MWANA MAMA PENINA MHANDO.

Leo katika safu ya Mwana mama, tunawaletea Penina Mhando ambaye anajulikana pia kama Penina Mlama. Huyu ni mwandishi wa NGUZO MAMA na nguli wa sanaa za maonyesho ambaye pia ni mwandishi mahiri wa tamthiliya za Kiswahili. Huyu ndiye mtunzi wa Hatia, Tambueni Haki Zetu, Heshima Yangu, Pambo  na Lina Ubani! Wakati Waswahili wanasema kwamba la kuvunda halina ubani, mama huyu anasema la kuvunda lina ubani! Mwenyewe aliigiza mchezo alioutunga mwenyewe wa Lina ubani na kuwasisimua watu wengi.
Huyu ni mama mpole na mnyenyekevu, hana mbwembwe za kisomi, maandishi yake yanachoma na kufikirisha zaidi ya anavyoonekana yeye mwenyewe. Ni mwanamapinduzi na mwanaharakati wa haki za binadamu kupindukia. Siku za hivi karibuni ameipumzisha kalamu yake lakini, kilichoandikwa kimeandikwa. Maigizo aliyoyatunga, yakitinga jukwaani ni lazima kila mtu aguswe na utunzi huo na kutambua msimamo wa mwandishi huyu mkimya anayependa kuzunguza kwa kalamu na maigizo.
Akiigiza sehemu ya Mama Liundi, kwenye kesi iliyovuma hapa Tanzania, ya mama aliyewanywesha watoto wake sumu kwa kisa cha kufuzwa na bwana wake, ndipo unapotambua uwezo mkubwa wa profesa Penina Mhando. Akiigiza unaona picha nzima kana kwamba tukio hilo ndo linatokea. Ni mama mwenye kipaji kikubwa na msomi ambaye anajishusha ili kutoa mchango wake katika jamii.
Huyu si mtu wa maneno, bali matendo. Inawezekana anatoa ujumbe kwa wasome wenzake kwa ujumbe wa maagizo: “ Mimi ni msomi kama nyinyi, fuateni mfano, jishushe tulijenge taifa letu, maana la Kuvunda lina Ubani”. Nimemlisha maneno hayo, lakini mwenye macho si lazima kumwambia tazama!
Mama Penina Mhando alikuwa mkufunzi wa Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam kwa miaka mingi kabla ya kwenda Nairobi Kenya kufanya kazi na Baraza la Wanawake Waelimishaji wa Afrika (Forum for African Women Educationalists – FAWE) , kwenye ofisi ya makao makuu, jijini Nairobi.
Mama huyu ambaye ni profesa, alizaliwa  mnamo mwaka 1948, katika Wilaya ya Kilosa, Mkoa wa Morogoro. Alifanikiwa kumaliza masomo ya juu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ambapo alipata: B.A (Hons) – Elimu, Lugha na Sanaa za Maigizo, M.A. – Sanaa za Maigizo, Ph.D – Sanaa za Maigizo.

Penina alifanya kazi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Idara ya Sanaa za Maigizo kwa kupanda ngazi kuanzia  Msaidizi wa Mkufunzi, Mkufunzi, Mkufunzi Mkuu hadi Mhadhiri Mshiriki.

Pia mama huyu alishiriki uongozi kwenye Idara hiyo ya Sanaa na Maigizo kama Mwongozi, Idara ya Sanaa ya Muziki na Maigizo, akiwa na majukumu ya kupanga na kuendesha mipango ya ukufunzi, utafiti na huduma kwa jamii, ushiriki wa kina katika mipango ya Maendeleo ya Maigizo ambapo maigizo yalitumika kama njia ya kuhamasisha jamii katika kiwango cha shina, kwenye maeneo ya vijijini:

Pia  Mwongozi Mshiriki wa Kitivo – Utafiti na Uchapishaji, Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii akiwa na majukumu ya kupanga, kusimamia na kukagua utafiti na sera ya uchapishaji na mipango katika idara kumi na mbili (12) za Kitivo. Majukumu haya yalikuwa pamoja na kuhamasisha upatikanaji wa fedha kwa utafiti wa Kitivo na uchapishaji,
ikiwa pamoja na majarida ya wakufunzi:

Pia Kaimu Mwongozi wa Kitivo, Kitivo cha Sanaa na Sayansi za Jamii Akiwa na majukumu ya kupanga, kuratibu na kukagua utafiti wa ukufunzi na huduma Ushiriki katika uwekaji wa sera zinazohusiana na mipango ya mafunzo. Uongozi wa idara kumi na mbili (12) na idara moja ya utafiti, zote zikiwa chini ya Kitivo:

