AFRICARE NA MCHANGO WAKE TANZANIA 5

AFRICARE NA MCHANGO WAKE KATIKA JAMII: TANZANIA.( 5)

Baada ya kuzunguka katika mikoa yote sita, jibu nililolipata, si la ni nani alichagua mikoa, wilaya na vijiji kwa vigezo gani; bali kwa mtizamo binafsi, ni kwamba vijiji vyote vitakavyonufaika na mpango huu wa kusogeza huduma ya umeme vimesheheni madini na rasilimali nyingi. Ardhi ya vijiji hivi ina rutuba na nzuri kwa uwekezaji wa kilimo, uwindaji, utalii na viwanda. Kwa maana hiyo inawezekana Wamarekani wenyewe walipendekeza ni mikoa ipi inufaike na huduma hiyo kwa malengo yao binafsi? Kwa kujua na kutambua faida watakayoipata kutoka kwenye mikoa hiyo pindi ikiwa na huduma ya umeme? Wakapendekeza na serikali yetu ikakubali? Au serikali yetu ilikubali kwa vigezo? Ni vipi hivyo? Nasubiri jibu!

Mfano, wilaya ya Morogoro vijijini, Kata ya Matombo, itanufaika na huduma hii ya umeme. Kata ya Matombo, inajulikana kwa uzalishaji wa matunda na mazao mengine mengi. Inaaminika kwamba msitu wa asili ya Kimboza umesheheni madini ya kila aina. Njia ya kwenda Matombo ni njia ya utalii na kuna uwezekano wa kuipanua njia hii kwa siku za usoni. Je, inawezekana mfuko wa changamoto za milenia unatumika kutengeneza miundombinu ya wawekezaji kutoka Amerika? Wakija kuwekeza wakute umeme? Kwao iwe ni rahisi kuvuta na kuutumia jinsi watakavyo? Ni msaada au ni upole wa njiwa na ujanja wa nyoka?

Dodoma, itanufaika na mradi huu! Sote tunajua kwamba Mkoa huu umesheheni madini muhimu sana. Wilaya ya Mpwapwa tayari ina machimbo yanayoendelea. Inawezekana zoezi zima la kusogeza umeme vijijini ni kuandaa miundombinu ya wawekezaji? Katika vijiji vya Tubugwe na Hogoro, wilaya ya Kongwa, asilimia tisini (90) ya wanavijiji walisema hawana uwezo wa kuuvuta umeme kuingiza kwenye nyumba zao. Mradi wa kuziboresha nyumba zao ungekuwa muhimu zaidi ya umeme. Na wale waliosema wanaweza kuuvuta, hawakuwa na uhakika wa kulipa bili kila mwezi.
Wilaya ya Geita, vijiji vingi vyenye machimbo ya dhahabu vitanufaika na mradi huu. Nyumba nyingi za wananchi hazina ubora wa kuunganisha umeme. Ni wazi huduma hii imewalenga wawekezaji zaidi ya wananchi. Geita, wana shida ya maji- wangepata mradi wa maji watu wengi wangepata huduma hii; Geita wana shida ya barabara; wanawake wajawazito wanapoteza maisha wakiwa njiani kwenda hospitali, usafiri ni shida; wanapanda pikipiki za Mchina ambazo si salama kwa maisha yao. Hoja hapa ni kwamba umeme itakuwa huduma ya wachache ambavyo maji na Ifakara, nao wako katika mpango huu.

Ni wazi nilipofika Ifakara, nilifikiri watu hawa wanaihitaji daraja la Mto Kilombero, zaidi ya umeme! Nina imani wangeshirikishwa, wangechagua daraja badala ya umeme! Mbali na ajali za kivuko zinazotokea mara kwa mara na kupoteza maisha ya watu, inashangaza kuona miaka hamsini baada ya uhuru, Tanzania imeshindwa kujenga daraja la kuiunganisha Ifakara na Mahenge. Upana wa mto pale kivuko kilipo ni mita hamsini au sabini! Kwa nini tushindwe kujenga daraja? Shughuli zinazofanyika kwenye kivuko hicho, mazao yanayovushwa na rasilimali nyingine zinazovuka kutoka Mahenge kwenda Ifakara na kwingineko ni nyingi kiasi cha kuhitaji daraja. Pato la Mahenge na Ifakara katika mfuko wa Taifa, linatosheleza kujenga daraja.

Kilombero, kijiji cha Kidogobasi, watanufaika na mradi huu. Inajulikana jinsi bonde la mto Kilombero lilivyo muhimu kwa kilimo cha miwa, mpunga na mahindi. Kiwanda cha sukari cha Kilombero, kinahitaji uwekezaji zaidi. Inawezekana kwamba Wamarekani wanaandaa miundombinu ya kuwekeza Kilombero siku za usoni? Kama wao ndo walipendekeza mikoa ya kuihudumia, basi watakuwa na lao jambo, kama ni serikali ilipendekeza; tuelelezwe vigezo maana kuma mikoa mingine ya Tanzania imeachwa nyuma kwenye huduma ya umeme na iko nje ya mpango huu wa mfuko wa milenia.

Lushoto na Makete, nao watanufaika na mradi huu. Mtu yeyote anayezifahamu vizuri wilaya hizi, atakubaliana na mimi kwamba hizi ni wilaya zenye maeneo mengi ya uwekezaji; kilimo, madini, makazi na utalii. Uwezekano wa Wamarekani kuwaandalia miundombinu watu wao kuja kuwekeza Tanzania ni mkubwa kuliko msaada wao kwa watu wa Lushoto na Makete.

Ni wazi umeme ni muhimu katika maendeleo, na Tanzania tunahitaji huduma hii; hoja hapa ni kwamba kuna mambo mengine ambayo ni muhimu zaidi, kama daraja, barabara, nyumba bora, kilimo cha uhakika kama vile umwagiliaji. Vijijini uchumi wao unategemea kilimo, bila maji ya uhakika hawawezi kuzalisha kiasi cha kumudu maisha kama kulipa bili za umeme. Kama mfuko wa changamoto za milenia, unakuja kama msaada, basi ungeangalia kwanza njia za kuinua uchumi wa watu wa vijijini ili wawe katika hali na uwezo wa kutumia umeme.

Tulipowahoji wenye uwezo wa kutumia umeme kule vijijini, mbali na mwanga walitaja kufanya biashara ya kucharge simu, kuonyesha video, kusaga nafaka na saloni za nywele. Hawafikirii zaidi ya hapo, hawana mawazo ya viwanda, kutumia umeme kusukuma maji ya kumwagilia katika mashamba yao na mambo mengine ya uzalishaji.


Haiwezekani Wamarekani wakatusaidia sisi bila wao kuwa na malengo yao; ni wapole kama njiwa, lakini wajanja kama nyoka. Wito wangu ni kwamba na sisi tusipokee msaada bila kuwa na malengo yetu; wao wanasogeza umeme kwenye maeneo yenye madini na yenye uwezekano wa kuwekeza kwenye mambo mbali mbali; hawana mpango wa kuanzisha vyanzo vipya vya kuzalisha umeme; basi sisi tuanze mkakati wa kusambaza umeme vijijini na kutoa elimu juu ya matumizi ya umeme sambamba na kuanzisha vyanzo vipya ya kuzalisha umeme. Kwa njia hii Wamarekani watanufaika na sisi tutavuna vya kutosha!

Nimalizie makala hii ndefu kwa kuwashukuru tena AFRICARE kwa mchango wao na kuwahimiza waendelee kutusaidia na hasa kuwawezesha watafiti, waandishi na watu wenye nia njema kuitembelea mikoa mbali mbali na kujifunza mengi.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

AFRICARE NA MCHANGO WAKE TANZANIA 4

AFRICARE NA MCHANGO WAKE KATIKA JAMII: TANZANIA.( 4 )

MIRADI YA CHANGAMOTO ZA MILENIA.

Kama ilivyodokezwa mwanzoni mwa makala hii ndefu, ni kwamba mwandishi wa makala hii ameshiriki katika miradi miwili ya AFRICARE, mradi wa Huduma Majumbani na Mradi wa Kusogeza huduma ya Umeme vijijini. Makala zilizotangulia zilielezea mradi wa huduma majumbani, na hizi zinazofuata sasa zitajikita juu ya mradi wa kusogeza huduma ya Umeme vijijini.

AFRICARE, inaratibu mradi huu wa kusogeza huduma ya umeme vijijini. Sasa hivi mradi huu umefikia hatua ya kuandaa fidia kwa wanavijiji watakaopisha njia ya umeme. Kama nilivyofanya kwenye makala zilizotangulia, sitafafanua undani wa mradi huu, hiyo ni kazi AFRICARE. Kinachofanyika hapa ni maelezo ya mwandishi aliyebahatika kushiriki hatua hii ya kuandaa fidia kwa wananchi watakaopisha njia ya umeme. Hatua hii ilimwezesha mwandishi kuzunguka kwenye mikoa sita ya Mwanza, Mbeya, Iringa, Tanga, Morogoro na Dodoma. Fursa hii ilimwezesha mwandishi kuhojiana na wanavijiji wengi na kujionea mwenyewe maisha halisi ya kule vijijini.

AFRICARE, ilimwangalia mwandishi kama kibarua wa kawaida aliyekuwa akishirikiana na wengine kutekeleza uratibu wa AFRICARE, mwandishi kwa upande wake aliichukulia fursa hii kama wakati mzuri wa kutafiti na kuandika baadhi ya mambo ambayo mara nyingi vyombo vya habari havitangazi wala kuandika. Na pia ni kutusaidia kutafakari juu ya misaada hii tunayopewa: Je ni misaada? Je, nani anaamua ni wapi pa kuipeleka hiyo misaada? Mradi wa kusogeza umeme uko kwenye mikoa sita ya Tanzania; je nani aliichagua mikoa hii? Haya ni maswali muhimu ya kutusaidia kutafakari na kuchochea uelewa wetu juu ya misaada hii inayotoka kwenye nchi zilizoendelea.

Miradi ya changamoto za milenia kwa walio wengi na hasa mijini (wasomi na waelewa) inajulikana kama Miradi ya Bush au fedha za Wamarekani. Miradi hii ni ya Barabara, maji, Afya, Elimu, umeme nk. Kiasi kikubwa miradi hii iko katika hatua za utekelezwaji. Vijijini miradi hii inajulikana kama miradi ya Mheshimiwa Jakaya Kikwete, maana wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa 2010 aliahidi vitu vingi ambavyo alijua kwa uhakika vitatekelezwa na mfuko wa miradi ya changamoto za Milenia. Washabiki wa CCM, wanaamini miradi hii ni utekelezaji wa Sera nzuri za chama chao.

Vyovyote vile, ni imani yetu kwamba miradi hii ikikamilika itawanufaisha watanzania wote? Na la muhimu ni kuangalia mbali zaidi; miradi hii ni misaada! Je katika dunia hii kuna msaada wa bure? Kuna mtu anatoa msaada bila ya malengo? Kwa nini mtu akusaidie wakati dola yake inapanda na shilingi yako inazama? Kama ana nia ya msaada kwa nini asihakikishe dola na shilingi vinapanda na kushuka wakati mmoja? Si hoja ya au ushawishi wa kuikataa misaada, ni namna ya kuingiza wazo la kuwa mpole kama Njiwa na mjanja kama nyoka. Tatizo letu kubwa hapa Tanzania na nchi nyingi za dunia ya tatu (AFRIKA) ni kufumbwa macho na upole wa njiwa. Anayeleta msaada ana lengo lake hivyo ni muhimu anayepokea msaada awe na matumaini na malengo ya muda mrefu pia! Bila kuumizana, anayetoa na anayepokea wanufaike sawa au kwa kupishana kidogo.

Katika makala hii nitajadili Mradi wa Kukarabati na uwekaji wa miundombinu mipya ya kusafirisha umeme katika baadhi ya mikoa ya Tanzania Bara na visiwani. Mradi huu ni wa kusogeza huduma ya umeme kwa wananchi. Hapa kuna maneno mawili ya kuangalia kwa umakini; Kusogeza na Kusambaza. Kitakachofanyika katika mradi huu, ni kusogeza umeme kwa wananchi. Maana yake ni kwamba kama umeme ulikuwa kilomita zaidi ya miamoja kutoka kijiji cha Nyambeba wilaya ya Sengerema, sasa umeme huu utakuwa ndani ya kijiji cha Nyambeba na kazi ya kuusambaza nyumba hadi nyingine itatekelezwa ama na serikali au wananchi wenyewe.

Kama nilivyosema mwanzoni, mradi huu unatekelezwa na Mfuko wa changamoto za Milenia (Fedha za Bush) na kuratibiwa na shirika lisilokuwa la kiserikali la AFRICARE, ambalo nalo pia ni shirika la Wamarekani. Nimebahatika kufanya kazi na AFRICARE katika baadhi ya miradi yao mfano ule wa Kaya, unaotekelezwa katika Mikoa ya Manyara na Mara na sasa huu wa kusogeza huduma ya umeme kwa wananchi.

