SAFINA MARIA MAGDALENA JESUS

MWANA MAMA MCHUNGAJI SAFINA MARIA MAGDALENA JESUS.

Leo katika safu yetu ya Mwana Mama, tunawaletea Mchungaji Safina Jesus. Yeye mwenyewe, anapenda ajulikane kwa jina lake kamili ambalo ni: Mchungaji Safina Maria Magdalena Victoria Jesus. Waliomfahamu siku za nyuma na hata alipokuwa akiishi na kufanya kazi nchini Uingereza, walimfahamu kwa jina la Safina Yussaph Haruna. Ni mwana mama aliyekulia kwenye imani ya Ukatoliki, akaingia kwenye imani ya  Uislamu na hatimaye kupokea wito wa kuwa mchungaji na kupokea kipaji cha uponyaji mwaka 2011, akiwa nchini Uingereza. Kwa ufupi ni kwamba ni mama aliyeonja imani zote, Ukristu wa dhehebu mbali mbali na Uislamu.
Hapana shaka kwamba uzoefu wake wa imani hizi zote ndo unamsukuma kuwa na hamu na shauku la kuanzisha nyumba ya ibada, kanisa la watu wote; wenye imani tofauti, maoni tofauti lakini wenye nia na lengo la kujenga jumuiya yenye mshikamano na upendo. Jumuiya yenye maendeleo na heshima kwa binadamu wote bila ubaguzi wa aina yoyote ile.
Mbali na mvuto wa mama huyu kwenye huduma ya uchungaji na uponyaji, ni mapenzi yake kwa watoto yatima. Amejipanga kufungua kituo cha watoto yatima kule Kigamboni, ili watoto hawa wapate elimu ya kuwasaidia kuacha kuzurura mitaani na kuomba omba. Yeye ana imani kwamba haitoshi kumsaidia mtoto Yatima chakula na nguo, maana mahitaji ya kila siku ni lazima yaendelee maisha yake yote; hivyo ni lazima kumsaidia mtoto yatima ili aweze kujisaidia mwenyewe.

KITUO cha watoto yatima kinatarajiwa  kujengwa jijini Dar es Salaam ambacho kitachukua watoto zaidi ya 1000 na kwamba watoto hao watapewa elimu ya ufundi kwa ajili ya kujiandaa na maisha ya kujitegemea na kuachana na kuombaomba
  “Watoto watajifunza kupitia walimu waliobobea ili kuweza kuwa chachu  ya kujiajiri baada ya umri wa kujitegemea na kuongeza nguvu kazi ya taifa. Hatuwezi kuendelea kuhubiri injili wakati watoto wako mitaani, hivyo lazima tuwe na njia mbadala za kuweza kusaidia taifa hili ikiwa ni pamoja na kujenga vituo vya watoto yatima ambao watapata elimu ya kiroho na elimu ya kujitegemea kwa kuwa na ujuzi,” alisema Safina .
Pia anasema alipokuwa nchini Uingereza kiu yake ilikuwa inamtuma kufanya jambo linalohusiana na watoto akiwa nchini Tanzania kwa kujenga kituo ambacho kitakuwa sehemu ya chuo kwa ajili ya watoto yatima na mitaani kupata elimu ya ujuzi mbalimbali.

