Picha ya Urais

SURA YA URAIS INAFANA VIPI NA UWAZIRI JE?

Kama maneno haya yangetamkwa na mtu ninayemdharau, mtu ambaye si mzalendo na akili yake ina kasoro kidogo, nisingepoteza muda wangu kuandika. Kwa vile ni maneno haya yalitamkwa  na mtu ninayemheshimu, tena kijana msomi, ni lazima niandike na kukaripia kwa nguvu zangu zote. Waswahili wanasema tusipoziba ufa tutajenga ukuta. Na kwamba rafiki wa kweli ni yule anayekueleza ukweli. Rafiki mbaya ni yule mnafiki anayekusifia wakati akijua anakudanganya. Labda nianze na swali: Sura ya “Urais” inafanana vipi na sura ya “Uwaziri” inafanana vipi? Je urais ni mashindano ya urembo? Tunaongozwa na sura au tunaongozwa na akili, hekima na busara? Rais wa Kenya, Mheshimiwa Uhuru Kenyatta, alipoulizwa akienda kwenye mahakama kule Holland, nchi ataiongozwa vipi, alijibu kwamba kuna twiter. Je tunahitaji sura ipi ya kutumia twiter? Au tunahitaji sura ipi ya kuweka misingi ya utawala bora, demokrasia na kufuata katiba ya nchi? Ni sura ya namna gani hiyo?
Mheshimiwa Januari Makamba, amesikika akiwahutubia vijana wa CCM kule Misenyi Kagera kwamba, CCM, bado ina nafasi kubwa ya kuliongoza taifa letu, maana akiangaza kwenye vyama vya upinzani haoni mtu yeyote mwenye sura ya Urais na hakuna mtu mwenye sura ya uwaziri. Kwamba vyama vya upinzani ni wanaharakati tu! Hakuna historia ya wanaharakati kuongoza nchi?
Ninajua kwamba Januari ni kada wa chama cha Mapinduzi, na yuko kwenye uongozi wa juu kwenye chama chake hicho, lakini sikutegemea kama angeweza kutoa matamshi kama haya ambayo yanaturudisha nyuma kabisa wakati wa utawala wa kifalme. Enzi ambazo uongozi ulitegemea familia na damu ya watu wateule. Hata kama ungekuwa na akili za kupindukia, bila kuzaliwa kwenye ukoo wa kifalme usingepata nafasi ya uongozi. Lakini leo hii wakati wa demokrasi, wakati wa vyama vingi, wakati wa kuwaingiza viongozi madarakani kwa kura, mtu anaweza kuongea juu ya sura ya Urais na sura ya uwaziri? Huku ni kwenda mbele au ni kurudi nyuma? Haya ni maneno ya kutamkwa na kijana au mzee ambaye anakaribia kumaliza maisha yake hapa duniani?
Tunaweza kusema kwamba labda Mheshimiwa Makamba, alikuwa anatoa vijembe vya kisiasa. Hili linawezekana na wala sina matatizo yoyote , lakini si Makamba, tunayemfahamu. Tunamfahamu Januari Makamba, mtu mwenye busara na hekima, mtu anayepima kila neno analotaka kusema. Mtu ambaye zaidi ya miaka minne, alikuwa msaidizi wa Mheshimiwa Rais  Jakaya Kikwete, akiandaa hotuba zake. Huyu si mtu wa kuropoka tu, ni mtu makini.
Vijembe kama vijembe, sina matatizo navyo. Angesema haoni mtu mwenye uwezo wa kuongoza nchi kwenye vyama vya upinzani, tungecheka tu na kufurahia vijembe  vyake, maana baada ya hotuba yake tungempelekea orodha ndefu ya watanzania wenye uwezo mkubwa kuongoza ambao si wanachama wa CCM, tungempelekea orodha ndefu ya watu wenye busara, hekima na kipaji cha hali ya juu kuongoza hata kwa viwango vya kimataifa. Tatizo langu kubwa ni pale anaposema, upande wa wapinzani haoni mtu mwenye “Sura” ya “Urais” na mwenye “Sura” ya “Uwaziri”. Sura hizi nzuri ziko CCM. Hizi ni sura gani? Maana kama hizo “sura” zinaendana na uongozi, basi Tanzania tungekuwa mbali; tusingekuwa na ufisadi wa kutisha; wimbo wa ufisadi hata mtoto aliyezaliwa leo anaufahamu, hivyo si lazima kutoa mifano