Tanzania bara, mradi huu utatekelezwa katika mikoa sita; Tanga, Morogoro, Mbeya, Iringa, Dodoma na Mwanza. Na sasa hivi ninapoandika makala hii mradi huu umefikia hatua ya kuandaa fidia kwa mali za wananchi zitakazoadhiriwa na mradi huu wa kukarabati na uwekaji wa miundombinu mipya ya kusafirisha umeme. Wananchi ambao mazao yao yataguswa na njia ya umeme, watalipwa fidia na wale ambao nyumba zao zitabomolewa watalipwa fidia au watajengewa nyumba nyingine.

Nilijaribu kufafanua tofauti kati ya kusogeza na kusambaza. Nikitaka kulenga kwa umuhimu wa huduma hii ya umeme, ingawa kusogeza huduma ya umeme ni muhimu, lakini pia kusambaza ni muhimu zaidi maana kama tutakavyoona ni kwamba wananchi wengi (zaidi ya azilimia 90) kule vijijini hawana uwezo wa kuvuta umeme. Aina maana kwamba huduma zote hizi za kusogeza na kusambaza zifanywe na mfuko wa changamoto za Milenia, shirika jingine au taasisi nyingine inaweza kujitokeza kufanya kazi ya kusambaza umeme vijijini, lakini ni lazima pia serikali ifikirie haraka mkakati wa kusambaza umeme vijijini. Na jambo jingine ambalo ni lazima liwe wazi kwa msomaji wa makala hii ni kwamba mradi huu hautengenezi vyanzo vipya vya kuzalisha umeme bali utatumia vyanzo vilele. Umeme wetu tuliouzoea ambao kila mwaka tunakuwa na tatizo la mgawo, ndo huo huo mfuko wa changamoto za milenia, utausogeza kwenye vijiji katika mikoa sita ya Tanzania Bara na visiwani. Labda, msaada huu ungeelekezwa zaidi katika kutengeneza vyanzo vipya vya umeme?

Nimezungukia mikoa yote sita na kupitia karibia vijiji vyote vitakavyonufaika na mradi huu. Swali langu kubwa kama mchambuzi wa maswala ya kijamii ni: Ni vigezo gani vilitumika kuichagua mikoa hii sita kunufaika na mradi huu? Je ni serikali ya Tanzania iliichagua mikoa hii (kwa vigezo gani?) au Wamarekani wenyewe waliichagua mikoa hii? Na je mikoa yenyewe ilitumia vigezo gani kuchagua wilaya, maana si wilaya zote katika kila mkoa zitapata huduma hii; na Wilaya zilitumia vigezo gani kuchagua vijiji, maana si vijiji vyote katika wilaya vitapata huduma hii. Hili ni swali la uchokonozi, lakini nafikiri ni muhimu katika mkakati mzima wa kuwa wapole kama njiwa na wajanja kama nyoka...... itaendelea.


Na,
Padri Privatus Karugendo.

AFRICARE NA MCHANGO WAKE TANZANIA 3

AFRICARE NA MCHANGO WAKE KATIKA JAMII: TANZANIA.( 3)

Baadhi ya vituo vya afya viko mbali na walengwa. Hii ni changamoto kubwa kwa wahudumu wa huduma majumbani. Lakini pia kuna swala zima na dawa za magonjwa nyemelezi. Serikali inatoa bure za kurefusha maisha kwa wagonjwa wanaoishi na virusi vya UKIMWI na wale wenye magonjwa mengine ya kusendeka. Upatikanaji wa dawa za magonjwa nyemelezi linabaki ni jukumu la mgonjwa mwenyewe. Kama dawa hizo hazipatikani kwenye Zahanati au vituo vya afya vya serikali unakuwa mzigo mkubwa kwa mgonjwa. Wahudumu wa kata, walilalamikia swala hili na kupendekeza kwamba serikali itoe pia huduma ya magonjwa nyemelezi kwa wagonjwa wenye magonjwa ya kusendeka.

Maambukizi mapya ni changamoto kubwa katika mpango mzima wa huduma majumbani na harakati za kupunguza kuenea kwa virusi vya Ukimwi. Kata ya Mererani, ni mfano mzuri. Wanaapolo, wakitoka machimboni na kujipumzisha kwenye mji mdogo wa Mererani na hasa maeneo ya Burudani kama vile Songambele, wanakuwa na kazi moja: Kupumzika na kustarehe. Wanakuwa na fedha na wanakuwa na uhakika wa kupata fedha nyingine kwa muda mfupi. Hivyo wanaitumia fedha: Wanakunywa pombe, wanatumia madawa ya kulevya na kufanya mapenzi. Tulishuhudia mirungi ikiuzwa waziwazi.

Binti, mhudumu wa kwenye Bar pale Songambele, alituelezea huku machozi yakidondoka; “ Wanaapolo wana fedha kweli. Wao kutoa laki tatu hadi tano si kitu, lakini sharti lao ni moja tu, kufanya mapenzi bila kinga. Umaskini wetu unatuponza. Mimi nikipata virusi vya UKIMWI, nitalaumu umaskini wa nchi yangu na serikali yetu inayoshindwa kupambana na Umasikini. Nikifikiria kulipa kodi ya nyumba, kulipa karo ya mtoto, kuwatunza baba na mama yangu, nashindwa kupambana na kishawishi cha wanaapolo.... nazipokea fedha zao na kusubiri matokeo!”

Mifano kama ya binti huyu ni mingi pale Mererani. Wanaapolo wanakwenda mbali hadi kuzisambaratisha familia za Mererani. Wanatumia nguvu ya fedha kuwarubuni wanawake na kuhakikisha wanawatenga na waume zao. Si kweli kwamba kila mwanaapolo ana virusi vya UKIMWI, lakini katika mfumo huu wa kufanya mapenzi kwa jeuri ya fedha ni vigumu kuhakikisha usalama wa wale wanaopenda kujikinga na maambukizo ya virusi vya UKIWMI.

Watoto wa kike na hasa wale wanasoma Sekondari za kutwa wanajikuta katika wakati mgumu. Tatizo la usafiri, maisha magumu kwenye familia zao, vishawishi vya kuishi maisha ya kileo: kutengeneza nywele na kuwa na simu za kisasa vinawasukuma kuzikubali fedha za Tanzanite. Matokeo yake ni mimba za utotoni, kukatisha masomo na kuanza kufanya kazi kwenye Nyumba za starehe pale Mererani. Mabinti wadogo tuliohojiana nao pale Mererani na ambao ni walengwa, wana historia ya kusikitisha. Wanaambukizwa katika umri mdogo na vurugu za Mererani haziwezi kuwaruhusu kujikinga na maambukizi mapya.

Umasikini umetajwa pote, Manyara na Musoma, kama changamoto kubwa kwa maambukizi ya UKIMWI. Maana imejidhihirisha wazi kwamba kuna wanaoanguka kwenye mtego kwasababu ya umasikini. Yule binti wa Mererani alitwambia kwamba akiambukizwa virusi vya UKIMWI, ataichukia serikali yetu inayoshindwa kupambana na umaskini. Wakati wa utafiti wetu tulitafakari sana juu ya swala hili la umasikini na kushindwa kuelewa ni kwa nini Tanzania ni masikini hivyo na watanzania tunaamini kwamba sisi ni masikini.

Wakati tunatoka Mererani kwenda Arusha, tulipitia ile njia ya kutokea Kijenge. Tulishuhudia ardhi nzuri na yenye rutuba, mashamba mazuri na makubwa yenye mfumo wa umwagiliaji. Mashamba ya kahawa ambayo sasa hivi yanabadilishwa kuwa mashamba ya maua. Tulielezwa kwamba maua haya yanauzwa nchi za nje na kuingizia Tanzania fedha za kigeni. Tulishuhudia idadi kubwa akina mama walioajiliwa kwenye mashamba haya ya maua wakitoka kazini kuelekea kwenye majumba yao. Ni imani yetu wanalipwa mshahara, labda kama ni ule wa kima cha chini unaolalamikiwa na chama cha wafanyakazi wa Tanzania.

Tulipokwenda Babati, Hanang na Mbulu, tulishuhudia pia mashamba makubwa na ardhi nzuri na yenye rutuba. Mbali na utajiri wa madini ya Mererani, Mkoa wa Manyara una utajiri mkubwa. Kilimo peke yake ni utajiri mkubwa ambao unaweza kuinua kipato cha Tanzania nzima. Mtu unabaki kushangaa, zimwi hili la umasikini linatoka wapi?

Safari ya kwenda Musoma, tulikatisha katika mbuga za wanyama; Ngorongoro na Serengeti. Tulishuhudia magari ya watalii yakiingia na kutoka kwenye mbuga hizi za wanyama. Ni wazi watalii hawa wanaingiza fedha nyingi kwenye mfuko wa taifa. Kila anayekatisha mbuga za wanyama ni lazima kulipa. Hata sisi tulilipa. Hizi fedha zinakwenda wapi? Kwa nini zisichangie kupunguza au kulitokomeza zimwi hili la umasikini wa Tanzania?

Wakati Mkoa wa Manyara ,kuna tishio la Wanaapolo na jeuri ya fedha katika kufanya mapenzi kuhusiana na maambukizi ya virusi vya UKIMWI. Mkoa wa Mara unatishiwa na utamaduni wa mfumo dume kwa upande mmoja na utamaduni wa Nyumba ntobu kwa upande mwingine. Ni vyema kutaja hapa kwamba Unyanyapaa uko juu sana mkoa wa Mara. Uwazi wa mtu kujitaja kwamba ana virusi vya Ukimwi tulioukuta Manyara, ni mdogo sana kule Mara. Walengwa wengi wa Mara, walitaja magonjwa ya kisukari, kifua kikuu na kuogopa kutaja UKIMWI, ingawa baadaye tuligundua kwamba karibia wote tuliohojiana nao walikuwa wakitumia madawa ya kurefusha maisha. Wanaogopa kujitangaza, wasitengwe na jamii. Ugonjwa huu wanauangalia kama laana na kwamba ni ugonjwa wa aibu. Elimu juu ya ugonjwa huu bado inahitaji katika Mkoa wa Mara.

Mfumo dume wa Mkoa wa Mara, ni kwamba baadhi ya wanaume wanapima afya zao kwa siri. Wakigundua wana virusi, wanaendelea kufanya tendo la ndoa na wake zao bila kinga. Lakini hata pale ambapo wanawake wanafanikiwa kufahamu hali ya afya ya waume zao, wanaume wanakataa kutumia kondomu. Wanawake hawana uamuzi juu ya afya zao na maisha yao. Huo ndio mfumo dume ambao unatishia juhudi za huduma majumbani.

Nyumba ntobu, utamaduni wa wanawake kuoa. Nao ni tishio kubwa. Mwanamke anaoa binti, anamtolea mahari, huyu binti anakuwa hana uhuru wa kufanya mapenzi na mwanaume anayemtaka. Mwenye uamuzi ni yule mwanamke aliyetoa mahari. Hivyo anaweza hata akaamua binti afanye mapenzi na mtu mwenye virusi vya UKIMWI, kama huyo mtu hajapima au amepima lakini ana mali nyingi. Utamaduni huu bado unaendelea katika Mkoa wa Mara na ni hatari kwa juhudi zinazofanyika za kuzuia maambukizi ya UKIMWI. Mfumo ambao unamzuia mtu kufanya uamuzi juu ya afya yake na maisha yake ni hatari kabisa kwa uhai wa mwanadamu.

Kwa kuhitimisha tunapendekeza Serikali iendelee na mradi huu wa Huduma Majumbani. Lakini pia Serikali iwasikilize walengwa. Kilio chao cha kuomba chakula kisikilizwe, kilio chao cha kuomba mitaji kifanyiwe kazi. Kilio cha kuomba usafiri kwenye vituo vya afya kishughulikiwe. Hakuna mashaka kwamba Serikali yetu inaweza kuyatekeleza yote haya. Mfano yale mabilioni ya Kikwete, kwa nini yasielekezwe kwa watu hawa ambao ugonjwa uliwanyang’anya mtaji wao na sasa dawa za kuongeza nguvu zimewarudishia uhai na nguvu na wako tayari kuchapa kazi. Kwa nini serikali isiwapatie mitaji kupitia usimamizi wa programu hii ya Huduma majumbani?
Pia ni muhimu Serikali kuyaelekeza mashirika ya yasiyokuwa ya kiserikali na hasa yale yanayotoka nje ya nchi ni maeneo gani yanahitaji huduma. Kuna hatari ya mashirika mengi kuelekeza huduma zao kwenye maeneo yale yale. Na inawezekana mashirika yakatoa huduma isiyokuwa kipaumbele cha walengwa. Kama walengwa wanahitaji mitaji, wanahitaji chakula, wanahitaji karo kuwasomesha watoto wao, wasipatiwe vipande vya sabuni na sukari. Asilimia kubwa ya bajeti ya mashirika haya ielekezwe kwa walengwa. Matumizi ya mashirika haya ya kununua magari na kuyatunza, kulipa mishahara ya watumishi, kuendesha semina na mengine mengi ni makubwa ukilinganisha na huduma inayotolewa kwa walengwa. Labda ndio maana walengwa wanalalamika na kudai kwamba wanafanywa mitaji?

