MWALIMU THEOPHILDA TINKASIMIRE TIKAWA

MWANA MAMA MWALIMU THEOPHILDA TINKASIMIRE TIKAWA.
 
Leo hii katika safu yetu ya Mwana mama tunawaletea Mwalimu Theophilda Tinkasimire Tikawa. Maarufu kama Mwalimu Tinka. Mama mwenye tabasamu na uchangamfu kila wakati, mwenye kuwapenda watu wote bila ubaguzi, mwenye kuipenda kazi yake ya ualimu na roho ya kuwasaidia watu wanaomzunguka na hasa wasiojiweza. Inawezekana sifa hizi zikawa zinapwaya kwa wale wanaomfahamu Mwana mama huyu kwa karibu, lakini safu hii imejitahidi kiasi cha kuzidi nusu ya sifa zake.  Mwalimu huyu wa miaka mingi anastaafu kazi ya ualimu mwezi huu baada ya kufikisha miaka 60 ya kuzaliwa.  Bila kuona mvi zinazokipamba kichwa chake, utafikiri ni binti mdogo wa miaka 30, yeye anajivunia mvi zake na hapotezi muda wake kuweka rangi za kubadilisha rangi ya nywele zake kama wafanyavyo wengine wanaogopa kuitwa “Bibi” au “Babu” kwa upande wa wanaume.

Mwalimu Tinka, ni mama wa watoto 4, wajukuu 12 na watoto wengine wengi aliowafundisha sehemu mbali mbali za Tanzania; Tanga, Tabora, Dar-es-Salaam, Mbeya na Karagwe. Mama huyu ambaye kauli mbiu ya maisha yake imekuwa “ Kukata tama ni dhambi” ni mfano wa kuigwa. Safu hii ilipoongea na mama huyu kwa nyakati tofauti, amekuwa akisisitiza kauli mbiu yake: “Unajua nilipofiwa na mme wangu, mnamo mwaka wa 1990, ningekata tama, nisingekuwa hivi nilivyo. Nisingeweza kuwasomesha watoto wangu na kuhakikisha wanakua vizuri na   kuweza kujitegemea. Sikukata tama, nilipambana na maisha na kumtegemea Mwenyezi Mungu, sikufikiria kuolewa tena, bali niliweka nguvu zangu zote kulijenga taifa langu la Tanzania kwa kufundisha watoto  na kuhakikisha ninawatunza watoto wangu” Alisema Mwalimu Tinka, akiongea na safu hii.

Wakati anapostaafu na bado ana nguvu, Mwalimu Tinka anatamani “ Kuzunguka Tanzania yote, nikitoa ushauri kwa wajane. Nimeishi maisha ya ujane, nafahamu matatizo  na uchungu wa kuwa mjane. Kama kuna kita ambacho siwezi kukisahau hadi naingia kaburini ni tukio na kufiwa na mme wangu. Hivyo natamani nieleze uzoefu wangu na kuwashauri wajane wenzangu wazikate tama, maana kukata tama ni dhambi. Tatizo lililo mbele yangu ni kutokuwa na uwezo wa fedha za kuizunguka Tanzania yote..” Anayasema haya kwa uchungu mkubwa, maana anaonyesha hamu na nia yake ya kutaka kuizunguka Tanzania nzima akiwashauri wajane.

Kwa vile ana wasiwasi wa kutoweza kupata fedha za kuizunguka Tanzania, nzima Mwalimu Tinka, ameaanza kuandika kitabu cha maisha yake. Anaamini, wajane na watu wengine wakikisoma watapata la kujifunza.
Mwalimu Theophilda TinkasimireTikawa, alizaliwa mnamo mwaka 1952 kijiji cha Kasheshe – Nyaishozi –Karagwe. Ni mtoto pekee wa Baba Paul Koliko na Mama Agnes Paul. Kati ya mwaka 1962 na 1968, alipata elimu ya msingi shule za Katoju na Nyaishozi –Karagwe. Hakuweza kuendelea na elimu ya Sekondari, isipokuwa alijiunga na Hospitali ya Nyakahanga –Karagwe, ambako alichukua mafunzo ya kuwasaidia manesi kwa miaka miwili, na baadaye kutoa huduma kama nesi msaidizi.

Wakati akiwa mfanyakazi wa Hospitali ya Nyakahanga, alikutana na mchumba wake Bwana Joseph Tinkasimile, aliyekuwa akifanya kazi Tanga, kama Afisa Maliasili wa Mkoa wa Tanga. Walifunga ndoa takatifu kwenye kanisa Katoliki Karagwe mwaka wa 1970 na kuhamia Tanga. Mungu aliwajalia kumpata Bruno mtoto wao wa kwanza mnamo mwaka 1971 na mtoto wao pili Felix mwaka 1972. Mnamo mwaka 1974, walijaliwa kumpata mtoto wao pekee wa kike Leticia Shubira Wamala na mwaka 1979 mtoto wao wa mwisho Victor alizaliwa.

