http://3.bp.blogspot.com/_qoN-WXqQXBQ/SdVSL3gU2GI/AAAAAAAACHk/YeBgWJbhTAA/s400/1p_habitat_0039.jpg


MWANA MAMA PROFESA ANNA KAJUMULO TIBAIJUKA.

Leo katika safu yetu ya Mwana Mama, tunawaletea Mheshimiwa  Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka. Lengo la safu hii ni kuandika habari za mwana mama ambaye ametoa mchango mkubwa katika taifa letu lakini habari zake hazijulikani. Ni kutokana na mfumo dume ambao daima unatoa nafasi kwa wanaume kuliko wanawake ndiyo maana historia yetu inaandikwa kana kwamba wanaume peke yao ndo wameishi na kuiendesha historia hiyo.
Ni wazi habari juu ya Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka, zimeandikwa sana. Hivyo huyu si mlengwa wa safu hii! Hata hivyo na mimi siandiki juu ya Anna Tibaijuka Profesa wa uchumi wa Cho Kikuu cha Dar-es-Salaam, najua mengi yameandikwa juu yake. Pia siandiki juu ya Anna Tibaijuka, aliyefanya kazi Umoja wa mataifa, ni wazi mengi yameandikwa juu yake na wala hakuna tena haja ya kuandika zaidi. Siwezi kusema ninaandika juu ya Anna Tibaijuka Mbunge, mjumbe wa NEC wa CCM, au waziri wa Ardhi Nyumba na makazi; kwa nafasi aliyo nayo sasa hivi habari zake zinaandikwa kila  gazeti na mitandao mbali mbali.
Katika safu hii ya Mwana Mama, naandika juu ya Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka, mwanzilishi wa BAWATA. Ni wazi kwa vile shirika hili lilifutwa na serikali, ilikuwa vigumu kuandika juu yake, lakini ukweli unabaki kwamba mchango wa muda mfupi wa shirika hili hautafutika.  Shirika hili lililojulikana kama Baraza la Wanawake Tanzania, lilianzishwa kwenye miaka ya tisini likiwa na lengo la kuwaunganisha wanawake wa Tanzania; kuwakomboa wanawake kutokana na mfumo dume uliojikita katika jamii yetu; kuwawezesha wanawake kielimu na kiuchumi. Shirika hili lililenga kuwaunganisha wanawake bila kuangalia itikadi zao za vyama vya siasa, dini zao na makabila yao. Mwenyekiti wa kwanza wa shirika hili alikuwa Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka; mwanamke shupavu anayejisimamia na si mwepesi wa kuyumbishwa. Kwa muda mfupi BAWATA, ilisambaa kama kimbunga na kuenea Tanzania nzima.
Akiwa mchumi wa masuala ya kilimo, Mama Anna Tibaijuka, alishafanya utafiti na kugundua matatizo yanayokwaza maendeleo ya wanawake wa Tanzania. Akagundua kwamba mgawanyiko uliopo kwenye makundi ya wanawake unadhoofisha nguvu zao na jitihada zao za kuleta maendeleo. Akajipanga kuinua maisha ya wanawake hawa kupitia umoja wao ndani ya shirika la BAWATA. Kama shirika hili lingeendelea leo hii tusingekuwa tunaongelea viti maalumu; wanawake wangekuwa wanapambana sambamba na wanaume kuingia Bungeni.
BAWATA, ilieleweka haraka kwa wanawake wa kawaida vijijini na  kwa wanawake waliopenda umoja. Wakati kulikuwa na vyama vya wanawake vya siasa, dini na makundi ya wasomi, BAWATA ililenga kuwaunganisha wanawake wote; na dalili za ukombozi zilianza kuonekana, maana Waswahili wanasema “ Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu”. Umoja wa wanawake waliopigania Uhuru wa taifa letu, ulikuwa bado kwenye kumbukumbu za wengi, na hasa viongozi (Wanaume) waliokuwa madarakani, walijua vizuri nguvu za umoja wa wanawake. Baada ya uhuru umoja huu wa wanawake ulisambaratishwa kwa kuwatenga wanawake kwa kuunda vikundi mbali mbali.
BAWATA, ilionyesha nia ya kufufua umoja na nguvu ya wanawake. Kwa wanaume wasiojiamini, waliona tishio la BAWATA. Bahati mbaya au nzuri, BAWATA iliibuka wakati wa vyama vingi vya siasa na kuelekea uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi wa 1995. Wenye uchu wa madaraka na hasa wanaume wanaofikiri walizaliwa kuitawala Tanzania, waliogopa umoja huu wa wanawake. Wangependa kuwaona wanawake wametengana kuliko kuungana. Woga ukatanda nchi nzima kwamba BAWATA, itajiingiza kwenye siasa na labda kuunga mkono vyama vya upinzani. Hivyo Serikali ikahakikisha shirika hilo linafutwa!
Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka, ninayemwandika katika safu hii ya Mwana Mama, alisimama imara kuitetea BAWATA yake. Hakukubali kuonewa, hakukubali kuyumbishwa na hakukubali vitisho. Alitetea hoja ya kuanzishwa BAWATA na taifa zima lilimuelewa. Hata hivyo 1994, serikali iliamua kuifuta BAWATA. Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka na wenzake wakakimbilia mahakamani kutetea haki yao huko. Kesi ilichukua muda mrefu, baada ya miaka 12, BAWATA iliibwaga Serikali mahakamani. Watu wote wanaopenda haki katika taifa letu, walimpongeza Profesa Isa Shivji, kwa kupambana hadi kufanikisha haki ya BAWATA kupatikana. Hata hivyo malengo ya wenye uchu wa madaraka yalishafanikiwa na wanawake wakatengwa vikundi vikundi kiasi ni vigumu kuwaunganisha tena.
