TGNP

TGNP NA MPANGO WA UTAFITI SHIRIKISHI WA URAGHABISHI.
 
Katika jitihada zake za kupambana na mfumo dume, uliberali mamboleo na mifumo yote kandamizi na kupambana ili rasilmali ziwanufaishe wanawake walioko Pembezoni, TGNP imeanzisha mpango wa utafiti shirikishi wa uraghabishi. TGNP, imeamua kuukumbatia mpango huu kwa vile unatoa nafasi pana ya ushirikishwaji hadi ngazi ya vijijini na kuchochea kuibua kero na changamoto nyingi ambazo zinahitaji majibu ya jamii nzima.
Mpango huu unatumika kama mbinu muhimu ya kujifunza, kutafakari, kuchambua na kutekeleza mikakati mbali mbali ya ujenzi wa Tapo la ukombozi wa wanawake kimapinduzi lililokita katika ngazi za msingi ya kijamii na lenye uwezo kwa kudai uwajibikaji katika kutoa huduma bora, kusimamia rasilimali za taifa ili ziwanufaishe makundi yaliyoko pembezoni hususani wanawake.
Lengo kuu na mpango huu wa utafiti shirikishi wa uraghabishi ni kuwezesha ushiriki wa wanawake, wanaume, makundi na mitandao katika ngazi ya jamii kufanya uchambuzi wa hali halisi kwa mrengo wa ukombozi wa wanawake kimapinduzi; kuibua kero na changamoto zinazokabili makundi husika  na za pamoja. Mpango huu pia unalenga katika kukuza uwezo na uelewa wa  uchambuzi wa kero zinazoikabili jamii.
Tamko la TGNP kwa vyombo vya habari lilitolewa tarehe 9.6.2013 ni la mpango huu ulioendeshwa kwenye wilaya tatu za Mbeya vijijini, kata ya Mshewe, Morogoro vijijini Kisaki na Kishapu – Shinyanga. Katika makala hii tutajadili mrejesho wa utafiti huu ambao ni wa aina yake.
Changamoto za uwekezaji na mgawanyo mbaya wa ardhi kwa wananchi, ilijitokeza katika utafiti huu na mfano mzuri ni Kata ya Mshewe Mbeya vijijini. Katika kata hii utafiti ulibaini mgawanyo mbaya wa ardhi kwa wawekezaji; ardhi nzuri na yenye rutuba imetolewa kwa wawekezaji kiasi kwamba wenyeji hawana mashamba na wanalazimika kuwa vibarua kwenye mashamba ya wawekezaji. Mbaya zaidi ni kwamba wawekezaji wenyewe wanawalipa kidogo. Mfano wanawake wanalipwa kati ya shilingi 2,500 hadi elfu3 kwa siku. Pamoja na kulikwa kidogo, wanakumbana na rushwa ya ngono na manyanyaso mengine hali inayosababisha ongezeko la magonjwa ambukikizi yakiwemo VVU na Ukimwi.
Changamoto hii ya mgawanyo mbaya wa ardhi imejitokeza pia katika kata ya Kisaki, Morogoro mjini, ambapo wakulima wadogo wadogo wanapambana na wafugaji. Kwa vile wafugaji hawana maeneo ya kutosha kwa mifugo yao, wanaingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima na kuleta vita mbaya. Kwa upande mwingine wafugaji wanatumia fedha kuwahonga viongozi ili wasisumbuliwe wanapoingiza mifugo kwenye mashamba ya wakulima. Matumizi ya fedha ni kupokonya wanyonge haki zao ni tatizo sugu kwa wananchi waishio pembezoni.
Suala jingine muhimu lililojitokeza kwenye utafiti huu wa TGNP kwenye wilaya tatu, ni upatikanaji wa maji safi na salama. Pamoja na sera ya taifa kwamba maji yawe umbali wa mita 400 kutoka kwa makazi ya watu, bado maeneo mengi hapa Tanzania yana tatizo kubwa la kupata maji safi na salama. Watu wa Kishapu na  Mshewe, ni miongoni mwa wananchi wa Tanzania ambao bado wana tatizo hili kubwa. Kijiji cha  Ilota- Mshewe, wananchi wanalazimika kuchangia maji machafu na mifugo. Tatizo hili la maji sai na salama ni kubwa sana katika vijiji vya Isoso na Lubaga katika kata ya Kishappu, wanawake wanatembea mwemdo mrefu na katika mazingira hatarishi kutafuta maji; mazingira haya yanasababisha mimba za utotoni, ubakaji na vipigo kwa wanawake wakichelewa kutoka kuchota maji. Na nyongeza ni kwamba muda mwingi na rasilmali vinatumika kusaka maji kitu kinachoongeza hali ya umasikini katika jamii ya watu hawa Kishapu.
