Nani anajali?

MTOTO WA AFRIKA, NI NANI ANAJALI?
 
Kauri mbi ya siku ya mtoto wa Afrika mwaka huu inasema: “Kuondoa Mila zenye kuleta madhara kwa watoto: Ni jukumu letu sote”. Tarehe 16.6.2013, kama kawaida ilikuwa ni siku ya Mtoto wa Afrika .Baadhi ya watu wameikumbuka, lakini inaelekea moto wake unaendelea kupunguka na kubakia ni siku ya watoto wa shule, kukutana na kuimba nyimbo, kucheza ngoma na maigizo. Watu wazima wanaanza kuikwepa siku hii. Jana kwenye taarifa za habari ilionekana asilimia kubwa ya watoto na asilimia ndogo sana ya watu wazima. Pamoja na jitihada za kuikwepa siku hii ukweli unabaki pale pale kwamba yaliyotokea Soweto miaka hiyo yanaweza kutokea tena popote kwenye nchi hizi za Kiafrika na Tanzania ikiwemo. Matendo ya ukiukwaji wa haki za watoto ikiwemo na uporaji wa ardhi yamekuwa mengi. Binafsi nimejenga utamaduni wa kuandika makala kila tunapoikumbuka siku hii ya mtoto wa Afrika. Ninaamini mchago wangu huu unaweza usiwanufaishe watanzania wa leo, lakini kama wasemavyo kwama “Kilichoandikwa kimeandikwa” ni imani yangu kwamba mchango wangu utawanufaisha hata watanzania wa kesho. Na ndiyo maana nimeamua kuuliza katika makala haya: Mtoto wa Afrika, ni nani anajali?
 
Kauri mbiu ya mwaka huu ni mwiba mkubwa kwetu sote. Tuna mfumo gani wa kuondoa mila zenye kuleta madhara kwa watoto wetu? Tuna mfumo gani wa kutokomeza uporaji wa ardhi, tuna mfumo gani wa kuwaambukiza watoto wetu moyo wa uwajibikaji na uzalendo? Tuna mfumo gani wa kujenga mila zenye ustaarabu na kuachana na mila za kishenzi kama zile zinazoanza kujitokeza katika jamii yetu: Watu wanapigwa wanaumizwa na wengine wanauwa, watu wanasingiziwa na kubambikiziwa kesi; wanaotenda matendo haya ya kinyama bado wanaendelea kudunda na kupandishwa vyeo. Tuna mfumo gani wa kuwafundisha watoto wetu kusema ukweli? Kuwa waaminifu, kuacha uchakachuaji, kuacha tabia ya kuuza bidhaa bandia. Tuna mfumo gani wa kufundisha uadilifu? Elimu mbovu ni kujenga mila zenye kuleta maafa! Tumeshuhudia watoto wetu wakishindwa vibaya, tumeshuhudia watoto wetu wakifundishwa kwa kutumia vitabu bandia ambavyo havina viwango: Alimu mbovu ni maafa matupu!
 
Mnamo mwaka 1976, Kule Soweto, Afrika ya kusini, maelfu ya watoto weusi wa shule waliingia mitaani na kufanya maandamano ya zaidi ya nusu kilomita, wakipinga elimu duni waliyokuwa wakiipata na kudai kufundishwa kwa lugha yao. Walifanya maandamano ya amani kwa lengo la kufikisha ujumbe kwa serikali ya makaburu. Ujumbe huu ulikuwa mchungu kwa wakubwa na hawakuwa tayari kuusikiliza. Kama kichaa anavyoweza kutumia bunduki kuua mbu, ndivyo makaburu walivyofanya kwa wanafunzi hao. Mamia ya wasichana na wavulana walipigwa risasi na kupoteza maisha yao.  Kwa vile bunduki inaua mwili, lakini fikra na roho vinaendelea kuishi, maandamano hayo hayakuzimwa kwa risasi! Machafuko yaliyofuatia tukio hili yalipoteza maisha ya mamia ya watu na kuacha majeruhi kadhaa.
 
Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoshuhudia matatizo mengi ya watoto. Tunashuhudia watoto wetu wanavyosukumwa kila siku kwenye daladala, watoto wanavyosoma kwa shida, shule za msingi wengine wanakaa chini, sekondari wanasoma bila kuwa na walimu wa kutosha, matokeo yake  wanafanya vibaya na kushindwa kuendelea na masomo ya juu. Lakini pia na wale wanaofanikiwa kuendelea na masomo ya juu, tunashuhudia wanavyonyanyaswa na Bodi ya mikopo. Tunashuhudia watoto wetu wakikoswa ajira, tunashuhudia watoto wetu wakibugia dawa ya kulevya, wakilewa pombe, wavulana wakisuka nywele na kujifananisha na wasichana, wasichana wakitembea nusu uchi na baadhi ya watoto wetu wakiikimbia nchi kwenda kuishi ughaibuni.  Kwa asilimia kubwa maisha ya mtoto wa Kitanzania, yanakuwa ni ya shida.
 
