UCHAGUZI MKUU 2005

MAKALA HII ILICHAPISHWA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005.

UCHAGUZI MKUU 2005, TUSEME UKWELI NA TUSIWAPOTOSHE WANANCHI.

Tunapoelekea uchaguzi mkuu wa 2005, tutayasikia mengi. Mengine ya ukweli na mengine ya uongo. Watu wataanza kupakana matope na kuharibiana majina. Kutakuwa na mapambano makali kati ya chama na chama, na ndani ya chama kutakuwa na mapambano kati ya mgombea na mgombea . Kila mtu anataka ashinde na kila chama kinataka kishinde. Hiyo ndiyo siasa na huo ndiyo ubinadamu!

Jambo la msingi ambalo tunapaswa kuliangalia kwa makini ili tuhesabike kati ya jamii iliyostaarabika na inayoheshimika duniani ni lazima tufanye siasa zinazozingatia ukweli. Ni jambo la kawaida katika ushindani wa kisiasa watu kutafuta kuangushana, na kila mmoja anataka kushinda, ili ushindi uwe wa amani, ni lazima washindani kueleza ukweli dhidi ya wapinzani wao. Maana kama lengo ni kuijenga Tanzania bora, yenye amani na utulivu, hakuna haja ya kuupindisha ukweli. Gharama ya kupindisha ukweli ni kubwa na yenye hasara kuliko faida.

Hapa Tanzania, ukiachia mbali kiti cha rais, nafasi nyingine zinazokuwa na ushindani mkubwa ni Ubunge na Udiwani. Hizi zote ni nafasi za uwakilishi. Mbunge anawawakilisha watu wa jimbo lake Bungeni na Diwani anawawakilishia watu wa kata yake kati vikao vya halmashauri ya wilaya. Nafasi hizi zinakuwa na siasa za uongo, chuki, umbea na uhasama. Ni bahati mbaya kwamba baadhi ya wale wanaochaguliwa kwenye nafasi hizi wanafikiria zaidi juu ya posho kuliko kuuzingatia na kuutafakari wajibu wao wa kuwawakilisha wananchi, wajibu wa kuelezea ukweli, kulinda ukweli na kuusimamia ukweli. Kazi hii ni ngumu kiasi kwamba kama watu wangeifahamu vizuri, ni wachache wangeikimbilia!

Siasa hizi za uongo, chuki, umbea na uhasama, zimeanza hivi sasa hata kabla ya muda wenyewe wa kampeni kutangazwa. Waheshimiwa wabunge wamekwishaanza kupita kwenye majimbo yao wakiwaelezea wananchi yale waliyoyafanya kwa kipindi cha miaka mitano inayokwisha na matarajio yao kwa kipindi kingine endapo watachaguliwa. Wengine wameanza kutaja jinsi walivyonunua majeneza kwenye misiba, walivyochangia kwenye misiba, walivyosaidia wagonjwa na wasiojiweza, walivyosaidia kulipa karo za baadhi ya watoto katika majimbo yao, walivyotoa kanga na vitenge, walivyotoa baiskeli na misaada mingine mingi. Kana kwamba kazi ya mbunge ni kutoa misaada! Kwa njia hii walio wengi wanafanikiwa kupindisha ukweli na kuwapotosha wananchi.

Mbali na wabunge walio Bungeni hivi sasa kuna wengine wanaotaka kuwania nafasi hizo. Hivyo wanaanza kutafuta mbinu mbali mbali zenye uongo na ukweli. Wengine wameanza kumwaga mapesa, wananunua kanga, vitenge, pombe na kuwapikia watu pilau. Na wengine wameanza kuvitumia vyombo vya habari kujitangaza na kueneza uongo dhidi ya wapinzani wao. Mfano mzuri ni habari iliyotoka kwenye gazeti hili tarehe 5.Juni, iliyokuwa na kichwa cha habari: “Jimbo la Chitatalilo lakodolewa macho”. Habari hii ililenge kuelezea hali ilivyo katika jimbo la Buchosa, Wilaya ya Sengerema, Mkoa wa Mwanza.

Mwandishi wa habari hii ambaye anaelekea anamfagilia mtu fulani au anajifagilia yeye mwenyewe maana siku hizi kila mtu anataka kuingia bungeni, anaelezea vizuri kile nilichokigusia hapo juu mwanzoni mwa makala hii; siasa za uongo, chuki, umbea na uhasama. Habari hii aliyoiandika kwa uchu na pupa, haikulenga kuelezea ukweli, bali kuwapotosha wananchi. Na hili si jambo zuri, ni jambo la kupiga vita kwa nguvu zote.
Mwandishi wa habari hii alilenga kuwaelezea watanzania kwamba Kamanda wa vijana wa CCM, wa Jimbo la Buchosa, alichaguliwa kwa mizengwe. Kama habari hii ingeishia katika kuelezea mizengwe na kudhibitishwa kwamba mizengwe ilitumika, basi hili lingebaki katika Chama Cha CCM na uongozi wake – hili lisingekuwa swala la Watanzania wote. Lakini habari hiyo iliendelea hivi: “ Katika kuthibitisha upendeleo huo aliouita wa wazi, alisema kamanda aliyetawazwa amesimamishwa kazi serikalini na kuwa hastahili kwa sasa kupewa heshima kama hiyo. Atawaongoza vipi vijana wakati jamii haijaambiwa kitu kilichofanya afukuzwe kazi?”

Ikiguswa serikali, hili ni swala la watanzania wote. Ingawa serikali yetu inaongozwa na Chama Cha Mapinduzi, lakini wafanyakazi wake wote si lazima wawe wanaCCM – na serikali inaongoza nchi nzima. Hivyo swala linaloigusa serikali ni lazima limguse kila Mtanzania.

Aliyechaguliwa kuwa Kamanda wa vijana jimbo la Buchosa ni Dk.Charles Tizeba. huyu ndiye aliyekuwa Mhandisi wa Jiji la Mwanza, wakati wa sakata la kituo cha mafuta kwenye Barabara ya Makongoro. Mhandisi huyu pamoja na wataalamu wengine wa Jiji la Mwanza, waliishauri serikali kwamba Kituo hicho cha mafuta hakikuwa Barabarani. Serikali haikusikiliza ushauri huo, ikaendelea na zoezi lake la kukivunja kituo hicho. Ukweli ni kwamba kituo hicho hakikuwa Barabarani, hakijawahi kuwa barabarani na hakitakuwa barabarani! Ikitokea huko mbeleni ikaamuliwa kupitisha barabara pale, basi itapita juu kwa juu kama barabara tunazozijua kwenye nchi zilizoendelea zinazopita juu. Kiwanja hicho kilipimwa kwenye miaka ya sitini. Aliyekimiliki miaka hiyo alikuwa na lengo kujenga kituo cha mafuta, alikiomba kiwanja hicho kwa lengo la kujenga kituo cha mafuta. Bahati mbaya hakuweza kufanya hivyo, alikiuza kiwanja hicho kwa mtu mwingine, na mwingine akauza kwa mwingine hadi alipokinunua huyu aliyejenga kituo kilichovunjwa na serikali. Tangia nyuma makusudio ya kiwanja hicho yalikuwa ni kujenga kituo cha mafuta. Mhandisi wa jiji ni mtu wa kujua historia hii yote na kuwa na uwezo wa kusoma ramani ya Jiji vinginevyo anakuwa amekinunua cheti!

Ramani ya Jiji ilivyochorwa, kama Dk.Tizeba, angekubali kwamba kituo hicho kiko barabarani angekuwa ameisaliti taaluma yake ya uhandisi. Leo hii tungekuwa tunaishinikiza serikali imnyang’anye liseni ya uhandisi! Maana hata mtu ambaye hakuenda shule anaweza kuona kwamba kiwanja hicho hakipo barabarani. Asingekuwa na tofauti na wale waliopitisha mikataba hewa ya IPTL na mingine ambayo hadi leo hii tunaipigia kelele.

Kwanini basi Serikali iliamua kukivunja kituo cha mafuta ambacho hakikuwa Barabarani? Haya ndiyo maswali ya kuiuliza serikali ili wananchi wafahamu ukweli. Utakuwa ni uonevu wa hali juu kuwasakama watu waliosimama kidete kuitetea taaluma yao na kusema ukweli.

Haiwezekani mtu anayetetea taaluma yake, anayesimama kwenye ukweli, asiyefanya kazi kwa kufuata tu kama robot, anayejisimamia na kuangalia maslahi ya taifa, awekwe msalabani na kushutumiwa kwa uzalendo wake.

Taifa letu linahitaji viongozi wanaojisimamia, wanaoheshimu taaluma zao, wazalendo na wanaosema ukweli. Tunahitaji viongozi ambao wako tayari kupoteza kazi zao na vyeo vyao vikubwa kwa kutetea ukweli.

Dr.Tizeba, angeweza kusema kwamba Kituo cha Mafuta kilikuwa barabarani, kwa vile Serikali ndivyo ilivyotaka, lakini ukweli ungebaki palepale kwamba Kituo hicho hakikuwa barabarani. Serikali zinakuja na kupita, lakini ukweli unabaki na historia inaweka kumbukumbu. Tunaona jinsi hadi leo Waafrika wanavyodai fidia ya matendo ya Utumwa na ukoloni.

Hivyo mtu anayesimama kutetea ukweli, hata akipoteza kazi, akapoteza mali au hata na maisha yake, vitu hivyo havipotei bure. Vinabaki kwenye kumbukumbu iliyotukuka.

Ni bora wananchi wakatambua hili kwamba wanapomtafuta mbunge wa kuwakilisha jimbo lao ni lazima wamtafute mtu mwenye uwezo na karama ya kutetea ukweli na kuusimamia bila kuyumbishwa na vitisho, rushwa, upendeleo au ubinafsi. Bunge ni chombo muhimu katika Taifa letu. Katiba inasema: “ Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katitika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii” (Ibara 63(2)).


Hivyo hiki ni chombo muhimu kinachohitaji watu makini, wazalendo na wasioupindisha ukweli.

Tuna utamaduni kwamba mkubwa hakosei na akikosea hawezi kuomba msamaha. Lakini kwa serikali inayoongozwa na sera ya Uwazi na Ukweli, ingekuwa bora ikaomba msamaha kwa kuvunja kituo cha mafuta ambacho hakikuwa barabarani, ili akina Tizeba, wasibebeshwe msalaba usiokuwa wao!

Na,
Padri Privatus Karugendo.

TUNAWAAMINI MAMA ZETU KUTULEA KWANINI LEO TUSIWAAMINI KUTUONGOZA?

MAKALA HII ILICHAPISHWA KWENYE GAZETI LA RAI 2005

TUNAWAAMINI MAMA ZETU KUTULEA KWANINI LEO TUSIWAAMINI KUTUONGOZA?

Mambo mawili yamenisukuma kuandika makala hii. Jambo la kwanza ni maneno ya mwandishi mmoja katika mojawapo ya magazeti ya hapa nchini. Maneno hayo au maoni hayo yalikuwa yanasema hivi: “ Nakumbuka Sheikh Yahya Hussein alitabiri kwamba mteule wa CCM kugombea urais wa Muungano angekuwa mwanamke .Sasa ameteuliwa Jakaya Kikwete (mwanamume); yeye amegeuza na kusema kwamba utabiri wake upo pale pale kwa kuwa Kikwete ana sura ya nyota ya kike, Haya si matusi kwa Kikwete?” (Tanzania Daima Jumapili 12.6.2005).

Kilichonigusa kwenye maoni haya si ule utabiri wa Sheikh Yahya Hussein, bali nilikerwa na maoni ya mwandishi anayesema kwamba kuifananisha sura ya Kikwete na kusema kwamba Kikwete ana nyota ya kike ni matusi. Hili ndilo ninapenda tujadili, tuelimishane na ikiwezekana jambo hili tulikemee.

Jambo la pili ni kwamba jana wakati nikiwa bado ninatafakari kwa kina juu ya udhalilishaji na unyanyasaji huu wa kijinsia nilitembelea ofisi za shirika la KIVULINI. Shirika hili linatetea haki za wanawake na hasa limelenga kuzuia ukatili majumbani. Lina makao yake Jiji Mwanza. Si kuwa na lengo la kuamsha majadiliano juu ya mwandishi anayefikiri kumfananisha mwanaume na mwanamke ni tusi, nilikwenda kwenye ofisi hiyo kwa mambo mengine, hasa juu ya ukatili majumbani, lakini ofisi hiyo ikazua jambo jingine ambalo linahusiana kwa karibu na lile la mwandishi niliyemzungumzia kwenye jambo la kwanza lililonisukuma kuandika makala hii. Kwenye ofisi hiyo nilikaribishwa na Bango, lenye maneno: “Tunawaamini mama zetu kutulea kwa nini leo tusiwaamini kutuongoza?”.

Hili la pili lilinikumbusha lile la kwanza na kuniingiza kwenye tafakuri ya nguvu. Hili Bango la KIVULINI, lililotolewa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto kwa kushirikiana na mashirika mengine ya kutetea haki za wanawake kama TAMWA, linaweza kuzaa mabango mengine kama kwa mfano: “ Tunawapenda wanawake, kwa nini basi tusiwathamini na kuuheshimu utu wao?” au “ Mungu ,kaumba jinsia mbili, mwanamke na mwanaume, kwa nini basi jinsia moja iwe bora kuliko nyingine?”.

Bango hili la KIVULINI bila shaka lilikuwa likilenga kwenye uchaguzi mkuu unaokuja. Ni bango la kuwakumbusha wapiga kura kwamba uongozi si wa wanaume peke yao. Pia ni bango la kuwakumbusha wanawake kwamba kama wanaaminika katika malezi ni lazima waaminike katika kuongoza. Hili ni bango la kuchochea fikira juu ya usawa wa kijinsia katika maisha yote ndani ya jamii yetu. Kwamba mtu kuwa mwanamke si bahati mbaya, si dhambi na wala si tusi! Kwamba mwanamke anaweza mambo muhimu katika jamii kama vile malezi.

Lakini hata tukirudi nyuma na kuangalia maisha ya kila siku. Ukitaka kuiona hasira ya mwanaume yeyote yule katika jamii yetu mwambie yeye ni mwanamke au ana mawazo ya kike. Ni lazima yatokee magomvi makubwa. Hakuna mwanaume anayependa kufananishwa na mwanamke! Upande mwingine ukimwambia mwanamke ni shupavu kama mwanaume, au ana hekima, busara na kipaji kama mwanaume anafurahi sana, ingawa kuna ukweli kwamba kuna wanawake shupavu, wenye hekima, busara na vipaji vingi hata kuwazidi wanaume. Wanaume hawapendi kufananishwa na wanawake! Inashangaza sana, maana wanawake wanatuzaa, wanatulea, wanalinda usalama wetu tukiwa watoto hadi tunapokuwa na akili ya kujitegemea, wanatupenda, wana huruma ya hali ya juu – lakini hakuna mwanaumme anayependa kufananishwa na huruma hii na upendo huu!

Wanaume, wanawapenda wanawake na kuwatamani tu. Mtu anaweza kupoteza pesa zote na mali yote akimtafuta mwanamke aliyemvutia na kuingia moyoni mwake. Watu wanatelekeza familia na kupoteza kazi wakiwatafuta wanawake waliowavutia, wengine wanajiingiza kwenye hatari ya kuambukizwa magonjwa na wakati mwingine wanapoteza maisha yao wakipigana kuwapata wanawake waliowavutia – lakini hakuna anayependa kufananishwa na kile anachokitafuta kwa gharama yoyote ile. Hakuna mwanaume anayependa kufananishwa na kiumbe anayependwa na kupinganiwa na kila mwanaume. Hivi kweli ni tusi kufananishwa na mwanamke au kuna kasoro Fulani katika mfumo wa jamii yetu, kasoro inayohitaji tiba ya haraka?

Malaya ni mwanamke, changudoa ni mwanamke, wazinzi ni wanawake. Ndoa ikivunjika anayelaumiwa kwa kutokuwa na uaminifu ni mwanamke. Lakini Malaya anatembea na mwanaume, changudoa anatembea na mwanaume, yeyote anayezini katika hali ya kawaida ni lazima azini na mwanamke. Anayelaumiwa kwa matendo yote hayo machafu ni mwanamke! Hivi ni kweli mwanamke ndiye anayefanya yote haya au kuna kasoro Fulani katika mfumo wa jamii yetu, kasoro inayohitaji tiba ya haraka?

Kusema kwamba Jakaya Kikwete ana sura na nyota ya kike ni tusi gani? Ukweli ni kwamba Kikwete, ana baba na mama. Kama sura yake haifanani na ya baba yake, itafanana na ya mama yake – au itachangia pande zote mbili. Hata tukiingia katika mambo ya kisayansi, ni lazima Kikwete, ana chembe chembe za uhai kutoka kwa baba na mama yake. Kumfananisha na mwanamke, haina maana atageuka na kuwa mwanamke. Lakini hata hivyo mwanamke ni mtu, ni binadamu. Hakuna dhambi mwanamke kumfanana mwanaume na mwanaume kumfanana mwanamke.

Mwenye mawazo kama haya kwamba kufanana na mwanamke ni matusi asingependa kabisa mwanamke achaguliwe kushika nafasi ya uongozi. Kama kumfanana mwanamke ni tusi, itakuwaje mwanamke akishika madaraka ya kuongoza au kufanya kazi ambazo wenye mawazo potofu wanaamini ni kazi za wanaume peke yao? Maana kama kumfanana mwanamke ni tusi, basi huyu ni kiumbe asiyekuwa na nafasi na wala hafai kuwepo!

Kwa bahati nzuri TLP na NCCR-Mageuzi, wameleta mapinduzi makubwa katika mtazamo huu potofu. Wamesimamisha wanawake kuwa wagombea wenza. Hili ni jambo la kupongezwa na kuigwa. Hii ni changamoto kubwa katika jamii inayotawaliwa na mfumo dume, jamii yenye watu wanaofikiri kwamba kumfanana mwanamke ni matusi. Jamii inayoamini kwamba wanawake hawawezi kitu zaidi ya kukaa jikoni kupika na kuipendezesha nyumba. Hata hivyo na hawa wa TLP na NCC-Mageuzi bado wananuka harufu ya mfumo dume, maana kama wangetaka kufanya mapinduzi ya kweli, basi wangewasimamisha wanawake kuwa wagombea urais! Kwanini mwanamke awe mgombea mwenza, asiwe mgombea Urais? Na mwanaume akawa mgombea mwenza? Wanawake wameonyesha uwezo huu katika nchi mbalimbali, inawezekana pia na hapa Tanzania, tukikubali kubadilika.

CCM , chama “dume”, chama chenye uzoefu wa kutawala kwa miaka mingi, bado kinatawaliwa na mfumo dume! Wagombea wa urais wa Muungano na Visiwani ni wanaume. Mgombea mwenza wa Muungano ni mwanaume, na katika historia yake ya kutawala CCM hakijawahi kuwa na mwenyekiti mwanamke, rais mwanamke, makamu wa rais mwanamke, waziri kiongozi mwanamke au waziri mkuu mwanamke. Ngazi za juu katika uongozi wa chama na serikali vinashikiliwa na wanaume! Si kweli kwamba CCM, haina wanachama wanawake wenye uwezo wa kuwa mwenyekiti au rais. Wapo akina mama wengi wenye uwezo wa kuongoza. Lakini tatizo ni kama bango la KIVULINI, Linavyosema: “ Tunawaamini mama zetu kutulea kwa nini leo tusiwaamini kutuongoza?”.

Ni nani asiyeamini katika malezi ya mama yake? Ni nani asiyemwaini mama yake? Mama ni kimbilio, mama ni ufunguo wa kufunga siri zote, mama ndiye anayejua udhaifu wa kila mja na kuutunza. Kama ni mwizi, atasema mtoto wake anasingiziwa. Mama huyo awe wangu au wako, hana tofauti na mama wengine, hana tofauti na wanawake wengine. Karama za mama ni zile zile. Karama hizi zilizojaa utu na wema, upendo na uvumilivu, unyenyekevu na kusamehe kama ni matusi, basi ni heri tusi hilo!

Waswahili wana msemo usemao: “Nani kama mama?” Maana yake ni kwamba mama ana ubora uliotukuka! Huwezi kuulinganisha ubora huu na kitu chochote kile. Mama huyo ni mwanamke! Mara nyingi ninajiuliza ni kwa nini wasiseme: “Nani kama baba?”. Walioutunga msemo huu walikuwa na maana kubwa: Hakuna anayemjali mtoto wake kama Mama, hakuna anayempenda mtoto wake kama mama na hakuna anayemlea mtoto na kumlinda kama Mama. Msingi wa familia ni mama. Mama akiyumba kimaadili, familia nzima inayumba! Hivyo mama ni kiongozi wa familia. Uzoefu huu wa kuziongoza familia, unaweza kuwa mchango mkubwa wa akina mama katika kuiongoza jamii yetu. Hata hivyo jamii inajengwa juu ya msingi wa familia. Wema wa akina mama, upendo wa akina mama, uvumilivu wa akina mama, unyenyekevu wa akinamama unaweza kuchangia kujenga jamii yenye upendo, wema unyenyekevu na uvumilivu – jamii isiyokuwa na vita wala mashindano. Ni ukweli usiopingika kwamba mfumo dume, unavuruga amani popote duniani. Wanaume hawana uvumilivu na unyenyekevu, wanaume wanapenda mashindano na wamejaa uchu wa madaraka!

Bahati mbaya akina mama hawapewi nafasi ya kuongoza. Wanawake hawajitokezi kugombea ubunge na udiwani, wengi wao wanasubiri nafasi za viti maalumu. CCM, kati ya wagombea 11 walijitokeza kuwania kiti cha urais hakuna mwanamke hata mmoja aliyejitokeza! Uongozi unabaki mikononi mwa wanaume na mbaya zaidi ni kwamba jamii imewapumbaza wanawake kuamini kwamba hawawezi. Kama mtu angeandika bango jingine lingesema hivi; “ Mama zetu mna uwezo wa kulea na kuongoza, mbona mnakubali kupumbazwa kwamba hamna uwezo wa kuongoza?”

Wapiga kura wengi ni wanawake. Wangekuwa wamejikomboa na kukombolewa, ingekuwa patashika kumpitisha mgombea mwanaume. Lakini sasa hivi Ukimpanga mwanaume na mwanamke, wanawake watamchagua mwanaume na kumuacha mwanamke mwenzao. Inasikitisha, ila ndiyo hali halisi!

Kwa vile wanawake wamepumbazwa, mtu anaweza kusema chochote juu yao, na wanakaa kimya bila kujitetea. Mfano kusema kwamba kumfananisha Mheshimiwa Kikwete na mwanamke ni tusi, tulitegemea akina mama walipigie kelele. Wasimame na kupinga kwa nguvu zote. Kumfananisha Kikwete, na mwanamke ni kumfananisha na binadamu wa jinsia nyingine, si kumfananisha mheshimiwa huyu na mnyama wa aina nyingine au kitu kingine chochote kisichokuwa na uhai.

Tunahitaji mabadiliko katika jamii yetu. Tunahitaji mfumo wa kutuelekeza katika kutegemeana, kushirikiana, kukamilishana na kuthaminiana. Tunahitaji mfumo wa kuleta uwiano katika jinsia. Mfumo ambao hautukuzi jinsia moja na kuinyanyasa nyingine.

Mfumo huu ungekuwa wa kiroho zaidi ya kisiasa. Dini zingetusaidia kuwaandaa watu kiroho, ili wajenge moyo wa kupendana na kuthaminiana miongoni mwa jinsia zote. Bahati mbaya dini zote tulizonazo zinaongozwa na mfumo dume! Haziwezi kuwa za msaada mkubwa. Mfumo wowote unaotukuza jinsia moja na kunyanyasa nyingine, hauwezi kujenga amani ya kweli, hauwezi kuleta uhuru wa kweli na hauwezi kujenga umoja wa kitaifa. Kama alivyosema Mwalimu Nyerere, kwamba ukishafanya ubaguzi wa aina yoyote ile, ni lazima mzimu wa ubaguzi ukuandame kila sehemu.

Tunapofikiria na kupanga mikakati ya kuboresha uchaguzi mkuu wa mwaka huu, na hili la kujenga mifumo ya kuleta usawa wa kijinsia tuliweka kwenye agenda.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

TWAHUBIRI MAJI TUKINYWA MVINYO?

MAKALA HII ILICHAPISHWA KWENYE GAZETI LA RAI 2005

TWAHUBIRI MAJI TUKINYWA MVINYO?

Kongamano la Kimataifa la ‘Kiswahili na Utandawazi’ la maadhimisho ya Jubilii ya Miaka 75 ya Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (TUKI) lililofanyika tarehe 4 hadi 7 mwezi huu Jijini Dar-es-Salaam, limeacha changamoto nyingi nyuma yake.

Changamoto ya kwanza ni kwamba nchi zaidi ya 21 ziliwakilishwa kwenye kongamano hilo. Na si kuwakilishwa tu, bali washiriki walitoa makala kwa lugha ya Kiswahili. Nchi hizi zinafundisha na kufanya utafiti wa lugha ya Kiswahili. Na nchi nyingine zimeanza zamani. Mfano Amerika imeanza kufundisha Kiswahili mwaka wa 1945! Mwakilishi wa Nigeria, katika kongamano hilo, aliimba wimbo wa Kiswahili uliokuwa umejaa hisia kali: “Mrembo, Mrembo, Mrembo wa Moyo wangu”. Mrembo huyu ni lugha ya Kiswahili! Nigeria ni kati ya nchi yenye lugha za Kiafrika kongwe na zinazungumzwa na watu wengi, lakini bado mtu kutoka Nigeria, anakiita Kiswahili; “Mrembo wa moyo wake”!

Jambo lakushangaza zaidi, na ndio maana hii ni changamoto, ni kwamba wawakilishi wa kutoka nje ya Afrika, waliweza kujieleza na kuongea Kiswahili kizuri sana. Na si kuongea tu, bali kubuni maneno mapya ya Kiswahili na kujadili muundo mzima wa lugha Kiswahili kwa kujiamini. Mfano neno kama dolesha, likimaanisha “Index” limebuniwa na Profesa Hinnebush, kutoka Amerika. Profesa huyu amebuni maneno mengine mengi kutokana na lugha za Kiafrika kuingia katika Kiswahili.

Mfano wajumbe kutoka Amerika, Ujerumani, na Finiland, walielezea utaalamu wao wa kukiingiza Kiswahili katika kompyuta. Wamebuni na kutengeneza programu za Kiswahili. Binti mdogo kutoka Ujerumani, Raija Kramer, ambaye bado anasoma chuo kikuu kule Ujerumani, ametuachia msamiati wa Kamusi Mkondoni (Online-Dictionary). Maana yake ni kwamba kamusi na msaada wa kujifunza Kiswahili kupitia mtandao ni kitu kinachowezekana hivi sasa. Mtu anayetaka kuhakikisha anaweza kubofya kwenye: http://dictionary.it-swahili.org

Mbali na msichana huyu kulikuwa na wengine waliotoa makala juu ya matumizi ya Kiswahili kwenye mtandao. Hawa pia walijielezea kwa Kiswahili sanifu. Ukweli huu unapatikana:http:www.juasun.net/home.html
, http://www.yale.edu/swahili. Ipo na mitandao mingine mingi ambayo inatumia lugha ya Kiswahili. Hili ni jibu kwa wale wote ambao wamekuwa wakipiga kelele kwamba Kiswahili hakiwezi kuimudu teknolojia.

Profesa Hurskainen, kutoka Finland, aliwashangaza wanakongamano kwa kutumia SALAMA software kwenye Kompyuta yake kuitafsiri Hotuba ya Rais Benjamin Mkapa, kutoka kwenye Kiswahili kwenda kwenye Kiingereza kwa dakika zisizozidi tatu. Kama hii imewezekana, tunataka Kiswahili kiimudu teknolojia inayofanana vipi?

Changamoto kubwa zaidi kuhusiana na hili ninalolijadili ni kwamba washiriki hawa wa kongamano kutoka nchi za nje au niseme nje ya Afrika: Amerika, Ujerumani, Denmark, Poland, Italia,China,Korea, Japan, Finland nk, wamejifunza Kiswahili nchini kwao. Wamejifunza Kiswahili kama lugha. Si kwamba walikitumia Kiswahili kwenye masomo mengine. Lakini wanakiongea Kiswahili vizuri sana. Hivyo hoja inayotolewa kila siku kwamba watanzania watafahamu vizuri Kiingereza wakifundishwa masomo yote kwa Kiingereza, haina msingi wowote. Kama Mjerumani, anaweza kujifunza Kiswahili na kukiongea vizuri akiwa Ujerumani, kwa nini Mtanzania asijifunze Kiingereza, Kijerumani au Kifaransa kama lugha na kuiongea vizuri? Siri kubwa ya mafanikio ya hawa watu ni kwamba wanazitumia lugha zao kujifunza lugha nyingine. Wanaweza kujifunza lugha nyingine na kufanikiwa kuzifahamu vizuri kwa vile wanazifahamu vizuri lugha zao.

Tatizo letu sisi ni kwamba tunataka kutumia lugha za kigeni kujifunzia lugha za kigeni. Badala ya kutumia lugha yetu kujifunzia lugha za kigeni kama wafanyavyo watu wote duniani. Tunataka kutumia lugha za kigeni kujifunzia mambo yote ya Elimu dunia. Matokeo yake ni kwamba lugha za kigeni zinatushinda na Elimu dunia tunaipata nusu nusu. Ndio maana hata na vitu vile ambavyo viko chini ya uwezo wetu vinafanywa na watu kutoka nje ya nchi yetu. Tukizubaa zaidi hata na lugha yetu tutafundishwa na watu kutoka nje ya nchi yetu!

Changamoto ya pili kutokana na Kongamano hilo ni kwamba wale watu wanaojiita Waswahili, wale wanaosema kwamba Kiswahili ni lugha yao ya taifa, ndio wanaokiharibu Kiswahili na kukwamisha maendeleo yake. Kama alivyosema Sangai Mohochi, kutoka Chuo kikuu cha Egerton, Kenya, kwamba twahubiri maji tukinywa mvinyo! Wakati washiriki wa kongamano kutoka nje ya Afrika ya Mashariki walikuwa wanajitahidi kutoa makala zao kwa lugha ya Kiswahili, baadhi ya wajumbe wa Afrika ya Mashariki walishindwa au kukataa kutoka makala zao kwa Kiswahili. Walitumia Kiingereza! Na hawa ni watu wanaoongea Kiswahili kizuri tu. Lakini hawakupenda kutumia Kiswahili kwenye kongamano la kimataifa la Kiswahili! Profesa mmoja kutoka Kenya, alikataa kutoka makala yake kwa Kiswahili kwa vile yeye alikuwa ni mtaalamu wa lugha na makala yake ilikuwa inahusu lugha kama lugha na si Kiswahili. Lakini washiriki wengine kutoka nje ya Afrika ya Mashariki waliokuwa wanaongelea kompyuta na matumizi ya programu za kompyuta walitumia lugha ya Kiswahili!

Mfano mwingine ni kwamba hapa Tanzania baadhi ya magazeti yanatumia lugha ambayo inakiuka misingi ya Kiswahili sanifu tunachokielewa na ambacho tunawafunza wanafunzi wa Afrika ya Mashariki na ughaibuni. Mifano ni pamoja na matumizi ya lugha ifuatayo:

- Kumbe Bilali alikuwa anabip tu!
- Waziri kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, ambaye pia alikuwa akibip..
- Chadema chatangaza kutafuta staa wa kupambana na Kikwete.
- Alifariki kitandani wakati akifanya mapenzi na demu wake
Mengine ni maneno kama vile sapoti, kumpiga sachi na kombaini.

Wakati akifunga Kongamano hilo, waziri mkuu Fredrick Sumaye, alitoa mifano mingi inayotumiwa na wabunge, kwa kuchanganya Kiswahili na Kiingereza na kuzalisha maneno ambayo si Kiswahili na wala si Kiingereza. Mfano neno kama “Kusupport” si Kiswahili na wala si Kiingereza. Haya yanafanywa na watu ambao ndio wangekuwa mstari wa mbele kukiendeleza na kukitetea Kiswahili. Bahati nzuri ni kwamba viongozi wa juu serikalini wamekuwa wakiuunga mkono matumizi ya lugha ya Kiswahili. Marehemu Mwalimu, Nyerere na Mzee Mwinyi, walikuwa mstari wa mbele. Ila lisiloeleweka hadi leo hii ni kwa nini hawakuhimiza jambo hili kuwekwa kwenye katiba, ikatambulika kisheria kwamba Kiswahili ni lugha ya Taifa. Labda hii ingesaidia zaidi kuipatia lugha hii heshima yake.
HH

Mfano mwingine ni ule aliouelezea Sangai Mohochi, kwamba Katika mkutano wa kwanza wa CHAKAMA uliofanyika mjini Arusha mwezi wa saba mwaka 2002, yalikuwepo majadiliano kuhusu maswala mbalimbali yanayohusiana na upendelezaji wa lugha. Miongoni mwa mambo yaliyotajwa na wajumbe ni uundaji wa msamiati katika lugha Kiswahili. Msemaji mmoja aliitaja istilahi moja ya Kiingereza kama pendekezo lake kuelezea dhana Fulani. Mjumbe mmoja ambaye ni profesa kutoka chuo kikuu kimoja wapo cha Afrika ya Mashariki alionekana kushangaa sana. Aliona istilahi iliyokuwa imetajwa haifai kwa dhana hiyo na akasema hivi “Waweza kuchezacheza na Kiswahili lakini si Kiingereza..” Maana yake ni kwamba Kiingereza ni muhimu sana na ni lazima kiheshimiwe zaidi ya Kiswahili au kwa maneno mengine Kiingereza ni lugha yenye misingi imara! Hayo ni matamshi ya profesa anayesema Kiswahili ni lugha yake ya taifa. Anahubiri maji akinywa mvinyo!

Mfano mwingine ni kwamba kila mwaka chuo kikuu cha Byreuth nchini Ujerumani huandaa kongamano la Kiswahili linalowakutanisha wasomi na wataalamu wengine wengi wa lugha ya Kiswahili kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu. Katika kongamano la 16 la Mei 2003, wajumbe walitoka sehemu nyingi, zikiwemo: Ubelgiji, Upolandi, Urusi, Uingereza, Marekani, Kenya, Tanzania, Uturuki pamoja na wenyeji wa mkutano huo Ujerumani. Makala zote zilitolewa kwa lugha ya Kiswahili isipokuwa mjumbe wa Kenya aliyetoa makala yake kwa lugha ya Kiingereza!

Mfano mwingine ni kwamba katika mkutano wa Chama cha Masomo ya Kiarika (African Studies Association) wa mwaka 2004 ulifanyika mjini New Orleans Marekani, kuliandaliwa jopo moja kuhusu lugha ya Kiswahili. Karibu washiriki sita walitoa makala kuhusu lugha ya Kiswahili. Makala zote isipokuwa moja ziliwasilishwa kwa lugha ya Kiswahili. Hiyo moja iliyotolewa kwa Kiingereza ilitolewa na profesa wa Kiswahili mzaliwa wa Afrika ya Mashariki! Hali hii ya wataalamu wa Kiswahili kutumia lugha ya Kiingereza wakati ambapo matumizi ya Kiswahili yangesaidia kudhihirisha kujitosheleza kwa lugha hiyo haijitokezi katika mawasilisho ya makongamano na mikutano mingine ya kitaaluma tu, bali pia katika uchapishaji kwa ujumla. Kwenye majarida ya kimataifa makala za kistahili zinaandikwa zaidi na wale waliojifunza Kiswahili kama lugha. Na Waswahili wenyewe wanaandika makala nyingi kwa kisingereza au Kifaransa au lugha nyinginezo za kigeni!

Changamoto ya tatu iliyojitokeza kwenye kongamano hili la Kiswahili ni kwamba kwa upande wetu hapa Tanzania, mjadala wa kutumia Kiswahili katika kufundisha ni lazima sasa ufike mwisho. Bila kufanya hivyo tutaaibishwa pale tutakapoletewa wataalamu kutoka nje ya nchi yetu, si tu kutufundisha kwa lugha yetu, bali pia kutufundisha lugha yetu! Maana kasi hii niliyoishuhudia kwenye kongamano ya wataalamu wengi wa lugha ya Kiswahili na matumizi yake katika mtandao kutoka nje ya Tanzania inatisha. Ingawa Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, kimeonyesha jitihada ya kukiendeleza Kiswahili kwa kutengeneza programu ya kompyuta ya Kiswahili, uwiano na wale wanaofanya kazi hiyo ni ndogo. Mfano kwenye Kongamano hili tu tulikuwa na watu kutoka Amerika, Ujerumani na Finland, wanaoshughulikia programu za Kiswahili na kukiingiza Kiswahili katika kompyuta. Amerika peke yake ilikuwa na wajumbe watatu. Wote maprofesa na wote wanakifahamu Kiswahili vizuri kiasi cha kukifundisha.

Ni bahati mbaya kwamba watanzania hawakujitokeza kwa wingi kushuhudia miujiza ya lugha yao wakati wa sherehe za TUKI. Labda matangazo ya sherehe hizi hayakuwafikia wengi. Yaliweza kufika Nigeria, Uganda, Kenya, Botswana, Malawi, Rwanda, Burundi, China, Korea, Japan, Amerika, Finland, Poland, Italia, Germany, Sweden nk, yakashindwa kufika Buguruni, Tandika, Changanyikeni, Mwanza, Bukoba, Mbeya na Arusha? Ni imani yangu kwamba vyombo vya habari (kama kweli vilikuwepo) vitasaidia kusambaza ujumbe wa Kongamano kwa watanzania wote, ili wafahamu kwamba sasa hivi mjadala umefungwa. Na kama hawakubali kuufunga watalazimishwa kuufunga kwa nguvu za kutoka nje ya nchi yetu. Ni bora sasa kila Mtanzania amfahamu kwamba Kiswahili ni lugha ya kufundishia. Kazi iliyobaki ni kuliweka hili katika katiba yetu. Tukumbuke pia kwamba Titi la mama ni tamu hata kama ni la mbwa!

Na,
Padri Privatus Karugendo.

NYERERE HAKUWA MALAIKA LAKINI.......

MAKALA HII ILICHAPISHWA KATIKA GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005

NYERERE HAKUWA MALAIKA LAKINI………

Sina hakika kuwa kuna Mtanzania yeyote anayeamini kwamba Mwalimu Nyerere, hakufanya makosa katika maisha yake. Mwalimu, alikuwa binadamu kama binadamu wengine. Yeye hakuwa malaika. Shutuma za yule anayejiita Mzee Ludger Bernard Nyoni na Ambrose Mashaka, zilizoandikwa kwenye gazeti hili zikifuatana( Tanzania Daima ya Juni 12 na Juni 19) si za kweli. Hakuna aliyesema Nyerere hakufanya makosa. Alifanya makosa lakini heshima yake ikabaki hadi leo hii, alifanya makosa watu wakaendelea kumpenda. Hata baada ya kustaafu, aliendelea kupendwa na kupata heshima si Tanzania peke yake bali dunia nzima. Mwalimu ni marehemu, lakini bado tunaendelea kumpenda!

Mimi ninafikiri la kujiuliza ni kwa nini watu wengine wafanye makosa na kuandamwa hadi kaburini na wengine wafanye makosa, lakini wasiguswe kwa lolote. Heshima yao ibaki na mapenzi yao kwa watu yaendelee kuwa palepale? Hili ndilo la kujadili kwa kina. Mobutu, alifanya makosa na kila mtu anamlaumu hadi leo hii. Lumumba naye alikuwa na makosa yake, lakini hadi leo hii dunia nzima inamlilia na kumpatia sifa na upendo usiokoma!

Tutofautishe yule anayefanya makosa kwa kulishughulika tumbo lake, heshima yake na mali zake na yule anayefanya makosa akilitanguliza taifa lake mbele. Hawa wawili wakifanya makosa ni lazima yaangaliwe kwa macho tofauti. Mzee Kawawa, alifanya makosa hapa na pale, lakini hadi leo hii anapendwa na kuheshimiwa na watanzania wote. Kila mtu anampima mzee Kawawa kwa maisha yake, kwa uzalendo wake kwa uaminifu wake, uadilifu wake na mapendo yake kwa nchi. Hakujilimbikizia mali, hakuwa na mpango wa kuliuza taifa letu, hakuwa na uchu wa madaraka. Alilitumikia taifa letu kwa moyo wake wote – ingawa hapa na pale alifanya makosa, watu walimpima kwa moyo wake na nia yake njema.

Tutofautishe makosa ya kukusudia na kufanya kwa bahati mbaya. Tutofautishe makosa ya kufanya kwa hila na njama, na makosa ya kufanya kwa kuelekezwa vibaya au kudanganywa na watu wenye nia mbaya, wenye malengo ya kutafuta heshima, vyeo na madaraka. Mara nyingi watu wanaofanya makosa ya bahati mbaya wakati wakiwa kwenye utumishi wa Umma, wanaendelea kuishi maisha ya unyenyekevu na uadilifu hata baada ya kustaafu.

Mzee Ludger Bernard Nyoni katika makala yake anasema hivi: “ Profesa Mukandala anasema Malecela alikataliwa kugombea kwa sababu wajumbe walifuata ushauri wa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere, eti akiwa Waziri Mkuu, Malecela alimshauri vibaya Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi kuhusu Muungano. Kama hilo lilikuwa kosa, basi hata mzee Mwinyi mwenyewe anahusika na kosa hilo, na hakupaswa, kushiriki kikao cha kumhukumu Malecela. Si ni yeye aliyepokea ushauri huo unaoitwa mbaya? Iweje hakuna mtu hata mmoja leo anayemsema na kumhusisha na uamuzi mbovu?….”

Hili ndilo la kujadili. Kwanini Malecela alaumiwe na Mwinyi asilaumiwe? Watu wengine waliounga mkono serikali tatu mbona hawakulaumiwa? Na si hili tu wakati wa Mzee Mwinyi, kuna mambo ambayo hayakuenda vizuri sana, uchumi uliyumba na rushwa ikawa imepamba moto. Kwa vile kila Mtanzania, amegundua uadilifu wa Mzee Mwinyi, hakuna anayemgusa wala kumunyoshea kidole.

Hata kabla ya kuwa Rais wa Tanzania, Mzee Mwinyi, alifanya makosa kule Shinyanga. Hakuchelewa kuwajibika, (ni watu wachache wanaokubali kuwajibika, hata ukiwasema na kuwaandikia vitabu, bado wanakuwa kichwa maji!) na wakati anateuliwa kugombea Urais, hakuna aliyekumbuka makosa yake ya Shinyanga. Kwanini? Uadilifu wake, unyenyekevu wake, uzalendo na uaminifu wake kwa Taifa.

Hapo ndipo Bwana Ambrose achunguze hoja zake. Atokane na tabia yake ya kuwaita watu wajinga, atumie hoja kujibu hoja, si kutumia matusi kujibu hoja. Achunguze hoja hii: “ Sita, Nimewasoma wote ,na nakubaliana na hoja za Nikita Naikata. Bado ziko palepale; kwamba mgogoro kati ya Nyerere na Malecela, na ambao inadaiwa aliuandikia kitabu, ni juu ya mfumo wa serikali tatu.”

Basi kama anayoyasema Ambrose ni ya kweli watu wengi wangekuwa wakifuatwa na mzimu wa Mwalimu. Mbona mzimu huu haumwandami Mzee Mwinyi? Hata leo angetaka kugombea angepata kura! Mbona wale wote wa G 55 hakuna anayeandamwa kama Malecela?

Ndio maana mimi nikasema kwamba ugomvi wa Malecela na Nyerere, una chanzo kingine ambacho hakuna anayekijua isipokuwa Nyerere na Malecela. Ingawa Ambrose Mashaka, aliponda hoja hii kwa matusi, ukweli utabaki palepale. Bila Malecela, kusema, ukweli huo utakufa na kufunikwa na kaburi la Nyerere na Malecela! Na hii haina maana kwa vile hatujui kilichowagombanisha, tuache kujadili juu yake. Ni mambo mengi tusiyoyajua chanzo chake, lakini tunajadili juu yake na kwa kufanya hivyo tunachokoza na kuchokonoa hadi ajitokeze wa kusema ukweli na kwa hili ni Malecela, ambaye bado anaishi!

Hata kama Nyerere, alifanya makosa, leo hii kwa vile ni marehemu ndipo akina Mzee Ludger Bernard, ambaye ni mwasisi wa TANU/CCM, wanajitokeza kutuelezea makosa yake? Itusaidie nini? Walishindwa nini kumsahihisha mwalimu akiwa hai? Eti watu walikuwa wanamuongopa? Watu waoga hawezi kutusaidia kujenga Taifa letu. Walishindwa kusema Nyerere akiwa hai, sasa wakae kimya! Wakubali kuhukumiwa na historia. Kama Mwalimu alikosea basi nao waliyashiriki makosa hayo kwa kimya chao! Sisi tunamsema Malecela, kwa vile yuko hai na bado ana wajibu na mchango katika Taifa hili. Wengine wote wanaoheshimika kama Mwalimu Nyerere, Mzee Kawawa na Mzee Mwinyi, walirithisha utawala wa nchi hii wakiwa na umri wa chini ya miaka 65! Malecela, ana miaka mingapi, na bado anataka kuendelea kuwa Mbunge?

Juzi Malecela, alivunja ukimya. Kwa kile kilichoitwa kuvunja ukimya. Mbona hakuwaunga mkono wale wote wanaompigania? Amevunja ukimya kwa kuutengeneza ukimya mwingine. Amevunja ukimya kwa kutangaza kugombea Ubunge! Bado anataka kulitumikia taifa hadi kaburini, hataki kurithisha!

Huyu anayejiita Mzee Ludger Bernard Nyoni, anahoji aliyoyafanya Mwalimu, akiwa Rais, na kuuliza eti alitumwa na nani. Anajifanya haifahamu Katiba ya taifa letu inayompatia madaraka makubwa Rais. Katiba yetu ibara ya 33 hadi 46, zinaongelea madaraka ya Rais. Kama Nyerere, alifanya kinyume, basi angeshitakiwa kuivunja Katiba. Hadi anakufa sikusikia shitaka lolote juu yake la kuivunja katiba! Kumkaribisha Obote, ni kosa gani? Huyu alikuwa mkimbizi kama wakimbizi wengine. Hadi leo hii Tanzania, bado tunawatunza wakimbizi. Wakati Obote, anapinduliwa tulikuwa bado tuna Jumuiya ya Afrika Mashariki. Bila kukimbilia kwetu, angekimbilia Kenya. Hili nalo ni kosa gani? Sijasikia kwamba wanapokuja wakimbizi linaitishwa Bunge ili lifanye uamuzi wa kuwapokea au kuwakataa wakimbizi. Kuwapokea wakimbizi ni mikataba ya Umoja wa Mataifa. Tanzania ni mwanachama wa Umoja wa mataifa.

Ambrose Mashaka, anasema Nyerere, hakupinga utandawazi na Ubinafsishaji. Nisingependa kujiingiza kwenye mjadala huu bila kufahamu huyu Bwana Ambrose, anafahamu kiasi gani juu ya Utandawazi. Anafahamu kiasi gani juu ya Azimio la Arusha na Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea. Ni wazi Utandawazi ni ukoloni na utumwa katika sura mpya – lakini Mwalimu Nyerere alipinga vibaya sana ukoloni na utumwa na ndiyo maana aliendelea kupinga Utandawazi na ubinafsishaji. Ingawa Bwana Ambrose Mashaka, hapendi utafiti na uchambuzi wa kisayansi na kujifanya kuifahamu historia nina wasiwasi wa kutotaka kutumia matusi kama yeye, lakini mambo mengi yanampiga chenga.

Mfano, ni kweli kwamba Kingi, Mukandala na Nikita, wanatoka mkoa wa Kagera. Ambrose, haoni ni kwanini nitaje Mkoa wao kuhusiana na Malecela. Hiyo ni historia. Malecela, alipanda ngazi kutokea Mkoa gani? Ngome yake kubwa ilikuwa wapi? Hata hivyo hawa wanaomtetea na kumpinga si kwa vile wanataka kuchukua kiti chake cha Ubunge, hakuna atakayetoka Kagera na kugombea ubunge Dodoma! Wanamtetea na kumpinga kwa vile wanamfahamu vizuri kama Mtanzania na wala si kama Mhaya au Mgogo. Hilo Ambrose, halioni?

Wale wote wanaojitokeza kumtetea Malecela, ni bora wamshauri astaafu siasa na kubaki mshauri na mlezi wa viongozi chipukizi. Kwa njia hii heshima yake itabaki na kulindwa vinginevyo anatafuta mwisho mbaya.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

ILANI INAYOJALI NI NYENZO YA MABORESHO

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005.

ILANI INAYOJALI NI NYENZO YA MABORESHO

Mwezi huu mwanzoni zilifanyika sherehe za Serikali za mitaa. Sherehe hizi zilikuwa za pekee kwa vile ilikuwa ni mara ya kwanza kufanya tathimini ya mfumo wa maboresho unaoendeshwa katika Serikali za mitaa nchi nzima. Lengo kubwa la maboresho katika mfumo wa serikali za mitaa ni kuyapeleka madaraka kwa wananchi. Ni kulenga katika kubadilisha mfumo uliokaa kichwa chini miguu juu; ni jitihada za kuweka mambo sawa kwamba serikali inawajibika kwa wananchi. Mfumo wa maboresho unakazia utawala bora, ushirikishwaji, majadiliano, vita dhidi ya rushwa nk.
Bahati nzuri sherehe hizi zilifanyika katika kipindi ambacho nchi yetu inaelekea kwenye uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani. Ni wakati mzuri wa watu kujifunza na kujiandaa kufanya uchaguzi kwa uangalifu na kwa malengo ya kuliendeleza taifa letu.

Wakati sherehe za Serikali za mitaa zikiendelea, kijana mdogo Deusdedit Jovin, alitoa kitabu chenye jina la: Ilani ya Uchaguzi Inayojali 2005. Kitabu hiki kimechapwa na Ruvu Publishers ya Dar-es-Salaam, na hivi sasa kinauzwa kwenye duka zote za vitabu. Sina hakika kama Deusdedit, alikuwa anafikiria sherehe za Serikali za mitaa wakati akiandaa Ilani hiyo. Nijuavyo mimi na kama ambavyo mtu atakayesoma kitabu cha Ilani hii na kugundua ni kwamba madumuni ya Ilani hii ya Uchaguzi ni manne. Kwanza, inalenga kuwawezesha wapiga kura kutathimini historia ya kila mgombea katika nyanja zake kisiasa; kuwawezesha wapiga kura kutathimini usahihi wa sera za Ilani za Uchaguzi; kuwawezesha wapiga kura kujua na kuelewa haki, wajibu na majukumu ya raia katika nchi yao na kuwawezesha raia kujua na kuelewa haki na majukumu ya serikali katika dola. Malengo mawili ya awali ni ya muda mfupi kuelekea uchaguzi utakaofanyika mwezi wa Oktoba. Malengo mawili yanayofuata ni ya muda mrefu kuelekea majukumu ya uraia.

Inawezekana kitabu hicho kutoka wakati wa sherehe za Serikali za mitaa ilikuwa ni bahati tu. Ambalo halitiliwi shaka ni kwamba Deusdedit, analenga kwenye uchaguzi unaokuja. Uchaguzi mzuri ni nyenzo kubwa ya serikali za mitaa. Uchaguzi mzuri utayaboresha maboresho. Uchaguzi mzuri utayapeleka madaraka kwa wananchi bila mabishano. Kama tujuavyo hadi sasa hivi wale wanaokwamisha mpango huu wa maboresho ni watawala wanaofikiri kwamba wao ni viongozi!

Ingawa Katiba yetu iko wazi juu ya jambo hili la kupeleka madaraka kwa wananchi. Kwamba wananchi ndio wenye madaraka, hali haiko hivyo. Mwenye madaraka ni serikali na chama “tawala”. Chama kinachotawala na mtu anayetawala hawezi kupeleka madaraka kwa wananchi. Watawala wote wa dunia hii, hawakutawala kwa kupeleka madaraka kwa wananchi. Watawala hawana majadiliano, hawana mfumo wa ushirikishwaji. Daima watawala si watu wa demokrasia. Kama tujuavyo bila demokrasia ni vigumu kujenga jumuiya ya watu iliyo Uhuru. Bila Uhuru hakuna haki – bila haki ni vigumu kujenga jumuiya inayowajibika na kujali.

Kabla ya ujio wa wakoloni tulikuwa na watawala. Hawa walitawala bila demokrasia na kusema kweli watu hawakuwa huru. Uhuru wao ulikuwa mikononi mwa watawala. Hakuna ubishi kwamba watu hawa hawakuwa huru. Wakati wa ukoloni pia nchi yetu ilianguka mikononi mwa watawala. Wakoloni walikuwa watawala na wala hawakuwa viongozi, hawakuwa na demokrasia na watu hawakuwa huru.

Hata baada ya uhuru, tuliendelea kuwa chini ya watawala badala ya kuwa chini ya viongozi. Ndio maana hadi leo tuna chama tawala badala ya Chama - Kiongozi. Kutawala na kuongoza ni vitu viwili tofauti. Anayetawala anafifiza uhuru wa wananchi na anayeongoza anafunua mwanya wa ushirikishwaji na majadiliano. Kiongozi ndiye anayeweza kuleta uhuru wa kweli miongoni mwa wananchi wake. Hivyo Ilani inayojali inatuelekeza kuwachagua viongozi na wala si watawala.

Kwa kujenga hoja hii Deusdedit, anasema “ Tukichukulia kwamba familia za Tanzania ni wasafiri katika gari moshi linalotambaa katika reli ya historia kuelekea milele ijayo, basi gari moshi hili linayo mabehewa ya aina mbili, Kuna mabehewa ya abiria na mabehewa ya mzigo. Zile familia milioni tano ni abiria katika mabehewa ya mizigo, wakati familia milioni moja zilizobaki na abiria katika mabehewa ya abiria.

“Katika mabehewa ya mizigo hakuna viti! Kwa hiyo, familia milioni tano zinasafiri zikiruka kichura katika matope ya umaskini, zikipiga miayo ya njaa ya haki na kuhema kutokana na kiu ya maendeleo. Kwao elimu, huduma za afya, nyumba bora, mazingira safi na salama, maji safi na salama, mavazi, malazi, barabara na miundombinu mingine ni bidhaa adimu!

“Kwa upande mwingine, katika mabehewa ya abiria kuna viti! Hivyo, zile familia milioni moja zinapata kifungua kinywa cha chai ya maziwa na mikate iliyopakwa asali, zinakula kuku kwa mirija, na kusuuza koo kwa mvinyo baridi! Kwao elimu, huduma za afya, nyumba bora, maji safi na salama, nishati , na miundombinu mingine ni bidhaa ya kawaida. Na kwa sehemu kubwa madereva wa gari la moshi wanatokana siyo na abiria katika mabehewa ya mizigo, bali abiria katika mabehewa ya abiria!

“ Kwa kuutambua ukweli huu mchungu, tunapoelekea uchaguzi mkuu lazima tujiulize maswali ..”

Maswali haya ndio yanajitokeza katika Ilani Inayojali.

Kiongozi yoyote anayeongoza wananchi wenye madaraka, wananchi walio huru ni lazima ajue na kutambua kwamba wananchi hao wana haki zao za msingi. Kiongozi anayetambua hayo na kuyafuata ndiye kiongozi bora. Bwana Deusdedit, amejitahidi kwa kiasi alichoweza kuzitaja haki hizo na kuzielezea. Haki zenyewe ni kama: Haki ya kuheshimiwa kama binadamu, haki za kiutamaduni, haki za kuishi, haki za kisaikolojia, haki za kijinsia, haki za kijamii, haki za kiuchumi, haki za kisiasa, haki za kiakili, haki za kidini, haki za kimaadili, haki za mshikamano Kitaifa Na Kimataifa, haki za kisheria, Haki za kuwa huru dhidi ya rushwa, haki ya kuwa huru dhidi ya umaskini.
Kiongozi anayezifahamu haki hizi, hawezi kusita kuupokea mfumo wa kupeleka madaraka kwa wananchi. Hivyo jitihada zote zinazofanyika za kuboresha mfumo wa serikali za mitaa, ni lazima zizingatie Ilani hii ambayo imechomoza na kuwa na picha ya Ilani Inayo Jali.

Mfano mzuri wa yale ninayo yasema unapatikana katika kitabu hiki ukurasa 21: “ Tunataka mgombea anayeamini kwa dhati kabisa kwamba akili na utashi ndizo sifa pekee zinazomtofautisha binadamu na mnyama hayawani, na kwamba kwa sababu hii, kila mtu anastahili kupewa fursa ya kutumia akili na utashi wake bila kulaghaiwa wala kulazimishwa kwa namna yoyote ile. Kumdanganya au kumnyima mtu habari muhimu zinazomwezesha kufanya maamuzi sahihi ni kwenda kinyume na kanuni hii, kwani katika hali hii atakosa fursa ya kutumia akili yake vizuri, Vile vile kumlazimisha ni kwenda kinyume na uhuru wa utashi alio nao!”

Ukurasa wa 27, tunapata ujumbe mwingine “ Tunataka mgombea anayefahamu kwamba Tanzania ni dola inayopaswa kuongozwa, siyo kwa mujibu wa kanuni za kifalme au kiimla, bali kwa kufuta kanuni kuu nne: kanuni za demokrasi, kanuni za jamhuri, kanuni za utawala wa sheria na kanuni za shirikisho”

Kitabu chote kimesheheni ujumbe mzito. Ujumbe ambao ukizingatiwa kwa makini, si kwamba utasaidia tu katika Uchaguzi ujao, bali utakuwa nyenzo kubwa ya kuboresha Serikali za mitaa. Kilio cha Mtanzania hivi sasa ni kuwa na Serikali za mitaa zilizo imara na zilizo msingi wa Uongozi katika taifa letu.

Na
Padri Privatus Karugendo

"THE DA VINCI CODE" SI NYOKA WALA NGE

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA RAI 2005

“THE DA VINCI CODE” SI NYOKA WALA NGE


“Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtapata ;pigeni hodi, nanyi mtakaribishwa. Aombaye hupewa, atafutaye hupata, na apigaye hodi hukaribishwa. Je, kuna ye yote miongoni mwenu ambaye mtoto wake akimwomba mkate atampa jiwe? Au, je, akimwomba samaki atampa nyoka? Kama, basi nyinyi, ingawaje ni waovu, mwajua kuwapa watoto wenu vitu vizuri, hakika Baba yenu wa mbinguni atafanya zaidi: atawapa mema yote wale wanaomwomba.”( Matayo 7:7-11).

Imani ni kupiga hodi, imani ni kuomba na imani ni kutafuta. Dini zote zinaishi kwa msingi huu: ni kupiga hodi, ni kuomba na kutafuta. Tunaambiwa kwamba atafutaye hachoki hadi pale anapofanikiwa kupata anachokitafuta. Kwa vile dunia yetu ina milango mingi ya kufunguliwa kabla mtu hajafikia mwisho wa safari ya maisha yake, ni lazima mtu aishi kwa kupiga hodi hadi mwisho wa maisha yake! Hivyo kupiga hodi si kazi ndogo. Vilevile na kutafuta si kazi ya mchezo. Katika kutafuta kuna mengi, kuna kupekua, kuna kuchimba, kuna kuhoji hili na lile. Ili mtu awe Mkristu wa kweli, awe Mwislamu wa kweli au awe muumini wa kweli wa dini yoyote ile ni lazima atafute bila kuchoka. Ni lazima aombe bila kukoma. Na kama anavyosema Matayo, Baba yetu wa Mbinguni, hawezi kutoa nyoka badala ya samaki, na hawezi kutoa mawe badala ya mkate! Mtu, akiomba samaki, akapata nyoka, au akaomba mkate akapata mawe, ajue amekosea, na sala yake inakuwa haikuelekezwa kwa Baba yetu aliye mbinguni, Baba mwenye wema, haki na huruma.

Je, kanisa letu hivi sasa linatoa mkate au mawe? Linatoa nyoka au samaki? Linatoa mayai au nge? Ni kanisa la masikini au matajiri? Ni kanisa linalosikiliza, linalojali na kuwakumbatia watu wa jinsia zote? Ni kanisa lenye wema, haki na huruma? Kilio cha Theolojia ya Ukombozi ni nini? Wanyonge wana sauti katika kanisa? Walei wana nafasi gani? Wanawake na vijana wana nafasi gani katika kanisa? Kuuliza maswali haya, kuchimba na kupekua zaidi ili kubainisha ukweli huu, si kulipinga kanisa. Mwenye wasi wasi na hili, imani yake ni bandia. Ninashindwa kuuona ukasuku katika kuhoji, katika kupiga hodi. Huwezi kupiga hodi bila ya kuwa na uhakika wa usalama ulio ndani ya nyumba, huwezi kupiga hodi bila kujua malengo na madhumuni ya wenye nyumba. Na wenye nyumba ni lazima wawe na uwezo wa kuelezea nyumba yao na yote yaliyo ndani ya nyumba yao, vinginevyo wanakuwa wapangaji wa muda! Kwa maoni yangu, kasuku ni yule anayepokea kila kitu bila kuhoji. Akipokea nyoka ni sawa, akipokea samaki ni sawa, akipokea mawe ni sawa na akipokea mkate ni sawa. Huyu ndiye kasuku asiyekuwa na uchaguzi wala utashi!

Jinsi Dk.Francis Rutaiwa, anavyoshangaa kwamba itawezekana vipi John, asiwe kwenye Karamu ya mwisho,(Angalia RAI Toleo 615: “ Karugendo ameshindwaje kuchambua The Da Vinci Code”) ndivyo na sisi tunaoutafuta ukweli, tunaotafuta na kupiga hodi, tunavyoshangaa ni kwa namna gani Maria Magdalena, apotee kwenye uso wa historia ya kanisa. Kwa John, inaweza kueleweka. Hata Dk. Francis Rutaiwa, anajua fika kwamba hakuna Injili hata moja inayotaja urafiki wa karibu kati ya Yesu na John. Hakuna Injili yoyote ile inayonyesha umuhimu wa John katika maisha ya Yesu Kristu. Tunachokisikia ni kwamba kuna mtume aliyependwa sana na Yesu. Jina la mtume huyu halitajwi kwenye Injili, ni namna gani mtume huyu alibatizwa jina la John, ni jambo la kufanyiwa utafiti. Hivyo kuwepo na kutokuwepo kwa John, kwenye karamu ya mwisho si jambo la kutia shaka. Kwa Maria Magdalena, ni tofauti. Na mtu yeyote anayeficha ukweli juu ya ukaribu wake na umuhimu wake katika maisha ya Yesu, hatupatii samaki, bali nyoka, hatupatii mkate bali mawe, hatupatii mayai bali nge!:

“Yesu alipofufuka mapema Jumapili, alijionyesha kwanza kwa Maria Magdalena, ambaye Yesu alikuwa amemtoa pepo saba. Naye Maria Magdalena akaenda, akawajulisha wale waliokuwa pamoja na Yesu, na wakati huo walikuwa wanaomboleza na kulia. Lakini waliposikia ya kwamba Yesu yu hai na kwamba Maria Magdalena amemwona, hawakuamini” ( Marko 16:9-10).

Injili zote nne zinakubali kwamba Maria Magdalena, ndiye alikuwa mtu wa kwanza kumshuhudia Yesu mfufuka. Imani ya Kikristu, ina msingi mkubwa katika kufa na kufufuka kwa Yesu Kristu. Tendo la ufufuko si jambo la kawaida na si jambo ambalo watu wangeweza kulikubali kwa urahisi. Inashagaza kuona Yesu, anaamua msalaba huu wa kushuhudia ufufuko wake kuuweka mikononi mwa Maria Magdalena, badala ya kuuweka mikononi mwa John, Petero au mitume wengine wanaume! Inawezekanaje mtu huyu aliyeaminiwa na Yesu hivyo, apotee kabisa katika uso wa sura ya historia ya Kanisa? Kuuliza swali hili si kulipinga kanisa. Ni kutaka kuutafuta ukweli. Jinsi umuhimu wa Maria Magdalena, unavyofunikwa ndivyo wanawake wote wananyimwa nafasi ya msingi katika kanisa, na hasa katika kanisa katoliki. Kuna ushahidi wa kutosha kuonyesha jinsi kanisa la mwanzo lilivyoongozwa na kutunzwa na wanawake. Ukweli huu unajionyesha kwenye matendo ya mitume na kwenye barua za mtakatifu Paulo. Hata hivyo Yesu mwenyewe na umati wake walitunzwa na wanawake!( Luka 8:1-3).

“Basi, Maria alichukua chupa ya marashi ya nardo safi ya thamani kubwa, akampaka Yesu miguu na kuipangusa kwa nywele zake. Nyumba yote ikajaa harufu ya marashi.”(Yohana 12:3).

Kitendo hiki kilileta utata na mashaka makubwa miongoni mwa mitume. Hawakupenda ukaribu ulioonyeshwa na Maria Magdalena kwa Yesu. Walitegemea Yesu, amkaripie na kumlaani. Lakini ukweli ni huu:

“Huyu mama amenimiminia marashi ili kunitayarisha kwa maziko. Nawaambieni hakika, po pote ulimwenguni, ambapo Habari Njema itakapohubiriwa, tendo hili alilofanya litatajwa kwa kumkumbuka yeye” (Matayo 26:12-13).

