MWANA MAMA, MA CLEMENTINA RUTABANZIBWA.

Leo katika safu yetu ya Mwana Mama, nawaletea Marehemu mama yetu Mpendwa Ma Clementina Rutabanzibwa na kuwatangazia wasomaji wangu maslahi binafsi kwamba huyu ni Mama yangu Mkubwa. Si kwa upendeleo bali mama huyu ni miongoni mwa mama wengi wanaolitumikia taifa letu, kwa uadilifu, uzalendo na uaminifu mkubwa lakini hawasikiki! Hatujajenga utamaduni wa kuandika historia ya watu wanaotoa mchango mkubwa wa maendeleo katika taifa letu na hasa wanawake. Makala hizi za Mwana Mama zinalenga kuujenga utamaduni huu. Hivyo hata kama Mama huyu asingekuwa jamaa yangu, ningeshika kalamu na kuandika juu yake.
 Ua letu limepukutika! Mama yetu Mkubwa Omugonzibwa Ma Clementina Rutabanzibwa, aliaga dunia tarehe 23.3.2013 na tulimzika kwa heshima zote za kidini, kiserikali, kiutamaduni, kijamii na mshikamano siku Jumamosi tarehe 30.3.2013 kijiji cha Ibura Bukoba. Ni machozi  ya furaha kwamba mama yetu amepumzika akiwa na umri wa miaka 85, baada ya kuugua kwa kipindi cha miaka 7, lakini pia ni machozi ya uchungu maana hatuwezi kuzungumza naye, hatuwezi kucheka naye na hatuwezi kucheza naye tena hasa zile ngoma za Waganda, ambazo alipokuwa akifurahi alizicheza kwa ustadi mkubwa. Ni mama ambaye hakuwa na makubwa na aliwapenda watu wote bila kutegemea chochote kutoka kwao, alikuwa mvumilivu na mcha Mungu! Mama yetu ni ua ambalo tulipenda liendelee kuchanua na kuzipamba familia zetu na jamii nzima. Lakini sasa ua letu la upendo, amani na mshikamano, limepukutika! Ni wajibu wetu sisi tuliobaki nyuma kuchanua na kupendeza! Huo ndio ujumbe wa maisha ya Marehemu Mama yetu  Ma Clementina. Upumzike kwa Amani mama yetu mpendwa.
Wakati wa ibada ya mazishi  ya Mama Clementinaya, Askofu Msaidizi Methodius Kilaini, alizitaja sifa nyingi za mama yetu; kwamba mama huyu mbali ya kuwa mchamungu na kuwalea watoto wake kwa msingi wa imani na maadili bora, alikuwa mama mwenye upendo kwa watu wote na ni miongoni mwa watu ambao walikuwa wakijitolea kutoa chakula bure kwa mapadre wa Jimbo katoliki la Bukoba. Alikuwa ni mama mwenye moyo wa kusaidia watu anaowafahamu na asiowafahamu. Ushuhuda huu wa Askofu Kilaini, uliungwa mkono na watu wote waliotoa salaam za rambirambi kutoka viongozi wa serikali na vyama vya siasa. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Makazi Profesa Anna Tibaijuka, naye alitaja maslahi binafsi kwamba huyu alikuwa kama mama yake mzazi pia aliziunga mkono  sifa alizozitoa Askofu Kilaini, alimtaja Mama Clementina, kama mfano wa kuigwa, kwamba ni mmoja kati ya wanawake wachache wa  taifa letu waliotoa mchango mkubwa lakini hawasikiki.
Marehemu Ma Clementina Tunu Mundigo ( au, kwa waliokuwa karibu naye alijulikana kama Ma Keleme) alizaliwa akiwa mtoto wa kwanza wa Mzee Clemence Mundigo na Ma Shelestina Mpabuka, tarehe 15 Desemba 1927 , huko Kagondo – Karugulu, Bukoba Vijijini. Alisoma shule ya msingi Bukoba na baadaye baba yake, ambaye alipenda na kuithamini elimu, alimpeleka mama yetu shule za Bwanda na baadaye Nabingo zote za huko Uganda. Ni wakati ambapo watoto wa kike walikuwa wanaachwa nyuma kielimu na kutoa upendeleo kwa wavulana, lakini baba yake na Ma Clementina, alikuwa wa pekee, alimsomesha binti yake hadi elimu ya juu. Kwa maneno mengine, Mama yetu alikuwa msomi ambaye hakujitukuza kama ilivyo jadi ya ndugu zake akina “Nshomile”. Alipoongea kingereza, ndipo mtu angeanza kuhisi kiwango chake cha elimu, vinginevyo baada ya mme wake kustaafu na kuishi kijijini hakuwa na tofauti  na wanawake wote wa vijijini.
Mnamo tarehe 21 Aprili 1948 Ma Keleme, alifunga ndoa takatifu na Omulangira Gosbert Marcel Rutabanzibwa ( sasa naye ni hayati) katika parokia  ya Rubya, Bukoba. Katika ndoa yao ya miaka 49 waliyoishi pamoja, walibarikiwa kupata watoto tisa, wa kike watano: Sr.Clementia, Hilda, Jean, Lucy na Adeline, na walipata watoto wa kiume wanne: Patrick, John-Bosco,Anthony na Victor. John-Bosco na Victor walikwishatangulia mbele ya haki. Ma Clementina, amejaliwa kuwa na wakwe, wajukuu na kitukuu.
Mme wa  mama yetu, Omulangira Gosbert Rutabanzibwa, ni miongoni mwa wasomi wa kwanza wa taifa hili. Ukienda Uhamiaji faili la kwanza na Pasi ya kusafiria nje ni la Mwalimu Nyerere, la pili ni la Mzee Kawawa na la tatu ni la Mzee Gosbert Rutabanzibwa. Alisoma na Marehemu baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, kule Makerere Uganda. Baada ya Uhuru, Omulangira Gosbert Rutabanzibwa, alilitumikia taifa letu kwa Nyanja mbali mbali. Alikuwa balozi wetu New Dehli (India), Ottawa (Canada) na Washington,DC (Marekani). Huko kote aliambatana na Mama yetu Ma Clementina. Kuna ushuhuda kwamba Mama yetu, aliwajali na kuwahudumia vizuri watanzania waliokuwa kwenye nchi hizi ambazo mme wake alikuwa balozi.
Pia kuna ushuhuda mwingine kwamba Ma Clementina, alijenga uhusiano katika nchi hizo za kigeni na kuendeleza utamaduni wa ukarimu wa Mtanzania. Kuna mwandishi wa vitabu wa Amerika, anayemtaja Ma Clementina kwenye kitabu chake kwa kushangazwa na kitendo cha mama huyu kumsindikiza kutoka kwenye nyumba ya Balozi wa Tanzania, hadi kwenye gari wakati wa kipindi kikali cha baridi. Ma Clementina, alimshangaza mzungu huyo kwa jibu lake: “ Utamaduni wetu sisi tunamsindikiza mtu akija kututembelea, kwa vile wewe una gari, ni lazima nikusindikize hadi kwenye gari lako..!”
Hizi ni baadhi ya sifa za Mama yetu, lakini kuna sifa nyingine nyingi. Mme wake alikuwa Balozi na kuiwakilisha serikali ya Tanzania, nchi za nje; sifa alizozipata Balozi Rutabanzibwa, zilikuwa na msingi mkubwa – nyuma ya sifa hizo ni Ma Clementina. Mama huyu aliwajibika katika kujenga na kulea familia yake katika misingi ya Kikristo na kizalendo miaka yote ya uhai wake. Kwa wengi waliomfahamu, alikuwa mama aliyejinyima mengi maishani ili familia yake, mme wake na  watoto wafike mbali kiroho na kimaisha. Kutokana na jitihada hizo, Balozi Rutabanzibwa, anatajwa kuwa miongoni mwa watu waliolitumikia taifa letu kwa uadilifu mkubwa. Watoto wa Ma Clementina wanaofanya kazi hapa Tanzania, wanatajwa kuwa ni miongoni mwa watanzania wachache wenye kulitumikia taifa hili kwa uzalendo uliotukuka. Hivyo mama huyu alikuwa na sifa ya kuitunza familia yake vizuri kwa kuiandaa kulitumikia taifa letu la Tanzania. Kifo chake si pigo tu kwa familia, ndugu na jamaa, bali ni kwa watanzania wote.
Mama yetu ni mfano bora wa msemo wa “ Mama ni moyo wa familia na mama ni mzazi wa taifa”. Mama yetu ametoa mchango mkubwa kwa  taifa letu kwa kuilea kwa maadili bora familia yake kiasi cha kutoa watu bora wa kulitumikia taifa letu kwa uzalendo mkubwa.
Tunamlilia mama yetu, tunamkumbuka na kumwombea ili Mwenyezi Mungu ampumzishe mahali pema peponi.
Na,
Padri Privatus Karugendo.
+255 754 633122
www. Karugendo.net


0 comments:

Post a Comment