TULIJADILI SWALA LA USHOGA KWA MAWAZO MAPANA.

Tamasha la jinsia la mwaka 2009, swala la  ushoga na usagaji lilijitokeza, tulilijadili na kuliandika kwa mapana na marefu yake. Baadhi ya wachangiaji waliunga mkono hoja chanya zilizotolewa juu ya swala zima la ushoga na usagaji, baadhi walipinga na wengine walilaani na kutukana. Tamasha la jinsia la mwaka huu swala hili limejitokeza tena na zamu hii kelele, matusi, kulaani vimekuwa  vingi kiasi cha kuvuruga amani na imani za watu wengi.

Kuna sababu mbili kuu zilizovuruga hali ya hewa juu ya swala hili la Ushoga; si kwamba nia ni kuunga mkono ushoga bali uelewa wa kulishughulikia jambo lililopo (Ushoga ni ukweli ulio katika jamii yetu, tunataka tusitake) ulifungwa na sababu mbili nitakazozitaja:

Moja, ni kwamba mashoga wamedai haki zao za msingi ziingizwe kwenye katiba, kwa vile kuna baadhi ya watu wanaofikiri Katiba ni mali yao, wao ndio watanzania na wao tu ndio wana haki ya kuishi na kusikilizwa swala la mashoga liliwachefua na mbili ni kwamba walijitokeza baadhi ya waandishi wa habari ambao kwa sababu zao binafsi waliamua kupotosha agenda nzima ya Tamasha la jinsia kwa kuandika kwamba Ushoga ni agenda ya TNGP kwenye Tamasha la jinsia.

Mada kuu ya Tamasha la jinsia la 2011 ilikuwa ni Ardhi, Nguvu kazi na maisha endelevu katika muktadha mzima wa Jinsia, Demokrasia na Maendeleo. Katika kujadili mada hii mambo mengi yalijitokeza  kama vile Katiba, ukatili wa wafanyakazi wa majumbani, uporwaji wa ardhi, ukosefu wa ajira, uchumi kukua wakati umasikini unaongezeka kwa kasi ya kutisha na mengine mengi likiwemo na hili la ushoga.

Waandishi wa habari wenye mtizamo finyu na wenye malengo yao binafsi, waliyaacha mengine yote na kuliwekea mkazo hili la ushoga na kuendelea kupotosha kwamba hii ni kazi ya TGNP. Tamasha la jinsia linaandaliwa na Mtandao wa Mashirika ya watetezi wa Haki za Binadamu na Usawa wa Kijinsia (FemAct). Huu ni muungano wa mashirika zaidi ya 40 mengi kati yao yakifanya kazi kama asasi za kiraia ndani ya Tanzania. FemAct inajihusisha zaidi na ujenzi wa usawa katika mipango ya maendeleo na usawa kati ya wanaume na wanawake. Uwepo wa FemAct ni kutokana na imani ya ukombozi wa umma kutokana na aina yoyote ya unyonyaji, na ambamo haki za wanawake ni haki za binadamu, na upatikanaji wake unakwenda sambamba na upatikanaji haki kwa makundi mengine ya -kijamii.

Hivyo kutaja kwamba Tamasha liliandaliwa na TGNP peke yao ni upotoshaji na kwamba agenda ya ushoga ni ya TGNP ni upotoshaji pia. Tamasha la Jinsia linaandaliwa na FemAct na ni jukwaa la wazi kwa watu wote na hasa watu wa pembezoni ambao sauti zao hazisikiki kabisa. Hivyo mashoga nao kama watu ambao sauti zao hazisikiki, walipata nafasi kwenye jukwaa la jinsia.

Hoja si kuunga mkono ushoga au kuukubali na kuubariki. Hoja iliyo mbele yetu ni kwamba ushoga upo na unashika kasi. Ushuhuda kutoka kwa mashoga wenyewe ni kwamba wateja wao ni mawaziri na wabunge. Ukisikiliza maelezo yao ni kwamba kwa namna moja ama nyingine kila mmoja wetu kwenye jamii yetu anashiriki. Hivyo dawa si kulaani au kuwatukana mashoga na jukwaa lililowapatia nafasi ya sauti zao kusikika. Tujiulize kama jamii ni kwa nini kuna mmomonyoko wa maadili na kwa wale wanaozifuata dini za kigeni, tujiulize ni kwa nini hatuzingatii tena Amri za mwenyezi Mungu?

