TUTAANDAMANA KULINDA HISTORIA YA TAIFA LETU.
 
Waziri Kombani anawashangaa wale wanaotaka kuandamana kupinga Serikali kuuza  jengo la Mahakama  ya Rufani. Kwa maoni yake, nina wasi wasi kusema ni maoni ya Serikali, maana serikali isiyolinda na kutetea historia ya taifa lake haifai kabisa kuwa madarakani, ni kwamba jengo hilo halina hadhi ya kutumiwa na majaji wetu, hivyo liuzwe na serikali ijengewe jengo jingine lenye hadhi ya majaji wetu.
 
Hoja inayochefua zaidi na kutilia mashaka uzalendo na uwezo wa kufikiri wa Waziri Kombani, ni pale alipolieleza Bunge kwamba Serikali imempata mbia ambaye yuko tayari kulinunua jengo hilo na “Kutujengea jengo jingine la mahakama ya rufani”. Alisema hivi: “Jamani pale wanapokaa majaji wetu ni aibu tupu, hapafai ndiyo maana hivi sasa tunafanya mazungumzo na mbia, ili ajenge jengo la kisasa kwa makubaliano ya kumuachia pale”.
 
Kwa nini serikali yetu itegemee mahitaji ya wabia na wawekezaji? Ina maana akijitokeza mbia anayetaka kutujengea Ikulu ya Kisasa, tukubali kuuza majengo ya kihistoria ya Ikulu yetu ya sasa? Akijitokeza mwekezaji anayetaka kujenga mji wa kisasa Ubungo na Tabata ,tuwaamishe wananchi wote wa maeneo hayo ili kumpisha mwekezaji? Akijitokeza mwekezaji anayetaka kukausha sehemu ya Bahari ili kujenga mji wa kisasa tukubali wazo hilo kwa sababu atakuwa anatusaidia kujenga majengo ya kisasa? Ujinga gani huu wa kuiishi kwa kutegemea matakwa ya wengine? Na mbaya zaidi kumtegemea mtu anayekuja kutengeneza faida? Kwa nini serikali kama inaona jengo la Mahakama ya rufani halina hadhi ya majaji wetu, isijenge jengo jipya? Hatuna uwezo wa kujenga Mahakama ya rufani mpaka tupate mbia? Mbona tunajenga barabara wenyewe? Mbona tumejenga Chuo cha Dodoma wenyewe na bado serikali ina mpango wa kufanya mambo mengine mengi? Ni bora Waziri Kombani ,angetueleza kwamba Serikali ilipitiwa kutaka kuuza jengo hilo na sasa imesitisha mpango huo badala ya hizi porojo za kuingia ubia na mwekezaji na kwamba mbia huyu “Atatujengea Mahakama ya rufani ya kisasa”
 
Labda ni kutokuelewa au kuonyesha kwamba Mawaziri wetu hawako pamoja wa wananchi. Wale wanaotaka kuandamana lengo lao ni kutetea jengo la kihistoria kuuzwa na kubomolewa. Kwamba jengo hilo halina hadhi kwa Majaji wetu si hoja. Serikali ina uwezo wa kujenga jengo jipya lenye hadhi kama ilivyojenga majengo mengine mengi. Hoja ni kwamba jengo la kihistoria lisivunjwe. Hatuangalii kama jengo hilo ni shule, hoteli, hospitali au mahakama. Duniani kote watu wanalinda historia ya majengo yao, historia ya utamaduni wao na historia ya mambo mengine yote yanayotunzika. Hii ndiyo hoja na ndiyo maana watu wako tayari kuandamana ili kulinda na kutetea jengo hili la kihistoria.
 
Kumezuka wimbi la kuyabomoa majengo ya zamani na kujenga majengo mapya na kisasa na hasa kwenye jiji la Dar-es-Salaam. Sura ya Jiji la Dar-es-Salaam, inaanza kubadilika. Itakuwa vigumu kwa vizazi vijavyo kuwa na picha ya jinsi Dar-es-Salaam ilivyokuwa. Baadhi ya watu wanashangilia kwamba majengo haya mapya ni maendeleo, na wengine wanashangilia kwamba sasa jiji linapendeza. Inategemea uzuri unapimwa kwa vigezo gani; kama kutizama juu na kuyaona maghorofa badala ya kuliona anga, nyota na mwezi, ndio uzuri, basi wanaoyafurahi majengo hayo wana haki. Lakini ndugu zetu ambao wamekuwa na utamaduni wa kujenga majengo marefu kwa miaka mingi, wanasema uzuri wa Jiji ni kusimama ukatizama juu ukaona anga, nyota na mwezi na kufurahia maajabu ya uumbaji wa Mwenyezi Mungu. Sasa hivi ukiwa katikati ya Jiji la Dar-es-Salaam, anga, nyota na mwezi vinaanza kupotea! Kinachoonekana ni haya maghorofa yenye vioo!
 
