MTWARA KUCHELE 1

MTWARA “KUCHELE”, VURUGU ZA MTWARA JIBU ANALO RAIS KIKWETE.
 
 
Moja ya ziara zake katika mkoa wa Mtwara, Rais Jakaya Mrisho Kiwete, aliwaambia watu wa Mtwara: “Mtwara Kuchele”, maana yake “ Mtwara kumekucha”. Ziara hii ilifanyika kabla ya vurugu za Mtwara. Mheshimiwa Rais aliwaambia watu wa Mtwara, kwamba gesi iliyovumbuliwa kwenye mkoa wao itaharakisha maendeleo na yeye atahakikisha viwanda vingi vinajengwa, vijana wanapata kazi , uchumi wa mkoa huo unapanda na mji wa Mtwara  unabadilika na kufanana Dubai. Na kwa matani, akawaambia , “ Ningekuwa na uwezo, ningehamisha gesi yote hii na kuipeleka Bagamoyo”. Maneno haya yako midomoni na moyoni mwa kila mtu wa Mtwara, aliyesikiliza hotuba hiyo ya Mheshimiwa Rais.
Tarehe 11.9.2013 mpaka tarehe 15.9.2013, nilifunga safari kwenda Mtwara, kuchunguza chanzo cha vurugu ya “Haitoki”. Hatukuzoea kusikia vurugu hizi mkoa wa Mtwara. Mwaka 2005, nilikuwa mwangalizi wa uchaguzi mkuu kupitia TEMCO; nilishuhudia upole wa watu Mtwara. Kampeni za wagombea mwaka huo wa uchaguzi zilitawaliwa na wali na vinywaji. Wakipikiwa wali na kunywa pombe za kienyeji, wanaimba na kucheza na kusahau matatizo mengine ya mkoa wao. Hivyo vurugu za gesi zilipotokea, watu wakafa na mali zikaharibiwa, kila mtu aliyeufahamu mkoa huu wa Mtwara, alishangaa na kujiuliza kulikoni.
Mtu wa kwanza niliyeongea naye, ni kijana wa Bajaji, ambaye kwa maoni yake kasheshe zote za vurugu za gesi zilianzishwa  na Hotuba ya Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete, ya kuibadilisha Mtwara kufanana na Dubai, ahadi ya kujenga viwanda na kuhakikisha vijana wanapata ajira.
“Huwezi kuamini, hotuba hiyo ya Mheshimiwa Rais, ilianza kuleta matunda, maana tulianza kuona watu wengi wanakuja kununua viwanja hapa Mtwara. Kuna mzee ninayemfahamu, aliuuza kiwanja chake ufukweni, kwa bei ya milioni mia mbili hamsini” alinieleza  huyu kijana wa Bajaji.
“La kushangaza, hata kabla ya kuliona jiwe la msingi la kuijenga Dubai ya Mtwara, tulisikia kwamba gesi inasafirishwa kwenda Bagamoyo”.  Hayo ni maneno ya kijana aliyenibeba kwenye Bajaji, kutoka maeneo ya Bima- Mtwara kuelekea Makao makuu ya kanisa la KKKT mjini Mtwara. Hakukubali kunitajia jina lake. “Tunaogopa sana siku hizi, jina langu likitokea gazetini, nitakamatwa na kupelekwa Gwantanamo, huko nitapigwa na kuteswa, kama ambavyo watu wengine wamepigwa na kuteswa, wengine hadi leo hii hawajarudi” alinieleza huyo kijana wa Bajaji. Gwantanamo ni kituo cha Jeshi cha Nalyendele. Kilikuwa ni kituo cha ukombozi wa nchi ya Msumbiji, lakini leo hii kimegeuka kuwa ni kituo cha mateso makubwa ya kunyamazisha sauti za “Gesi haitoki”
“Utani ukawa ukweli, gesi inakwenda Bagamoyo. Rais wetu alitwambia angekuwa na uwezo, angesomba gesi yote na kuipeleka Bagamoyo. Wakati huo tulijua ni utani. Tunamjua Rais ana utani mwingi. Lakini baada ya kuambiwa kwamba mabomba yatasafirisha gesi yetu ya Mtwara kwenda Bagamoyo, tukajua sasa si utani bali ni kweli. Na tulijua, maana Rais wa nchi ana uwezo wote...” Aliendelea kunieleza kijana wa Bajaji.
Kwa maelezo ya kijana huyu ni kwamba wazee walipoona Dubai ya Mtwara inayeyuka, walitaka kuwa na maongezi na Mkuu wa Mkoa, ili kujua kulikoni. Lakini kwa kiburi, Mkuu wa Mkoa, alikataa kukutana nao. “ Hivyo wazee walipanga kuitisha maandamano, lakini Mkuu wa Mkoa aliyapiga marufuku maandamano hayo” Aliendelea kunieleza huyu kijana wa Bajaji.
Kwa maoni ya kijana huyu wa Bajaji, kama Mkuu wa Mkoa wa Mtwara angelikubali kuwasikiliza wazee au kuwakubalia maandamano yao, vurugu, vifo na uharibifu wa mali uliojitokeza Mtwara usingekuwepo. Alihitimisha maongezi yetu kwa kusema “ Vurugu za Mtwara chanzo chake ni ahadi za Mheshimiwa Rais Kikwete na kiburi cha Mkuu wetu wa mkoa...”
Ingawa sababu za vurugu zinatajwa mbili ambazo ndizo kubwa, bado kuna mambo mengine mengi, kama mpasuko ndani ya chama cha CCM mkoani Mtwara,   elimu ndogo watu waliyonayo juu ya masuala ya gesi na suala zima la ushirikishwaji. Kila mtu unayezungumza naye kwenye mji wa Mtwara, atakwambia kwamba suala zima la gesi limezungukwa na usiri mkubwa na wananchi hawakushirikishwa. Hata na viongozi wa serikali za mitaa, madiwani na wenyeviti wa mitaa, wanalalamika kutoshirikishwa.
Inashangaza kusikia watu wakisema kwamba gesi inakwenda Bagamoyo, hakuna anayesema inakwenda Dar-es-Salaam. Pia uelewa  wa gesi, kuhusu uchimbaji wake hadi hatua ya kuisafirisha ni mdogo, maana nilielezwa juu ya mzee mmoja ambaye ni mvuvi wa miaka mingi, siku moja aliona meli kubwa baharini, akarudi na kutangaza kwamba meli zimeanza  kuinyonya gesi na kuisafirisha bila hata serikali kujua. Kumbe hizo ni meli zinazofanya maandalizi ya kuanza kuchimba gesi baharini.
Pamoja na uelewa mdogo wa masuala ya gesi, wana hoja nzito: Kama mchakato wa gesi unachua miaka mingi kumi na  tano hadi ishirini kama wataalam wanavyoeleza, kwa nini wanaona magari yamebeba mabomba na vituo vya mabomba haya vimewekwa sehemu mbali mbali kutoka Mtwara hadi Dar-es-Salaam? Maandalizi yanaoyesha gesi inaondoka kesho ama keshokutwa!
Siku tano nilizokaa Mtwara, nikijaribu kutafiti na kuchunguza chanzo cha vurugu za “Gesi haitoki”, uharibifu wa mali na vifo vilivyotokea, nilipata majibu yanayofanana kwa karibu sana na maoni ya kijana wa Bajaji. Niliongea na viongozi wa serikali, vijana wa vijiweni, wazee, wanawake, viongozi wa dini, wafanyabiashara, vyama vya siasa, na wote majibu yalifanana! Ukimtoa diwani mmoja wa CCM, aliyekubali jina lake kutajwa wengine wote hawakutaka kwa kuogopa kupelekwa Gwantanamo. Hivyo si busara hata kulitaja jina la Diwani huyo wa CCM.
Mbali na sababu mbili kubwa za kuanzisha vurugu za gesi nilizozitaja hapo juu, watu wa Mtwara, wazee  kwa vijana wanaimba historia ya machungu ya  mkoa  wao. Kwamba: Kulikuwa na reli inatoka Nachingwea hadi Mtwara, lakini iling’olewa; Kwamba kulikuwa na mtambo wa kusukuma maji, lakini uliondolewa na kupelekwa sehemu nyingine; Kwamba kulikuwa na mpango wa Mtwara corridor  lakini ulipotelea kusikojulikana; Kwamba Bandari ya Mtwara ndiyo yenye kina kirefu na uwezo wa kupokea meli nyingi kwa wakati mmoja, lakini ilitelekezwa na vifaa vingine kuondolewa na kupelekwa Dar-es-Salaam, Kwamba uwanja wao ndege ni miongoni mwa viwanja vikubwa vya mwanzo kabisa baada ya uhuru, lakini kiwanja chao cha ndege kilitelekezwa, wakasikia vikiendelezwa viwanja vingine kama vile cha Kilimanjaro na cha Dar-es-Salaam; Kwamba kulikuwa na kiwanda cha kubangua korosho, lakini hakipo tena; kwamba kwa vile Mtwara ulikuwa ni uwanja wa mapambano ya kuikomboa Msumbiji, hakuna aliyependa kuwekeza au kufanya kazi Mtwara; Kwamba kulikuwa na kilimo cha pamba lakini kimekufa jumla; kwamba barabara ilikuwa mbaya hadi siku za hivi karibuni walipojengewa daraja la Mkapa na Barabara ya lami ambayo hata hivyo bado zaidi ya kilomita thelathini  hazijakamilika; Kwamba bei ya korosho imeendelea kuwa chini na umasikini umeongezeka na kubwa zaidi kwamba ahadi za Songosongo kuleta maendeleo mkoa wa Lindi mbona hazijatekelezwa?