Binafsi, nimeamua mwaka huu niandike juu ya Mtoto wa Afrika  na uporaji wa ardhi na mtoto wa na elimu mbovu. Kwanini, nimeamua kuandika hivyo: chanzo cha siku ya mtoto wa Afrika, ni maasi yaliyofanywa na watoto wa Soweto, kwa kukataa kunyanyaswa. Walikuwa wakipata elimu duni ukilinganisha na ile ya Wazungu. Pia, walitaka elimu inayotolewa kwa lugha yao. Kule Soweto, watoto walianza kutambua kwamba wale waliokuwa wakifundishwa katika shule nzuri ndio waliokuwa wakipata kazi nzuri na vyeo vya juu katika serikali. Hali ya kutamani hali bora ya maisha kwa siku za mbele, hali ya kutaka kuwa na vyeo na nafasi nzuri za kazi, iliwafanya wanafunzi kukataa elimu duni waliyokuwa wakiipata. Hawakuogopa nguvu za jeshi la Makaburu. Walikuwa tayari kupambana bila silaha – na kweli wengi wao walipoteza maisha. Watoto wa Soweto, walitambua kwamba kujifunza kwa lugha za kigeni wasingepata maarifa yenyewe. Walitaka wafundishwe kwa lugha ya kwao, lugha inayofanana mazingira yao, lugha inayogusa maisha halisi, lugha inayoweza kuharakisha maendeleo. Hoja yangu ni kwamba Bila kuwa waangalifu, inawezekana na sisi hapa Tanzania, tunaandaa Tanzania ya kesho yenye maasi kama ya Soweto.
 
Bila kuwa na elimu nzuri na bora, watoto wetu wakasoma na kupevuka kifikra6/15/2013, tutakuwa tunajiandalia majanga ya Soweto; bila kuwa na ardhi ya kuwarithisha watoto wetu tunakuwa tunaliandalia taifa letu migogoro na majanga ya Soweto.
 
Kumetokea wimbi la uporaji wa ardhi. Watu wenye fedha wananunua ardhi kubwa kwa kisingizio cha kuwekeza. Matokeo yake vijana wengi watajikuta hawana ardhi na wataikataa hali hii. Na tunavyosikia kwenye vyombo vya habari sehemu nyingine hali hii imekataliwa mapema. Tunasikia kule Manyara jinsi watu wanavyovamia mashamba, kukata mazao na kuwashambulia wanao miliki mashamba. Tukio la Tegeta, la kukatana mapanga katika harakati za vijana kufukuzia mbali waporaji wa ardhi, ni la kusikitisha na kutafakarisha; na ni fundisho pia kwamba vijana wakiamua kudai ardhi yao, patachimbika.
 
Mgogoro wa ardhi wa Loliondo, tumeshuhudia jinsi ulivyovuruga amani kwenye maeneo hayo na kupanda mbegu ya maasi na chuki kwa vizazi vijavyo. Mashirika mbali mbali yasiyokuwa kiserikali yamepiga kelele juu ya suala hili la uporaji wa ardhi, lakini kelele hizi zimekuwa kama ile sauti iliayo nyikani. Mashirika haya yamekuwa yakijitahidi kutengeneza majukwaa ya majadiliano, ili watanzania tukae pamoja na kujadiliana juu ya uhai wa taifa letu.
 
Ardhi ni muhimu sana kwa maisha yetu ya leo na vizazi vijavyo; uchumi wetu unategemea kilimo; bila ardhi hatuwezi kulima, hatuwezi kupata chakula na mazao ya kuuza na kujipatia fedha za kigeni. Hivyo ni muhimu sote kusimama pamoja kupinga wimbi hili kubwa la kupora ardhi yetu. Tuhakikishe kila Mtanzania ana ardhi yake ya kutosha na kupiga vita kwa nguvu zote ardhi kuwa mikononi mwa watu wachache.
 
Tunapoikumbuka siku mtoto wa Afrika, ni bora tukazingatia umuhimu wa ardhi kuwa ustawi wa mtoto wa Afrika. Tukiilinda ardhi yetu leo, tunaepusha machafuko ya ardhi kesho na keshokutwa.  Pia tunapoikumbuka siku ya  mtoto wa Afrika ni muhimu sana kutambua elimu  bora kwa watoto wetu italiepusha taifa letu na wimbi kubwa la machafuko. Hivyo basi, Mtoto wa Afrika, ni nani anajali? Ni mimi? Ni wewe, ni yeye? Ni wao au ni sisi sote! Mungu ibariki Tanzania, Mungu wabariki watoto wote wa Afrika.
Na,
Padri  Privatus Karugendo.
+255 754 633122

0 comments:

Post a Comment