Mtu, tunayemheshimu kama Januari Makamba, akiacha kuona matatizo ya taifa letu, akaacha kuona changamoto ya Katiba, changamoto ya muungano wetu, changamoto ya kufuata na kutekeleza mfumo wa demokrasia katika taifa letu, changamoto ya kuondoa umaskini, changamoto ya kupambana na rushwa na ufisadi, changamoto ya kupambana na bidhaa bandia, changamoto ya kupambana na madawa ya kulevya, changamoto ya kuondoa msemo wa “ Tutawasaka popote walipo na kuwafikisha mbele ya sheria”: Tulisikia hivyo kwa Ulimboka, Kibanda, Mwangosi, Kamanda Barlow,  Mabomu ya Arusha, Mauaji ya Padri wa Zanzibar na Sasa wasichana Wazungu wamemwagiwa tindikali. Hakuna anayekamatwa na kufikishwa mbele ya sheria.. ni misemo ya kutowajibika! “Tutawasaka popote walipo na kuwafikisha mbele ya sheria”. Badala ya  kupambana na kutowajibika na uzembe mwingine katika taifa letu, Januari Makamba, anatwambia “Sura”. Sura inaweza kupambana na changamoto zote hizo hapo juu?
Uongozi ni mashindano ya urembo? Kwamba mtu kabla ya kugombea ahakikishe anajipamba na kujiremba, kujifunza namna ya kutembea na kuongea kwa madaha? Uongozi unategemea sura ya mtu? Kwamba awe na sura nzuri? Kusema kwamba vyama vya upinzani havina mtu mwenye sura ya urais, maana yake hakuna mwenye sura nzuri au sura ya urais inafanana vipi? Uongozi ni sura au ni akili, busara na hekima? Uongozi ni mtu kuwa na fikra pevu au kuwa na sura ya kuvutia?
Tanzania, sasa hivi iko njia panda na tunapita kwenye kipindi cha mpito. Ni wakati ambapo tunahitaji kiongozi mwenye upeo mkubwa, kiongozi mwenye akili nzuri, kiongozi ambaye hafungamani na upande  wowote ule, kiongozi ambaye hafungamani na imani za kidini, kiongozi ambaye hafungamani na “Upuuzi” wa ushabiki wa vyama vya siasa. Tunahitaji kiongozi aliyejikomboa kutoka kwenye minyororo ya ukabila na ukanda. Tunahitaji kiongozi anayeangalia Tanzania kwa umoja wake; kiongozi mzalendo anayeheshimu haki za binadamu na usawa wa kijinsia. Tunahitaji Kiongozi anayeguswa na matatizo ya watanzania wote. Nina mashaka makubwa kama sifa hizo hapo juu zinaendana na sura ya mtu.
Ubaguzi wa hatari kubwa katika dunia yetu hii, ni kuwadhamini watu kwa kuangalia sura zao, kuangalia rangi ya ngozi, kuangalia pua na nywele, ufupi na urefu, unene na wembamba. Leo hii utasema hawana sura ya urais, kesho utasema hawana sura ya “utanzania”, kesho kutwa utasema hawana sura “ukabila” na hasa kabila lako. Na mwisho utasema hawa si wenzetu! Na matokeo yake ni mapambano ya kutisha ambayo sina haja ya kutoa mifano, maana sote tunaifahamu. Ubaguzi wa sura ni hatari na si wa kushabikia. Kama Mheshimiwa Januari Makamba, ni muungwana na analitakia taifa letu mema, asimame na kuomba msamaha kwamba maneno yale kule Misenyi, alimponyoka na ulimi uliteleza. Tutaelewa na kumsamehe, vinginevyo anajiweka kwenye kapu la watu wa kuogopwa katika taifa letu.
Mategemeo makubwa ya taifa letu ni vijana wetu. Lakini kama vijana wenyewe wanaanza kuchanganyikiwa kiasi cha kuchanganya uongozi na sura, badala ya kuuona mnyororo wa uongozi ambao ni akili, hekima, busara na uzalendo, ni hali ya hatari. Ni lazima sote kwa pamoja kushirikiana kuliokoa taifa letu, tukiendeleza ushabiki wa “Kipuuzi” na kuendelea kuamini kwamba kuna watu wateule waliozaliwa kuongoza au kuishi maisha bora zaidi ya wengine, tutaliangamiza taifa letu badala ya kuliokoa.
Na,
Padri Privatus Karugendo

0 comments:

Post a Comment