Ukisoma kwenye kumbukumbu za wamisionari wa kwanza walioeneza Ukristu barani Afrika, wanaungama wazi kwamba Waafrika waliziishi na kuzishika Amri kumi za  Mungu, hata kabla ya kuletewa imani za kigeni: Walimpenda na kumwabudu Mungu, kiasi kila familia ilikuwa na madhabahu ndani ya nyumba. Mungu, alikuwa karibu, waliongea naye, walikula naye na kulala naye kwenye nyumba zao. Mungu wao aliyaongoza maisha ya kila siku, alikuwa Mungu wa mvua, Mungu wa jua, Mungu wa ziwa na bahari, Mungu wa uzima, Mungu wa mavuno, Mungu wa misitu na uwindaji nk. Kila ukoo uliunganishwa na Mungu, chini ya madhabahu ya ukoo na kila kijiji kiliunganishwa na Mungu, chini ya madhabahu ya kijiji. Watoto waliwaheshimu wazazi wao, walipokea ushauri wao na kuchota hekima kutoka kwenye hazina ya wazazi wao. Uhalifu haukuwepo, hata kama uhalifu ungetokea kwa bahati mbaya, familia, ukoo au kijiji, ingemwajibisha mhalifu na kumrekebisha. Nyumba hazikuwa na milango wala mlizi na wala wizi haukutokea. Ndoa zilizokuwa nyingi zilikuwa za mme mmoja wanawake wengi, lakini wanaume walikuwa waaminifu kwa wake zao, watoto wote walitunzwa sawa. Hakukuwepo kitu kama watoto wa mitaani au nyumba za watoto yatima, kila mtoto alitunzwa kwenye familia: “Kitanda hakizai haramu”! Tendo la ndoa kabla ya ndoa lilikuwa mwiko, hivyo haikuwa kawaida msichana kubeba mimba kabla ya ndoa. Umalaya ,uchangudoa, ushoga na usagaji ni misamiati ambayo haikujulikana kabisa.

Ingawa Ukristu unahimiza ndoa ya mme mmoja mke mmoja. Uzinzi umeshamiri katika nyakati hizi tulizomo. Unafiki katika ndoa umeongezeka, walio wengi katika ndoa za Kikristu wanamtunza mke mmoja kwenye nyumba ya ndoa, lakini wanakuwa na nyumba ndogo kibao. Wengine wanashindwa kabisa kuwatunza watoto wa nje ya ndoa kwa kuliogopa kanisa. Hivyo ndoa nyingi za Kikristu zinachangia kuzalisha watoto wengi wa mitaani na  yatima ambao baba zao wanaishi kwa furaha na amani katika ndoa zao na kupokea sakramenti ya Ekaristi takatifu kila Jumapili na kutoka sadaka kubwa kubwa makanisani!

Mbali na unafiki, uzinzi, kutowajibika na ukosefu wa uaminifu katika ndoa za Kikristu, tumeshuhudia pia mambo kama ushoga na usagaji ambayo hayakujulikana katika jamii za Kiafrika. Umalaya na uchangudoa ni vitu vigeni katika jamii zetu. Imezuka na tabia ya wazazi kutembea na mabinti zao, wengine kwa siri na kwa makubaliano, na walio wengi ni kwa kuwabaka. Pia imezuka tabia ya ubakaji kwa jinsia zote mbili, mara nyingi wanaotendewa vitendo hivi ni watoto wadogo walio chini ya umri wa miaka kumi! Hili ni jambo ambalo lisingetokea kwenye jamii za Kiafrika kabla ya ujio wa dini za kigeni.

Mtu anaweza kujiuliza ni kwa nini jamii za Waafrika ziliishi na kuzishika Amri Kumi za Mungu kabla ya Ukristu na kushindwa kuziishi na kuzishika baada ya kuhubiriwa “Neno” la Mungu?
Hapa kuna mambo matatu ya kuchambua:

-         Wamisionari walikazania kubatiza na kumwingiza kwenye imani mtu mmoja mmoja. Walifikiri kila mtu alikuwa huru na kuishi kwa kujitegemea. Hawakuugundua ushawishi wa jamii nzima kwa mtu mmoja mmoja na jinsi jamii za Kiafrika zilivyokuwa zimesukwa kwa mshikamano. Walitakiwa kuibatiza jamii nzima, badala ya kumbatiza mtu mmoja mmoja. Bahati mbaya hawakuwa na mfumo huu na hadi leo hii kanisa halijafanikiwa kuubuni! Bado kanisa linakazania imani ya mtu mmoja mmoja: “Okwo omuntu achuma omwoyogwe aba nikwo abintungwa” ( Jinsi mtu anavyoishughulikia roho yake ndivyo anavyopata neema). Mfumo huu hauwezi kusaidia watu kuzishika Amri za Mungu. Ni mfumo wa kuendekeza ubinafsi na ubinafsi ni sumu ya Amri za Mungu!
-         Wamissionari waliamini kwamba masakramenti yangefanya miujiza ya kuwabadilisha watu. Haikuingia akilini mwao kwamba, utamaduni, mila na desturi na hali mbaya ya uchumi vingekwamisha nguvu za sakramenti. Badala ya  kuubatiza utamaduni na kuuboresha, wenyewe walikazana kuufuta! Mfano matendo mabaya(dhambi) katika jamii za Kiafrika yalishughulikiwa na jamii nzima. Ilikuwa ni haki ya kila mwanajamii kufahamu ni mtu gani ametenda mambo mabaya. Kila mtu aliruhusiwa kumsuta na kumsaidia kujirekebisha yule aliyetenda dhambi. Hivyo watu waliogopa kutenda dhambi ili wasiwekwe hadharani. Wamisionari walileta mfumo mpya, dhambi ikawa jukumu la mtu binafsi, yeye na Mungu wake kupitia kwa padri. Mtu anatenda makosa katika jamii, anakimbia kimya kimya kuungama kwa padri na kuondolewa bila ya jamii kushirikishwa. Mfumo huu uliongeza kasi ya kuzivunja Amri Kumi za Mungu. Hakuna aliyekuwa anaona aibu ya kutenda dhambi, maana akitenda dhambi hawekwi  hadharani, hakuna wa kumsuta – bali ana mchawi wake wa kumwondolea na kumwombea msamaha kwa Mwenyezi Mungu. Kwa vile anatenda dhambi sirini na kutubu sirini, anaweza kuendelea kutenda dhambi na kuleta madhara makubwa katika jamii. Ni wazi kabisa kwamba wale wanaotembea na mashoga, wanaungama na kuondolewa: Hawatukanwi wala kulaaniwa! Dhambi inabaki kwa mashoga, hawa ndio wanatukanwa na kulaaniwa!
-         Wamissionari walieneza neno la  Mungu, kwa kumfuasa Kristu. Kwa vile Kristu alifundisha na kuwatibu watu, basi nao walijenga mashule na mahospitali. Matokeo ya shule hizi za wamisionari hayakuwa mazuri kama walivyoyategemea. Karibu viongozi wote wa Afrika Huru walipitia katika shule za wamisionari. Mfano Mobutu, aliyepora nchi yake mali nyingi na kuwaacha watu wengi katika umasikini unaonuka, aliyechinja ndugu zake bila huruma na kusababisha vita ya DRC isiyoisha, alisomea kwenye shule za wamisionari. Nchi kama Burundi, ambayo imetawaliwa na ukabila na mauaji ya kutisha, viongozi wake wote wamelelewa katika shule za wamisionari. Kwa sababu ya uwezo mdogo wa kiuchumi, si watu wengi waliopata nafasi ya kuingia kwenye shule zilizoanzishwa na wamisionari, hivyo shule badala ya kujenga jamii moja, zilizalisha matabaka. Tabaka la wasomi walioishi maisha kama ya wamisionari na wakoloni na tabaka la watu wa kawaida ambao hawakuenda shule. Baada ya huru, tabaka hizi zilienda hadi leo hii. Tabaka hizi zinachangia kuvuruga amani katika nchi nyingi za Kiafrika. Hivyo shule za wamisionari hazikusaidia kumjenga mtu anayezishika na kuziishi Amri kumi za Mungu! Kwanini basi shule hizi zilishindwa hivyo, ni makala nyingine
-         Kwa vile wamisionari hawakuubatiza uchumi, mahospitali waliyoyaanzisha, leo hii yanawahudumia watu wenye kipato. Ni jambo muhimu kuwa na hospitali na ni jambo jema kuzishughulikia afya za watu, lakini wamisionari waliwalenga watu wa kipato cha chini na walilenga katika kutoa huduma. Hali halisi na uchumi wa dunia ya leo ulivyo jambo hili haliwezekani. Tujuavyo Waafrika walio wengi wana kipato cha chini, hivyo hawawezi kupata huduma katika hospitali hizi. Hivyo hayana uwezo wa kuponya na kufanya miujiza kama ya Yesu.

Hoja ninayoijenga kwenye makala hii ni kwamba badala ya kuwalaani na kuwatukana mashoga na majukwaa yanayowapatia nafasi ya sauti zao kusikika, tujadili jinsi ya kuunda mifumo ya kuboresha maadili yetu kama taifa na kutanzua matatizo mengine mengi katika taifa letu. Tuna tatizo la katiba, tume huru ya uchaguzi, uchumi mbovu, uporaji wa ardhi, huduma mbovu za -kijamii, uongozi mbovu, elimu duni, unyanyasaji wa kijinsia na sauti za walio pembezoni kutosikika kwenye vyombo vya maamuzi. Hivyo tusilijadili swala la ushoga peke yake, tulijadili ndani ya mawazo mapana maana lina mambo mengine mengi yanalolizunguka.

Na,
Padri Privatus Karugendo.


0 comments:

Post a Comment