Hapa ni mwisho wa sehemu ya kwanza juu ya miradi miwili ya AFRICARE, ambayo mwandishi wa makala hii alishiriki. Makala ifuatayo itaelezea juu ya mradi wa pili wa kusogeza huduma ya umeme vijijini.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

AFRICARE NA MCHANGO WAKE TANZANIA 2

AFRICARE NA MCHANGO WAKE KATIKA JAMII: TANZANIA.( 2)

Pamoja na mafanikio niliyoyataja, bado huduma hii ya Huduma Majumbani ina changamoto kubwa. Tulipoongea na walengwa katika utafiti wetu kuna mambo matatu ambayo yalitajwa kila kata tuliyoitembelea. Walengwa, na hasa wale wanaoishi na virusi vya ukimwi wanaishukuru sana serikali kwa kuwapatia dawa za kurefusha maisha. Pamoja na shukrani hizi wanaiomba serikali iwasaidie chakula na hasa kwa kipindi hiki ambacho hawajaweza kujitegemea. Hoja yao ni kwamba madawa haya yana nguvu sana. Mtu akiyatumia ni lazima ale vizuri. Bahati mbaya wengi wao hawawezi kumudu zaidi ya mlo mmoja kwa siku. Na kuna wagonjwa wengine waliolazimika kuacha dawa kwa vile hawakuwa na chakula. Mbali na chakula, walengwa hawa wanaoiomba serikali kuwapatia mtaji, ili waanzishe miradi ya kujitegemea. Kwa vile baada ya kutumia dawa za kurefusha maisha wana afya na nguvu za kufanya kazi wasingependa kulishwa kama watoto wadogo. Wanapenda kujitegemea! Tatizo ni mtaji maana walio wengi ugonjwa umerudisha nyuma maendeleo yao. Baadhi walipendekeza wapate mitaji ya mtu mmoja mmoja, lakini walio wengi waliomba serikali iwapatie mitaji ya kuendeleza vikundi vyao vya kusaidiana.

Ombi la tatu la walengwa wa Huduma majumbani ni usafiri. Wanapendekeza vituo vyote vya afya viwe na usafiri wa kuwahudumia wagonjwa wenye magonjwa ya kusendeka. Kiasi kwamba mgonjwa akizidiwa akimbizwe kwenye kituo cha afya au Hospitali ya Wilaya. Wanasema, kama Serikali haiwezi kumudu kununua magari, hata Bajaji inaweza kusaidia katika maeneo fulani yasiyokuwa na milima mikali. Pamoja na usafiri wa kituo cha afya, walengwa hawa wanapendekeza wahudumu wao wa kata ni bora wakipatiwa usafiri wa baiskeli au pikipiki maana wahudumu wengine wanatembea mwendo mrefu kuwafikia walengwa.

Changamoto nyingine ambayo inaleta utata mkubwa katika kuwahudumia wagonjwa wanaoishi na virusi vya UKIMWI, ni pale wao wanaofikiri wanatumiwa kama mtaji. Kuna baadhi waliokataa kuhojiwa. Wanasema wanahojiwa mara nyingi na mashirika mbali mbali. Mashirika hayo yakipata fedha haziwafikii walengwa. Hoja hii ilijitokeza mara nyingi katika utafiti wetu na hasa pale ilipobainika kwamba baadhi ya wahudumu si waaminifu. Misaada inayotolewa na mashirika mbali mbali kwenda kwa lengwa haiwafikii. Misaada mingine inapotelea wilayani, lakini hata ile inayofanikiwa kufika kwenye kata haifiki kwa walengwa na ikifika inakuwa ni nusu na wakati mwingine walengwa wanapigiwa simu kwenda kwa muhudumu kuchukua mizigo yao na kuondoa dhana nzima ya huduma majumbani. Katika kata zingine tulizotembelea, walengwa walipendekeza kwamba wahudumu wa kata wawe ni walengwa wenyewe. Wanashindwa kuelewa mtu asiyekuwa mlengwa anaguswa na huruma gani?

Walitoa mfano wa wahudumu wanaogombania walengwa. Yakijitokeza mashirika ya kutoa misaada, wahudumu wananyang’anyana wagonjwa. Tulishuhudia jambo hili wakati wa utafiti. Unakuta mhudumu hajawahi kumtembelea mlengwa, akisikia kuna watu wanafanya utafiti au kuna shirika la kuleta misaada anatengeneza orodha ndefu na wakati mwingine kuingilia wagonjwa wanaohudumiwa na muhudumu mwingine.

Lakini pia kuna hili tatizo la mashirika kuleta misaada bila kuongea na kujadiliana na walengwa. Wanawaletea chakula wakati wao wanahitaji majembe na mbegu ili walime na kujitegemea kwa chakula. Wanawaletea sabuni na sukari wakati wao wanahitaji mitaji ili waanzishe miradi ya kujitegemea. Kuna haja ya kuwasikiliza walengwa kabla ya kuwaletea misaada. Na tatizo jingine linalojitokeza ni pale mashirika yanapowahudumia walengwa kwa ubaguzi. Ukiliondoa Shirika la World Vision, tuliambiwa mashirika mengine na hasa yale ya kidini yana ubaguzi. Walio wengi wanawahudumia waumini wao.

Wahudumu tuliowahoji walilalamikia ushirikiano hafifu kati yao na viongozi wa serikali za mitaa. Hii nayo ni changamoto kwa huduma majumbani. Wakati wahudumu wanajitahidi kutunza maadili yao ya kutotoa siri za wagonjwa, viongozi wa serikali za mitaa wanatoa shinikizo la kutaka majina ya walengwa wote kuorodheshwa na kutundikwa kwenye ubao wa matangazo. Kisingizio kikiwa usambazaji wa huduma. Wahudumu wanapokataa kufanya hivyo kunatokea kutoelewana na kunyimwa ushirikiano kutoka kwa viongozi wa serikali za mitaa. Pia serikali za mitaa hazina mpango wa kuwashughulikia walengwa wa magonjwa ya kusendeka.

Pia kuna changamoto ya imani za dini na utamaduni. Viongozi wa dini hawapendi kusikia wahudumu wa huduma majumbani wakipita kwenye kaya wakifundisha matumizi ya kondomu. Viongozi wa dini wanasisitiza uaminifu na kuacha kabisa. Ukweli wenyewe ni kwamba uaminifu na kuacha kabisa ni vitu visivyowezekana. Utamaduni nao unaingilia kati, mfano mfumo dume na Nyumba ntobu.

Changamoto nyingine, ni kwamba wahudumu wa msingi wengi ni wanawake. Kama mgonjwa ana hali mbaya, kiasi cha kutofanya kazi. Wanawake wanakuwa na mzigo mkubwa wa kumtunza mgonjwa na wakati huo huo kutafuta muda wa kuihudumia familia nzima, kama vile kutafuta chakula, kutafuta kuni, kuchota maji na kupika. Ni matukio machache tulipokuta wanaume na watoto ni wahudumu wa msingi. Ingekuwa vizuri kwa mashirika yanayotoa mafunzo kwa wahudumu wa msingi, kuyatoa mafunzo hayo kwa wanafamilia wote bila kujali jinsia, ili akijitokeza mgonjwa kwenye familia wote watoe huduma, mzigo asiachiwe mwanamke peke yake.

Wakati walengwa, wanaishukuru serikali kuwapatia dawa za kurefusha maisha, wale wanaofikiri hawajaambukizwa ( wengi wao hawajapima afya zao) wanailaumu serikali kuwafufua watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI. Wanafikiri kuwapatia dawa za kurefusha maisha ni njia ya kuueneza ugonjwa huu. Ingawa kusema kweli unyanyapaa umepungua kwa kiasi kikubwa na hasa Mkoa wa Manyara, bado kuna mawazo kwamba ni bora wagonjwa wenye virusi vya ukimwi wafe, ikiwa ni mkakati wa kupunguza maabukizi mapya. Tuliohojiana nao kwa sharti la kutotaja majina yao, walisema serikali ni adui wa umma. Walitoa mfano wa wagonjwa wanaowafahamu ambao walikuwa kwenye dakika zao za mwisho hapa duniani, lakini walipotumia dawa za kurefusha maisha wamepona na wanaendelea na tabia yao ya kufanya mapenzi kwa vurugu na bila kinga. Wanasema maambukizi mapya yanasababishwa na serikali kwa uamuzi wake wa kusambaza dawa za kurefusha maisha. Siku za nyuma watu waliuogopa UKIMWI, maana walijua ugonjwa huu ni kifo. Leo hii hakuna mwenye kuogopa maana kupata virusi vya UKIMWI si kifo tena. Dawa zipo na serikali inazitoa bure.

Haya ni mawazo ambayo baadhi ya wahojiwa wetu waliyatoa, haina maana tunakubaliana nayo. Tunapingana nayo vikali, maana tunaamini kila mtu ana haki ya kuishi. Tumeyatoa kwenye ripoti hii ili kuelezea yale tuliyoyapata katika utafiti wetu. Ni vizuri serikali na wale wote wanaoendesha vita ya kupambana na UKIMWI na kutoa huduma kwa wagonjwa wanaoishi na virusi vya UKIMWI, kuelewa mawazo ya upande mwingine.

ARVs zimeonyesha uwezo mkubwa wa kurefusha maisha. Kuna malalamiko kwamba baadhi ya wagonjwa wanapata madhara, na tumeambiwa wakati wa utafiti kwamba Tanzania, imeamua kubadilisha aina ya ARVs zilizokuwa zikitumika na kuingiza mpya. Jambo la kushangaza ambalo bado tunafuatilia kwa ukaribu ili kupata ukweli wake ni kwamba walengwa wamebadilishiwa dawa bila kupimwa upya. Kuna ambao ARVs za zamani zilikuwa zimewakubali na ingekuwa ni busara kuendelea na hizo. Uamuzi wa kuwabadilishia wagonjwa wote dawa na kuwaanzishia mpya ni wa kutilia shaka. Ndio maana nikasema tunafuatilia kwa karibu ili kubaini ukweli wake. Mkoa wa Mara, tulisikia malalamiko kutoka kwa walengwa kwamba dawa hizi mpya zina madhara makubwa kuliko zile za zamani na baadhi ya walengwa wameamua kuachana na hizi mpya na ni bahati mbaya kabisa kwamba hawawezi kuzipata zile za zamani. Hii ni changamoto kubwa kwa mpango mzima wa huduma majumbani maana watakutana na maswali ambayo hawatakuwa na majibu yake.... itaendelea.

Na,
Padri Privatus Karugendo.
0754 633122
pkarugendo@yahoo.com
www.karugendo.com

AFRICARE NA MCHANGO WAKE TANZANIA

AFRICARE NA MCHANGO WAKE KATIKA JAMII: TANZANIA.( 1)

AFRICARE, ni shirika lisilokuwa la kiserikali, la kimataifa linalofanya kazi zake dunia nzima na linajishughulisha na maswala ya kijamii. Shirika hili linafanya kazi pia hapa Tanzania, makao makuu yakiwa Dar-es-Salaam na matawi yake kule Manyara, Mara, Mwanza, Iringa, Dodoma nk.

Mwandishi wa makala hii amebahatika kufanya kazi na AFRICARE kwenye miradi miwili tofauti. Mradi wa kwanza ulikuwa ni utafiti juu ya Huduma Majumbani katika mikoa ya Manyara na Mara; utafiti ulifanyika mwaka jana mwezi wa sita. Na mradi wa pili ni ule Changamoto za Milenia wa kusogeza huduma ya umeme katika mikoa sita ya Tanzania bara; Tanga, Morogoro, Iringa, Dodoma, Mbeya na Mwanza, kazi iliyofanyika kwezi Januari na Februari mwaka huu.

Lengo la makala hii ni kuishukuru AFRICARE kwa mchango wake katika jamii ya watanzania. Mbali na huduma za moja kwa moja wanazoelekeza kwa walengwa wao kule vijijini; kuna huduma nyingine zisizokusudiwa moja kwa moja kama kuwawezesha watafiti na wafanyakazi wake wa muda mfupi kupata fursa hadimu ya kuitembelea mikoa mbali mbali ya Tanzania. Huu ni mchango mkubwa maana kama mtu angeamua binafsi kuizungukia mikoa hiyo, angetumia gharama kubwa na wakati mwingine haiwezekani. Kwa wengine fursa hii inakuwa ni kibarua cha kupata fedha na aina Fulani ya utalii wa ndani. Kwa mwandishi, mchambuzi na mchokonozi, hii ni fursa hadimu ya kuchota mengi na kuyasambaza kwa manufaa ya watanzania wote.

Matokeo ya utafiti wa Huduma Majumbani, ni jukumu la AFRICARE, kuyaweka wazi. Makala hii, si taarifa rasmi ya utafiti ule, bali ni maoni ya mwandishi aliyepata bahati ya kufanya kazi na AFRICARE. Bahati hii ya kuzunguka mikoa minane: Manyara, Mara, Tanga, Mbeya, Morogoro, Iringa, Dodoma na Mwanza; itunufaishe wote kwa kupata habari na kujifunza mambo mapya kutoka mikoa hii.

Hivyo makala hii itakuwa na sehemu mbili kuu; kwanza ni utafiti wa Huduma majumbani uliofanyika mwaka jana kwenye mikoa miwili na sehemu ya pili itakuwa juu ya Mradi wa Changamoto za Milenia wa kusogeza huduma ya Umeme vijijini.

HUDUMA MAJUMBANI: MAFANIKIO NA CHANGAMOTO

Hadi leo hii mwongozo wa Serikali kuhusu Huduma Majumbani ni ule uliotolewa mwaka 2005. Hata hivyo serikali iko mbioni kutoa mwongozo mwingine. Ni matumaini yetu kwamba mapungufu na changamoto zinazojitokeza kwenye huduma hii zitapata majibu chanya kwenye mwongozo mpya.