“Uamuzi wa kusafirisha gesi kutoka Mtwara hadi Bagamoyo, umeamsha mshikamano miongoni mwa wananchi, kusema kweli imetonesha vidonda vya historia ya machungu ya Mkoa wetu. Na kusema ukweli hakuna aliye nyuma ya vurugu hizi; ni mshikamano wa wananchi wa Mtwara” alinieleza diwani wa CCM, ambaye jina lake nalitunza kwa sasa.
Kufuatana na maelezo ya diwani huyu ni kwamba vuguvugu za “Gesi haitoki” zilikuwa na hatua kuu nne:
Baada ya kusikia matangazo ya kuisafirisha gesi kutoka Mtwara kwenda Bagamoyo, na baada jitihada za kukutana na kuzungumza na Mkuu wa Mkoa kushindikana, wanamtwara waliibuka na kauli mbiu ya: “ Gesi kwanza, vyama baadaye”. “Vyama vyote vya siasa viliungana na kuwa na sauti moja juu ya gesi” alinieleza diwani huyu wa CCM.
Hatua ya pili, ilikuja na kauli mbiu ya “ Gesi kwanza, uhai baadaye”. Hapa ndipo mapambano yalianza baina ya polisi na wananchi. Kijana wangu wa Bajaji aliniambia kwamba mapambano hayo yalikuwa makubwa na yakutisha! “Kama wananchi tungelikuwa na silaha, mapambano haya yangekuwa mabaya sana” Alinieleza kijana huyu.
Hatua ya tatu ya vuguvugu na vurugu za Gesi katika Mkoa wa Mtwara, ilikuja na kuli mbiu ya “Gesi haitoki” .Hapa ndipo serikali ilipoamua kutumia nguvu kubwa, mali ziliharibiwa na watu walikufa. Hadi sasa serikali inasema walikufa watu watatu. Lakini kuna habari za pembeni zinazosema watu waliokufa kwenye machafuko haya ni zaidi ya 18,  na wengine wanasema ni kama 100! Hata hivyo hadi leo hii bado watu wanakamatwa, wanapelekwa Gwantanamo, wanateswa na wengine hadi leo hii hawajarudi kwenye majumba yao.
Hatua ya nne ya vuguvugu na vurugu za Gesi ni “Gesi itoke tu lakini...”. Sasa hivi kila mtu unayekutana naye Mtwara, anasema “Gesi itoke”. “Wameamua kutuletea jeshi letu la Wananchi, kutupiga na kutufanya vibaya, Gesi itoke, lakini tutasusia shughuli zote za serikali na tunawasubiri kwenye uchaguzi wa 2015” Alinieleza mfanyabiashara ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini.
Tarehe 14.9.2013, tulishuhudia Mwenge wa Uhuru ukiingia Mtwara kimya kimya kwa ulinzi wa kutisha. Siku tatu kabla ya ujio wa Mwenge, vipepererushi na ujumbe mfupi kwenye simu za viganjani ulianza kupita kuwahamasisha watu kususia sherehe za Mwenge. Ni kwamba Mtwara, wanaheshimu sana ujumbe mfupi wa simu, hata bila kujua unatoka wapi; ujumbe ukisema maduka yasifunguliwe, agizo linatekelezwa; ujumbe ukisema hakuna kutoka nje, mitaa inashinda bila watu. Hivyo na ujumbe wa kususia sherehe za Mwenge, ulitekelezwa kiasi kikubwa; Wanafunzi na wafanyakazi wa serikali ndio waliojitokeza kuupokea Mwenge wa Uhuru.
