UPORAJI WA ARDHI NA USALAMA WA CHAKULA


Kofi Annan, amelalamika kwamba mwaka 2010 peke yake, ardhi yenye ukubwa sawa na Ufaransa limeuza katika bara la Afrika. Na huu ni uuzaji uliofanyika ndani ya mwaka mmoja. Hali ilivyo ni kwamba uuzaji huu utaendelea. Ni wazi Kofi Annan, anatumia lugha ya kistaarabu kusema kwamba Ardhi imeuzwa, lakini maana yake ni kwamba ardhi hii inaporwa na viongozi wa Afrika na kuuzwa kwa wawekezaji wa nje ambao wanapewa hati mili ya miaka 99 au wananunua moja kwa moja.

Wakati ardhi ya Afrika unauuzwa na kuporwa tunaambiwa kwamba idadi kubwa ya binadamu wanaokabiliwa na uhaba wa chakula wanaishi katika nchi ambazo bado ni maskini .Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na Shirika la Chakula na Kilio la Umoja wa Mataifa –FAO, dunia hii na watu wapatao milioni 925 wenye njaa; kati yao asilimia 98 wanaishi katika nchi zinazoendelea na wengi wa hao ni familia za wakulima maskini wanaomiliki ardhi chakavu au maeneo ambayo huathiriwa na mafuriko au ukame wa mara kwa mara. Aidha, takwimu zinaonyesha kwamba mtu mmoja kati ya watano hamiliki ardhi anayoitumia.

Theluthi mbili la wahenga wa njaa huishi sehemu za vijijini, hasa barani Asia na Afrika. Idadi kubwa ya watu hawa hutegemea kilimo, hawana vyanzo vingine vya kujipatia riziki na ustawi wao. Kwa sababu hii maisha yao ni tete, hawana uhakika. Wengi wao wanahamia mjini kwa lengo la kusaka ajira, hivyo miji inafurika watu maskini na makazi yaliyojengwa kiholela.

Kwa maana nyingine ni kwamba umiliki wa ardhi ni muhimu katika kuhakikisha usalama wa chakula. Na si ardhi tu, bali ardhi nzuri na yenye rutuba. Tumesikia kwamba asilimia kubwa ya watu maskini wanamiliki ardhi chakavu. Ardhi yenye rutuba wanauziwa wawekezaji ambao wanaitumia kufuatana na mahitaji yao.


Chalinze, Bagamoyo, Ruvu Basin, Rukwa na Zanzibar, Waarabu watakuja kulima mpunga kwa kushirikiana na JKT. Na hapa “Kushirikiana” ni lugha ya kistaarabu, katika hali halisi ni uporaji ule ule, maana mikataba kama hii inakuwa ni siri kama ilivyo mikataba ya madini na uwekezaji mwingine. Wakulima wetu ambao wengi wao hawana hati miliki ya ardhi yao, watatolewa kwenye mashamba ili kuupisha mradi mpya wa kilimo cha Waarabu. Ni uporaji ule ule wa ardhi unaoendelea katika taifa letu.

Tumesikia yanayotokea kule Manyara, wananchi wakipambana na wawekezaji kugombania ardhi, tunayasikia pia ya Kilombero na kule Kagera, Misenyi, wakubwa walitaka kuwafukuza wananchi kwenye ardhi yao ili wao watengeneza maeneo ya ufugaji. Uporaji wa ardhi unaendelea sehemu zote; vijijini na mijini. Bila kufuata sheria na kuwa na viongozi walio makini na wazalendo, kuna hatari ardhi kumilikiwa na watu wa chache au kujikuta tunatumbukia ndani ya ukoloni wa kujitafutia wenyewe.


Juzi, ITV, walionyesha kipindi maalumu cha sakata la Nyamongo. Hadithi ni ile ile, ardhi imeporwa na wawekezaji wa mgodi wa dhahabu. Wananchi wanabaki kuwa watumwa ndani ya nchi yao. Hawana ardhi ya kulima chakula na hawana ardhi ya kuchimba madini. Watu hawa wameishi miaka yote wakichimba madini na kuuza ili kupata kipato cha kuendesha maisha yao. Sasa “Uwekezaji” huu unaofanywa katika mfumo wa uporaji, umewalazimisha wananchi wa Nyamogo, kuishi katika hali ya umasikini na utumwa. Tumeshuhudia jinsi Jeshi la Polisi, lilivyo simama kidete kuwalinda wawekezaji wa Nyamongo na kuwaua wananchi wa Tanzania.