Huduma Majumbani, ni huduma inayowalenga wagonjwa wenye magonjwa ya kusendeka. Magonjwa haya ni kama vile Kifua Kikuu, Kisukari, kifafa na Ukimwi. Serikali kwa kushirikiana na mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha huduma hii inawafikia walengwa.

Kwa kutumia wahudumu wa Kata, ambao kwa kawaida ni kumi na na wanne huduma hii imekuwa ikisambaa hadi vijijini na kwenye kaya zenye wagonjwa wanaosumbuliwa na magonjwa ya kusendeka. Huduma hii ambayo ni pamoja msaada wa kisaikolojia na kijamii, unasihi na ufuasi, ushauri nasaha, habari za virusi na ukimwi, msaada wa kisheria, elimu ya lishe, elimu ya usafi, elimu ya miradi ya kukuza na kuongeza kipato, elimu ya uzazi wa mpango, kuzuia maambukizo kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, rufaa kwenda vituo vya afya, rufaa ya kujiunga na vikundi vya watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi, rufaa kwenda kwenye Mashirika yanayotoa misaada, imekuwa ikitolewa na wahudumu wa kata wakishirikiana na wahudumu wa msingi kwenye kaya.

Utafiti uliofanyika mwezi wa sita mwaka jana kwa lengo la kutathimini utoaji huduma majumbani katika Mikoa ya Manyara na Mara ulibaini mafanikio na changamoto katika huduma hii. Mwandishi wa ripoti hii alishiriki kikamilifu kwenye utafiti huu uliochukua muda siku kumi na nne. Kwa kuheshimu matakwa ya walioshiriki utafiti huu; wahojiwa na wadodosaji, sitataja majina. Nitaelezea mafanikio na changamoto na ikibidi kutaja maeneo.

Katika Mkoa wa Manyara, utafiti ulifanyika katika wilaya za Babati Mjini na Babati Vijijini, Hanang, Simanjiro na Mbulu. Babati Mjini zilitembelewa kata za Babati mjini, Bagara na Bonga. Babati vijijini zilitembelewa kata za Galapo, Magugu na Mamire. Kwa upande wa wilaya ya Hanang, kata zilizotembelewa ni Katesh, Nangwa, Ganan na Endasaki. Wilaya ya Simanjiro, utafiti ulifanyika katika kata za Orkesumet, Mererani na Emboret. Na Wilaya ya Mbulu, utafiti ulifanyika katika kata za Mbulu Mjini, Daudi na Haidom.

Mkoa wa Mara, utafiti ulifanyika katika wilaya za Musoma mjini, Musoma Vijijini na Rorya. Musoma mjini kata zilizotembelewa ni Makoko, Nyasho na Nyakato. Upande wa Musoma vijijini, zilitembelewa kata za Kiriba, Kukirango na Suguti. Wilaya mpya ya Rorya, zilitembelewa kata za Korio, Nyamtinga na Nyamunga.

Katika kata zote zilizotajwa, walengwa walihojiwa kwa kutumia dodoso la kaya, dodoso la mlengwa na baadaye kulikuwa na mikutano ya majadiliano na walengwa, wahudumu wa msingi na wahudumu wa Kata. Pia yalifanyika majadiliano na wakuu wa vituo vya afya vya serikali na vya kidini.

Mafanikio makubwa yaliyojitokeza kwenye wilaya zote tulizozitembelea ni huduma ya dawa. Wagonjwa wa magonjwa ya kusendaka wanapata dawa. Kwa wale wanaoishi na virusi vya UKIMWI, wamepata afya tena na wanaweza kufanya kazi. Ni matukio machache sana tulipomkuta mgonjwa amelala. Na pia ni matukio machache tulipomkuta mgonjwa wa VVU, kuugua ndani ya miezi mitatu kiasi cha kushindwa kufanya kazi.

Mafanikio mengine ni mafanikio ya mfumo wa huduma majumbani kuanzia Wilayani kwenda kwenye vituo vya Afya kupitia kwa mhudumu wa kata kwenda hadi kwenye wahudumu wa msingi na hatimaye kumfikia mlengwa. Ingawa kuna kasoro za hapa na pale, mfumo umesukwa vizuri.

Pia elimu ya unasihi na ufuasi, elimu ya ushauri nasaha, elimu ya lishe na usafi, elimu ya kujikinga na Virusi vya Ukimwi, elimu ya unyanyapaa, imeenea hadi vijijini. Haya ni mafanikio makubwa sana na ya kupongezwa.

Ushirikiano wa serikali na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali ni mafanikio makubwa maana uhai wa mwanadamu ni kazi yetu sote na ni lazima vita dhidi ya adui anayetishia uhai wetu tupambane kwa pamoja. Mashirika mengi yamejitokeza kutoa misaada ya kufanikisha mpango wa huduma majumbani.

Watu wengi tulioongea nao walikuwa wamepima afya zao. Wengine wamepima na kutoa majibu kwa ndugu, jamaa na marafiki, na wengine wamepima na imebaki ni siri yao. Tulichoambiwa ni kwamba wahudumu wa huduma majumbani wamefanya kazi kubwa ya kuwashawishi na kuwaelekeza kwenda kupima.

Kuna vikundi mbali mbali vya walengwa wanaoishi na virusi vya UKIMWI vilivyoanzishwa kwa lengo la kusaidiana kiuchumi, kuhimizana kufuata ratiba ya dawa, kufarijiana, kuelimishana na kushirikiana kupambana na unyanyapaa. Vikundi hivi vimesaidia pia utekelezwaji wa huduma majumbani na vimekuwa vikiungwa mkono na mpango huo wa Huduma Majumbani.

Kila mhudumu wa Kata, anapata mfuko wa dawa (Kit) , hivyo anaweza kuwasambazia dawa wagonjwa wasiokuwa na uwezo wa kusafiri kufika kwenye vituo vya afya. Pia mhudumu huyu anasaidia kuwaibua wagonjwa wengine na kuwaorodhesha ili wapate huduma..... Itaedelea.

Na,
Padri Privatus Karugendo.
0754 633122
pkarugendo@yahoo.com
www.karugendo.com

Uchambuzi wa Kitabu cha Azimio la Arusha

UCHAMBUZI WA KITABU: AZIMIO LA ARUSHA.


1. Rekodi za Kibibliografia.

Jina la kitabu kinchohakikiwa hapa ni Azimio la Arusha na Siasa ya Tanu Juu ya Ujamaa na Kujitegemea.Kilitolewa na idaraya ya Habari ya TANU, Dar-es-salaam 1967. Kilipigwa chapa na kiwanda cha Uchapishaji cha Taifa. Kijitabu hiki kina kurasa 40, na anayekihakiki hapa ni Mimi Padri Privatus Karugendo.

11. Utangulizi

Tunakumbuka kifo cha Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Baba wa Taifa letu la Tanzania. Na mwaka huu, ni wa uchaguzi mkuu. Hivyo ni bora kujikumbusha mawazo ya Mwalimu kupitia kwenye maandishi yake na hasa hoja yake nzito iliyojipenyeza kupitia kwenye kitabu hiki kidogo cha Azimio la Arusha, ambacho yeye alikifananisha kama msahafu au ndugu yake na msahafu, maana alisema daima alitembea na vitabu hivyo viwili; Biblia na Kijitabu hiki cha Azimio la Arusha.

Kitabu hiki kimegawanyika katika sehemu kuu tano. Sehemu ya kwanza inaongea juu ya Imani ya TANU, Sehemu ya pili inaongea juu ya Siasa ya Ujamaa. Sehemu ya tatu inaongea juu ya siasa ya Kujitegemea. Sehemu ya nne inaongea juu ya uanachama na sehemu ya tano ndiyo inaongea juu ya Azimio la Arusha.

111. Mazingira yanayokizunguka kitabu

Baada ya Uhuru kulikuwa na changamoto nyingi kwa nchi changa za Afrika. Mapinduzi ya kila mara yalikuwa yakizikumba nchi hizi. Ubeberu ulikuwa ukikodolea macho Afrika, na wakoloni walitaka kuendendelea kuitawala Afrika utokea mbali. Wakati huo kukiwa na pande mbili zinazopingana. Upande wa mabepari ukiongozwa na nchi za Ulaya Magharibi na Amerika na Ukomunisti ukiongozwa na Urusi na China. Tanzania kwa kuamua siasa ya ujmaa, ilijikuta inawekwa kwenye kapu la wakomunisti, ingawa msimamo wa Mwalimu Nyerere ulikuwa wazi wa siasa za kutofungamana na upande wowote.

Viongozi wa Afrika walikuwa na uchu wa mali, na kutaka kuishi maisha kama ya wakoloni. Walitaka mishahara mikubwa, walitaka kuwa na hisa kwenye makampuni na walitaka kufanya biashara.

Mwaimu Nyerere, aliona hatari ya kuruhusu viongozi kuiga maisha ya wakoloni waliofukuzwa. Alifikiri njia pekee ya kuwahakikisha Tanzania, inaendelea kwa pamoja kwa kuwainua watu wa chini ni kuanzisha mfumo wa kuongoza mapambano hayo. Azimio la Arusha lililenga kujenga na kusimika Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea katika Taifa letu.

Azimio la Arusha, halikupata mafanikio makubwa, kwa vile halikuungwa mkono na watu wengi. Walio wengi walifanya kazi ya unafiki. Hawakufuata Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea kutoka moyoni. Hivyo juhudi zote za Azimio la Arusha, za kutaifisha njia kuu zote za uchumi kuwa mikononi mwa Umma, kwa kuanzisha Mashirika ya Umma, zilishindwa vibaya sana na uchumi ulididimia.

Bila mjadala wa Kitaifa Azimio la Arusha, lilikufa na kuzikwa kule Zanzibar. Kilichofuata hapo si Ubepari – bali Ubeberu wenye kunakishiwa na Utandawazi. Kilio cha leo ni kwamba turudishe saisa ya Ujamaa na Kujitegemea!

1V. Muhtasari wa Kitabu.

Sehemu ya kwanza ya kitabu hiki inaeleza Juu ya Imani na Madhumuni ya TANU. Imani zote ni muhimu, lakini kwa uzito wa uchambuzi huu ni bora tukataja ya (h) na (i) ambazo zinasema hivi; “ Kwamba ili kuhakikisha kuwa uchumi wa nchi unakwenda sawa. Serilai lazima iwe na mamlaka kamili juu ya njia muhimu za kuuza uchumi; na Kwamba ni wajibu wa Serikali, ambayo ni watu wenyewe kuingilia kati kwa vitendo maisha ya uchumi ya Taifa ili kuhakikisha usitawi wa raia wote na kuzuia mtu kumnyonya mtu mwingine au kikundi kimoja kunyonya kikundi kingine na kuzuia limbikizo la utajiri kufikia kiasi ambacho hakipatani na siasa ya watu wote kuwa sawa” (uk 2).

Na sehemu hii naungana na sehemu nyingine upande wa Madhumuni ya TANU, inayosema hivi: “ Kuona kwamba Serikali ya nchi yetu inasimamia barabara njia kuu za kuzalisha mali na inafuata siasa ambayo itarahisisha njia ya kumiliki kwa jumla mali za nchi yetu” (uk.4)

Sehemu ya pili ya kitabu hiki inaelezea juu ya Siasa ya Ujamaa: Kwamba katika Siasa ya Ujamaa hakuna Unyonyaji; “ Nchi yenye Ujamaa kamili i nchi ya wafanyakazi: Haina ubepari wal ukabaila. Haina tabaka mbele za watu: tabaka ya chini ya watu wanaoishi wka kufanya kazi, na tabaka ya juu ya watu wanaoishi kwa kufanyiwa kazi...” (uk.5)

Kwamba kwenye ujamaa njia kuu za uchumi ziko chini ya wakulima na wafanyakazi; “ Namna ya pekee ya kujenga na kudumisha ujamaa ni kuthibitisha kuwa njia kuu zote za uchumi wa nchi yetu zinatawaliwa na kumilikiwa na wakulima na wafanyakazi....” (uk.6)

Wizard of the Crow

UHAKIKI WA KITABU: WIZARD OF THE CROW

1. Rekodi za Kibibliografia.

Jina la kitabu kinachohahikiwa hapa ni WIZARD OF THE CROW, Kimeandikwa na Ngugi wa Thiong’o. Mchapishaji wa kitabu hiki ni East African Educational Publishers na amekipatia namba ifuatayo katika sekwensia ya vitabu duniani (ISBN): 978- 9966- 25 –491-9. Kitabu kina kurasa 768 . Na anayekihakiki sasa hivi katika safu hii ni mimi Padri Privatus Karugendo.

II. Utangulizi

Wizard of the Crow, au Mchawi wa Kunguru kwa lugha yetu ya Kiswahili na Murogi wa Kagogo kwa lugha ya Kikuyu ni hadithi ndefu kuliko zote zilizoangikwa na Ngugi wa Thiong’o. Hadithi hii iliandikwa kwanza kwa lugha ya Kikuyu na kutafsiri wa na mwandishi mwenyewe kwenye lugha ya Kiingereza. Ni hadithi ambayo kule Kenya watu wanasomeana na kusimuliana kwenye vilabu vya pombe, kwenye starehe mbali mbali na vijiweni. Ni wazi kwenye lugha ya Kikuyu, itakuwa inaburudisha sana kuliko kwenye Kiingereza.