Tendo hili linatajwa wapi katika Kanisa Katoliki? Ni nani anayemkumbuka Maria Magdalena kwa tendo lake alilofanya la kuisafisha miguu ya Yesu Kristu? Uzushi wa Dan Brown, uko wapi? Kanisa linawakumbuka mitume wanaume peke yao. Kanisa la Mtakatifu Petero, la Roma, limepambwa na sanamu za mitume wanaume. Hakuna sanamu ya kuonyesha kumbukumbu ya Maria Magdalena, akisafisha miguu ya Yesu Kristu. Yanakumbukwa mambo mengine, lakini yale ambayo Yesu, mwenye alisema yatakumbukwa yametupwa kapuni! Kwanini mtu anayeisoma Injili kwa makini na kutafakari asihoji jambo hili, kwa nini isionekane wazi kwamba kuna kusudi la kuficha ukweli? Kuna tatizo gani Maria Magdalena, akipewa hadhi sawa sawa na Mtakatifu Petero? Kuna tatizo gani mwanamke akiwa Padri, Askofu, Kadinali au Papa? Ni wapi Kristu mwenyewe alipoelekeza kwamba wanawake wasishike nafasi ya uongozi?

“Walipokuwa katika safari, waliingia katika kijiji kimoja. Hapo mwanamke mmoja, aitwaye Marta, akamkaribisha. Marta alikuwa na dada yake aitwaye Maria; huyu aliketi karibu na Yesu akisikiliza mafundisho yake. Marta, lakini alikuwa anashughulika na mambo mengi ya kufanya. Basi, akamwendea Yesu, akamwambia, ‘Bwana, hivi hujali hata kidogo kwamba dada yangu ameniacha nitumikie peke yangu? Mwambie basi anisaidie.’ Lakini Bwana akamjibu, ‘ Marta wee, unahangaika na kusumbuka kwa ajili ya vitu vingi. Kitu kimoja tu ni cha lazima. Maria amechagua kitu bora zaidi ambacho hakuna mtu atakayekiondoa kwake.” ( Matayo 10:38-42).

Hiki kitu alichokichagua Maria ni kitu gani? Ni kitu gani hiki ambacho hata Yesu, ambaye ni Mungu, anakitambua kwamba ni kitu muhimu na bora? Ni kitu gani hiki ambacho Yesu, anasema kwamba hakuna mtu atakayekiondoa kwake? Tunaambiwa kwamba Maria, alikuwa ameketi karibu na Yesu, akisikiliza mafundisho yake. Inawezekana kitu hicho ni Neno la Mungu? Inawezekana Maria Magdalena, ni mtu pekee aliyelisikia neno la Mungu na kulishika? Inawezekana neno hili ndilo lililompatia moyo wa ujasiri wa kumfuata Yesu hadi msalabani? Ujasiri ambao hatuusikii kwa mitume wanaume? Inawezekana ndio sababu iliyomsukuma Yesu, kujionyesha kwanza kwa Maria Magdalena, baada ya ufufuko?

“Mtu akinipenda atashika neno langu, na Baba yangu atampenda, nasi tutakuja kwake na kukaa naye.”( Yohane”( Yohane14:23).

Je, inawezekana kile kitu alichokipata Maria Magdalena, ni kwamba Baba na Mwana walikuja kwake na kukaa naye? Inawezekana kwa njia hii Maria Magdalena, alishiriki Umungu wa Kristu? Maana kutokana na yale tunayoyasoma kwenye Injili, ni kwamba Maria Magdalena, alimpenda Yesu Kristu. Na kama alimpenda, alilishika neno lake, na kama alilishika neno lake ni lazima Baba na Mwana walikuja na kukaa naye? Na kama hili ni kweli, basi huyu ndiye mwamba wa kuwa msingi wa kanisa la Yesu Kristu! Inawezekana sifa anayopewa Mtakatifu Petero, ni ya Maria Magdalena? Injili ya Magdalena, inafichuzwa ugomvi mkubwa uliokuwepo kati ya Maria Magdalena na Mtakatifu Petero; uvomvi uliokuwa unasababishwa na wivu. Hata hivyo Injili nyingine zinaonyesha kwamba hakukuwa na uaminifu kati ya Petero na Maria Magdalena, maana Petero, hakuamini ujumbe wa Maria Magdalena, kwamba Yesu amefufuka hadi yeye aliposhuhudia Kaburi wazi!

Sifa hii ya mtu kuwa na kitu bora na muhimu; “ Maria amechagua kitu bora zaidi ambacho hakuna mtu atakayekiondoa kwake”, tunaisikia kwa Maria Magdalena peke yake. Pia, sifa ya mtu kukumbukwa siku zote; “ Nawaambieni hakika, po pote ulimwenguni, ambapo Habari Njema itakapohubiriwa, tendo hili alilofanya litatajwa kwa kumkumbuka yeye”, tunaisikia kwa Maria Magdalena peke yake. Sifa ya mtu wa kumshuhudia Yesu Mfufuka, kitu ambacho ni msingi wa imani ya Kikristu, anayo Maria Magdalena. Iwe je tena mtu mwenye sifa zote nyeti, afutike kabisa katika uso wa historia ya kanisa?

Ingawa Dan Brown, analileta hili kwa njia ya riwaya, haina maana ni kitu cha kipuuzi. Riwaya, zina mafundisho, riwaya zinaubeba ukweli wa maisha katika jamii. Riwaya zinatumika kuielimisha jamii. Yesu, mwenyewe alitumia riwaya, katika mafundisho yake. Msamaria mwema ni riwaya, mtoto mpotevu ni riwaya. Kuna riwaya nyingi katika mafundisho ya Yesu Kristu. Hata Agano la kale, limetawaliwa na riwaya tupu!

Tunataka tusitake sasa hivi dunia inapita katika changamoto kubwa. Kuna maswali mengi yanayohitaji majibu. Kanisa kama sehemu ya dunia, haliwezi kukaa pembeni, ni lazima lishirikiane na dunia nzima kutoa majibu; kama linatoa samaki liseme linatoa samaki, kama linatoa nyoka liseme linatoa nyoka na ni kwa nini, kama linatoa mikate, liseme linatoa mikate, na kama linatoa mawe, liseme ni kwa nini, kama linatoa mayai liseme na kama linatoa nge liseme ni kwa nini. Sasa hivi dunia nzima inaongea lugha ya demokrasia, je kanisa linaongea lugha hii? Sasa hivi dunia inakazania majadiliano na ushirikishwaji, je kanisa linayazingatia haya? Kuna swala zima na usawa wa kijinsia na vita dhidi ya mfumo dume, je Kanisa, na hasa kanisa katoliki linasema nini kuhusiana na wimbi hili la mageuzi?

Ndio maana mimi nikawaomba Maaskofu wetu na wanateolojia wakisome kitabu cha “The Da Vinci Code”, ili waweze kutuongoza katika mjadala huu ambao haukwepeki na waweze kutufungulia mlango wa nyumba yenye ukweli na usalama. Jaziba, imani ya woga na unafiki, uongo, kupindisha ukweli na matusi kama ya Dk.Francis Rutaiwa, haviwezi kutufikisha mbali!

Na,
Padri Privatus Karugendo.

KUTOKA TANGANYIKA KWENDA TANZANIA

Tuesday, August 02, 2005


MAKALA HII ILICHWAPWA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005


KUTOKA TANGANYIKA KWENDA TANZANIA.


Ninaandika makala hii nikiwa Tanganyika! Nisieleweke vibaya. Mimi siko kwenye kikundi cha wale wanaotaka serikali tatu: Ya Muungano, Ya Tanganyika na ya Visiwani. Mimi ni mfuasi wa wale wanaotaka serikali mbili, ya Muungano na ya Visiwani. Pamoja na msimamo wangu huo, ukweli ni kwamba sasa hivi niko Tanganyika! Nimemaliza juma zima bila kusikia radio yoyote ile ya Tanzania! Si kwamba mimi sina uzalendo, hapana, hata ningetamani vipi kusikiliza RFA, Radio Tanzania na nyinginezo, isingewezekana! Ni bahati kwamba ninaweza kunasa radio za Rwanda na Uganda! Wale wenye uwezo kidogo, wanaweza hata kunasa luninga za Rwanda na Uganda. Kwa njia hii mtu akiwa Tanganyika, atapata habari za nchi jirani kuliko habari za nchi yake mwenyewe! Ikiwa bahati magazeti yakafika Tanganyika, basi yatakuwa ni ya siku tatu au nne zilizopita! Inawezekana kupata gazeti la siku hiyo la nchi ya jirani, lakini ndoto kupata gazeti la siku hiyo katika maeneo ya Tanganyika. Mtandao wa Voda na Celtel unapatikana kwa kupanda juu ya mti au kusimama kwenye vichuguu! Ni bahati kwamba sikuuugua, ningeshambuliwa na malaria, labda ungekuwa ni mwisho wa maisha yangu. Nimeshuhudia vifo vya watoto wadogo ambavyo kama si kuishi Tanganyika, basi watoto hao wasingepoteza maisha yao! Umbali wa kilomita 40, nauli ni shilingi 1,500 hadi 2,000! Ukilinganisha na Tanzania, ambako kwa nauli hiyo mtu anatembea zaidi ya kilometa 150! Gari dogo lenye uwezo wa kupakia watu wanne tu, linapakia zaidi ya watu kumi!

Inawezekana ile Tanganyika ya kabla ya uhuru ilikuwa bora kuliko Tanganyika ya leo. Sina maana ya kuubeza uhuru tulioupata, lengo langu ni kubeza hali ya kuangalia maendeleo ya upande mmoja tu. Maendeleo ya Tanzania, maendeleo ya mijini, maendeleo ya watu wachache, bila kuangalia maendeleo ya taifa zima la Tanzania.

Si nia yangu kuweka chumvi, lakini soda inayonunuliwa kwa shilingi 200 Tanzania, hapa Tanganyika inanunuliwa shilingi 350! Chupa ya bia inayonunuliwa shilingi 900 hadi 1000 kule Tanzania, hapa Tanganyika, inanunuliwa 1,300!

Tanganyika hakuna maji. Hakuna umeme na hakuna huduma nyingi muhimu. Watu wanatembea zaidi ya kilometa 5 hadi 10 kutafuta maji. Wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 1995, mbunge wa Tanganyika, alitoa ahadi ya kusambaza maji kwenye jimbo lake, sasa miaka kumi imepita bila ahadi hii kutekelezwa! Mbali na ahadi hii ya maji kuna ahadi nyingine zilizotolewa, ahadi ambazo zinafanana na nyingine zinazotolewa kwenye maeneo mengi ambayo yanajumuika kuitengeneza Tanganyika, iliyo tofauti na Tanzania.

Hakuna barabara ya lami Tanganyika. Sasa hivi wakati wa kiangazi ni vumbi mtindo mmoja. Udongo wenyewe ni mwekundu, hivyo sasa hivi kila kitu ni rangi nyekundu. Wakati wa mvua vumbi inageuka kuwa matope na kusababisha utelezi na kukwamisha usafiri.

Nimeongea na watu mbali mbali wa hapa Tanganyika. Maoni yao hayatofautiani na yale ya Watanganyika wengine wanaoishi maeneo mengine ya Tanganyika. Wengi wao wana maoni kwamba Tanzania, ni mijini na Tanganyika ni vijijini. Hata hivyo wale waliofanikiwa kutembea sehemu mbali mbali za nchi yetu wanatofautisha vijiji na vijiji. Wanasema huwezi kulinganisha vijiji vya mkoa wa Kilimanjaro na vijiji vya mikoa mingine mfano na vya Tanganyika, hii niliyomo. Lakini kwa ujumla vijiji vingi vya Tanzania, vinaishi Tanganyika! Havina tofauti kubwa, matatizo yanafanana: Ukosefu wa barabara, umeme, maji na huduma nyingine kama hospitali na shule bora.
Umeme, utaukuta mijini, ingawa miji mingine haina umeme wa uhakika, lakini unawaka. Maji ya bomba utayakuta mijini, ingawa pia, miji mingine usambazaji wa maji ni wa matatizo, lakini huduma hii inapatikana ukilinganisha na wale wanaoishi Tanganyika. Huduma ya hospitali zenye uhakika, unazikuta mijini. Shule zenye huduma nzuri unazikuta mijini. Jitihada zote za maendeleo zimeelekezwa mijini. Ingawa ukweli unabaki pale pale kwamba asilimia ya watanzania walio wengi wanaishi vijijini.

Kishawishi cha wale walio wengi ni kufanya safari ya kutoka Tanganyika kwenda Tanzania. Kutoka vijijini kwenda Mijini. Hii ni safari ambayo sasa hivi ni vigumu sana kuizuia.

Jambo linaloshangaza, ambalo mpaka sasa sina jibu lake ni kwamba, kule Tanzania, ambako kuna huduma za kila aina, kule ambako uchumi wake ni mzuri kiasi, kila kitu kinakuwa na bei nafuu. Lakini Tanganyika, ambako huduma ni mashaka, uchumi unachechemea, watu wana maisha magumu, kila kitu ni cha bei ya juu. Sukari bei juu, mafuta ya taa bei juu, soda bei juu, nauli bei juu! Inakuwaje wenye kipato wanunue vitu kwa bei ya chini na wale wasiokuwa na kipato walipe bei ya juu?

Ni nani atafika Tanzania, atamani kurudi Tanganyika? Sasa hivi kuna mipango ya kuwakusanya vijana wote wanaoishi mijini bila kazi kuwasukuma vijijini. Eti waende wakalime! Kwa maana nyingine watoke kwenye maisha nafuu na kwenda kwenye maisha ya juu. Watoke kule ambako vitu vinanunuliwa kwa bei ya nafuu, waende kule ambako vitu ni bei ya juu.

Kwa muda wa juma moja nilioishi Tanganyika, nitapinga kwa nguvu zangu zote nikisikia mpango wa kuwarudisha vijana vijijini. Warudi kule kufanya nini? Kwa nini tuwalazimishe vijana wetu kuendelea kuishi Tanganyika, wakati neema zote ziko Tanzania? Kwani vijana waendelee kuishi vijijini wakati maisha ya neema yako mijini?

Sasa hivi ni kipindi cha uchaguzi. Wale wote wanaotegemea kugombea nafasi za ubunge wanaikimbia Tanzania na kuelekea Tanganyika. Wanakuja na ahadi nyingi za maji, barabara, shule, mahospitali nk. Baada ya uchaguzi, wanaanza tena kukiikimbia Tanganyika na kuelekea Tanzania! Tanganyika, ni maandalizi ya Tanzania! Vijiji ndivyo vinavyoandaa maisha bora na yenye neema ya mijini. Na kwa bahati mbaya vijiji hivyo vinaendelea kuogelea katika dimbwi la umasikini!

Mtu yeyote kama yupo, atakayetaka kuzuia wakimbizi wa kutoka Tanganyika, kwenda Tanzania, ni lazima afanye jitihada kubwa ya kuitokomeza Tanganyika. Jitihada ya kueneza huduma muhimu nchi nzima. Jitihada za kuleta neema na maisha bora sehemu zote za nchi yetu, iwe vijijini na wala si mijini. Isitokee soda inayonunuliwa shilingi 200 sehemu moja ya nchi iuzwe shilingi 350 sehemu nyingine ya nchi ileile. Isitokee watu kufa kwa kushindwa kupata huduma ya hospitali. Isitokee sehemu moja ya nchi watu wanakula na kusaza na kutupa wakati sehemu nyingine ya nchi watu wanakufa kwa
njaa.

Hizi siku nilizomaliza hapa Tanganyika, nilijawa na mawazo mengi kichwani mwangu. Hivi viongozi wetu wanaotaka kuchaguliwa kuliongoza taifa letu wanafahamu kwamba nchi yetu bado imegawanyika katika sehemu mbili kubwa? Wanajua kwamba bado tuna Tanganyika na Tanzania? Wanajua kwamba kuna watanzania ambao bado hawana huduma ya maji, umeme, hospitali, mashule na hawana chakula cha kutosha? Wanajua kwamba watu wengine wanaishi kwenye neema kubwa wakati wengine wanaishi kwenye Jehanamu? Na je, wana sera gani ya kutokomeza matabaka haya ambayo yanaendelea kuongezeka? Na, je ni lini tutaimaliza safari hii ya kutoka Tanganyika kuelekea Tanzania? Ni lini Tanzania, itakuwa moja, yenye neema, amani na maisha tele?

Na,
Padri Privatus Karugendo.

DIRA YA UCHAGUZI: KUJALI MANUFAA YA WOTE

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005

DIRA YA UCHAGUZI: KUJALI MANUFAA YA WOTE.

Maaskofu wa Kanisa katoliki la Tanzania wametoa barua yao ya kiuchungaji ikilenga uchaguzi mkuu ujao. Kwa lugha nyingine wametoa Ilani yao ya uchaguzi. Ilani hii inaungana na nyingine nyingi ambazo zimekwisha kutolewa na makundi mbali mbali, dini mbali mbali, vyama vya siasa na watu binafsi. Ni jambo la kutia moyo kuona kwamba watanzania wengi wanalitakia mema taifa letu. Maana Ilani zote zinasisitiza utawala bora, utawala wa kidemokrasia, ushirikishwaji, mshikamano nk.

Ningependa kuamini kwamba wale wote wanaotunga Ilani hizi wanakuwa hawalengi kitu Fulani kinachoitwa “Serikali”, wanakuwa wanaelekeza Ilani zao kwa watanzania wote na wao wakiwemo! Wakisisitiza demokrasia, basi wao watakuwa wa kwanza kuhakikisha demokrasia inafuatwa. Litakuwa jambo la kushaganza wakihubiri demokrasia wakati wao wanaishi kinyume na demokrasia, Wakihubiri rushwa, basi wao wawe mstari wa mbele kuipinga rushwa na matunda yake: Wazikatae sadaka zinazonuka harufu ya rushwa, na waikatae misaada inayoelekea kupatikana kwa njia za rushwa. Wakiongelea kupiga vita umasikini, wawe ni watu wanaoufahamu vizuri umasikini, mtu anayetembelea VX, usafiri wa ndege na nyumba ya kifahari atakuwa si mkweli akiongelea umasikini. Wakiongelea kutetea ukweli, basi wao wawe wa kweli kiasi cha kutotia shaka: Si ukweli wa CCM, CHADEMA, TLP, Kanisa Katoliki, Anglikana au Islam, uwe ukweli wa watanzania wote!

Kwamfano Maaskofu wetu wanasema:
“ Sisi Maaskofu wa Kanisa Katoliki la Tanzania, tukiongozwa na Imani, tunao wajibu na mwito wa kudhihirisha hazina ya Mungu iliyo ndani mwetu katika utukufu wa Mungu Baba. Hii ni pamoja utayari wetu wa kupigania ukweli siku zote tukiamini kuwa Mungu yuko upande wetu kila tunapobaki waaminifu kwake” (Ufu 2: 10,11; Ybs 4:23).

Kwa vile barua hii ya kiuchungaji imeelekezwa kwenye uchaguzi mkuu, ninakuwa na kishawishi cha kufikiri kwamba ni ya watanzania wote. Hivyo basi Ukweli wanaosema kwamba wako tayari kuupigania ni ukweli wa namna gani? Ni ukweli unaokubaliwa na watanzania wote? Waislamu, Wakristu, Wahindu na wale wa dini za jadi. Je ni ukweli ambao wangependa watu wengine waushike na kuufuata, au ni ukweli ambao ni wajibu nao kuufuata? Hata Kibwetere, aliwachoma waumini wake moto akitetea ukweli kwamba muda wao wa kuishi duniani ulikuwa umefikia kikomo, na Mungu, aliwahitaji watu wake kule Mbinguni!

Maaskofu wanataja wasia waliopewa na Marehemu Baba Mtakatifu Papa Yohana Paulo wa pili:
“ Ushirikiano kati ya Kanisa na Serikali katika mambo mhimu yahusuyo jamii unapaswa kuongezwa; na ni matumaini yangu kwamba wengine watafuata njia mliyoonyesha katika jambo hili. Nina hakika kwamba wataendelea kuhimiza kwamba hatua madhubuti zinaandaliwa ili kupunguza umaskini na kuongeza utoaji wa elimu kwa madhumuni ya kuwawezesha maskini kusaidiana wao kwa wao” (Vatikani Machi 11, 2005).

Je, ni nani atawafanya maskini wasaidiane wao kwa wao? Matajiri wanaweza kuwasaidia maskini Je, maaskofu wetu wako kwenye kundi gani? La matajiri au maskini? Je, elimu inatolewa? Kanisa linawasaidia vipi wale wasioweza kulipia elimu? Je Kanisa linatoa elimu ya Mungu (Theolojia) kwa watu wote? Bila theolojia, watu watapata mwanga mzuri wa maadili, imani na umaana wa maisha ya hapa duniani? Tuangalie hali yenyewe. Kama Ilani hii ni ya watanzania wote, ni bora kutafakari kwa makini juu ya maneno haya ya Marehemu Papa Paulo wa Pili. Kama hii ni ilani tunayoiweka mbele yetu, maana yake nini? Ni lazima tujue maskini ni nani, na ni nani wa kuhimiza maskini kusaidiana, kwa hali ya kawaida ni vigumu tajiri kuhimiza maskini kusaidiana! Na ni vigumu mtu asiyekuwa na mwanga wa elimu, kutoa mwanga kwa wengine.

Ukurasa wa sita wa Ilani hii, maaskofu wanasema hivi: “ Uchaguzi wa tarehe 30 Oktoba, 2005 ni nafasi pia kwa watu kutoa maoni yao, kueleza mahitaji yao na kupendekeza mambo yanayopaswa kufanyika katika eneo lao wanamoishi. Kwa hiyo, uchaguzi sio tu kwenda kupiga kura bali ni kushiriki pia katika mikutano ya kampeni ili kupata fursa ya kuuuliza wagombea maswali juu ya maoni na mapendekezo yao katika kutengeneza na kutekeleza sera za nchi.”

Ni kiasi gani maaskofu wetu wanawaruhusu waumini kutoa maoni yao, kuelezea mahitaji yao au kutunga sera juu ya mambo mbali mbali katika imani yao. Wanafamilia wanashirikishwa na kusikilizwa kiasi gani? Maana kama maaskofu wetu wanashinikiza ushirikishwaji ni lazima wawe mstari wa mbele kuonyesha ushirikishwaji kwa matendo!

“ Tunapaswa kulinda kwa uangalifu maisha ya familia. Huo ndio msingi wa jamii yetu ambayo leo hii inakabiliwa na mabadiliko mengi yanayodhoofisha uhai wa familia. Sera za umma lazima ziwe makini ili kuweka miongozo na taratibu za kuimarisha na kulinda ndoa, kutoa fursa ya elimu kwa watoto na vijana wetu, kushughulikia vema matatizo ya afya na magonjwa ambayo kwa watu wetu ni ya hatari na nje kabisa ya uwezo wao kugharimia tiba yake; kuweka sera safi ya upatikanaji makazi bora kwa familia changa na kuwezesha kila mwananchi apate pato la uishi maisha ya kiutu. Virusi vya UKIMWI (VVU) na maradhi ya ukimwi yamesababisha hali tete ya familia kwa kiasi kibaya vile kwamba akina mama na watoto ndio wahanga wakuu wa janga hili”.

Je, maaskofu wetu wenyewe wanazishughulikia kiasi gani ndoa hizi? Maana hakuna kitu kinachohofisha uhai wa familia kama maandalizi mabovu. Msimamo wao juu ya matumizi ya Kondomu, umeziingiza ndoa nyingi kwenye matata na hatari kubwa. Familia nyingi ziko hatarini kufyekwa na ugonjwa huu wa UKIMWI. Ilani yao hii inakuja na msimamo gani? Ni kutetea uhai au kupinga uhai? Ni kutetea ukweli au kipinga ukweli. Wengine wanasema kwamba ukweli ni kwamba Kondomu inazuia asilimia 98 maambukizo ya virusi vya UKIMWI. Maaskofu wanasema ukweli ni uaminifu na kuacha kabisa. Ukiingia kwenye ukweli wenyewe ni kwamba uaminifu na kuacha kabisa ni vitu ambavyo havijulikani hapa duniani!

Hata tukiachana na UKIWMI, na kuliangalia swala lote na ndoa na familia. Ni kiasi gani Maaskofu wetu wanajihusisha na maandalizi ya ndoa. Mafundisho ya siku tatu wakati vijana wanajiandaa kufunga ndoa yanatosha kuiandaa familia ili ipokee changamoto za kijamii na kuweza kuwa msingi imara wa jamii? Ni wapi vijana wetu wanafundishwa mahusiano? Je, tutazilinda vipi hizi ndoa kama hakuna maandalizi ya kuzijenga? Maaskofu wetu hawana familia, wanaishi nje ya familia, hawayajui matatizo na changamoto ya familia, wanawezaje kuziongelea familia? Ni kujidanganya kutoa Ilani ya kitu mtu asichokifahamu vizuri wala kukiishi. Waumini, wanaweza kutoa Ilani inayogusia familia, si Maaskofu!

Maaskofu wetu wanasema hivi:
“ Ni ukweli usiofichika kwamba mfumo huo wa soko huria unawanufaisha tu wale walio katika uchumi rasmi mkubwa kutokana na kukua kwa uchumi. Wengi wa watu wetu wamo katika shughuli ndogondogo za uzalishaji mijini na wengi mno wako vijijini wakijishughulisha na shughuli ndogo za ufugaji, uvuvi na kilimo cha kujikimu tu. Mipango yetu ya uchumi haiwajali vya kutosha hao wote. Katika ziara zetu za kiuchungaji tunakutana na hali ngumu za maisha ya watu wetu vijijini na miji. Kama Taifa tunapaswa kuliangalia tatizo hili kwa makini zaidi na kulitafutia marekebisho ya haraka”.

Ni kweli kwamba Maaskofu wetu wanaijua hali ngumu ya watu kule vijijini? Wanajua maana mtu kwenda kuteka maji zaidi kilomita tano? Wanajua matatizo ya usafiri? Wanajua matatizo ya kukoswa matibabu? Mbona watu hao maskini wa vijijini hawakomi kutoa sadaka? Wanashindwa kuwatibisha watoto wao, lakini wanapata pesa za sadaka? Ni nani wa kuwaelimisha kwamba badala ya kutoa sadaka, wanunue dawa za watoto, maana maisha ya watoto ni muhimu sana kuliko sadaka. Je, hii ni kazi ya kitu kinachoitwa serikali?

Ni vyema kuandika Ilani. Ni imani yangu kwamba ni wajibu wa maaskofu wetu, lakini hoja ni je, maaskofu wetu wanaitekeleza Ilani hii kwa matendo? Je inawahusu nao pia au ni kitu wanachotaka kifanywe na wengine?

Na,
Padri Privatus Karugendo.

JUKWAA LA KIMATAIFA LA WANANCHI

MAKALA HII ILICHAPWA KWENYE GAZETI LA RAI 2005


JUKWAA LA KIMATAIFA LA WANANCHI

Niungame wazi kwamba kabla ya kuhudhuria warsha juu ya Jukwaa La Kimataifa La wananchi, iliyofanyika kikanda(Mwanza, Kagera na Mara) Bukoba, tarehe 27 na 28 mwezi huu, nilikuwa sijapata kusikia lolote juu ya jukwaa hili. Nina imani si mimi peke yangu ambaye hakuwa na habari juu ya kitu hiki. Mwanzo mwa warsha, hata wanawarsha wengine walionyesha dalili za kutofahamu vizuri Jukwaa hili maana yake nini.

Nilivyokuwa nikishangaa juu ya Jukwaa hili ndivyo na warsha wengine walivyokuwa wakishangaa. Mbali na Jukwaa lenyewe kulikuwa na mambo mengine ya kushangaza kidogo katika warsha hii. Mfano, tulikuwa na wawezeshaji wawili. Mmoja kijana sana miaka 24 na mwingine mzee wa makamo miaka 54? Jinsi walivyokuwa wakishirikiana na kuendesha warsha kwa amani na utulivu ni jambo la kushangaza kidogo. Lakini pia kijana mdogo huyo kutoka Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, alionyesha ukweli kwamba na vijana wanaweza na kwamba Jukwaa la Wananchi, ni wananchi wote, vijana, wazee, wanawake, wasiojiweza nk. Labda kwa vile nimeanza kuongelea mambo ya kushangaza ni bora nidokeze na hili. Kwamba wana warsha wa kutoka Mwanza ma Mara, walishangaa sana kusikia kwamba “Mwekezaji” aliyeukarabati uwanja wa Kaitaba, uwanja ambao wananchi wa Kagera, waliamini ni mali yao na wamekuwa wakiutumia kwa shughuli mbali mbali, kama vile sherehe za Saba saba, Nane nane na maonyesho ya Kilimo, mwaka huu wamezuiwa kuutumia! Sherehe za Nane nane za mwaka huu zitafanyika nje ya uwanja katika maeneo ambayo hayaendani na shughuli kama hizo. Shida ni kwamba “Mwekezaji” amekatalia uwanja wake! Kwa vile warsha ilikuwa juu ya Jukwaa la Wananchi, wanawarsha walisema hilo ni la kushikia bango. Mwekezaji mwingine, ameamua kujenga Choo, kando kando ya Ziwa! Labda, na wawekezaji wengine wataamua kuendelea kujenga vyoo kando kando ya choo. Kama huyu hajakemewa na kushikiwa bango, basi na wengine watajifunza! Hayo ni ya Bukoba, wakati vuguvugu la uchaguzi linashika kasi. Niendelee na mada yetu: Jukwaa la Kimataifa la Wananchi. Lakini pia ni imani yangu kwamba baadhi ya watanzania wana habari juu ya Jukwaa hili, maana warsha iliyoendeshwa Bukoba, ilikuwa ya mwisho kati ya warsha zilioendeshwa kikanda nchi nzima. Warsha hizi zimeendeshwa Kanda ya Zanzibar, inayounganisha Unguja na Pemba, Kanda ya kusini, inayounganisha Lindi na Mtwara, Kanda ya Nyanda za juu, inayounganisha Ruvuma, Mbeya na Rukwa, Kanda ya mashariki, inayoziunganisha Coast, Morogoro, Iringa na Tanga, Kanda ya magharibi, inayoziunganisha, Shinyanga, Dodoma na Kigoma.

Pamoja na ukweli huu kwamba Jukwaa hili limekwisha sambaa nchi nzima, bado nina wasiwasi kwamba kuna baadhi ya watanzania ambao hawajapata kusikia kitu chochote juu ya Jukwaa hili.

Jukwaa la Kimataifa la Wananchi “ Citizen’ Global Platform” (CGP), ni Jukwaa la Kiraia lililoanzishwa kutokana na mchakato wa Helsinki, ambao ni mchakato mwingine unaohusu masuala ya Utandawazi na Demokrasia ulioanzishwa na Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje za Tanzania na Finland ( Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete wa Tanzania na Mheshimiwa Erkki Tuomioja wa Finland)- linalidhamiria kuboresha demokrasia na kuthamini uwazi kati ya nchi za kaskazini na zile za Kusini kwa kuongeza ushirikiano. Jukwaa hili lina agenda kuu katika Utandawazi na Demokrasia.

Mchakato wa Helsinki, una malengo mazuri ambayo bila ufuatiliaji yataozea kwenye karatasi kama mipango mingine mizuri inayoibuka na kuzama bila ya kutekelezwa. Malengo ya mchakato huu ni: - Kuongeza demokrasia na usawa katika ushirikiano wa kimataifa kwa kuwezesha kuwepo kwa uwanja mpana wa majadiliano wenye kujumuisha watu wengi, Kuendeleza ushirika uliojikita katika usawa wa makundi mbalimbali ya kijamii ya kiwemo ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali kutoka pande zote, kusini na kaskazini mwa utawala wa kidunia. Kuwawezesha washika dau kuunda nguvu za pamoja ili kuleta mabadiliko ya lazima katika utawala wa kidunia. Kusaidia ushiriki na ushirikishwaji wa mawazo ya watu wa kusini na vyama vya kiraia katika uundaji wa sera zenye mrengo wa kidunia. Kukuza na kusaidia michakato ya kidemokrasia ya watu wengi iliyojikita katika Tamko la Milenia la Umoja wa Mataifa ili kupunguza umaskini.

Hivyo basi, vyama vya kiraia vya nchi hizi mbili(Tanzania na Finland) viliamua kuansisha jukwaa hili liitwalo Jukwaa la Kimataifa la Wananchi la Tanzania, ili kuhakikisha sauti za vyama vya kiraia zinasikika kwenye masuala ya kuiendesha dunia hii au utoaji maamuzi. Jukwaa la Kimataifa la Wananchi la Tanzania lilianzishwa kutoa nafasi na njia za kupata nguvu/uwezo jamii ya karaia kuweza kutoa mawazo mbadala na kuwa na sauti juu ya demokrasia na wakati wa kutoa maamuzi hasa yale yanayofanywa kimataifa.

Kama sehemu ya uanzilishi wake, baadhi ya malengo ya kuanzisha jukwaa hili la Kimataifa la Wananchi hapa nchini yalikuwa ni kupima matarajio, matumaini na utendaji bora wa jamii ya kiraia. Kituo cha Huduma za Kimaendeleo cha Finland (KEPA) na United Nations Association (UNA Finland) kwa upande mmoja, na Umoja wa AZISE Tanzania (TANGO) na UNA Tanzania kwa upande mwingine, wanaendesha mradi huu (Jukwaa la Kimataifa la Wananchi) kwa pamoja.
Tangu kuzinduliwa kwa Jukwaa hili mnamo mwezi Juni Mwaka 2004, limetekeza masuala kadhaa yaliyosaidia kukuza uelewa wa jamii ya kiraia nchini hasa juu ya masuala ya kimataifa. Lakini ukweli ni kwamba Jukwaa hili lilikuwa halijafika kwa wananchi walio wengi. Uamuzi wa kuendesha warsha nchi nzima zinazowakutanisha washiriki kutoka mashirika yaliyo katika ngazi ya mkoa na wilaya walio wanachama wa TANGO na UNA, mashirika changamfu, viongozi wa serikali za mitaa, madiwani, na waandishi/vyombo vya habari kwa kuzingatia usawa wa kijinsia, wanawake, vijana, wanaume na wenye ulemavu, mwaka huu ulikuwa unalenga kulisogeza Jukwaa hili kwa wananchi. Lengo kuu likiwa ni kufikisha ujumbe na maamuzi yaliyomo katika ripoti ya mwisho ya mchakato wa Helsinki kwa wananchi walio wengi wa Tanzania na kujaribu kuona kama wananchi wanaweza kuanzisha majukwaa yao wenyewe madogo kwa ngazi zile walizomo ili kukuza demokrasia na kuhakikisha kunakuwa na utandawazi wenye kujali watu na haki za binadamu.

Ili kuweza kuainisha vizuri mambo ya kujifunza kutoka Kusini na Kaskazini Jukwaa la Raia la Kiulimwengu limeelekeza jitihada zake katika makundi matatu ya kimkokoto:
- Njia mbadala za utatuzi wa matatizo ya kidunia
- Ajenda ya Uchumi ya Kidunia
- Usalama wa Binadamu.

Hali ya sasa ya ulimwengu haiwavutii wengi. Matatizo mengi yaliyopo duniani hivi sasa yanavuka mipaka ya kijiografia na kisiasa. Kwa kiasi kikubwa mifumo ya kimataifa imeleta matatizo mengi hivi sasa kuliko huko nyuma. Matatizo kama: Umaskini, ukosefu wa usawa, tofauti za kiuchumi na kiteknolojia, demokrasia na utawala bora na nchi kuwa na maamuzi huru yanahitaji ufumbuzi mpya, chini ya mfumo mpya wa kiulimwengu. Kwa njia tunahitaji njia mbadala za utatuzi wa matatizo ya kidunia. Njia mbadala ni lazima iwe inazingatia Ushirikiano, ushiriki na kuzingatia mpango wa maendeleo ya Milenia.


Mashirika ya kimataifa ya uchumi kama; Benki ya dunia (WB), shirika la fedha la kimataifa (IMF), na shirika la biashara la kimataifa (WTO) yamepoteza uhalali na mvuto katika mtazamo wa watu wengi, kwa mwonekano wa wengi yanajitokeza kama kivuli cha ubabe wa mataifa tajiri na njia ya kukandamiza mataifa yanayoendelea, hali hii ikidhihirishwa na uwepo wa umaskini wa kutisha wa mataifa mengi ya kusini na huku pengo kati ya nchi tajiri na maskini likiendelea kukua siku hadi siku. Hali hii inatulazimisha kuwa na ajenda ya uchumi ya dunia. Mkokoto huu unajaribu kuibua mapendekezo katika nyanja ya uchumi wa Dunia ukiwa na lengo la kutengeneza mfumo mzuri wa uchumi wa dunia katika mtazamo wa kuwepo na utadawazi wenye kunufaisha wengi. Ni lazima kuwepo mfumo thabiti/imara wa uchumi wa kimataifa.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa kuona hatari nyingi zinazomwelekea binadamu wa kawaida kama athari za asili na zinazosababishwa na binadamu, aliamua kuunda Tume ya Usawa wa Binadamu mnamo Januari mwaka 2000. Tume, iliyoundwa na watu mashuhuri duniani, ilipewa muda wa miaka miwili yaani baina ya 2001-2003. Masuala yaliyolengwa yalijumuisha migogoro, maendeleo na kusikiliza kero za watu walio katika mazingira yasiyo salama. Shughuli kubwa katika usalama wa kibinadamu ni namna ya kupunguza mfumo usio sawa kiuchumi na kisiasa. Hivyo ajenda ya Usalama wa Binadamu ni muhimu na ni bora kujadiliwa katika ngazi za chini katika jamii kupitia mifumo kama hii ya Jukwaa la Raia la Kiulimwengu.

Maoni yaliyotoka kwenye warsha zilizofanyika nchi nzima yataunganishwa kwenye mkutano utakao fanyika mwezi wa nane katikati kule Dar-es-Salaam, ili kupata sauti ya pamoja ya wawakilishi wa Tanzania, katika mkutano wa Helsinki utakaofanyika Septemba 7-9 2005, utakao angalia ni jinsi gani wabunge wetu wanashiriki kuhakikisha taasisi za kimataifa zinawajibika, ni jinsi gani nchi wahisani zinatimiza ahadi zao za kufikia malengo ya maendeleo ya milenia na ni jinsi gani mataifa ya dunia yanakabiliana na tatizo la dunia la maswala ya afya.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

TABIA HIZI ZITAENDELEA HADI LINI?

MAKALA HII LICHAPISHWA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005.

TABIA HIZI ZITAENDELEA HADI LINI?

Tarehe 23 mwezi huu kuna ugeni mkubwa Wilayani Magu. Ni ugeni wa kimataifa. Tunasikia kwamba Rais Benjamin William Mkapa, ataambatana na marais wengine watatu wa nchi jirani kufungua awamu ya pili ya mradi wa TASAF wilayani Magu. Habari zinazopatikana ni kwamba Wilaya ya Magu, imefanya vizuri kwenye utekelezaji wa mradi wa TASAF awamu ya kwanza. Kwa vile mradi huu unaendeshwa kwenye nchi nyingine za Afrika, basi marais wageni watakuja kujifunza Magu.

Wenyeji wa Magu, wanakubali kwamba TASAF, imefanya kazi nzuri kwa upande wa mashule, mahospitali na majengo, lakini mradi wa barabara na madaraja imeboronga! Hayo ni maoni ya wenyeji, lakini msemaji mkuu ni serikali. Hivyo ni lazima tuamini kwamba TASAF, ya Magu, imefanya kazi nzuri na ni haki ya Magu, kuupata ugeni mkubwa na kupongezwa.

Kwamba TASAF, imefanya vizuri au vibaya si lengo la makala hii. Na wala si lengo la makala hii kuuliza Magu, kuna nini. Mbali na TASAF, kuna mambo mengi Magu, mfano wavuvi wadogo wanaendelea kunyanyaswa kiasi hawezi kulifaidi ziwa linalowazunguka, uvuvi haramu unaendelea na kushamiri, huku wavuvi wadogo wakisingiziwa kwa uvuvi huo, ambavyo ukweli ni kwamba vigogo ndio wanaongoza miradi hiyo ya uvuvi haramu na viwanda vya samaki vya Wahindi vinaendeleza biashara ya unyanyasaji. Magu, ni wilaya iliyoshambuliwa sana na ugonjwa wa UKIMWI kwa vyanzo ambavyo si kazi ngumu kuvidhibiti! Uzembe kutojali na kutowajibika watu wanaendelea kufa na kuambukizwa virusi. Magu kuna mengi, watumishi wa serikali hawana nyumba, barabara mbovu na tatizo la huduma ya maji. Ni mengi na baadhi rais atasomewa kwenye risala! Lengo la makala hii ni kuhoji tabia zilizozoeleka tangia uhuru za kufanya maandalizi makubwa na kutumia pesa nyingi wakati kiongozi wa ngazi za juu na hasa rais anapotembelea sehemu mbalimbali.

Wanaoijua historia ya nchi hii wanasema kwamba Mwalimu Nyerere, alikataa kulala kwenye nyumba Fulani wakati anatembea mikoani kwa sababu nyumba ilikuwa inanuka harufu ya rangi. Inawezekana nyumba hiyo ilipakwa rangi masaa machache kabla ya Mwalimu kuwasili. Ipo mifano mingine ya namna hii na mingine ni vituko vya mwaka. Mfano shamba la mahindi liliopandikizwa miche iliyokuwa imeng’olewa kutoka kwenye shamba jingine. Mwalimu hakuchelewa kugundua ujanja huo. Viongozi hao waliwajibishwa.

Karne hii kuendeleza vitendo vya kuandaa mazingira mazuri kwa vile rais anatembelea sehemu Fulani ni kurudisha nyuma maendeleo. Si busara kusimamisha kazi kwa vile Rais, anatembelea sehemu Fulani. Rais anapoitembelea sehemu Fulani, anakuwa kazini na wala si likizo ya kula, kunywa na kucheza ngoma. Kama anakagua utekelezaji ni lazima awakute watu kazini. Nchi zilizoendelea zinafanya hivyo. Ni upuuzi mtupu kutumia pesa nyingi kwenye vinywaji na viburudisho vingine wakati wa kufungua miradi ya maendeleo ambayo karibu nusu yake ni mkopo.

Sasa hivi kuna maandalizi makali mjini Magu. Wiki hii nzima inayotangulia ujio wa Rais Mkapa, ofisi zimefungwa. Wakubwa wote wa wilaya, wilaya za jirani na hata kutoka Mkoani, wanakimbia huku na kule kuandaa ujio wa rais. Haya ndio anayapinga Mheshimiwa Lipumba. Kazi zinasimama, ingawa watu hawa watalipwa mshahara kamili mwishoni mwa mwezi. Nchi zilizoendelea mtu hulipwa mshahara kufuatana na masaa aliyofanya kazi. Hakuna mtu katika nchi zilizoendelea analipwa kwa kumaliza juma zima bila kuingia ofisini eti kwa vile alikuwa akiandaa ujio wa rais. Haya yanafanywa na nchi tajiri kama Tanzania!!

Mji wa Magu, ambao ni mchafu siku zote, sasa unasafishwa usiku na mchana. Takataka zilizokuwa zikizagaa kila kona ya mji sasa zinasombwa na kupelekwa kusikojulikana. Mji wa Magu haukuwa na choo( Public toilet), sasa choo inajengwa usiku na mchana! Uwanja wa Sabasaba ambao ni maarufu kwa shughuli kubwa za kijumuia kama vile sherehe za kiserikali, kijadi, soko na mnada, haukuwa na choo. Kwa vile rais Mkapa, atakaribishwa kwenye uwanja huu, choo inajengwa usiku na mchana. Choo hii inajengwa na wafungwa, Wanajenga kwa malipo au kama sehemu ya adhabu ya kifungo chao, ni maswali ya kujibiwa na viongozi wa wilaya ya Magu.

Wafungwa wanashinda wanachimba choo siku nzima, bila chakula bila maji ya kunywa. Hakuna anayejali utu wao au haki zao zi kibinadamu. Kazi ni moja, choo ziwe tayari kabla ya ujio wa rais! Kazi ni moja, sifa! Ili Rais awasifu viongozi wa Magu, kwamba wana (Public Toilet). Na baada ya ujioa wa Rais, Mbunge, ashike bango kwamba aliwajengea watu vyoo kwenye uwanja wa soko. Atumie bango hilo kuombea kura!

Swala hili la vyoo limelalamikiwa na watu wengi. Waandishi wa habari wameandika juu ya jambo hili, hakuna lililotendeka hadi ujio wa Rais. Maana yake ni nini? Ni kwamba uwezo na nyenzo za kujenga vyoo zipo, tatizo hakuna mtu wa kuwasukuma watendaji kutimiza wajibu zao. Au ni kwa vile mbunge hakai kwenye jimbo lake, anakuja wakati wa kuomba kura! Haya si maendeleo na wala si uwajibikaji!

Mbaya zaidi, watoto wa shule za msingi na walimu wao wanakatisha vipindi kufanya kazi za kusafisha uwanja wa sabasaba na maandalizi mengine kama nyimbo, ngoma na burudani nyingine. Hii ni dhambi kubwa tunayowatendea watoto wetu. Badala ya kukaa darasani na kujifunza tunawatumia kufanya kazi ambazo si zao. Haya si maendeleo na wala si uwajibikaji ni unyanyasaji wa watoto!

Ni vyema Rais, kuwatembelea watu wake na kukagua miradi ya maendeleo. Lakini si kitendo cha maendeleo watoto kukatisha masomo kuandaa ujio wa rais. Hata hivyo si kazi ya watoto wa shule kusafisha uwanja wa sabasaba ambao uko kwenye maeneo ya mji. Hizi ni kazi ambazo Halmashauri ya Wilaya inawajibika kuzishughulikia.

Barabara za Mji wa Magu, zimejaa mashimo. Sasa hivi mashimo haya yanazibwa na barabara zinaanza kupendeza. Akiondoka rais, barabara zitarudia hali yake ya kawaida!

Mji wa Magu, una tatizo sugu la Maji. Inawezekana kupita mwezi, bila sehemu Fulani ya mji kupata mgao wa maji kutoka idara ya Maji. Sasa hivi kwa vile kuna ugeni wa Rais, maji hayakatiki. Akiondoka Rais, anaondoka na maji. Matatizo yanakuwa ni yale yale.

Mishahara ya wafanyakazi wa Halmashauri inachelewa kila mwezi. Kisingizio ni kwamba hakuna pesa. Lakini pesa za kutengeneza barabara, kukarabati huduma ya maji, kujenga vyoo, kusafisha mji, kujenga vibanda, kununua vinywaji na vyakula vya msafara wa rais, zinapatikana! Kwani zipatikane pesa nyingi za kutengeneza mambo ya muda, na zisipatikane pesa za kutengeneza vitu vya kudumu na ambavyo ni muhimu?

Viongozi wanaokumbuka wajibu zao kwa vile rais anakuja kuwatembelea, si viongozi wanaolifaa taifa letu wakati huu tunapopigana kujiingiza katika mifumo ya utandawazi, soko huria, demokrasia, utawala bora na uwajibikaji.

Nimeandika makala hii kabla rais hajatembelea Wilaya ya Magu. Ni bora wasaidizi wake waisome na kumpatia habari. Aje akijua kwamba barabara nzuri atakazoziona mjini Magu, Usafi wa mji wa Magu, huduma ya maji na huduma nyingine za jamii kama vile vyoo, ni vitu vilivyoshughulikiwa wiki moja kabla ya ziara yake. Tena ajue kwamba watoto wa shule walikatisha masomo ili kuandaa ujio wake.

Wananchi wanakerwa kabisa na tabia za viongozi hawa wanaoshindwa kuwajibika hadi Rais, atakapowatembelea. Kwa vile hakuna jukwaa la maoni, wananchi wanabaki na hasira. Hivyo ni bora Rais, akakemea tabia hizi za viongozi wachovu. Na pale panapobidi si dhambi viongozi kama hawa kuwaomba wakastaafu kwa manufaa ya Umma. Kwa vile Rais Mkapa, anaelekea mwisho wa utawala wake, ni vyema akaacha amesafisha njia kwa yule atakayerithi nafasi yake. Hii itamsaidia mfuasi wake maana hataanza kazi kwa kupanda chuki ya kuwatimua viongozi wabovu. Pamoja na yote hayo, Karibu Magu, Rais wetu mpendwa na msafara wako. Karibu mgeni mwenyeji apone!

Na,
Padri Privatus Karugendo.

JABIR IDRISSA

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005.

JABIR IDRISSA

Nimeshangazwa sana na mahojiano baina ya Waziri wa Habari wa Zanzibar na BBC kuhusiana na mwandishi Jabir Idrissa. Waziri wa Habari wa Zanzibar, anasema Jabir, amezuiwa kuandika makala zake kutoka Zanzibar, kwa vile hana cheti, kibali au kwa maneno mengine hayuko kwenye orodha ya waandishi wa habari wa Zanzibar, wanaotambulika! Kufuatana na maelezo yake Jabir, amekuwa akiandika kwa kuvunja sheria ya habari ya Zanzibar. Sheria hiyo ilitajwa na kifungu chake, mimi sikuona umuhimu wa kuikumbuka!

Sitaki kujifanya mtaalam wa sheria. Inawezekana kweli Jabir Idrissa, amevunja sheria ingawa si kwamba ameanza kuandika leo! Amevunja sheria au hakuivunja sheria hiyo ni kazi ya mahakama! Ukweli ni kwamba mtu yeyote aliyesikiliza mahojiano hayo atakubaliana na mimi kwamba sababu zilizotolewa hazijitoshelezi. Zilielekea kuwa sababu za kisiasa zaidi ya sababu za kulisaidia taifa letu na watu wake!

Kinachonishangaza ni kuona Waziri wa habari, anashindwa kutofautisha kati ya mwandishi wa habari anayetoa “Hard story” na mwandishi anayeandika kuchambua mambo Fulani katika jamii. Hili ndilo ninataka kuongelea. Hivi ni vitu viwili tofauti. Kuandika habari na kuchambua habari si kitu kile kile. Ninafikiri hapa tunahitaji msaada wa wataalam waliobobea katika uandishi wa habari ili watusaidie kuondoa utata huu ambao inaelekea utakwamisha maendeleo ya Taifa letu na kurudisha nyumba demokrasia na uhuru wa vyombo vya habari.

Unajua Kiswahili chetu ndio hivyo bado kina misamiati michache. Watu wamekuwa wakichanga mambo haya. Mwandishi wa habari na mwandishi wa makala wote wanaitwa waandishi wa habari. Ni kweli kwamba wote ni waandishi, lakini uandishi una aina mbali mbali na sheria mbali mbali. Huwezi kumlinganisha mwandishi wa habari (hard story) kwenye gazeti na mwandishi wa vitabu au mwandishi wa mashairi, tenzi, barua na nyimbo.

Jabir, alikuwa akiandika makala na wala si “Hard Story”. Yeye alikuwa hafanyi kazi ya kutoa ripoti juu matukio, bali alikuwa akichambua, akichokoza mawazo na kuchochea watu kufikiri na kutafakari juu ya matukio mbali mbali katika jamii yetu. Mtu kufikiri, kutafakari na kushirikisha wengine yale aliyoyatafakari anahitaji cheti gani, kibali gani, orodha gani na sheria gani? Kuandika makala ni sawa na kuandika kitabu. Tuna vitabu vingi vya hadithi vyenye mafundisho na uchambuzi wa mambo mbali mbali. Waandishi wa vitabu hivi wanapata kibali gani na kuifuata sheria gani?

Kuandika makala ni sawa na kutunga mashairi. Tuna watu wengi wanatunga mashairi mbalimbali kuhusu siasa, uchumi, dini, maadili, malumbano na wakati mwingine matusi. Washairi hawa ni wengi na wanaandika kwenye magazeti mbali mbali. Wanapata kibali gani na kuifuata sheria gani?

Kuandika makala ni sawa na kutunga mchezo wa kuigiza kama ile tunayoiangalia kwenye Luninga, mfano kama Wingu, Sayari, Taswira, Uhondo wa Ngoma, Jakamoyo nk. Watunzi wa michezo hii wanapata vibali gani na kuifuata sheria gani?

Kuandika makala ni sawa kutunga wimbo unaochambua mambo mbali mbali katika jamii. Saida Karoli, anapotunga nyimbo zake, anapata kibali gani na kufuata sheria gani? Kuna nyimbo mpya za kizazi kipya zinachipuka kila kukicha na zimesheheni ujumbe na uchambuzi mzito. Nyimbo hizi zinaimbwa kwenye redio, kwenye luninga – zinawafikia watanzania wote. Vijana hawa wanapata kibali gani na wanafuata sheria gani.

Kuandika makala ni sawa na kutunga wimbo wa taarabu. Zanzibar inajulikana kwa taarabu. Tujuavyo taarabu zina ujumbe mwingi, vijembe, matusi, siasa, uchambuzi, kusifia serikali, kuibeza serikali nk. Watunzi wa taarabu wanapata vibali gani na wanafuata sheria gani?

Kuandika makala ni aina fulani ya usanii kama vile kuchonga vinyago au kuchora picha. Jinsi makala inavyotoa ujumbe ndivyo hivyo hivyo vinyago na michoro vinatoa ujumbe. Vinyago vingi vinabeba ujumbe mzito. Kwa mtu anayeguswa na usanii atapata ujumbe sawa na yule anayesoma makala kwa kuangalia tu kinyago. Watu wengi wanapenda kuangalia katuni kwenye magazeti – mara nyingi katuni zinabeba ujumbe mzito, nyingine zinasifia serikali, nyingine zinaichambua serikali, nyingine za kuchochea na nyingine za kuunga mkono jitihada za serikali. Hawa wanaochora katuni wanapata vibali gani na kufuata sheria gani?

Kuandika makala ni sawa na mtu kutoa maoni yake kwenye redio au luninga. Tunasikia watu wakihojiwa kwenye redio mbali mbali. BBC, VOA, Sauti ya Ujerumani nk, hawa wanapata vibali gani na wanafuata sheria gani. Barua za maoni tunazozisikia kwenye redio mbali mbali zinaandikwa kwa kibali gani na kwa sheria gani?

Makala ni barua ya maoni iliyoandikwa kwa urefu, kwa kuzingatia utafiti, ukweli na umuhimu wa mada inayozungumziwa. Katika gazeti la RAI, makala ya Jabir Idrissa, inaitiwa Waraka Kutoka Unguja. Makala ni barua ya wazi kwa jamii. Ni kibali gani na sheria gani inahitajika kwa mtu kuandika barua kwa rafiki zake, ndugu zake na watanzania wenzake?

Kuandika makala kwenye gazeti ni sawa na kuandika makala kwenye Blogu ndani ya mtandao. Watu wanaoandika makala kwenye Blogu zao ndani ya mtandao wanapata kibali gani na wanafuata sheria gani? Jabir, anazuiwa kuandika kwenye magazeti, lakini makala zake zitawekwa kwenye mtandao. Ni vigumu kuingia kwenye mtandao na kuzizuia makala za Jabir. Ni imani yangu kwamba watanzania wengi sasa hivi wanasoma habari ndani ya mtandao. Hali hii ya kumzuia Jabir, kuandika inaonyesha jinsi Serikali ya Zanzibar ilivyobaki nyuma ya wakati na bado inakumbatia mifumo ya kizamani.

Kama kuna sheria ya kumzuia mtu kufikiri, kutafakari kuwa mbunifu na kuwashirikisha wengine, tafakari zake na ubunifu wake, basi sheria hiyo ni batili na imepitwa na wakati. Si sheria ya kuitumia wakati huu. Tutachekwa na dunia nzima!

Wito wangu ni kwa vyombo vya habari vyote kushirikiana kumtetea Jabir. Kuruhusu hili litendeke Zanzibar, ni kuliruhusu litendeke bara pia. Kuliruhusu hili litendeke kwa Jabir, ni kuliruhusu litendeke kwa mwingine pia. Vyombo vya habari vionyeshe ushirikiano wa kutetea uhuru wa vyombo vya habari na uhuru wa watu kutoa maoni bila vitisho.

Siwezi kushangaa kusikia kwamba Jabir Idrissa, si Mzanzibari. Hizi ndizo silaha za watu walifilisika kisiasa, watu wasioheshimu uhuru wa vyombo vya habari na haki ya mtu kujieleza na kutoa mawazo.

Leo ni Jabir Idrissa, jana ilikuwa Nabwa na kesho ni mwingine. Ni lazima tufikie mahali tukue, tutoke katika utoto na ujinga wa kisiasa. Dunia yetu imeingia kwenye utandawazi kiasi ni vigumu kuendelea kucheza michezo ya kitoto. Utamzuia mtu kuandika kwenye gazeti, lakini huwezi kumzuia kuingia kwenye mtandao na kuendelea kueneza mawazo yake dunia nzima.

Binafsi ninaona, badala ya kumfungia Jabir, kuandika, kitu ambacho hakina maana yoyote ile zaidi ya kuonyesha ulimwengu kwamba sisi bado tuko gizani, ni bora angejitokeza mtu kule Zanzibar, wa kukanusha yote anayoyaandika Jabir. Kwa njia hii kutazuka mjadala na majadiliano na mwishowe ukweli utajitenga na Uongo.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

MTU KUVUTIWA NA JINSIA YAKE

MAKALA HII LICHAPWA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005.

MTU KUVUTIWA NA JINSIA YAKE

Tunataka tusitake, ni lazima sasa tuanze kujadili juu ya tukio la Padri Kulawiti. Hili si tatizo la Kanisa katoliki peke yake. Ni tatizo la dunia nzima iliyokubali kujiingiza kwenye kijiji kimoja cha utandawazi. Misamiati kama ushoga na usagaji limekuwa jambo la kawaida. Tumeanza kushuhudia ndoa za mashoga na wasagaji. Huu si wakati wa kukaa kimya na kuendelea kufunika mambo, kuendeleza “usiri” na kukaribisha giza badala ya mwanga. Huu ni wakati wa majadiliano, utafiti, kuelimishana na kusaidiana.

Tarehe 1Oktoba 1986 Kadinali Ratzinger (sasa ni Papa Benedict wa 16), alitoa mwongozo wa Kanisa Katoliki juu ya watu wanaovutiwa na jinsia zao (homosexuality). Mwongozo huu ilikuwa ni barua aliyowaandikia Maaskofu wote wa Kanisa Katoliki:
“ON THE PASTORAL CARE OF HOMOSEXUALS”. Katika barua hii Kadinali Ratzinger, aliwakumbusha maaskofu juu ya mwongozo mwingine kuhusu swala hili hili uliotolewa Desemba 1975: “ Declaration of Certain Questions Concerning Sexual Ethics” uliosisitiza kwamba hali ya mtu kuvutiwa na jinsia yake ifanyiwe utafiti na ichukuliwe kwa uangalifu na busara.

Katika barua hiyo Kadinali Ratzinger, aliwashauri maaskofu kwamba hali ya mtu kuvutiwa na jinsia yake inahitaji wachungaji (mapadri) wenye kufanya utafiti kwa uangalifu mkubwa, wenye kujali, wa kweli na wenye theolojia isiyokuwa ya msimamo mkali.

Ingawa Kadinali Ratzinger, anapinga hali hii na kuiona kama hali Fulani ya ugonjwa na kufanya mambo kinyume na maumbile, anashauri watu wenye matatizo ya kuvutiwa na jinsia zao wasitengwe. Wapatiwe huduma za kiroho, washauriwe na kuvumiliwa hadi pale watakapobadilika.

Tatizo linalojitokeza kwenye barua hii ni kwamba Kadinali Ratzinger, anapinga hali hii kwa kutumia biblia. Msingi mkubwa wa hoja yake ni Biblia. Mfano anatumia kitabu cha mwanzo ambacho kinaelezea kwamba Mungu, aliwaumba Mwanamke na Mwanaume. Pia katika agano jipya anatoa mifano ya Mtakatifu Paulo anapolaani vitendo vya kulawiti na kufira.

Kama nilivyosema mwanzoni mwa makala hii kwamba matendo ya ushogo na usagaji si matatizo ya Wakristu peke yao. Haya ni matatizo ya dunia nzima. Hivyo kuyapinga ni lazima tuwe na misingi inayokubalika kwa watu wote. Ikibidi na sayansi itumike. Si watu wote wanaoamini kuumbwa kwa mwanamke na mwanaume kama kunavyoelezwa kwenye Biblia. Hata hivyo si watu wote wanaoiamini Biblia.

Lakini hata ukitumia biblia utakutana na changamoto. Ebu tuangalie mistari hii kutoka kwenye barua ya kwanza ya Paulo kwa wakorinto:
“ Au, je, hamjui kwamba watu wabaya hawataurithi Utawala wa Mungu? Msijidanganye! Watu wanaoishi maisha ya uasherati, wanaoabudu sanamu, wafiraji au walawiti, wanyang’anyi, wachoyo, walevi, wenye kusengenya, walaghai, hao wote hawatashiriki Utawala wa Mungu” (1Wakorinto 1:9).

Wakati sisi tunaishikia bango kubwa hali ya mtu kuvutiwa na jinsia yake, wakati tunalaani matendo ya kulawiti, kufira, usenge, ushoga na usagaji, Paulo, anazichanganya dhambi hizi na dhambi nyinginezo kama vile uchoyo, ulevi, kusengenya na kulaghai. Na bahati mbaya hakutofautisha ili kuonyesha ni dhambi ipi ni ndogo na ipi ni kubwa. Kama ushoga na usagaji zingelikuwa ni dhambi kubwa kuliko nyingine, basi Paulo, angezitaja peke yake ili kuuonyesha mkazo. Lakini yeye anaziweka kwenye ngazi moja na dhambi nyingine. Tuna watu wangapi katika jamii zetu wanaosema uongo, walevi, walaghai na wanaosengenya? Na je hawa tumewashikia bango mara ngapi kama tunavyowashikia mashoga? Je, wachoyo ni wangapi? Dunia yetu imegawanyika katika makundi ya maskini na matajiri kwa sababu uchoyo wa mali ni mkubwa sana. Hili tumelishikia bango? Hili tunalilaani kama tunayolaani ushoga na usagaji? Katika hali ya kawaida uchoyo wa mali ni dhambi kubwa, maana uchoyo wa mali unasababisha vita, mashindano na kuvuruga amani katika dunia yetu. Ushoga umeleta vita? Umeleta matabaka katika jamii? Hili ni jambo la kujadiliana kwa kina na wala si kulipinga kwa kufuata mkumbo.

Pia tukiangalia Barua ya Paulo kwa Waroma tutakutana na kitu kilele:
“ Kwa hiyo, Mungu amewaacha wafuate tamaa mbaya. Hata wanawake wanabadili matumizi yanayopatana na maumbile ya miili yao kwa yale yasiyopatana na maumbile. Nao wanaume hali kadhalika, wanaacha kufuata matumizi ya maumbile ya mume na mke wakawakiana tamaa wao kwa wao. Wanaume wanafanyiana mambo ya aibu, na hivyo wanajiletea wenyewe adhabu wanayostahili kwa vitendo vyao viovu…Wamejaa kila aina ya uovu, dhuluma, ulafi na ufisadi. Wamejaa wivu, uuaji, ugomvi, udanganyifu na nia mbaya; husengenya, na kusingiziana……” (Waroma 1:18-32).

Hivyo kufuatana na maoni ya Paulo, ugomvi, uuaji, wivu, udanganyifu, dhuluma, ulafi na ufisadi, ni tamaa mbaya kama ilivyo kuacha kufuata matumizi ya maumbile ya mme na mke na watu kuwakiana tamaa wao kwa wao (wanawake kwa wanawake na wanaume kwa wanaume). Kwa maoni ya Paulo, hizi ni dhambi ambazo ni lazima zishughulikiwe kwa pamoja.

Barua ya kwanza ya Paulo kwa Timoteo, inafafanua vizuri kile ninachotaka kusema:
“ Twajua kwamba Sheria ni njema, kama ikitumiwa ipasavyo. Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba sheria haziwekwi kwa ajili ya watu wema, bali kwa ajili ya wahalifu na wasiotii, wasiomcha Mungu na wenye dhambi, watu wasio na dini na wa kidunia. Watu wanaowaua baba na mama zao, au wauaji wowote wale; sheria imewekwa kwa ajili ya waasherati, wafiraji, wanaowaiba watu, waongo, na wanaoapa uwongo au wanaofanya chochote ambacho ni kinyume cha mafundisho ya kweli.” (1 Timoteo 1:8-10).

Kama tunasema kwamba ushoga na usagaji ni kinyume na maumbile, kama tunasema mashoga na wasagaji wana kasoro, ni wagonjwa na wana kilema kikubwa, basi tukubali kwamba na wasema uongo, walafi, mafisadi, wasengenyaji wana kasoro, ni wagonjwa wana kilema kikubwa na wanaishi kinyume na maumbile!

Hata tukiachana na Biblia. Tukiangalia Mwongozo wa kanisa Katoliki kuhusu swala hili uliotolewa Desemba 1975 na ule wa Kadinali Ratzinger, yote inakazia Utafiti juu ya hali ya mtu kuvutiwa na jinsia yake. Je jambo hili limefanyika? Tuangalie hapa Tanzania. Utafiti huu umefanyika? Kanisa katoliki la Tanzania limejenga mazingara ambamo watu wenye kilema hiki wanaweza kujitokeza wazi na wakakubalika na kusaidiwa bila kungoja matukio kama lile la padri kulawiti. Kadinali Ratizinger, alishauri kwamba watu wenye matatizo haya wasitengwe, wapatiwe huduma zote za kiroho, wasikilizwe na kusaidiwa kwa kutumia hekima na busara kubwa. Tumesikia kwamba huyu Padri aliyelawiti, amesimamishwa kutoa huduma za kiroho. Je, huku si kumtenga? Kama kuna mapadri wengine wenye matatizo kama haya watakubali kujitokeza ili wasaidiwe? Je, kama kuna waumini wengine wenye matatizo kama haya watajitokeza? Kama padri amesimamishwa kutoa huduma za kiroho si waumini wakijitokeza watafungiwa huduma za sakramenti na kutengwa na kanisa?

Tusikae kimya. Tujadiliane, tufanye utafiti, tuelimishane na kusaidiana ili tuweze kuendelea kuishi hapa duniani kwa furaha, heshima na matumaini.

Na,
Padri Privatus Karugendo.