Kwa kuangalia kwa nje, ni kwamba sasa hivi Mtwara kuna utulivu, lakini hakuna amani. Kuna utulivu kwa vile jeshi linatumia nguvu na watu hawana tena jukwaa la kutoa maoni yao, wanaishi kwa woga. Jeshi linaweza kutesa miili yao na kuweka utulivu wa nje tu, lakini ndani ya mioyo yao wana makovu makubwa na hasira. Mtu mwenye hekima, angeshughulikia kuponya makovu na wala si kuendelea kutumia nguvu kubwa kuwalazimisha watu kukubali yale wasiyoyaelewa vizuri na wala kufahamu jinsi watakavyofaidika nayo.
Baadhi ya watu wameamua kuishi porini kwa kuogopa nguvu za Jeshi. “Kuna mtu aliyekaa porini siku saba kwa kuwaogopa wanajeshi. Mtu huyu alikuwa ni dreva kwenye kampuni Fulani ya mhindi, baada ya siku saba aliporudi kazini, alifukuzwa kwa utoro. Kitendo cha kumfukuza kilimshutua sana, na baada ya siku chache alikufa kwa shinikizo la moyo. Mifano kama hii tunayo mingi, lakini tumeamua kukaa kimya” Alinieleza mwenye kiti wa mtaa ambaye hakutaka jina lake litajwe.
Ubakaji, kuwangilia watu kinyume na maumbile, udhalilishaji na mateso mengine ni baadhi ya vitu vinavyotajwa kutokea na kuendelea kutokea Mtwara. “Vurugu zote hizi Mbunge wetu wa Mtwara mjini alisimama upande wa wananchi na kutetea haki za Mkoa wetu bila woga. Hata Mkuu wa wilaya ya Mtwara, alikuwa upande wetu. Hawa wawili wanakubalika na wakisema jambo tunasikia, ingawa tumemgomea Mkuu wetu wa Wilaya kushiriki sherehe za Mwenge”. Alinielezea mama mmoja ambaye alionekana kama mwanasiasa, lakini hakutaka kusema ni wa chama gani
“Si kweli kwamba hatutaki Gesi itoke na kuwanufaisha watanzania wengine. Hoja yetu ni je Gesi ikitoka, sisi tunabaki na hali gani? Umasikini? Dubai yetu iko wapi? Kama ni kuisafirisha Gesi kwenda kuiuza nchi za nje kwa nini isisafirishwe kwa kupitia bandari ya Mtwara? Kama ni kuzalisha umeme, kwa nini mitambo ya kuzalisha umeme isijengwe Mtwara, na umeme ukasafirishwa kwa  nguzo?”  Alilalamika kiongozi mmoja wa dini niliyeongea naye.
Katika harakati za kurudisha imani ya wananchi, serikali imewapeleka baadhi ya watu wa Mtwara , nchini Thailand kujifunza mafanikio ya miradi ya Gesi. Lakini kuna manung’uniko kwamba safari hiyo haikuwa ya lazima, ni matumizi mabaya ya fedha, wakati kuna kipindi cha Baragumu la Msimbati, kinachorushwa kwenye luninga na kuelezea mafanikio ya Gesi ya Songosongo. Kwa nini watu hawa wasingepelekwa Songosongo kujifunza mafanikio ya huko kuliko kutumia fedha nyingi kuwasafirisha watu kwenda nchini Thailand? Hata hivyo na uchaguzi wa nani aende Thailand, haukuwa wa wazi. Tulipoongea na mmoja kati ya wale  waliokwenda Thailand, alisema  “ Mimi nafikiri nilichanguliwa kwa vile niko karibu na Waziri Fulani”
Mtu wa kumaliza vurugu za Mtwara, ni Rais mwenyewe. Kila mtu tuliyeongea naye, alitoa jibu hili. “Tunamtaka Rais wetu aje hapa abadilishe usemi wake, aje atwambie kwamba sasa Dubai ni ndoto, mbali na hapo hatumtaki mtu yeyote hapa...” Alinieleza mzee ambaye ilionyesha ana ushawishi mkubwa kwenye jamii inayomzunguka..
Kwa kifupi ni kwamba watu wa Mtwara wamepoteza imani na Mkuu wao wa Mkoa, hawataki kumsikia waziri wa Elimu, ambaye wanasema alikwenda Mtwara kuwatukana: “Mtwara mnafanya kazi ya kutiana  mimba mambo ya Gesi mtayafahamu?” Hawataki kumsikia Shehe Mkuu wa Mkoa. Pia hawataki kumsikia waziri wa  nishati na madini, ambaye naye wanasema aliwatukana. Wanamtaka Rais wao ambaye wakati wa kuomba kura, alienda kuongea nao, na sasa wanataka aende aongee nao.
Na,
Padri Privatus Karugendo
+255 754 633122

0 comments:

Post a Comment