TULIYATABIRI NA SASA YAMETIMIA: KANALI FABIAN MASAWE NI MKUU WA MKOA WA KAGERA.

Baada ya uchaguzi mkuu wa 2010, niliandika makala juu ya vurugu zilizotokea Karagwe na hatimaye Tume ya Uchaguzi kumtangaza mbunge wa CCM mshindi kinyume kabisa na matarajio ya wapiga kura wa Jimbo la Karagwe. Kwa faida ya wale ambao pengine hawakupata kuisoma makala hiyo, na kwa vile yale niliyoyatabiri ya Mkuu wa Wilaya kuzawadia Ukuu wa mkoa  kwa kuhakikisha majimbo yote ya Wilaya ya Karagwe, yanabaki CCM yametokea, narudia sehemu ya makala hiyo:

“Naandika makala hii kama wito kwa wapenda amani, demokrasia,  na watu wenye busara na hekima kushirikiana  pamoja kulaani kitendo kilichotokea kule Karagwe cha jeshi la polisi kuwapiga mabomu na risasi za moto wananchi waliokusanyika kwenye ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Karagwe, kusubiri majibu ya kura za mbunge wao. Watu waliumizwa, walitishwa na wengine wamelazwa hospitali. Mbaya zaidi matokeo ya uchaguzi mkuu yalitangazwa chini ya ulinzi mkali wa polisi. Haiwezekani mwakilishi wa wananchi kutangazwa chini ya ulinzi mkali wa polisi. Hili ni jambo la kulaani na kuonya kwamba hili halivumiliki. Viongozi wa dini wasikae kimya, wajitokeza na kulaani wazi wazi, jinsi tulivyoshuhudia wakijitokeza kukemea udini katika uchaguzi Mkuu, ndivyo hivyo hivyo wajitokeze na kukemea serikali kutumia vyombo vya dola kupora haki ya wananchi ya kujichagulia mwakilishi wampendaye.

“Watu wamepigwa mabomu na risasi za moto na wengine hadi leo hii wako hospitali. Serikali imetumia jeshi la polisi kushinikiza Tume ya Uchaguzi katika Jimbo la Karagwe, kumtangaza mshindi wa CCM Bwana Gosbert Blandes. Wananchi, waliopiga kura walikusanyika kwenye ofisi ya Mkurugenzi wa wilaya ya Karagwe, baada ya kuitwa kusikiliza matokeo. Na kufuatana na watu walivyopiga kura, walikuwa na imani ya kutangazwa mgombea wa upinzani. Kwa kuogopa hilo Serikali iliagiza jeshi la polisi kutoka mkoani Bukoba , kuja Kayanga, kuwatisha na kuwatawanya wananchi waliokuwa wakisubiri matokeo. Na mbaya zaidi ni kwamba baada ya kuwatawanya wananchi hao, jeshi la polisi lilivuka mipaka na kuingia sokoni Kayanga na kuwapiga mabomu ya machozi watu waliokuwa sokoni wakijifanyia shughuli zao. Ni unyama kama tunaoushuhudia kwenye nchi zinazotawaliwa kidikteta.

“Habari tulizozipata kutoka Karagwe, ni kwamba baada ya kuwatawanya watu, kesho yake jeshi la polisi lilizingira Ofisi ya Mkurugenzi na matokeo ya uchaguzi kutangazwa chini ya ulinzi mkali. Baada ya matokeo mshindi aliyetangazwa Bwana Gosbert Blandes, alisindikizwa kwa ulinzi mkali kupanda ndege kuondoka Karagwe, na baada ya siku moja, alionekana Karagwe, akisindikizwa na polisi kuelekea kijijini kwao. Kwa nini mwakilishi wa wananchi, asindikizwe kwa ulinzi wa polisi?

“Kuingilia uhuru wa watu kumchangua mwakilishi wanayempenda ni kitu kisichovumilika. Kama wanavyosema watu wa Karagwe, kuingilia uhuru wa uchaguzi wao ni sawa na kuibaka demokrasia. Wananchi hawa  wameporwa haki yao na jambo hili ni la kupigia kelele. Ni jambo la kulaani. Watu wa Karagwe wana matatizo chungu mbovu hivyo wanahitaji mwakilishi wa kuweza kuyatambua matatizo yao na kuyawasilisha Bungeni. Karagwe kuna matatizo ya barabara na hasa kipindi cha mvua, kuna matatizo ya kutokuwa na dawa kwenye vituo vya afya, kuna shida ya kutokuwa na walimu kwenye sekondari za kata, kuna tatizo la bei ya Kahawa kuendelea kushuka, kuna tatizo la maji kiasi kwamba watu wanasafiri zaidi ya kilomita kumi kutafuta maji, kuna tatizo la kusambaza umeme vijijini, kuna tatizo la nyumba za walimu wa shule za msingi na sekondari, kuna tatizo la ujenzi wa nyumba bora na za kisasa, Wabunge waliotangulia walishindwa kuwasaidia watu kupunguza matatizo hayo. Hata mbunge huyu aliyetangazwa kwa mtutu wa bunduki, kwa kipindi alichokaa  Bunge, ameshindwa kuyawasilisha matatizo ya Karagwe. Alisikika Bungeni, wakati Tembo walipoivamia Karagwe. Vinginevyo akiwa Bungeni anajielekeza kwenye matatizo ya Jimbo la Ubungo maana yeye na familia yake wanaishi Ubungo. Watoto wake hawasomi kwenye sekondari za kata na mke wake hafahamu matatizo  ya maji wanayoyapata wanawake wenzake wa kule Karagwe.

Kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita Bwana Gosbert Blandes, hakuonyesha kuguswa na matatizo ya Karagwe. Hata kwenye kura  za maoni ndani ya chama cha CCM ilijionyesha wazi kwamba wanachama wenzake hawakuridhishwa na utendaji wake, alifanikiwa kupita kwa mbinu na kutumia fedha kuwahonga wapiga kura. Kuna ushahidi wa kuaminika kwamba hata uchaguzi mkuu wana CCM walio wengi hawakumpigia kura Bwana Blandes, walifuata wito wa “Usichague chama, mchague mtu” kwa vile watu wa Karagwe wana hamu ya maendeleo baada ya kuachwa nyuma kwa miaka mingi, walikuwa na hamu ya kumchagua mbunge wa kusukuma mbele maendeleo ya Jimbo lao bila kuangalia anatoka chama gani.

“Uchaguzi umekwisha na tutaanza kusikia majigambo ya CCM kwamba wameshinda kwa kishindo. Majivuno haya yana msingi gani wakati majimbo mengine kama Karagwe, ushindi umelazimishwa kwa mtutu wa bunduki? Inawezekana hili limetokea maeneo mengi, maana kila jimbo lililochelewesha matokeo, mshindi ameibuka kuwa wa chama cha upinzani. Kama mwelekeo ni “ Hakuna aliyeshinda na aliyeshindwa” na ule unafiki wa “Ushindi ni wa watanzania wote” majigambo ya  ushindi wa kishindo yanatoka wapi? Mipango ya kujipanga upya ili kuyakomboa majimbo yaliyonyakuliwa na wapinzani yanatoka wapi? Kama si kugombania fito kwa nini tusijifunze sote kukubali kushindwa?

Kuna uzushi mwingine tunaousikia, au ni uvumi? Kwamba wakuu wa wilaya wamepewa ahadi ya kupandishwa kuwa wakuu wa mikoa kama watahakikisha majimbo katika wilaya zao  hayachukuliwi na wapinzani. Hivyo ni kazi yao kufanya wawezavyo ili CCM ipate ushindi hata kama kura zinasema vinginevyo. Hili likitokea kwa Karagwe, kwamba watu wameporwa haki yao ya kumchagua mwakilishi wanayempenda, wamepigwa mabomu na kuumizwa ili Mkuu wa wilaya apate Ukuu wa mkoa, laana hii itamwandama huyu mkuu wa Wilaya ya Karagwe hadi vizazi vijavyo”

Wakati nikiandika makala hiyo sote tulifikiria ni uzushi au uvumi tu, maana Rais wa nchi anayewapenda watu wake, hawezi kukubali kuzima uhuru wao wa kuchagua kwa kumpandisha mtu cheo. Kumbe haukuwa uzushi wala uvumi ni  ukweli ,maana sote tumeshuhudia aliyekuwa Mkuu wa wilaya wakati wa uchaguzi Mkuu wa 2010, Kanali Fabian Masawe, ameteuliwa kuwa mkuu wa mkoa, na kama matusi vile kwa watu wa Karagwe, ameteuliwa kuwa mkuu wa Mkowa wa Kagera, ili ahakikishe hakuna upinzani mkoa wa Kagera.

Hapana shaka kwamba watu wa Karagwe, watakuwa wameliona hili; Kanali Masawe, amewatumia kupanda cheo. Aliuzika uhuru wao wa kujichagulia mtu wanayemtaka, ili yeye afufuke akiwa na cheo kikubwa na labda baada ya kuhakikisha ameua kabisa upinzani Mkoani Kagera, apande zaidi ya hapo? Ni wakati wa watu wa Karagwe kusema hapana!: Wasimame pamoja na kusema: Tumeonewa kiasi cha kutosha, tumeibiwa kura zetu kiasi cha kutosha, tumeporwa ushindi wetu kiasi cha kutosha, sasa tunataka mapinduzi!

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment