetumia kiasi gani, tumebakiza kiasi gani? Na mwaka unaoanza tutazalisha nini, tutatumia kiasi gani na tutabakiza kiasi gani. Ngonjera nyingine ni mfumo wa kuwasilisha bajeti ambao tumeurithi kutoka wapi? Bila kubadilisha mfumo huu tutabaki kuwa watu wa porojo na maneno bila kufikia maendeleo ya kweli.

Inawezekana Mheshimiwa Zitto Kabwe, alishutuka kuona serikali inasema kupunguza posho wakati bado kuna mabilioni ya shilingi yametengwa kwa ajili ya posho bila maelezo ya kina kwamba posho hizi zitatolewa kwa misingi ipi na kwa nani? Labda hili lingeelezwa vizuri kwenye hotuba ya bajeti, asingeibua hoja hii ya posho ambayo imepandisha joto ndani ya Bunge na kutishia kuleta mgawanyiko.

Tunataka tusitake hoja hii ya posho  ni kipima joto kwa wabunge wetu. Tumekuwa tukilalamika kwamba baadhi ya wabunge wetu wanaingia Bungeni kutafuta posho na wala si kuwawakilisha wananchi waliowatuma; tumekuwa tukisema kwamba uwakilishi wa kweli ni ule wa mvuvi kumwakilisha mvuvi, mkulima kumwakilisha mkulima; mfugaji kumwakilisha mfugaji; mwanakijiji kumwakilisha mwanakijiji mwenzake na mtu wa mjini kuwawakilisha wenzake wa mjini. Kinyume na hapo ni usanii wa kutafuta posho; tumeliandika hili na kulieleza kwa kina; wengine walifikiri ni uzushi, ila sasa baada ya mheshimiwa Zitto kuliweka bayana na yeye kutangaza na kuandika barua kwa Spika akiomba posho zake zifutwe ukweli umejionyesha wazi.

Wabunge wengi wamekuja juu na kulalamika, hawataki posho zao ziguswe na hasa wakati huu ambapo ndio tumetoka kwenye uchaguzi mkuu. Baadhi yao walitumia fedha nyingi kwenye uchaguzi na wanatafuta njia za kurudisha fedha hizo; kwa hesabu tulizozipata za Mbunge kuondoka na zaidi ya shilingi 150,000 kwa siku, inatia matumaini kwamba Mbunge anaweza kufanikiwa kuyalipa madeni yake. Hata Mheshimiwa Augustine Mrema, ambaye walio wengi tuliamini ni mpambanaji na mtetezi wa wanyonge; ukiachia mbali harakati zake za miaka ya nyuma, juzi juzi hapa tumeshuhudia kwenye vyombo vya habari alivyokuwa akiwachachafya watumishi wa Halmashauri za wilaya juu ya matumizi mabovu ya fedha za umma; naye amesimama kupinga posho zisifutwe akisema kwamba Zitto alizikuta posho na ataondoka na kuziacha!

Huu ni wakati mzuri wa wananchi kuwapima wabunge wao. Je wanaguswa na posho zao tu au wanaguswa na mambo mengine ndani ya bajeti tuliyosomewa juzi. Wataipitisha bajeti kwa kushangilia au watahoji vipengele vyote?;

Tumeambiwa kwenye bajeti iliyosomwa juzi kwamba serikali itapunguza safari za viongozi nje na ndani ya nchi.  Je mwaka jana safari hizi zilikuwa ni ngapi na zilitumia fedha kiasi gani? Na mwaka huu zitapungua kutoka ngapi hadi ngapi? Tumesikia kwamba serikali itapunguza semina, warsha na makongamano; ni maneno kama yale ya bajeti ya mwaka jana. Je mwaka jana semina zilikuwa ni ngapi na zilitumia fedha kiasi gani? Tumeambiwa kwamba serikali itaacha kununua magari ya kifahari; je mwaka jana ilinunua mangapi na mwaka huu inatarajia kununua mangapi?

Hoja inayojengwa hapa ni je wabunge wetu watakuja juu kuhoji baadhi ya mambo yaliyokwenda tenge kwenye bajeti kama walivyokuja juu na kuonyesha mshikamano wakati wa kutetea posho zao? Wabunge watapiga kelele bei ya sukari ishuke? Watapiga kelele bei ya mafuta ishuke? Watapiga kelele ili mwananchi wa kawaida kijijini auze kahawa zake, korosho zake na pamba yake kwa bei nzuri na kuiweka fedha yake mfukoni? Jinsi wabunge wanavyopiga kelele kuiweka posho yao mfukoni ndivyo wananchi wanavyopiga kelele kuuza mazao yao kwa faida na kushuka kwa gharama ya bidhaa muhimu katika matumizi ya siku kwa siku kama vile mafuta ya taa, sukari, mchele na usafiri. Ndio maana nikasema hoja hii ya posho ni kipima joto. Ndio wakati wa kutambua wabunge wanaowawakilisha wananchi na wabunge wanaoyawakilisha matumbo yao. Na dawa yao ni moja tu! Ni kuwanyima kura kwenye uchaguzi mkuu wa 2015.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

 



0 comments:

Post a Comment