Pia,Ofisa Mkuu wa Ukufunzi (Deputy Chancellor) Akiwa na majukumu ya kusimamia, kuratibu na kukagua shughuli za utafiti na ushauri katika Vitivo vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na vyuo viwili vishiriki. Chuo Kikuu cha Dar-es Salaam kina Vitivo 10 na Taasisi za Utafiti 10.Majukumu yalikuwa uwekaji wa sera uhamasishaji wa fedha kutoka serikalini na kwa wafadhili kwa kuendesha mipango ya utafiti sehemu/vifaa vya ukufunzi, pamoja na mafunzo kwa wafanyakazi na walimu, Uratibu wa shughuli za kawaida za utawala za Chuo Kikuu zinazohusiana na uingiaji (Admissions) wa Wanafunzi, Utafiti na Uchapishaji, Maendeleo ya /Walimu na Wafanyakazi, Stashahada za Juu, Uhusiano wa Nje na Miradi, Ukufunzi katika Chuo Kikuu, Ualimu na Uajiri.

Pia alishirikia shughuli za kijinsia kwenye chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam kama  Mratibu wa Kitengo cha Uendeshaji wa Shughuli za Kijinsia cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Akishughulikia upungufu wa uwiano wa kijinsia katika uingizaji wa wanafunzi, uajiri na wakufunzi na wafanyakazi, masomo pamoja na maslahi yote kwa ujumla Mratibu wa Mradi wa TUSEME ambao unatumia sanaa katika kumwezesha msichana kufanya vizuri zaidi katika masomo Mratibu wa Mpango wa Sanaa ya Maigizo kwa Maendeleo ambao unatumia Sanaa ya Maigizo kuwawezesha wanawake katika vijiji kupata mafanikio katika maendeleo.

Pia mama huyu ameshiriki mambo mengi ya kijamii kama, Mratibu wa mpango wa kumwendeleza mtoto kupitia sanaa katika shule za msingi jijini Dar es Salaam.
ufundishaji wa waalimu na kuendesha Tamasha la Watoto la Maigizo Na mambo mengine kama vile; Mwanachama - Chama cha Sanaa cha Paukwa, Mratibu - Kikundi cha Maigizo cha Watoto cha Chuo Kikuu wakati ule akiwa Mratibu - TUSEME: Elimu ya Demokrasia kwa wanafunzi wasichana na shule za sekondari nchini Tanzania, Mwanachama - Kamati ya Uendeshaji wa Semina za Lugha katika mabadiliko yanayotarajiwa katika muundo wa ukufunzi, Mwanachama - Chama cha Wanawake wa Afrika katika Utafiti na Maendeleo (African Associationfor Women for Research and Development– AWARD).

Tunzo ambazo Prof. Penina Mlama amewahi kupata ni kama ifuatavyo: Tunzo ya Nane ya Utafiti wa Sayansi ya Jamii katika Afrika ya Mashariki na Kusini, Tunzo ya Utafiti wa Masomo ya Marekani – New York University ,Tunzo ya Mfuko wa Rockerfeller katika Sayansi ya Jamii kwenye Upembuzi wa Maendeleo, Shindano Maalum la Jinsia na Maendeleo – Shirika la Utafiti wa Sayansi ya Jamii katika Afrika Mashariki, Mwigizaji Bora wa Kike katika filamu ya “Mama Tumaini” TFC/NORAD, Tamasha la Filamu la SADDC, Harare, Tunzo ya Shaaban Robert kwa Uhamasishaji wa Kiswahili nchini Tanzania, 1999, iliyotolewa na Baraza la Kiswahili la Taifa
Mwanamke wa Mwaka – Taasisi ya Marekani ya Maisha ya Watu, USA.

Katika maisha yake ya kazi yake, Prof. Penina Mlama amejishughulisha
na kazi nyingi za utafiti wa kina, na kuweza kuchapisha idadi kadhaa ya
vitabu na makala, pamoja na utengenezaji wa filamu na maigizo mengi.

Huyo ndo Mama Penina Mhando, ambaye amefanya mambo mengi, ingawa hasikiki sana siku hizi, lakini mchanga wake katika taifa letu ni mkubwa.

Na,
Padri Privatus Karugendo.
+255 754 633122
www.karugendo.net.












0 comments:

Post a Comment