Kati ya mwaka 1976 hadi 1977, Mwalimu Tinka, alijiunga na chuo cha Ualimu Korogwe na kusoma ualimu daraja la C. Katika hatua hii hawezi kumsahau mshauri wake Mama Mazoko wa Bukoba, ambaye ndiye aliyemshauri asomee ualimu na kuendelea kumshauri mambo mengi katika maisha yake. Hadi leo hii Mama Mazoko, bado ni mshauri wa karibu wa Mwalimu Tinka. “ Mama huyu ndiye alitoa ushauri nisikatwe mguu nilipopata ajali ya pikipiki kwenye miaka ya tisini. Bila ushauri wa mama Mazoko, leo hii ningekuwa na mguu mmoja. Hivyo Mama huyu siwezi kumsahau kwenye maisha yangu, alinishauri nisomee ualimu, na umenisaidia kwenye maisha yangu na kuwasaidia wengi na bado anaendelea kunishauri” . Alieleza Mwalimu Tinka, wakati alipoongea na safu hii ya Mwana Mama.

Baada ya kuhitimu.  Mwalimu Tinka, alianza kazi ya kufundisha Shule ya Msingi Kibasila – Dar-es-Salaam mnamo mwaka 1978. Mnamo mwaka wa 1979, alihamia shule ya  msingi Kitete –Tabora. Akiwa Tabora, aliteuliwa kuwa Afisa Utamaduni wa michezo wa Manispaa(Mji) wa Tabora. Mwaka 1982 - 1983, Mwalimu Tinka alihamia shule ya msingi Uyole Mbeya. Na mwishoni mwa mwaka wa 1983, alihamia Wilaya ya Karagwe na kufundisha shule ya msingi Rwambaizi hadi mwaka2002. Kati ya 2002 na 2003, alifundisha kwenye shule mbili za msingi Nyamilima na Kituntu kule Karagwe.

Mnamo mwaka 2004, Mwalimu Tinka, alihamia tena Dar-es-Salaam na kufundisha shule ya msingi Kizinga hadi mwaka 2005. Baada ya hapo hadi mwezi huu anapostaafu alikuwa anafundisha shule ya msingi Toangoma na amejenga makazi yake huko hukoToangoma.
Kwa vile Mwalimu Tinka, hakusoma masomo ya sekondari, kati ya mwaka 1999 na 2000 alisoma na kushinda mitihani ya sekondari na kujipatia cheti cha kidato cha nne. Pia mwaka 2011, alipata masomo maalumu ya mwaka mmoja ya ualimu wa Chekechea. Lakini pia amepata fursa ya kusoma nje ya nchi masomo ya Demokrasia na Uongozi nchi ya Denmark mwaka 1997.

Mwalimu Tinka, amekuwa mama mshauri kwa watu wengi. Bwana Kaboko wa Dar-es-Salaam na Profesa Faustine Kamuzola wa Chuo Kikuu cha Mzumbe Morogoro, ni miongoni mwa watu walionufaika na ushauri wa Mwana mama huyu.

Mwana Mama huyu, mbali na ualimu amekuwa kishiriki shughuli mbali mbali katika jamii kama vile siasa na shughuli za kidini. Amekuwa mwanachama wa UWT na aligombea nafasi za Ubunge wa viti maalumu, ingawa hakufanikiwa kuchaguliwa. Hata hivyo aliendelea kujishughulisha na kazi za UWT na CCM.

Kwa upande wa shughuli za kidini, Mwalimu Tinka, alikuwa mwenyekiti wa WAWATA jimbo katoliki la Rulenge, kwa kipindi cha miaka mitatu. Kazi hii aliifanya kwa moyo wake wote na kipindi hicho ndipo alipata nafasi ya kusafiri sana ndani na nje ya nchi.

Ukitoa kichwa chake kuwa na mvi, anaonekana ni kijana! Siri yake ni nini? Anasema ni matokeo ya kutotunza kinyongo rohoni mwake. Amejaliwa karama ya kusamehe! Amekumbana na migogoro mingi katika maisha yake na hasa baada ya kumpoteza mme wake. Waliomsema vibaya, waliomzulia mambo ya uongo, aliwasamehe, hakuweka kinyongo rohoni mwake. Mfano kuna wakati alisingiziwa kumshitaki mwalimu mkuu aliyekuwa amevujisha mtihani wa darasa la saba, mgogoro huu ulikuzwa hadi mtoto wake Victor akapigwa vibaya na kuumizwa na watu wasiojulikana. Ingawa uchunguzi uliweza kubaini waliotendea kitendo hicho  kwa mtoto wake, Mwalimu Tinka, aliwasamehe watu hao.

Hivyo tuna mengi ya kujifunza kutoka kwa Mwana mama huyu anayestaafu kazi  ya ualimu mwezi huu. Amekuwa Mwalimu wa mfano shule zote alizozifundisha, amekuwa ni Mwalimu anayewapenda watoto, kuwajali na kuwashauri, amekuwa mama, mzazi wa mfano kwa kuwalea watoto wake kwa maadili mema, amekuwa ni mjane aliyesimama imara bila kuyumba, kuwakwaza watoto wake na kuikwaza jamii. Bahati nzuri watoto wake hawakumwangusha, anamshukuru Mungu kwa Baraka zake.
Safu hii, inamtakia Mwalimu Theophilda Tinkasimire Tikawa, maisha marefu wakati anapoanza maisha yake ya kustaafu!
Na,
Padri Privatus Karugendo
+255 754 6331 22

0 comments:

Post a Comment