Mwana mama huyu alizaliwa Iringa mnamo mwaka 1979, Baba yake anatokea Iringa, wakati mama yake anatokea Bukoba. Baada ya masomo yake, alifanya kazi kwenye jiji la Dar-es-Salaam na hasa kwenye sekta ya mahoteli. Baadaye alihamia nchini Uingereza na kuishi kwenye bonde la Bevois na kufanya kazi Bexhill,East Sussex kwenye kanisa la Mtakatifu Barnabas. Ni wakati huo alipoitwa kumtumika Bwana Yesu.
Mama huyu, alipata daraja la uchungaji kutoka kwa Mheshimiwa sana Askofu Mkuu Richard Palmer, wa Episcopal Free Church ya Southampton. Na baada ya kumpatia daraja hilo Askofu Mkuu huyo alisema hivi juu ya Mama huyu: “ Nafurahi sana kuwa na mchungaji huyu kama mtumishi, nafikiri atakuwa mzuri sana, ni mtu aliyejitoa kwa moyo wake wote kwa huduma hii”.
Lengo la mama huyu hapa Tanzania, ni kujenga uhusiano kati ya Kanisa la Mtakatifu Barnabas na Tanzania; kuamusha imani ya kumpenda na kumtumikia bwana Yesu Kristu kwa matendo. Pia ana ndoto za kupanua huduma hii kwenye nchi mbali mbali za Afrika na popote pale ambapo roho mtakatifu atamwelekeza.
Wakati anajiandaa kupata sehemu ya kujenga nyumba ya Ibada, anaendelea kusali na kuhubiri kwenye nyumba yake maeneo ya Kimara. Anawakaribisha watu wa imani zote, maana lengo lake kubwa ni kuijenga jumuiya ya watoto wa Mungu, wanaokutana kusali pamoja na kushirikiana kujenga jumuiya yenye amani na maendeleo.
Mama huyu anapinga mwenendo wa Mashoga na wasagaji; anapinga kwa nguvu zote watu wanaokubali na kukumbatia utamaduni huu, pia anapinga kwa nguvu zote wanaowalaani na kuwatenga mashoga na wasagaji.  Msimamo wake ni kwamba watu hawa pia wanahitaji huruma ya mwenyezi Mungu. Kazi ya jamii si kuwatenga watu hawa na kuwalaani, bali ni kwasikiliza, kusali nao na kutafuta njia ya kuwasaidia na kuwabadilisha. Anatoa ushuhuda wa kuwasaidia baadhi ya watu hawa na sasa wameachana na tabia hiyo. Hivyo nyumba yake ya ibada inawakaribisha wa watu wa aina zote.
Pia Mama huyu ni miongoni mwa wanaoamini kwamba Bwana Yesu, aliliacha kanisa lake mikononi mwa Mwanamke, yaani Maria Magdalena. Biblia inaeleza vizuri kwamba Maria Magdalena, ndiye aliyesifiwa na Bwana Yesu, kuyafahamu mafundisho yake na kuyashika. Ingawa baadaye mfumo dume, uliingia kanisani mnamo mwaka 321 ukiongozwa na Mfalme Constatine wa himaya ya Warumi, na kubadilisha ukweli wote wa kanisa kuachwa mikononi mwa mwanamke. Hivyo anawahimiza wanawake popote walipo kujitokeza kuliongoza kanisa. Wanawake kujitokeza kupokea huduma ya uchungaji na utumishi.
Mambo manne yanamtofautisha mama huyu na wachungaji wengi tuliowazoea: Kwanza ni mtizamo wake juu ya watoto Yatima; lengo lake la kuwasaidia watoto yatima ili baadaye wajisaidie wenyewe ni tofauti na nyumba za watoto yatima tulizozizoea za kuwapatia chakula, malazi, matibabu na wakati mwingine masomo, bila mpango mzima wa kuwaandalia maisha ya baadaye.
Pili, msimamo wake juu ya mashoga na wasagaji ni tofauti kabisa na kauli nyingine ambazo tumezizoea na kuzisikia. Hili la kuwapokea, kuwasikiliza na kuwasaidia kubadilika ni jipya kabisa na ni jambo zuri na la kuungwa mkono na wanaharakati wote wa kutetea haki za binadamu.
Tatu; mpango wake wa kuwashirikisha watu wote wa imani mbali mbali, kusali pamoja na kufanya kazi pamoja, ni muhimu sana hasa wakati huu ambapo dalili za kutoelewana miongoni mwa imani mbali mbali hapa chini linaanza kujitokeza.
Nne, imani yake kwamba Kanisa liliachwa kwenye Uongozi wa mwanamke, ni jambo linalomtofautisha Mwana mama huyu na wachungaji wengine tuliowazoea. Hivyo huyu ni Mwana mama wa mfano kwetu sote. Huyo ndiye Mchungaji Safina Maria Magdalena Victoria Jesus.
Na,
Padri Privatus Karugendo.
+255 754 633122

0 comments:

Post a Comment