Tujifunze kutoka kwa Mandela



TUJIFUNZE KUTOKA KWA MZEE MANDELA

Wakati dunia nzima inaendelea kumwombea Mzee Mandela, apate afya njema na kupona ugonjwa uliomlaza kitandani zaidi ya majuma mawili sasa, ni lazima watanzania tujifunze kutoka kwake. Mzee Nelson Mandela, ni kati ya watu wachache waliofanikiwa kuyaishi na kuyashika mafundisho magumu. Mafundisho ambayo waliowengi tunayaita ndoto, lakini tunayafundisha na kuwahimiza watu wengine wayashike na kuyafuata.Alipohukumiwa kifungo cha maisha,Mzee Mandela, alipokea hukumu hiyo bila ya woga, ni kitu alichokifahamu hata kabla ya kuanza mapambano na serikali ya makaburu. Alifahamu nguvu na uwezo wa serikali ya makaburu. Alijua walivyokuwa wameshikilia vyombo vya dola na silaha nzito nzito, alijua angekamatwa na kufungwa au kuuawa.Pamoja na kuyajua yote hayo aliamua kuendelea kupambana na makaburu kwa vile alitanguliza uhai wa taifa lake na wala si uhai wa maisha yake binafsi. Lakini pia alijua jinsi nguvu na uwezo wa makaburu vilivyokuwa vinaishia kwenye kuutesa mwili wake bila ya kuwa na uwezo wa kuigusa roho yake hata hivyo mafundisho magumu ambayo roho yake haikuwa na uwezo wa kuyakwepa yalikuwa mbele ya macho yake:
 “ Msiwaogope wale wauao mwili lakini hawawezi kuiua roho. Afadhali zaidi kumwogopa yule awezaye kuuangamiza mwili pamoja na roho..” (Matayo 5:28).
Makaburu waliutesa mwili wa mzee Mandela, alifanyishwa kazi za suluba,alidhalilishwa,alipokonywa uhuru wake,alinyimwa uhuru wa kuwa na familia yake,alinyimwa uhuru wa mawasiliano, alipofiwa na mtoto wake wa kiume, alinyimwa ruhusa ya kuhudhuria mazishi yake. Unyama wote aliofanyiwa akiwa gerezani uliugusa na kuutesa kwa kiasi kikubwa mwili wake tu,lakini roho yake ilibaki madhubuti. Alipochaguliwa kuwa Rais wa kwanza mwafrika wa Afrika ya kusini huru, Mandela, alimshangaza kila mtu pale alipowakumbatia adui zake na kukaa nao meza moja ya chakula. Hakulipiza kisasi! Unyama aliotendewa gerezani,haukuigusa roho yake! Mzee Mandela, amekuwa mwalimu wa kuwafundisha watu kuishi na kuyashika mafundisho magumu, mambo ambayo tumezoea kuyaita ndoto.Watanzania tuna utamaduni wa kuogopa mwenye nguvu na uwezo wa kuua mwili.Pia tuna utamaduni wa kulipa kisasi, wawe ni viongozi wa dini au viongozi wa serikali,tabia hii ipo. Tujifunze kwa Mzee Mandela: Mwili unateswa, unanyanyaswa na kudhalilishwa na mwanadamu, lakini roho ya ukweli, amani na wema viko juu ya uwezo wa mwandamu! Hakuna mwanadamu mwenye uwezo wa kuiua roho ya wema, hata kama mtu huyo angekuwa na nguvu za kidunia kama za Amerika!Pia tujifunze kwamba ukipambana na mtu, ukimshinda, mnashikana mikono na kukumbatiana – si kujenga chuki wala uhasama!

 Watu wanaouona mwanga huu wameanza kugundua kwamba yale tunayoita mafundisho magumu na ndoto yanawezekana, Mzee Mandela, ametuonyesha mfano:
Mmesikia kwamba ilisemwa: ‘Jicho kwa jicho, jino kwa jino’. Lakini mimi nawaambieni, usimlipize kisasi mtu mbaya. Mtu akikupiga kofi shavu la kulia, mgeuzie pia shavu la pili..” (Matayo 5:38-39).
 Haya ni mafundisho magumu ambayo yamewashinda watu wengi hata na wale walioyafundisha na kuyaeneza. Hadi leo hii hata viongozi wa dini bado mafundisho haya yanawapatia shida. Bado wanashikilia ‘Jicho kwa jicho, na jino kwa jino’. Migogoro inayowakumba viongozi  wa dini inasababishwa na kutokubali kupigwa shavu la kulia, na kugeuza la kushoto. Wakipigwa kofi, wanarudisha. Hii inavuruga amani na kuleta magomvi yasiyoisha. Mandela, hakurudisha kofi! Alisamehe! Mafundisho magumu yalikuwa mbele ya macho yake na roho yake iliyoandaliwa kwa umakini na kwa miaka mingi haikuwa na uwezo wa kuyakwepa:
Mmesikia kwama ilisemwa:  ‘Utampenda jirani yako, lakini utamchukukia adui yako.’ Lakini mimi nawaambieni,wapendeni maadui wenu na kuwaombea wale wanaowadhulumu ninyi…” ( Matayo  5:43-44).

Tunakumbuka jinsi Mzee Mandela, alivyowashauri wamarekani:  “Tumejifunza jinsi ya kuishi na maadui zetu, nanyinyi mjifunze kuishi na maadui zenu..”

Tume ya maridhiano ya Afrika ya Kusini, ilifanya kazi kwa uhuru na kumsikiliza kila mtu. Haikuwa na upendeleo wala kukikumbatia chama tawala. Haki ilitendeka kwa kila mwanachi na watu wote walifurahia kazi yake.Hizo zilikuwa mbinu za Mzee Mandela, za kukumbatia mafundisho magumu ya kumpenda adui.

 Mzee Mandela, alipompoteza mtoto wake wa kiume kwa ugonjwa wa UKIMWI, kwa masikitiko makubwa(maana huyu ndo mtoto pekee wa kiume aliyekuwa amebakia) alitangaza wazi mbele ya vyombo vya habari bila aibu kwamba mtoto wake alikufa kutokana na ugonjwa wa UKIMWI. Hapa pia mafundisho magumu ambayo roho yake haikuwa na uwezo wa kuyakwepa yalikuwa mbele ya macho yake:
Jihadharini na chachu ya Wafarisayo, yaani unafiki. Kila kilichofunikwa kitafunuliwa, na kila siri itajulikana. Kwa hiyo, kila mlichosema gizani, watu watakisikia katika mwanga, na kila mlichonong’ona, faraghani,milango imefungwa,kitatangazwa juu ya nyumba.” (Luka 12:1-3).
Hili limekuwa fundisho jingine kutoka kwa Mzee Mandela, la mafundisho magumu ambayo wengi wetu na hasa Barani Afrika, kusini mwa jangwa la Sahara, tumekuwa tukidhani ni ndoto. Tumezoea kusikia watu mashuhuri wakifa kutokana na shinikizo la damu,kisukari, ugonjwa wa muda mrefu na ugonjwa wa ghafla nk. Ni nadra kusikia mtu mashuhuri amekufa kwa UKIMWI. Ugonjwa huu, umezungukwa na unafiki mkubwa.Ndo maana ugonjwa huu umekuwa wa hatari katika nchi zetu hizi masikini. Ugonjwa unafichwa na unafiki unaendelea kutawala.Hawa watu mashuhuri wanaokufa kwa shinikizo la damu wanatoa mwanya wa wenzi wao kuendelea kusambaza virusi vya UKIMWI, hakuna anayeshughulika kuchukua tahadhari maana shinikizo la damu si ugonjwa wa kutisha kama UKIMWI!! Matokeo yake ni janga kama tunavyoendelea kushuhudia. Ni lazima tumpongeze Mzee Mandela, kwa ujasiri wake na tuendee kujifunza kutoka kwake.

Mzee Mandela, alipougua ugonjwa wa saratani ya kibofu cha mkojo, alitangaza wazi. Hakuficha ugonjwa wake.Alipatiwa matibabu, na sasa anaendelea kuishi! Hapa Tanzania, tumewapoteza watu wengi kwa ugonjwa huu kwasababu ya aibu na unafiki! Pia watu wanakufa kwa kuficha magonjwa ya zinaa yanayotibika kwasababu ya aibu na unafiki. Magonjwa yakigusa sehemu za siri, watu wanakuwa na aibu.Aibu hii inatokana na mawazo ya kulichukulia tendo la ngono kama la aibu. Ingawa kuna ukweli kwamba si magonjwa yote yanayozishambulia sehemu za siri yanasababishwa na tendo la ngono. Baadhi ya watu wakiugua sehemu za siri, wanataja kichwa,tumbo na mgongo. Madaktari wanatibu kichwa,tumbo na mgongo, kumbe mgojwa ana saratani ya kibofu cha mkojo au magonjwa mengine ya zinaa. Inapotokea bahati ya kuugundua ugonjwa,mgonjwa anakuwa amezidiwa na kufa! Aibu na unafiki vinasababisha vifo visivyokuwa vya lazima katika taifa letu na katika nchi nyingine za Kiafrika.


                                                                                 
Lengo la makala hii ni kuonyesha jinsi tulivyo na mambo mengi ya kujifunza kutoka kwa Mzee Mandela. Bahati mbaya viongozi wetu wa dini na serikali ni woga. Hatujapata viongozi wa kuyashika na kuyaiishi mafundisho magumu kama alivyofanya Mzee Mandela. Hatujapata viongozi wasiogopa macho na masikio ya watu, viongozi wasiojali kudhalilishwa na ikibidi kuupoteza uhai wao katika harakati za kutetea ukweli na kupingana na unafiki.

Tunapojifunza kutoka kwa Mzee Mandela, ni lazima tumwangalie yeye na historia yake. Si kwamba misimamo yake hii ya kuishi na kuyashika mafundisho magumu, ilimnyeshea kama mvua. Ni mtu aliyefanya  maandalizi, ni mtu aliyeitafuta elimu akiwa na malengo katika maisha yake – hakusoma tu kwa vile kusoma ni lazima – hakusoma kuishinda maitihani, bali alisoma kwa vile alikuwa na lengo la kuikomboa nchi yake. Lengo hili lilijaa kwenye roho
yake. Hata ungeupiga na kuumiza mwili wake, usingeliligusa lengo lililokuwa kwenye roho yake.Alijiandaa kwa maamuzi magumu –alijua jinsi njia ya kulifikia lengo lake ni kupitia kwenye maamuzi magumu. Alijifunza na kujiandaa kulitanguliza taifa lake kwa kila kitu. Hakuaangalia tumbo lake,cheo chake au biashara yake (mambo ya mwili) aliangalia uhai wa taifa zima(mambo ya kiroho) . Mungu amsaidie, hata uhai wake ukiondoka, tutaendelea kuishi na roho yake.
Na,

0 comments:

Post a Comment