Hadithi hii inamhusu kiongozi wa nchi huru ya kubuni ya bara la Afrika yenye jina la Aburiria. Kiongozi huyu ana magonjwa matano yanayomsumbua na moja wapo ya magonjwa haya ni hasira ambayo watu wanaamini ilisababishwa na mke wake. Mama huyu pamoja na kuwekwa kizuizini na kuteswa, alikataa kutoa machozi. Kiongozi huyu alitamani sana kuyaona machozi ya mke wake, ili ajione kama mshindi. Lakini mama huyu alikataa kulia. Ingawa jina halitajwi, lakini aina ya utawala anaouchora mwandishi unazigusa nchi zote za Afrika na kwa karibu zaidi nchi yake ya Kenya. Uchu wa madaraka, kutesa wapinzani, majungu, kujipendekeza, utajiri wa kupindukia, ukatili na unyanyasaji wa wanawake, kupora mali ya nchi na kupendelea mambo ya nchi za nje kiasi cha mtu kutamani kujibadilisha kuwa kama mzungu, ni magonjwa yaliyojaa katika nchi zote za Afrika.

Hadithi yenyewe ina vitabu sita, maana yake ni vitabu sita ndani ya kitabu kimoja. Bei ya kitabu hiki ni shilingi 45,000! Hivyo kwa kuogopa gharama ya kitabu na watu kuogopa kukinunua, mchapishaji, amejaribu kuvichapa vitabu hivi sita tofauti. Lakini mimi nimesoma kitabu kimoja chenye vitabu vyote sita. Ni vitabu sita vyenye mwendelezo wa hadithi moja.

Vitabu hivi sita ni : Mashetani wa madaraka, ambacho ni ukurasa wa kwanza hadi wa 45, Mashetani wa foleni, ukurasa wa 45 hadi 271, Mashetani wa kike, ukurasa wa 271 hadi 467 Mashetani wa Kiume, ukurasa wa 467 hadi 637 Mashetani waasi ukurasa 637 hadi 727 na Mashetani wenye ndefu ukurasa 727 hadi 768.

Kabla ya kufanya uhakiki wa kitabu hiki ningependa kuelezea mazingira yanayokizunguka.




III. Mazingira yanayokizunguka kitabu

Ukisoma vitabu vya Ngugi vya zamani kama vile Weep Not, Child alichokiandika mwaka 1964, na The River Between alichokiandika mwaka 1965 na vingine vya siku za karibuni kama vile Matigari cha 1987, unakuwa na hisia juu ya majina ya wahusika, kwamba majina hayo ya Kikuyu yanabeba ujumbe mzito ambao msomaji anaenelea kuutambua jinsi anavyosoma hadithi. Hivyo msomaji ambaye si Mkikuyu, hapati uhondo mzima, kwa kutofahamu maana ya majina ya Kikuyu.

Nilipokutana na Ngugi, miaka kumi iliyopita, katika mahojiano naye aliikubali wazo hili la majina ya Kikuyu kubeba maana kubwa kwenye vitabu vyake. Aliniambia kwamba kila jina, kama yalivyo majina yote ya kiafrika, linakuwa na maana fulani inayohusiana na hadithi husika. Mwaka jana, nilikutana tena na Ngugi, Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, alinielezea kwamba sasa kwenye kitabu chake cha Wizard of The Crow, amejitahidi kutumia na majina ya Kiswahili, ili hata wale ambao si wa Kikuyu, waweze kufurahia hadithi kwa kuunganisha matukio na majina ya wahusika. Bado ni tatizo kwa wale ambao si Waswahili na si wa Kikuyu, bado kuna haja ya kuyatafsiri majina haya ili ujumbe wa hadithi hii uwafikie watu wote bila ya kikwazo.

Baadhi ya majina ya mawaziri wa Kiongozi wa nchi Ya Aburiria, yako kwenye Kiswahili; mfano Waziri wa Mambo ya nchi za Nje ni Machokali. Huyu ndo macho ya kiongozi wa nchi ya Aburiria, anaangalia kila kitu ndani na nje ya nchi. Waziri huyu alipoona macho yake hayaoni vya kutosha, ili kumfurahisha Kiongozi wa nchi, alifunga safari na kwenda nchi za nje ili macho yake yafanyiwe upasuaji ili yawe makubwa zaidi. Picha ya kuchorwa Kwenye gamba la kitabu, Machokali, anaonekana na macho yasiyokuwa ya kawaida. Waziri wa nchi kwenye ofisi ya Kiongozi wa nchi ya Aburiria, amepewa jina la Sikiokuu, huyu ndo sikio la Kiongozi, kazi yake ni kusikia kila linalosemwa juu ya Kiongozi. Kwa vile masikio yake yalikuwa madogo, kwa kutaka kumfurahisha kiongozi, alifunga safari na kwenda nchi za nje kuyapanua masikio yake. Kwenye gamba la kitabu, anaonekana akiwa na masikio makubwa kichwa kidogo!

Mawaziri na viongozi wengi katika nchi ya Aburiria, walibadilisha viungo vyao vya mwili ili viweze kutoa huduma nzuri kwa Kiongozi wa nchi. Big Ben Mambo, alifanya upasuaji wa ulimi, ili urefuke zaidi, aweze kutoa amri za kijeshi nchi nzima. Na waziri mwingine alipanua pua zake, ili aweze kunusa hatari yoyote ile inayoweza kuwa imelengwa kwa Kiongozi. Na waziri mwingine alifanya upasuaji wa kuongeze ukubwa wa midogo yake, ili aweze kufikisha ujumbe wa kiongozi nchi nzima, kwenye picha iliyo kwenye gamba la kitabu, anaonekana waziri huyu na midomo yake mikubwa kupita kiasi.

Jina jingine linalotumika kwa Kiswahili ni Tajirika. Huyu anapata vyeo vikubwa, anachanganyikiwa na kutamani kuwa kama mzungu, hadi mwishowe anapata nafasi kubwa katika uongozi wa nchi ya Aburiria. Bahati mbaya kwa msomaji ambaye si Mkikuyu, majina ya wahusika wakuu Nyawira, Kamiti na Kaniuru, yanabaki kwenye Kikuyu. Mwandishi, angetoa tafsiri ya majina haya, msomaji angepata uhondo zaidi.

Wizard of the Crow, unaanza kama mzaa. Nyawira na Kamiti, wanamapinduzi wanaoupinga utawala wa Aburiria, walifukuzwa na vikosi vya usalama wakati wa vurugu za kupinga wazo la Kiongozi wa Aburiria, la kujenga mnara kama ule wa Babeli, mnara wa kwenda Mbinguni. Walipokimbizwa na kuingizwa kwenye makazi ya watu, waliamua kuingia kwenye nyumba na kuandika bango lenye Maneno “Wizard of the Crow”, maana yake ni nyumba ya hatari. Polisi aliyekuwa akiwafukuza kwa kuogopa nyumba ya mchawi wa Kunguru, aliogopa kuendelea kuwafukuza. Na Waafrika tunavyoamini uchawi, polisi huyo alirudi kwenye nyumba hiyo kesho yake ili apate huduma. Kiongozi wa nchi alipata habari kwamba polisi wake, aliwafukuza wenye fujo hadi wakatokomea kwenye nyumba mbali na mji; hivyo akaamua kumpandisha cheo kwa kazi yake nzuri aliyoifanya. Polisi yeye akafikiri na kuamini kwamba amepandishwa cheo kwa nguvu za “Wizard of the Crow”.

Polisi huyu, akaeneza habari kwamba kuna Mchawi, mwenye nguvu. Kwamba yeye amepanda cheo kwa nguvu za Mchawi wa Kunguru. Viongozi wote wakakimbilia kwa Mchawi wa Kunguru. Hadi Kiongozi wa Nchi alipokwenda Amerika, kuomba fedha za kujenga mnara wa Babeli, akaugulia kule, madaktari wakatibu na kushindwa, mpango ulifanyika kumsafirisha Mchawi wa Kunguru kwenda hadi Amerika, kumtibu Kiongozi wa nchi.

Kama mzaha vile, lakini inaaminika kwamba viongozi wengi wa Afrika, wanasafiri na wachawi wao. Watu hawa wanapata posho na kutunzwa vizuri. Mchawi, akiamua safari isifanyike, inafutwa bila ya maelezo! Hivyo si kwamba Ngugi, anazua mambo ya kuchekesha tu, bali ni ukweli unaoishi kwenye mazingira ya uongozi wa nchi za Afrika.

Wizard of the Crow, ni kama ilivyo kwa Babu wa Loliondo. Jambo linaanza kama mzaha, lakini linapanuka hadi foleni ya magari elfu moja. Ukisoma kitabu hiki unashangaa sana jinsi Waafrika tunavyofanana kwa mawazo, na jinsi tusivyopenda utafiti. Tunapenda miujiza, ambayo mara nyingi ni kupumbazwa. Ngugi, ametumia mfano wa uchawi na kunogesha hadithi yake, kama afanyavyo mwandishi Gabriel Garcia Marquez.

Ngugi wa Thiong’o, alizaliwa mwaka 1938 kule Kenya. Alisoma Chuo Kikuu cha Makerere Uganda na baadaye Chuo Kikuu cha Leeds, Uingereza. Kitabu chake cha Kwanza Weep Not, Child kiliandikwa mwaka wa 1964. Na mwaka 1965, akaandika kitabu chake cha pili cha The River Between. Na mwaka 1967, aliandika A Grain of Wheat. Mwaka 1982, aliandika Devil on The Cross. Ameandika michezo ya kuigiza kama ule ya “ Nitaoa nikipenda” na kitabu kingine cha Matigari. Sasa hivi anaishi na kufundisha kule California.
Baada ya maelezo haya sasa tuone kitabu chenyewe kwa muhtasari.

IV. Muhtasari wa Kitabu

Hii ni hadithi ya kubuni. Nchi yenyewe inaitwa Aburiria na iko Bara la Afrika. Kama nilivyosema mwanzo, ni wazi jina hili Aburiria, litakuwa na maana fulani katika lugha ya Kikuyu na kama kungekuwa na tafsiri yake, basi hadithi ingenoga kuanzia mwanzoni. Hii ni hadithi ambayo msomaji hapendi imalizike, ni ndefu lakini inachekesha, inasikitisha na kuburudisha; kiasi mtu anatamani iendelee bila mwisho.

Kiongozi wa nchi hii ya Aburiria, ni mwakilishi wa viongozi wengi wa Afrika. Badala ya kuangalia matatizo ya watu wake, anataka kujenga mnara wa kwenda mbinguni. Mnara kama ule wa Babeli. Mawaziri wake, kwa kujipendekeza, wanaunga mkono wazo hili na kupendekeza kwamba ili lifanikiwe nchi iombe mkopo kutoka Benki za chi za nje, ni mfano wa IMF na Benki ya dunia.

Mbali na wazo hili la kiwendawazimu, Kiongozi wa Aburiria, ana tabia ya kuwanyanyasa wanawake. Anatembea na watoto wadogo; mke wake wanapokuja juu na kumkanya, Kiongozi huyu anaamua kumfungia mke wake kizuizini milele yote. Hata hivyo mama huyu anakataa kuonyesha dalili zozote zile za unyonge, anagoma kulia, anagoma kuomba msamaha. Hali hii inamchanganya kiongozi kiasi cha kuugua na kuwa na kilema (hasira) cha maisha rohoni mwake.

Hivyo hadithi yote inazunguka juu ya utawala wa Kiongozi huyu, upinzani juu ya utawala wake, magomvi ya madaraka baina ya mawaziri wake, visa na visasi, sauti ya ukombozi inayoongozwa na Mama Nyawira, ambaye yeye na Kamiti, kwa pamoja wanatengeneza “Mchawi wa Kunguru”.

Hadithi hii imegawanyika katika vitabu sita. Kitabu cha kwanza ni Mashetani wa Madaraka, kitabu cha pili ni mashetani wa foleni, kitabu cha tatu ni mashetani wa Kike, kitabu cha nne ni mashetani wa kiume, kitabu cha tano ni mashetani waasi na kitabu cha sita ni mashetani wenyewe ndevu.

Kamiti, anayekuja kuwa Mchawi wa Kunguru kwa kushirikiana na Nyawira., amesoma India na kupata digrii mbili. Anaporudi Aburiria, hafanikiwi kupata kazi. Kila anapokwenda kutafuta kazi, anaambiwa kazi zimejaa. Anaamua kujitosa kwenye harakati za kupinga utawala wa kiongozi wa Aburiria, katika harakati hizi anakutana na Nyawira; wanashirikiana kuunda taasisi ya “Mchawi wa Kunguru”. Hawakuwa na lengo hilo ila baada ya kufukuzwa na polisi, katika harakati za kujiokoa, wakajikuta wanatengeneza Bango, na kuandika kwamba nyumba yao ni ya mchawi wa Kunguru. Hivyo mchawi wa Kunguru “Wizard of the Crow” ni Kamiti na Nyawira; wote kwa nyakati tofauti walifanya kazi hii ya Mchawi wa Kunguru. maana yake mabadiliko katika jamii yataletwa kwa ushirikiano wa Mwanamke na mwanaume.

Uchawi ( Wizaard of the Crow) wao ni wa kisomi: Wanajua daima watu wanasumbuliwa na matatizo ya kisaikolojia. Hivyo wanajitahidi kuwasoma wateja wao na kuwaelekeza pole pole ili wayatanzue matatizo yao wenyewe. Walijua kabisa kwamba viongozi wote wa Aburiria walikuwa na ugonjwa wa kutaka madaraka, walikuwa na ugonjwa wa kutaka fedha; hivyo waliweza kuwaelekeza huko, na viongozi hao walipona magonjwa yao ya mawazo. Kwa njia hii, jina la mchawi wa Kunguru likawa kubwa; na watu bila kujua siri kwamba mchawi huyu ni watu wawili, yaani mwanamke na mwanaume, wakafikiri ni mtu mmoja mwenye uwezo wa kujibadilisha; siku nyingine utamkuta ni mwanamke na siku nyingine ni mwanaume.

Wachawi hawa wasomi, wanapotaka kufanya tendo la ngono kwa mara kwanza; mambo yanakwama kwa vile hawakuwa na kondomu. Ngugi, amekuwa makini kutuonyesha uchawi wa kisomi. Kama wangekuwa wachawi wa kawaia, basi hata na tendo la ngono lingekwenda kichawi kwa kufanya ngono bila kinga. Maana yake ni kwamba, mwandishi anaandika juu ya uchawi, lakini hana imani na uchawi!

Tajirika, anateuliwa kuwa Mwenyekiti wa kamati ya kujenga Mnara wa Babeli. Anapoteuliwa, makampuni ya ujenzi yanaanza kujikomba kwake na kumletea bahasha. Tajirika, anajiona amekuwa tajiri na sasa ana kila kitu, labda kitu kimoja: SURA ya KIZUNGU. Anatamani awe mzungu. Mawazo haya yanamchanganya, hadi anaugua ugonjwa usiojulikana. Alibakia kusema neno moja tu ambalo ni “Kama”, kwa maana “ Kama ningekuwa mzungu”. Baadaye, Tajirika, kama ilivyo kawaida ya Waafrika, anatibiwa ( kwa ujanja) na Mchawi wa Kunguru.

Foleni ya watu wanaotaka kazi kwa Tajirika, inakuwa ndefu kupita kiasi. Na foleni nyingine za mahitaji mengine mengi zinaanza nchi nzima. Nchi inakumbwa na ugonjwa wa foleni. Mawaziri wengine wanachukia foleni hizi, lakini wengine wanataka ziendelee kama ishara ya watu kuunga mkono wazo la kiongozi wao la kujenga Mnara wa Babeli. Mwandishi, ametumia foleni, kuonyesha jinsi wananchi walivyo na matatizo mengi.

Baada ya hapo mambo mengi yanatukia; kuanzia wivu, majungu, visasi, hadi kumchonganisha Tajirika na mke wake. Matokeo yake Tajirika, anaanza tabia ya kumpiga mke wake. Sauti ya wanawake ( sauti ya umma) kikundi kilichokuwa kinaongozwa na Nyawira, na kuendesha mapambano chini kwa chini na wakati mwingine wazi wazi, kilimteka Tajirika na kumfikisha kwenye mahakama ya wanawake. Adhabu yake, ilikuwa akatwe uume wake. Aliachiwa kwa msamaha na kuonywa kwamba akijaribu tena kumpiga mke wake, atapata adhabu hiyo.

Mahakama ya wanawake ni sehemu inayochekesha sana kwenye kitabu hiki. Mahakama hii inamaliza kiburi cha wanaume. Maana, mwanaume anakamatwa na wanawake zaidi ya watano, wanamwangusha chini na kumkalia juu. Wanawake wengine wanamzunguka na kuanza kutoa hukumu. Anavyoandika Ngugi, ni kama wanawake wenyewe wanakuwa uchi! Mwanamke mmoja anashikilia upanga wenye makali na kutishia kuukata uume wa mshitakiwa. Lengo zima ni kumtaka mshitakiwa aungame kutoka rohoni kwamba hatarudia tena kumpiga mke wake.

Habari zikavuma nchi nzima kwamba kuna mahakama ya Wanawake; wanaume wakaogopa kuwapiga wake zao. Kikundi hiki cha wanawake cha kupigania haki na uhuru wa nchi ya Aburiria kilikuwa na mikakati mingi na uwezo wa kuingia sehemu nyeti bila kufahamika. Sikukuu ya kuzaliwa Kiongozi wa nchi ya Aburiria, kikundi hiki kilijipenyeza hadi jukwaani, kama kikundi cha ngoma, kumbe kilikuwa na ujumbe mkali. Kilimtaka Kiongozi wa nchi ya Aburiria, kumwachia huru mke wake aliyekuwa amewekwa kizuizini.

Kiongozi wa nchi ana safari ya kwenda Amerika, kutafuta fedha za kujenga Mnara wa Babeli. Bahati mbaya mapendekezo yake yanakataliwa na benki za Ulaya. Matokeo hayo yanamfanya Kiongozi anapatwa na ugonjwa wa ajabu. Mwili wake unaanza kutanuka, madaktari wanajaribu kumtibu wanashindwa. Hadi wasaidizi wa Kiongozi, wanafikria “Wizard of the Crow”. Mipango inafanywa kumtuma “Mchawi” kutoka Afrika, kwenda Amerika kumtibu Kiongozi. Habari zinavuma kwamba Kiongozi ana mimba! Mchawi, anafanikiwa kiasi fulani kumtibu Kiongozi na kumwezesha kurudia Afrika.

Mawaziri wa nchi ya Aburiria, wanaendelea kusalitiana na kuoneana wivu na kuchongeana kwa Kiongozi. Kama ilivyo kawaida ya viongozi wa Afrika, mawaziri hawa wanapotea mmoja baada ya mwingine. Tajirika, aliyeteswa wakati Kiongozi akiwa Amerika, anapanda ngazi hadi kufikia kileleni.

Tofauti na hadithi nyingine ambazo Ngugi, amekuwa akiziandika, zikiishia na mauaji na kumwaga damu. Hii ya Mchawi wa Kunguru, ina matumaini. Pamoja na kuelezea vituko vya uongozi wa Afrika, bado kuna matumaini. Sauti ya wananchi, inayoongozwa na Nyawira na wapambanaji wengine, inachomoza na kuleta matumaini katika nchi ya Aburiria.


V. TATHIMINI YA KITABU.

Nianze kwa kumpongeza Ngugi, kwa kazi hii nzuri sana aliyoiandika. Kusema kweli hadithi hii inaburudisha na kufikirisha. Ni hadithi ya kuchekesha; mtu unacheka mwanzo wa kitabu hadi mwisho. Ni vituko vya kweli na viongozi wetu wanafanya vituko hivyo: wananunua magari ya kifahari, wanajenga nyumba za kifahari, wakati wananchi wanaishi kwenye umasikini wa kutupwa. Pili nimpongeze pia kwa kusikia kilio chetu na kujaribu kuyatafsiri baadhi ya majina ya wahusika kwenye lugha ya Kiswahili. Ukisoma Machokali, unapata picha ya mhusika, ukisoma Sikiokuu, unapata picha ya mhusika na matendo yake. Ukimsoma Tajirika, unaona kabisa vitendo vyote vya utajiri na ulafi wa Waafrika.

Tatu, ni kwamba tofauti na vitabu vingine ambavyo mwandishi ameviandika siku za nyuma, hadithi hii inaonyesha matumaini. Pamoja na maovu yote ya viongozi wa Afrika, bado Ngugi, anatuaminisha kwamba kuna matumaini. Cheche ya Sauti ya wananchi inaleta matumaini.

Nne, inagawa baadhi ya Wakenya nilioongea nao juu ya kitabu cha “Wizard of the Crow” wanamponda Ngugi, kwa kuandika mambo ya kizamani. Kwa kuendelea kushambulia ukoloni na ubeberu; wanasema Kenya ya leo ina mambo mapya na mawazo ya Ngugi, hayana nafasi tena, bado mimi namuunga mkono kwa msimamo wake. Matatizo ya Afrika yaliletwa na Ukoloni ambao uliutukuza ubeberu na unaendelea kuutukuza. Matatizo ya Afrika yanaletwa na viongozi kama vile wa Aburiria, wanaoshughulikia madaraka na kusahau kuyashughulika matatizo ya wananchi. Matatizo ya Afrika yanaletwa na watu kama Bwana Tajirika, anayetamani kubadilisha sura yake ili awe mzungu.

Tano, Ngugi, amefanikiwa kuwachora vizuri mawaziri wa Kiongozi wa Aburiria. Kule kujipendekeza na kushindwa kumshauri vizuri kiongozi. Ile hali ya kutaka kubadilisha viungo vya miili yao; kuwa na masikio makubwa, macho makubwa, midomo mikubwa na ulimi mrefu ni kuelezea hali ya kutojiamini na kutaka kujipendekeza kwa kiongozi ili kupata faida. Ni wazi Ngugi, ameweka chumvi katika kulielezea hili, lakini ndo ukweli wenyeweye. Wasaidizi wa viongozi wa Afrika wanaogopa kusema ukweli kwa kubembeleza nafasi ya kazi.

Sita, Kisa chote cha “Wizard of the Crow” kinaonyesha jinsi Ngugi, alivyo mwandishi makini na anaifahamu Afrika na matatizo yake. Waafrika tunapenda uchawi, tunapenda miujiza ili tupate mafanikio maishani bila kufanya kazi. Tunachoma misitu na kuharibu mazingira, huku tunaingia makanisani na misikitini kuomba Mungu atupatie mvua; tunaziachia raslimali zetu kusombwa na wageni, na baadaye tunalia kwamba sisi ni masikini; tunaingia kwenye nyumba za ibada kumwomba Mungu aondoe umasikini kwenye jamii zetu. Viongozi wa Aburiria, waliamini kwamba Mchawi wa Kunguru, alikuwa na nguvu za pekee, alitibu na kujua mambo mengine mengi, alikuwa na siri ya mti unaootesha fedha! Kwamba matawi yake ni fedha. Hata kiongozi wa nchi aliamini kwamba mti huo upo, na hivyo hata Benki za Ulaya zikikataa kumpatia fedha ya kujenga mnara wa Babeli, basi mti huo wa kuzalisha fedha ungemsaidia. Ni mfano kama ule wa Loliondo, ambako watu wanaamini kikombe kimoja kinaweza kutibu magonjwa zaidi ya sita na kwamba Mungu, ana uwezo wa kufahamu na kuelekeza kwamba shilingi mia tano zinatosha kulipia matibabu hayo.

Saba, kule kuonyesha kwamba matumaini ya ukombozi wa Afrika yako mikononi mwa wanawake, ni jambo la kupongezwa. Miaka hamsini ya uhuru wa Afrika, wanaume wamelisaliti bara hili; wameleta umasikini mkubwa, wameleta vita ya wenyewe kwa wenyewe; wameleta mauaji kama yale ya Burundi, Rwanda ,DRC, Uganda, Somalia na sasa Libya na kwingineko. Sasa ni zamu ya wanawake, kuliongoza Bara la Afrika. Ngugi, anamchora Nyawira, kama mama wa matumaini.

VI. HITIMISHO.

Ni wazi ningependa kuwashauri wasomaji wangu kukinunua kitabu hiki na kukisoma. Pamoja na ukweli kwamba bei ya kitabu hiki ni kubwa, tunaweza kutafuta mbinu za kukipata. Hata mimi nilisoma cha mwingine. Niliazima na kukisoma. Tukitaka kusoma, kuna njia ya kupata vitabu.

Kuna haja ya kutasiri kitabu hiki kwenye lugha ya Kiswahili. Taasisi ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, imefikisha miaka Hamsini ya kuwepo kwake. Nafikri mojawapo ya kusherehekea miaka hii hamsini, ingekuwa kufanya kazi ya kutafsiri vitabu kama hiki cha Ngugi. Anayoyaandika Ngugi, yanatugusa Waafrika sote. Hivyo tafsiri kwa Kiswahili, ingesaidia kitabu hiki kusomwa na watu wengi.

Pamoja na pongezi nilizompatia Ngugi, bado ana kazi ya kuhakikisha anatoa tafsiri ya majina ya wahusika kwenye hadithi zake. Ni sawa mengine ameyaweka kwenye lugha ya Kiswahili, lakini kitabu chake kinasomwa na watu wengine ambao si Waswahili. Labda kama mwishoni mwa kitabu , angejaribu kuweka ufafanuzi wa majina anayoyatumia ujumbe wake ungewafikia watu wengi na kwa haraka zaidi.

Na,
Padri Privatus Karugendo.






















Wizard of the Crow

UHAKIKI WA KITABU: WIZARD OF THE CROW

1. Rekodi za Kibibliografia.

Jina la kitabu kinachohahikiwa hapa ni WIZARD OF THE CROW, Kimeandikwa na Ngugi wa Thiong’o. Mchapishaji wa kitabu hiki ni East African Educational Publishers na amekipatia namba ifuatayo katika sekwensia ya vitabu duniani (ISBN): 978- 9966- 25 –491-9. Kitabu kina kurasa 768 . Na anayekihakiki sasa hivi katika safu hii ni mimi Padri Privatus Karugendo.