Hoja ninayojaribu kuijenga kwenye makala hii ni kwamba tunaendelea kuuza ardhi wakati tukishuhudia tishio kubwa la uhaba wa chakula. Wanaoinunua ardhi yetu wanaweza kuamua kuifanyia chochote wanachotaka; wanaweza kulima mazao ya kuzalisha mafuta badala ya mazao ya chakula; wanaweza kuamua kuitumia ardhi hiyo kufugia wanyama na kuwafukuza wananchi wote wanaoishi maeneo hayo.

Mwaka 2008, tulishuhudia uhaba wa chakula ulioikumba dunia yote. Na uhaba huu wa chakula utaendelea, maana kuna mabadiliko ya tabia nchi, lakini pia na uhaba wa ardhi utachangia kiasi kikubwa tatizo hili. Ndio maana inashangaza kuona pamoja na tishio lililo mbele yetu bado  tunakubali kuiuza ardhi yetu kwa wageni.

Tangu tupate Uhuru, taifa letu limeshindwa kufaidika na fursa zilizopo katika sekta ya kilimo. Tulikuwa usingizini kwa muda mrefu hadi mwaka 2007/08 tulipozinduka kutokana na kimbunga cha uhaba wa chakula duniani kote. Tumeibuka na wimbo wa Kilimo Kwanza; wimbo ambao unatuelekeza kwenye kilimo cha mashamba makubwa – mashamba ya wawekezaji wa nje badala ya kuwaendeleza wakulima wadogo wadogo ambao wamekuwa uti wa mgongo wa kilimo kwa miaka yote.

Hapa Tanzania sehemu kubwa ya chakula tunachokula huzalishwa na wakulima wadogo ambao wastani wa mashamba yao ni kati nusu hekta na hekta tatu. Wanawake ndio wazalishaji wakuu wa mazao ya chakula na ya kuuza. Na kuna ukweli usiopingika kwamba akina mama ndio wazalishaji wakuu wa mazao ya chakula katika nchi zinazoendelea. Hata hivyo, mila, desturi na mifumo ya -kijamii haiwatendei haki. Kwani wanawake ndio wanaoathiriwa zaidi na njaa na umaskini kuliko wanaume. Mwanamke mjamzito asiyepata chakula anachostahili, hupungukiwa damu na kudhoofika. Matokeo yake I kuzaa mtoto mwenye uzito mdogo sana na ukuaji wa mashaka.

Mahitaji ya wanawake wakulima ni mengi, yakiwemo fursa ya kuchangia mawazo wakati wa kupanga nini kifanyike na jinsi gani kifanyike, umiliki wa rasilimali hasa ardhi, ushiriki wao katika kutunga sera na kufanya maamuzi yanayohusu utendaji kazi. Katika masuala haya, mara nyingi wanawake hupewa fursa ndogo ya kuhusishwa, au hawahusishwi kabisa. Na wimbi hili jipya la uporaji wa ardhi linafanyika bila kuwahusisha wanawake. Kesho na kesho ukitokea uhaba wa ardhi kutokana na uporaji huu, mwanamke ndiye wa kwanza kuteseka maana  kwa kiasi kikubwa hadi leo hii ndiye msingi wa usalama wa chakula katika ngazi ya kaya. Hakuna usalama wa chakula bila kumiliki ardhi!

Hivyo kilimo kwanza kingelenga kuendeleza wakulima wadogo wadogo na hasa akina mama wanaohangaika usiku kucha kuhakikisha kuna usalama wa chakula katika ngazi ya kaya. Wakulima wakubwa hawa wanaokuja kwa mgongo wa uwekezaji hawawezi kutuhakikishia usalama wa chakula katika ngazi ya kaya. Watakuja kuchimba madini, watakuja kulima miti ya mbao, watakuja kulima mazao ya kuzalisha mafuta na watakuja kutengeneza mbuga za kitalii. Usalama wa chakula katika ngazi ya kaya unabaki mikononi mwa wakulima wadogo. Hivyo ni jukumu la serikali yetu kuhakikisha wakulima wadogo wanaendelezwa na kulindwa na hii ni pamoja na kukomesha wimbi hili la uporaji wa ardhi.

Na
Padri Privatus Karugendo.

 



0 comments:

Post a Comment