Tukiliacha hili swala uzuri, kuna hoja nyingine ya hizi fedha zinazojenga majengo haya yanayofumuka ndani ya Jiji la Dar-es-Salaam zinatoka wapi? Je ni fedha za wabia? Na kama ni fedha za wabia kuna usalama? Hawa wanaojenga majengo makubwa kwa fedha nyingi hivyo si kesho na keshokutwa watataka kumiliki na ardhi yetu? Si watataka kututawala? Kama majengo haya yanajengwa kwa fedha yetu sisi wenyewe kama ambavyo ningetaka mimi mwenyewe kuamini, iweje bado tunalia kuwa kwenye umasikini? Iweje tunafikiri kujenga majengo makubwa hivyo kabla ya kuwa na uhakika wa mfumo wa kusambaza maji, kabla ya kuwa na barabara za uhakika kuingia na kutoka kwenye Jiji letu la Dar-es-Salaam? Lakini pia tunaweza vipi kufikiria kujenga majengo kwa gharama kubwa wakati watanzania wengi hawa nyumba bora na salama? Watanzania wengi hawana huduma ya maji, hawana shule nzuri, hawana hospitali na wengine hawana uwezo wa kupata milo miwili kwa siku?
 
Tukitaka kuwa na vitu vipya na vya kisasa kwa gharama ya kupoteza vile vya zamani, basi taifa letu halitakuwa na historia. Na taifa lisilokuwa na historia yake, basi hilo ni taifa mfu! Lakini pia tunaanza kujenga utamaduni wa hatari sana, huu wa kuendesha maisha yetu kwa kutegemea wawekezaji. Hawa jamaa wanakuja kwa lengo la kutafuta faida na wala si lengo la kutusaidia kujenga taifa letu.
 
Kwa nini mtu atujengee Mahakama ya Rufani? Kwa vile anatupenda sana? Kwa  vile ni ndugu yetu? Kwa vile ana uchungu na maendeleo yetu? Mbona bei ya mafuta inapanda, thamani ya dola inapaa, wakati shilingi yetu inazama na bei ya mazao yetu ya biashara inakwenda chini siku hadi nyingine? Wa kulijenga taifa hili ni sisi watanzania na wala si hao wawekezaji. Wa kulinda historia yetu ni sisi wenyewe na wala si wageni kutoka nje.
 
Majengo ya kizamani yamejengwa kwa ufundi wa aina yake, na ufundi huu haupatikani tena! Vifaa vingi vilivyojenga majengo ya zamani ni vifaa vya hapa hapa kwetu. Ujenzi wa sasa hivi unategemea sana vifaa kutoka nje ya nchi. Hivyo ujenzi wa sasa hivi ni biashara; hata na mbia huyo anayesema atatujengea Mahakama ya Rufani kwa makubaliano ya kubomoa jengo letu la kihistoria, analenga biashara zaidi ya msaada. Vifaa vya ujenzi vitaagizwa kutoka nje na kuvinufaisha viwanda vya nje na kujenga uchumi wa nchi zao. Hakuna mtu wa kutoa msaada katika dunia hii ya soko huria, utandawazi, ubepari na ubeberu. Kwa maana hiyo katika zama hizi za upole wa njiwa na ujanja wa nyoka, tunahitaji viongozi wenye kuona mbali si hawa wa aina ya Mama Kombani.
 
Hivyo ni bora Waziri Kombani na wengine wa aina yake kutambua kwamba Maandamano ya kupinga kubomolewa kwa Jengo la Hoteli ya Forodhani yako pale pale. Kukubali kubomolewa jengo hili ni mwanzo wa kukubali kubomoa kila kitu; tutabomoa mashule yetu ya zamani, tutabomoa mahospitali yetu, tutabomoa majengo ya kihistoria ya Mkemia mkuu, tutabomoa Ikulu yetu hadi tutabomoa na uhuru wetu! Tuna wajibu wa kuilinda historia yetu kwa gharama yoyote ile; historia yetu ni urithi wetu na tuna wajibu kwa kurithisha urithi huu kwa vizazi vijavyo.
 
Na,
Padri Privatus Karugendo

0 comments:

Post a Comment