II. Utangulizi

Wizard of the Crow, au Mchawi wa Kunguru kwa lugha yetu ya Kiswahili na Murogi wa Kagogo kwa lugha ya Kikuyu ni hadithi ndefu kuliko zote zilizoangikwa na Ngugi wa Thiong’o. Hadithi hii iliandikwa kwanza kwa lugha ya Kikuyu na kutafsiri wa na mwandishi mwenyewe kwenye lugha ya Kiingereza. Ni hadithi ambayo kule Kenya watu wanasomeana na kusimuliana kwenye vilabu vya pombe, kwenye starehe mbali mbali na vijiweni. Ni wazi kwenye lugha ya Kikuyu, itakuwa inaburudisha sana kuliko kwenye Kiingereza.

Hadithi hii inamhusu kiongozi wa nchi huru ya kubuni ya bara la Afrika yenye jina la Aburiria. Kiongozi huyu ana magonjwa matano yanayomsumbua na moja wapo ya magonjwa haya ni hasira ambayo watu wanaamini ilisababishwa na mke wake. Mama huyu pamoja na kuwekwa kizuizini na kuteswa, alikataa kutoa machozi. Kiongozi huyu alitamani sana kuyaona machozi ya mke wake, ili ajione kama mshindi. Lakini mama huyu alikataa kulia. Ingawa jina halitajwi, lakini aina ya utawala anaouchora mwandishi unazigusa nchi zote za Afrika na kwa karibu zaidi nchi yake ya Kenya. Uchu wa madaraka, kutesa wapinzani, majungu, kujipendekeza, utajiri wa kupindukia, ukatili na unyanyasaji wa wanawake, kupora mali ya nchi na kupendelea mambo ya nchi za nje kiasi cha mtu kutamani kujibadilisha kuwa kama mzungu, ni magonjwa yaliyojaa katika nchi zote za Afrika.

Hadithi yenyewe ina vitabu sita, maana yake ni vitabu sita ndani ya kitabu kimoja. Bei ya kitabu hiki ni shilingi 45,000! Hivyo kwa kuogopa gharama ya kitabu na watu kuogopa kukinunua, mchapishaji, amejaribu kuvichapa vitabu hivi sita tofauti. Lakini mimi nimesoma kitabu kimoja chenye vitabu vyote sita. Ni vitabu sita vyenye mwendelezo wa hadithi moja.

Vitabu hivi sita ni : Mashetani wa madaraka, ambacho ni ukurasa wa kwanza hadi wa 45, Mashetani wa foleni, ukurasa wa 45 hadi 271, Mashetani wa kike, ukurasa wa 271 hadi 467 Mashetani wa Kiume, ukurasa wa 467 hadi 637 Mashetani waasi ukurasa 637 hadi 727 na Mashetani wenye ndefu ukurasa 727 hadi 768.

Kabla ya kufanya uhakiki wa kitabu hiki ningependa kuelezea mazingira yanayokizunguka.




III. Mazingira yanayokizunguka kitabu

Ukisoma vitabu vya Ngugi vya zamani kama vile Weep Not, Child alichokiandika mwaka 1964, na The River Between alichokiandika mwaka 1965 na vingine vya siku za karibuni kama vile Matigari cha 1987, unakuwa na hisia juu ya majina ya wahusika, kwamba majina hayo ya Kikuyu yanabeba ujumbe mzito ambao msomaji anaenelea kuutambua jinsi anavyosoma hadithi. Hivyo msomaji ambaye si Mkikuyu, hapati uhondo mzima, kwa kutofahamu maana ya majina ya Kikuyu.

Nilipokutana na Ngugi, miaka kumi iliyopita, katika mahojiano naye aliikubali wazo hili la majina ya Kikuyu kubeba maana kubwa kwenye vitabu vyake. Aliniambia kwamba kila jina, kama yalivyo majina yote ya kiafrika, linakuwa na maana fulani inayohusiana na hadithi husika. Mwaka jana, nilikutana tena na Ngugi, Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, alinielezea kwamba sasa kwenye kitabu chake cha Wizard of The Crow, amejitahidi kutumia na majina ya Kiswahili, ili hata wale ambao si wa Kikuyu, waweze kufurahia hadithi kwa kuunganisha matukio na majina ya wahusika. Bado ni tatizo kwa wale ambao si Waswahili na si wa Kikuyu, bado kuna haja ya kuyatafsiri majina haya ili ujumbe wa hadithi hii uwafikie watu wote bila ya kikwazo.

Baadhi ya majina ya mawaziri wa Kiongozi wa nchi Ya Aburiria, yako kwenye Kiswahili; mfano Waziri wa Mambo ya nchi za Nje ni Machokali. Huyu ndo macho ya kiongozi wa nchi ya Aburiria, anaangalia kila kitu ndani na nje ya nchi. Waziri huyu alipoona macho yake hayaoni vya kutosha, ili kumfurahisha Kiongozi wa nchi, alifunga safari na kwenda nchi za nje ili macho yake yafanyiwe upasuaji ili yawe makubwa zaidi. Picha ya kuchorwa Kwenye gamba la kitabu, Machokali, anaonekana na macho yasiyokuwa ya kawaida. Waziri wa nchi kwenye ofisi ya Kiongozi wa nchi ya Aburiria, amepewa jina la Sikiokuu, huyu ndo sikio la Kiongozi, kazi yake ni kusikia kila linalosemwa juu ya Kiongozi. Kwa vile masikio yake yalikuwa madogo, kwa kutaka kumfurahisha kiongozi, alifunga safari na kwenda nchi za nje kuyapanua masikio yake. Kwenye gamba la kitabu, anaonekana akiwa na masikio makubwa kichwa kidogo!

Mawaziri na viongozi wengi katika nchi ya Aburiria, walibadilisha viungo vyao vya mwili ili viweze kutoa huduma nzuri kwa Kiongozi wa nchi. Big Ben Mambo, alifanya upasuaji wa ulimi, ili urefuke zaidi, aweze kutoa amri za kijeshi nchi nzima. Na waziri mwingine alipanua pua zake, ili aweze kunusa hatari yoyote ile inayoweza kuwa imelengwa kwa Kiongozi. Na waziri mwingine alifanya upasuaji wa kuongeze ukubwa wa midogo yake, ili aweze kufikisha ujumbe wa kiongozi nchi nzima, kwenye picha iliyo kwenye gamba la kitabu, anaonekana waziri huyu na midomo yake mikubwa kupita kiasi.

Jina jingine linalotumika kwa Kiswahili ni Tajirika. Huyu anapata vyeo vikubwa, anachanganyikiwa na kutamani kuwa kama mzungu, hadi mwishowe anapata nafasi kubwa katika uongozi wa nchi ya Aburiria. Bahati mbaya kwa msomaji ambaye si Mkikuyu, majina ya wahusika wakuu Nyawira, Kamiti na Kaniuru, yanabaki kwenye Kikuyu. Mwandishi, angetoa tafsiri ya majina haya, msomaji angepata uhondo zaidi.

Wizard of the Crow, unaanza kama mzaa. Nyawira na Kamiti, wanamapinduzi wanaoupinga utawala wa Aburiria, walifukuzwa na vikosi vya usalama wakati wa vurugu za kupinga wazo la Kiongozi wa Aburiria, la kujenga mnara kama ule wa Babeli, mnara wa kwenda Mbinguni. Walipokimbizwa na kuingizwa kwenye makazi ya watu, waliamua kuingia kwenye nyumba na kuandika bango lenye Maneno “Wizard of the Crow”, maana yake ni nyumba ya hatari. Polisi aliyekuwa akiwafukuza kwa kuogopa nyumba ya mchawi wa Kunguru, aliogopa kuendelea kuwafukuza. Na Waafrika tunavyoamini uchawi, polisi huyo alirudi kwenye nyumba hiyo kesho yake ili apate huduma. Kiongozi wa nchi alipata habari kwamba polisi wake, aliwafukuza wenye fujo hadi wakatokomea kwenye nyumba mbali na mji; hivyo akaamua kumpandisha cheo kwa kazi yake nzuri aliyoifanya. Polisi yeye akafikiri na kuamini kwamba amepandishwa cheo kwa nguvu za “Wizard of the Crow”.

Polisi huyu, akaeneza habari kwamba kuna Mchawi, mwenye nguvu. Kwamba yeye amepanda cheo kwa nguvu za Mchawi wa Kunguru. Viongozi wote wakakimbilia kwa Mchawi wa Kunguru. Hadi Kiongozi wa Nchi alipokwenda Amerika, kuomba fedha za kujenga mnara wa Babeli, akaugulia kule, madaktari wakatibu na kushindwa, mpango ulifanyika kumsafirisha Mchawi wa Kunguru kwenda hadi Amerika, kumtibu Kiongozi wa nchi.

Kama mzaha vile, lakini inaaminika kwamba viongozi wengi wa Afrika, wanasafiri na wachawi wao. Watu hawa wanapata posho na kutunzwa vizuri. Mchawi, akiamua safari isifanyike, inafutwa bila ya maelezo! Hivyo si kwamba Ngugi, anazua mambo ya kuchekesha tu, bali ni ukweli unaoishi kwenye mazingira ya uongozi wa nchi za Afrika.

Wizard of the Crow, ni kama ilivyo kwa Babu wa Loliondo. Jambo linaanza kama mzaha, lakini linapanuka hadi foleni ya magari elfu moja. Ukisoma kitabu hiki unashangaa sana jinsi Waafrika tunavyofanana kwa mawazo, na jinsi tusivyopenda utafiti. Tunapenda miujiza, ambayo mara nyingi ni kupumbazwa. Ngugi, ametumia mfano wa uchawi na kunogesha hadithi yake, kama afanyavyo mwandishi Gabriel Garcia Marquez.

Ngugi wa Thiong’o, alizaliwa mwaka 1938 kule Kenya. Alisoma Chuo Kikuu cha Makerere Uganda na baadaye Chuo Kikuu cha Leeds, Uingereza. Kitabu chake cha Kwanza Weep Not, Child kiliandikwa mwaka wa 1964. Na mwaka 1965, akaandika kitabu chake cha pili cha The River Between. Na mwaka 1967, aliandika A Grain of Wheat. Mwaka 1982, aliandika Devil on The Cross. Ameandika michezo ya kuigiza kama ule ya “ Nitaoa nikipenda” na kitabu kingine cha Matigari. Sasa hivi anaishi na kufundisha kule California.
Baada ya maelezo haya sasa tuone kitabu chenyewe kwa muhtasari.

IV. Muhtasari wa Kitabu

Hii ni hadithi ya kubuni. Nchi yenyewe inaitwa Aburiria na iko Bara la Afrika. Kama nilivyosema mwanzo, ni wazi jina hili Aburiria, litakuwa na maana fulani katika lugha ya Kikuyu na kama kungekuwa na tafsiri yake, basi hadithi ingenoga kuanzia mwanzoni. Hii ni hadithi ambayo msomaji hapendi imalizike, ni ndefu lakini inachekesha, inasikitisha na kuburudisha; kiasi mtu anatamani iendelee bila mwisho.

Kiongozi wa nchi hii ya Aburiria, ni mwakilishi wa viongozi wengi wa Afrika. Badala ya kuangalia matatizo ya watu wake, anataka kujenga mnara wa kwenda mbinguni. Mnara kama ule wa Babeli. Mawaziri wake, kwa kujipendekeza, wanaunga mkono wazo hili na kupendekeza kwamba ili lifanikiwe nchi iombe mkopo kutoka Benki za chi za nje, ni mfano wa IMF na Benki ya dunia.

Mbali na wazo hili la kiwendawazimu, Kiongozi wa Aburiria, ana tabia ya kuwanyanyasa wanawake. Anatembea na watoto wadogo; mke wake wanapokuja juu na kumkanya, Kiongozi huyu anaamua kumfungia mke wake kizuizini milele yote. Hata hivyo mama huyu anakataa kuonyesha dalili zozote zile za unyonge, anagoma kulia, anagoma kuomba msamaha. Hali hii inamchanganya kiongozi kiasi cha kuugua na kuwa na kilema (hasira) cha maisha rohoni mwake.

Hivyo hadithi yote inazunguka juu ya utawala wa Kiongozi huyu, upinzani juu ya utawala wake, magomvi ya madaraka baina ya mawaziri wake, visa na visasi, sauti ya ukombozi inayoongozwa na Mama Nyawira, ambaye yeye na Kamiti, kwa pamoja wanatengeneza “Mchawi wa Kunguru”.

Hadithi hii imegawanyika katika vitabu sita. Kitabu cha kwanza ni Mashetani wa Madaraka, kitabu cha pili ni mashetani wa foleni, kitabu cha tatu ni mashetani wa Kike, kitabu cha nne ni mashetani wa kiume, kitabu cha tano ni mashetani waasi na kitabu cha sita ni mashetani wenyewe ndevu.