Ukosefu wa huduma bora za afya ni suala jingine lililoibuliwa na mpango wa utafiti shirikishi wa uraghabishi. Mfano kati  ya wanawake 20 walihojiwa katika kijiji cha Ilota, Mbeya vijijini ni mwanamke mmoja tu ndiye aliyetaja kujifungulia hospitali. Umbali wa hospitali na vituo vya afya unawalazimisha wanawake wengi kuzalia nyumbani kwa wakunga wa jadi. Hii ni hatari kwa mama na mtoto na kuna ukweli wa wanawake wengi kupoteza maisha wakati wa kujifungua na watoto kutopata huduma muhimu za chanjo wakiwa na umri chini ya miaka 5.
Kata ya Kisaki Morogoro vijijini, tatizo si hospitali wala kituo cha afya, tatizo ni dawa na wahudumu wa afya katika vijijini vya Gomero, Station na Nyarutanga. Vijiji hivi vina majengo mazuri, lakini hakuna dawa na wahudumu. Mbali na tatizo hilo, pia inapobidi wananchi wanachangia gari la wagonjwa silingi 70,000, ili kumpeleka mama mja mzito kwenye hospitali ya Mkoa Morogoro mjini. Hali hii ni hatari, maana wanawake wengi wanaweza kupoteza maisha yao kwa kushindwa kulipia hizo shilingi elfu 70,000.
Ukiachia masuala hayo yaliyotajwa hapo juu, utafiti huu wa TGNP, ulibaini kwamba tatizo la msingi ni uongozi mbovu na rushwa. Hili lilitajwa kila sehemu iliyofanyiwa utafiti. Kwamba uongozi mbovu na rushwa vinasababisha ukosefu wa huduma za msingi kwa wanawake na wanaume walioko pembezoni. Na kwamba kuna usiri wa taarifa za mapato na matumizi, viongozi kutowashirikisha wananchi katika masuala ya maendeleo, viongozi ngazi za vijiji kuruhusu video za ngono na viongozi kutotekeleza ahadi zao kwa wananchi.
Ni mengi yaliyojitokeza kwenye utafiti huu, ila yametajwa machache ili kufikisha ujumbe kwa wahusika, ili wajaribu kutafuta majibu ya kuondoa unyanyasaji wa wanawake na wasichana katika wilaya hizi zilizotembelewa na watafiti wa TGNP pamoja na maeneo mengine ndani ya taifa letu. Mfano tatizo la maji linasababisha vipigo kwa wanawake, ubakaji, elimu duni kwa wasichana, mimba za utotoni na ukosefu wa kipato.
Serikali kuu na serikali za mitaa zinaweza kuyatumia matokeo ya utafiti huu kurekebisha matatizo yaliyoorodheshwa hapo juu: Mfano serikali kuirejesha ardhi ya Kata ya Mshewe inayomilikiwa na wawekezaji wa n nje na ndani ya nchi, kwa manufaa ya wananchi sasa na vizazi vijavyo. Pia serikali itenge maeneo ya wafugaji katika kata ya Kisaki, ili kuepesha mapigano kati ya wakulima na wafugaji.
Huduma ya kupatikana maji safi na salama ishughulikiwe katika vijiji vilivyotajwa na ambavyo havikutajwa. Utafiti huu umeonyesha wazi kwamba maji safi na salama ni muhimu kwa watanzania wote. Huduma ya hospitali pia nayo iboreshwe. Pia ni muhimu kuwepo na mfumo wa kuwawajibisha viongozi wote wanaokiuka maadili ya kazi zao ili kuondokana na aina zote za rusha na ukatili wa kijinsia hasa ukatili kwa wanawake na wasichana.
Lakini pia viongozi wawakilishi hususan madiwani na wabunge wanaweza kutumia matokeo ya utafiti kudai uwajibikaji wa serikali kwa wananchi katika ngazi zote kupita bajeti, ripoti ya mkaguzi wa serikali, kudai sera ya haki ya uhuru wa wananchi na mikakati mbali mbali ya maendeleo.
Vyombo vya habari, taasisi za utafiti na makundi ya kiraia yanaweza pia kuutumia mpango huu wa utafiti shirikishi wa uraghabishi kuibua masuala ya wanajamii na kujenga uwezo wa wanajamii kuhoji na kudai uwajibikaji. Hapana shaka kwamba mpango huu wa utafiti shirikishi na uraghabishi ndio unafaa kabisa kubainisha chanzo cha vurugu za Mtwara. Mpango huu unamruhusu kila mshiriki kuzungumza bila kuogopa na kwa njia hii ya uraghabishi, watu wanajifunua na kujiweka wazi.
Na,
Padri Privatus Karugendo.
+255 754 633122
www.karugendo.net

0 comments:

Post a Comment