Sina uhakika, baada ya kushinda kesi BAWATA, iliendelea na shughuli  zake na wala hili si lengo la makala hii kwa leo. Hoja yangu ya leo, ni Mwana Mama aliyeanzisha shirika la kuwaunganisha wanawake wa Tanzania, akashirikiana na wenzake kuliunda na kulisimika, likasambaa nchi nzima, lakini serikali ikaliogopa na kulifuta. Mwana Mama huyo, akapambana mahakamani na kushinda kesi. Hoja yangu ni kuandika juu ya Mwana Mama shupavu, mwana mama anayejisimamia, mwana mama asiyeyumbishwa, mwana mama mwenye mtizamo wa umoja na uzalendo, Mwana Mama Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka.
Baada ya kufutwa BAWATA na baadaye kidogo kifo cha mme wake, kilichomgusa kwa kiasi kikubwa na kuiumiza familia yake wengi walifikiri huo ungekuwa mwisho wa mwanamke huyu machachari, lakini Mwana Mama huyu alipaa hadi anga za kimataifa, hadi kuingia kwenye siasa za hapa nchini na kufanya kazi ndani ya mfumo wa serikali iliyofuta shirika lake la BAWATA! Ni namna gani anaweza kufanya kazi ndani ya mfumo huo ni swali la kujiuliza!
Hivyo twaweza kusema kuna sura mbili za Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka? Sura ya kwanza ikiwakilisha mwana mama msomi, mpambanaji, shupavu, asiyeyumbishwa na mtetezi wa wanyonge na sura ya pili ikimwakilisha Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka, mwana mama wa kimataifa, mwanasiasa , mbunge na waziri?
Nilipokutana naye mwezi wa tatu mwaka huu, alizikataa sura mbili za Anna  Tibaijuka. Binafsi nilisifia sura ya Anna Tibaijuka wa BAWATA.  Kwa mshangao aliniuliza “  Unafikiri sasa hivi mimi ni dhaifu?” aliendelea: “ Mimi ni Yule Yule wa BAWATA, ni Yule Yule asiyeyumbishwa, ni Yule Yule mtetezi wa wanyonge, mpambanaji na mzalendo.. tofauti ni muda na nyakati tofauti na matatizo tofauti, lakini mtu bado ni Yule Yule na msimamo ni ule ule wa haki na wajibu..”.
Nikashuhudia maneno yake wakati wa Kigoda cha tano cha Mwalimu Nyerere. Wakati viongozi wa serikali walisusia tamasha hilo linalofanyika kila mwaka,  kwa kisingizio kwamba Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam kina tabia mbaya ya kuwazomea viongozi wa serikali, Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka , alikuwa kiongozi pekee wa serikali aliyehudhuria na kusimama jukwaani kutoa hoja zake kwa kujiamini. Mada yenyewe ilikuwa nyeti: Juu ya kilimo na suala zima la umiliki ardhi katika nchi za Afrika. Ingawa idadi kubwa ya wachangiaji walikuwa na msimamo wa kilimo cha wakulima wadogo wadogo na Profesa Anna Tibaijula, alilijua hilo, bado alisimama kidete kutetea sera za serikali za kuendeleza kilimo kwa kutumia makampuni makubwa ya uwekezaji.  Hakukwepa kuelezea mpango mzima wa kutoa ardhi kwa wawekezaji. Bila kupinga moja kwa moja kilimo cha wakulima wadogo wadogo, alijenga hoja kwamba sasa hivi watanzania wanakimbilia mijini na kufikia 2025, Jiji la Dar-es-Salaam litakuwa na watu zaidi ya milioni 10, na itakuwa hivyo kwenye miji mingine. Bila kuangalia mbali na kuendelea na kilimo cha wakulima wadogo wadogo tutakwama mbeleni. Hakuna aliyemzomea, alishangiliwa hadi anamaliza hotuba yake.
Tumeshuhudia pia bungeni, wakati Mawaziri wanafanya mbinu za kuchomoa hoja binafsi za wabunge wa upinzani na kuhakikisha hazijadiliwi bungeni, Profesa Anna Kajumulo Tibaijuka anapambana na hoja hizo. Si mtu anayeogopa hoja na mawazo tofauti. Pia jitihada zake za kuhakikisha haki inatendeka katika umilikaji wa ardhi ndani ya taifa letu ni ushuhuda wa kutosha kwamba Profesa Anna Tibaijuka  wa BAWATA bado ni Yule Yule. Na bila kumung’unya maneno, huyu ana sifa zote za kuandikwa kwenye safu yetu ya Mwana Mama.
Na,
Padri Privatus Karugendo.
+255 754 633122


1 comments:

MAJARIBIO said...

Tunashukuru sana father kwa kutuandikia juu ya watu muhimu sana wenye mchango mkubwa sana kwenye taifa letu na hasa wa mama,kiukweli huyu mama ana mchango mkubwa sana kwenye taifa letu na anasifa zote nzuri kwa nchi hii hasa katika kipindi hiki ambacho watu wengi wamepoteza imani kwa viongozi wao,mama huyu ni mchapakazi,anayesimamia haki na sheria,hasiye yumbishwa na tamaa na ni mtetezi wa wanyonge,jasiri na msema kweli,mama huyu ni mffano kwa viongozi wengi hapa nchini,naomba viongozi waige mfano wake,pia watanzania naomba sana tuthamini michango yao na kiukweli tuwape nguvu watu muhimu na wanao onyesha juhudi za kweli za ukombozi wa taifa letu,tuache ushabiki usio kuwa na maana,wale wanao stahili pongezi na support yetu kama mama huyu tuwape nguvu ili waweze kulifikisha taifa hili mbali sana.

Post a Comment