Kamiti, anayekuja kuwa Mchawi wa Kunguru kwa kushirikiana na Nyawira., amesoma India na kupata digrii mbili. Anaporudi Aburiria, hafanikiwi kupata kazi. Kila anapokwenda kutafuta kazi, anaambiwa kazi zimejaa. Anaamua kujitosa kwenye harakati za kupinga utawala wa kiongozi wa Aburiria, katika harakati hizi anakutana na Nyawira; wanashirikiana kuunda taasisi ya “Mchawi wa Kunguru”. Hawakuwa na lengo hilo ila baada ya kufukuzwa na polisi, katika harakati za kujiokoa, wakajikuta wanatengeneza Bango, na kuandika kwamba nyumba yao ni ya mchawi wa Kunguru. Hivyo mchawi wa Kunguru “Wizard of the Crow” ni Kamiti na Nyawira; wote kwa nyakati tofauti walifanya kazi hii ya Mchawi wa Kunguru. maana yake mabadiliko katika jamii yataletwa kwa ushirikiano wa Mwanamke na mwanaume.

Uchawi ( Wizaard of the Crow) wao ni wa kisomi: Wanajua daima watu wanasumbuliwa na matatizo ya kisaikolojia. Hivyo wanajitahidi kuwasoma wateja wao na kuwaelekeza pole pole ili wayatanzue matatizo yao wenyewe. Walijua kabisa kwamba viongozi wote wa Aburiria walikuwa na ugonjwa wa kutaka madaraka, walikuwa na ugonjwa wa kutaka fedha; hivyo waliweza kuwaelekeza huko, na viongozi hao walipona magonjwa yao ya mawazo. Kwa njia hii, jina la mchawi wa Kunguru likawa kubwa; na watu bila kujua siri kwamba mchawi huyu ni watu wawili, yaani mwanamke na mwanaume, wakafikiri ni mtu mmoja mwenye uwezo wa kujibadilisha; siku nyingine utamkuta ni mwanamke na siku nyingine ni mwanaume.

Wachawi hawa wasomi, wanapotaka kufanya tendo la ngono kwa mara kwanza; mambo yanakwama kwa vile hawakuwa na kondomu. Ngugi, amekuwa makini kutuonyesha uchawi wa kisomi. Kama wangekuwa wachawi wa kawaia, basi hata na tendo la ngono lingekwenda kichawi kwa kufanya ngono bila kinga. Maana yake ni kwamba, mwandishi anaandika juu ya uchawi, lakini hana imani na uchawi!

Tajirika, anateuliwa kuwa Mwenyekiti wa kamati ya kujenga Mnara wa Babeli. Anapoteuliwa, makampuni ya ujenzi yanaanza kujikomba kwake na kumletea bahasha. Tajirika, anajiona amekuwa tajiri na sasa ana kila kitu, labda kitu kimoja: SURA ya KIZUNGU. Anatamani awe mzungu. Mawazo haya yanamchanganya, hadi anaugua ugonjwa usiojulikana. Alibakia kusema neno moja tu ambalo ni “Kama”, kwa maana “ Kama ningekuwa mzungu”. Baadaye, Tajirika, kama ilivyo kawaida ya Waafrika, anatibiwa ( kwa ujanja) na Mchawi wa Kunguru.

Foleni ya watu wanaotaka kazi kwa Tajirika, inakuwa ndefu kupita kiasi. Na foleni nyingine za mahitaji mengine mengi zinaanza nchi nzima. Nchi inakumbwa na ugonjwa wa foleni. Mawaziri wengine wanachukia foleni hizi, lakini wengine wanataka ziendelee kama ishara ya watu kuunga mkono wazo la kiongozi wao la kujenga Mnara wa Babeli. Mwandishi, ametumia foleni, kuonyesha jinsi wananchi walivyo na matatizo mengi.

Baada ya hapo mambo mengi yanatukia; kuanzia wivu, majungu, visasi, hadi kumchonganisha Tajirika na mke wake. Matokeo yake Tajirika, anaanza tabia ya kumpiga mke wake. Sauti ya wanawake ( sauti ya umma) kikundi kilichokuwa kinaongozwa na Nyawira, na kuendesha mapambano chini kwa chini na wakati mwingine wazi wazi, kilimteka Tajirika na kumfikisha kwenye mahakama ya wanawake. Adhabu yake, ilikuwa akatwe uume wake. Aliachiwa kwa msamaha na kuonywa kwamba akijaribu tena kumpiga mke wake, atapata adhabu hiyo.

Mahakama ya wanawake ni sehemu inayochekesha sana kwenye kitabu hiki. Mahakama hii inamaliza kiburi cha wanaume. Maana, mwanaume anakamatwa na wanawake zaidi ya watano, wanamwangusha chini na kumkalia juu. Wanawake wengine wanamzunguka na kuanza kutoa hukumu. Anavyoandika Ngugi, ni kama wanawake wenyewe wanakuwa uchi! Mwanamke mmoja anashikilia upanga wenye makali na kutishia kuukata uume wa mshitakiwa. Lengo zima ni kumtaka mshitakiwa aungame kutoka rohoni kwamba hatarudia tena kumpiga mke wake.

Habari zikavuma nchi nzima kwamba kuna mahakama ya Wanawake; wanaume wakaogopa kuwapiga wake zao. Kikundi hiki cha wanawake cha kupigania haki na uhuru wa nchi ya Aburiria kilikuwa na mikakati mingi na uwezo wa kuingia sehemu nyeti bila kufahamika. Sikukuu ya kuzaliwa Kiongozi wa nchi ya Aburiria, kikundi hiki kilijipenyeza hadi jukwaani, kama kikundi cha ngoma, kumbe kilikuwa na ujumbe mkali. Kilimtaka Kiongozi wa nchi ya Aburiria, kumwachia huru mke wake aliyekuwa amewekwa kizuizini.

Kiongozi wa nchi ana safari ya kwenda Amerika, kutafuta fedha za kujenga Mnara wa Babeli. Bahati mbaya mapendekezo yake yanakataliwa na benki za Ulaya. Matokeo hayo yanamfanya Kiongozi anapatwa na ugonjwa wa ajabu. Mwili wake unaanza kutanuka, madaktari wanajaribu kumtibu wanashindwa. Hadi wasaidizi wa Kiongozi, wanafikria “Wizard of the Crow”. Mipango inafanywa kumtuma “Mchawi” kutoka Afrika, kwenda Amerika kumtibu Kiongozi. Habari zinavuma kwamba Kiongozi ana mimba! Mchawi, anafanikiwa kiasi fulani kumtibu Kiongozi na kumwezesha kurudia Afrika.

Mawaziri wa nchi ya Aburiria, wanaendelea kusalitiana na kuoneana wivu na kuchongeana kwa Kiongozi. Kama ilivyo kawaida ya viongozi wa Afrika, mawaziri hawa wanapotea mmoja baada ya mwingine. Tajirika, aliyeteswa wakati Kiongozi akiwa Amerika, anapanda ngazi hadi kufikia kileleni.

Tofauti na hadithi nyingine ambazo Ngugi, amekuwa akiziandika, zikiishia na mauaji na kumwaga damu. Hii ya Mchawi wa Kunguru, ina matumaini. Pamoja na kuelezea vituko vya uongozi wa Afrika, bado kuna matumaini. Sauti ya wananchi, inayoongozwa na Nyawira na wapambanaji wengine, inachomoza na kuleta matumaini katika nchi ya Aburiria.


V. TATHIMINI YA KITABU.

Nianze kwa kumpongeza Ngugi, kwa kazi hii nzuri sana aliyoiandika. Kusema kweli hadithi hii inaburudisha na kufikirisha. Ni hadithi ya kuchekesha; mtu unacheka mwanzo wa kitabu hadi mwisho. Ni vituko vya kweli na viongozi wetu wanafanya vituko hivyo: wananunua magari ya kifahari, wanajenga nyumba za kifahari, wakati wananchi wanaishi kwenye umasikini wa kutupwa. Pili nimpongeze pia kwa kusikia kilio chetu na kujaribu kuyatafsiri baadhi ya majina ya wahusika kwenye lugha ya Kiswahili. Ukisoma Machokali, unapata picha ya mhusika, ukisoma Sikiokuu, unapata picha ya mhusika na matendo yake. Ukimsoma Tajirika, unaona kabisa vitendo vyote vya utajiri na ulafi wa Waafrika.

Tatu, ni kwamba tofauti na vitabu vingine ambavyo mwandishi ameviandika siku za nyuma, hadithi hii inaonyesha matumaini. Pamoja na maovu yote ya viongozi wa Afrika, bado Ngugi, anatuaminisha kwamba kuna matumaini. Cheche ya Sauti ya wananchi inaleta matumaini.

Nne, inagawa baadhi ya Wakenya nilioongea nao juu ya kitabu cha “Wizard of the Crow” wanamponda Ngugi, kwa kuandika mambo ya kizamani. Kwa kuendelea kushambulia ukoloni na ubeberu; wanasema Kenya ya leo ina mambo mapya na mawazo ya Ngugi, hayana nafasi tena, bado mimi namuunga mkono kwa msimamo wake. Matatizo ya Afrika yaliletwa na Ukoloni ambao uliutukuza ubeberu na unaendelea kuutukuza. Matatizo ya Afrika yanaletwa na viongozi kama vile wa Aburiria, wanaoshughulikia madaraka na kusahau kuyashughulika matatizo ya wananchi. Matatizo ya Afrika yanaletwa na watu kama Bwana Tajirika, anayetamani kubadilisha sura yake ili awe mzungu.

Tano, Ngugi, amefanikiwa kuwachora vizuri mawaziri wa Kiongozi wa Aburiria. Kule kujipendekeza na kushindwa kumshauri vizuri kiongozi. Ile hali ya kutaka kubadilisha viungo vya miili yao; kuwa na masikio makubwa, macho makubwa, midomo mikubwa na ulimi mrefu ni kuelezea hali ya kutojiamini na kutaka kujipendekeza kwa kiongozi ili kupata faida. Ni wazi Ngugi, ameweka chumvi katika kulielezea hili, lakini ndo ukweli wenyeweye. Wasaidizi wa viongozi wa Afrika wanaogopa kusema ukweli kwa kubembeleza nafasi ya kazi.

Sita, Kisa chote cha “Wizard of the Crow” kinaonyesha jinsi Ngugi, alivyo mwandishi makini na anaifahamu Afrika na matatizo yake. Waafrika tunapenda uchawi, tunapenda miujiza ili tupate mafanikio maishani bila kufanya kazi. Tunachoma misitu na kuharibu mazingira, huku tunaingia makanisani na misikitini kuomba Mungu atupatie mvua; tunaziachia raslimali zetu kusombwa na wageni, na baadaye tunalia kwamba sisi ni masikini; tunaingia kwenye nyumba za ibada kumwomba Mungu aondoe umasikini kwenye jamii zetu. Viongozi wa Aburiria, waliamini kwamba Mchawi wa Kunguru, alikuwa na nguvu za pekee, alitibu na kujua mambo mengine mengi, alikuwa na siri ya mti unaootesha fedha! Kwamba matawi yake ni fedha. Hata kiongozi wa nchi aliamini kwamba mti huo upo, na hivyo hata Benki za Ulaya zikikataa kumpatia fedha ya kujenga mnara wa Babeli, basi mti huo wa kuzalisha fedha ungemsaidia. Ni mfano kama ule wa Loliondo, ambako watu wanaamini kikombe kimoja kinaweza kutibu magonjwa zaidi ya sita na kwamba Mungu, ana uwezo wa kufahamu na kuelekeza kwamba shilingi mia tano zinatosha kulipia matibabu hayo.

Saba, kule kuonyesha kwamba matumaini ya ukombozi wa Afrika yako mikononi mwa wanawake, ni jambo la kupongezwa. Miaka hamsini ya uhuru wa Afrika, wanaume wamelisaliti bara hili; wameleta umasikini mkubwa, wameleta vita ya wenyewe kwa wenyewe; wameleta mauaji kama yale ya Burundi, Rwanda ,DRC, Uganda, Somalia na sasa Libya na kwingineko. Sasa ni zamu ya wanawake, kuliongoza Bara la Afrika. Ngugi, anamchora Nyawira, kama mama wa matumaini.

VI. HITIMISHO.

Ni wazi ningependa kuwashauri wasomaji wangu kukinunua kitabu hiki na kukisoma. Pamoja na ukweli kwamba bei ya kitabu hiki ni kubwa, tunaweza kutafuta mbinu za kukipata. Hata mimi nilisoma cha mwingine. Niliazima na kukisoma. Tukitaka kusoma, kuna njia ya kupata vitabu.

Kuna haja ya kutasiri kitabu hiki kwenye lugha ya Kiswahili. Taasisi ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, imefikisha miaka Hamsini ya kuwepo kwake. Nafikri mojawapo ya kusherehekea miaka hii hamsini, ingekuwa kufanya kazi ya kutafsiri vitabu kama hiki cha Ngugi. Anayoyaandika Ngugi, yanatugusa Waafrika sote. Hivyo tafsiri kwa Kiswahili, ingesaidia kitabu hiki kusomwa na watu wengi.

Pamoja na pongezi nilizompatia Ngugi, bado ana kazi ya kuhakikisha anatoa tafsiri ya majina ya wahusika kwenye hadithi zake. Ni sawa mengine ameyaweka kwenye lugha ya Kiswahili, lakini kitabu chake kinasomwa na watu wengine ambao si Waswahili. Labda kama mwishoni mwa kitabu , angejaribu kuweka ufafanuzi wa majina anayoyatumia ujumbe wake ungewafikia watu wengi na kwa haraka zaidi.

Na,
Padri Privatus Karugendo.