TUJIFUNZE KUTOKA KWA MZEE MANDELA

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA RAI 2005.

TUJIFUNZE KUTOKA KWA MZEE MANDELA

Mzee Nelson Mandela, ni kati ya watu wachache waliofanikiwa kuyaishi na kuyashika mafundisho magumu. Mafundisho ambayo walio wengi tunayaita ndoto, lakini tunayafundisha na kuwahimiza watu wengine wayashike na kuyafuata. Alipohukumiwa kifungo cha maisha, Mzee Mandela, alipokea hukumu hiyo bila ya woga, ni kitu alichokifahamu hata kabla ya kuanza mapambano na serikali ya makaburu. Alifahamu nguvu na uwezo wa serikali ya makaburu. Alijua walivyokuwa wameshikilia vyombo vya dola na silaha nzito nzito, alijua angekamatwa na kufungwa au kuuawa. Pamoja na kuyajua yote hayo aliamua kuendelea kupambana na makaburu kwa vile alitanguliza uhai wa taifa lake na wala si uhai wa maisha yake binafsi. Lakini pia alijua jinsi nguvu na uwezo wa makaburu vilivyokuwa vinaishia kwenye kuutesa mwili wake bila ya kuwa na uwezo wa kuigusa roho yake hata hivyo mafundisho magumu ambayo roho yake haikuwa na uwezo wa kuyakwepa yalikuwa mbele ya macho yake:
“ Msiwaogope wale wauao mwili lakini hawawezi kuiua roho. Afadhali zaidi kumwogopa yule awezaye kuuangamiza mwili pamoja na roho..” (Matayo 5:28).
Makaburu waliutesa mwili wa mzee Mandela, alifanyishwa kazi za suluba, alidhalilishwa alipokonywa uhuru wake, alinyimwa uhuru wa kuwa na familia yake, alinyimwa uhuru wa mawasiliano, alipofiwa na mtoto wake wa kiume, alinyimwa ruhusa ya kuhudhuria mazishi yake. Unyama wote aliofanyiwa akiwa gerezani uliugusa na kuutesa kwa kiasi kikubwa mwili wake tu, lakini roho yake ilibaki madhubuti. Alipochaguliwa kuwa Rais wa kwanza Mwafrika wa Afrika ya kusini huru, Mandela, alimshangaza kila mtu pale alipowakumbatia adui zake na kukaa nao meza moja ya chakula. Hakulipiza kisasi! Tulivyozoea, angelilipiza kisasi kama ilivyofanyika kule Rwanda, baada ya RPF kuingia madarakani au magomvi na kutoelewana miongoni mwa vyama vya kisiasa kwenye baadhi ya nchi za Afrika na Tanzania, ikiwemo! Unyama aliotendewa gerezani, haukuigusa roho yake! Mzee Mandela, amekuwa mwalimu wa kuwafundisha watu kuishi na kuyashika mafundisho magumu, mambo ambayo tumezoea kuyaita ndoto. Watanzania tuna utamaduni wa kuogopa mwenye nguvu na uwezo wa kuua mwili Pia tuna utamaduni wa kulipa kisasi, wawe ni viongozi wa dini au viongozi wa serikali, tabia hii ipo. Tujifunze kwa Mzee Mandela: Mwili unateswa, unanyanyaswa na kudhalilishwa na mwanadamu, lakini roho ya ukweli, amani na wema viko juu ya uwezo wa mwanadamu! Hakuna mwanadamu mwenye uwezo wa kuiua roho ya wema, hata kama mtu huyo angekuwa na nguvu za kidunia kama za Amerika! Pia tujifunze kwamba ukipambana na mtu, ukimshinda, mnashikana mikono na kukumbatiana – si kujenga chuki wala uhasama!

Watu wanaouona mwanga huu wameanza kugundua kwamba yale tunayoita mafundisho magumu na ndoto yanawezekana, Mzee Mandela, ametuonyesha mfano:
“ Mmesikia kwamba ilisemwa: ‘Jicho kwa jicho, jino kwa jino’. Lakini mimi nawaambieni, usimlipize kisasi mtu mbaya. Mtu akikupiga kofi shavu la kulia, mgeuzie pia shavu la pili..” (Matayo 5:38-39).
Haya ni mafundisho magumu ambayo yamewashinda watu wengi hata na wale walioyafundisha na kuyaeneza. Hadi leo hii hata viongozi wa dini bado mafundisho haya yanawapatia shida. Bado wanashikilia ‘Jicho kwa jicho, na jino kwa jino’. Migogoro inayowakumba viongozi wa dini inasababishwa na kutokubali kupigwa shavu la kulia, na kugeuza la kushoto. Wakipigwa kofi, wanarudisha. Hii inavuruga amani na kuleta magomvi yasiyoisha. Mandela, hakurudisha kofi! Alisamehe! Mafundisho magumu yalikuwa mbele ya macho yake na roho yake iliyoandaliwa kwa umakini na kwa miaka mingi haikuwa na uwezo wa kuyakwepa:
“Mmesikia kwama ilisemwa: ‘Utampenda jirani yako, lakini utamchukukia adui yako.’ Lakini mimi nawaambieni ,wapendeni maadui wenu na kuwaombea wale wanaowadhulumu ninyi…” ( Matayo 5:43-44).

Tunakumbuka jinsi Mzee Mandela, alivyowashauri Wamarekani: “Tumejifunza jinsi ya kuishi na maadui zetu, na nyinyi mjifunze kuishi na maadui zenu..”

Tume ya maridhiano ya Afrika ya Kusini, ilifanya kazi kwa uhuru na kumsikiliza kila mtu. Haikuwa na upendeleo wala kukikumbatia chama tawala. Haki ilitendeka kwa kila mwananchi na watu wote walifurahia kazi yake. Hizo zilikuwa mbinu za Mzee Mandela, za kukumbatia mafundisho magumu ya kumpenda adui.

Juma lililopita Mzee Mandela, alimpoteza mtoto wake wa kiume kwa ugonjwa wa UKIMWI. Kwa masikitiko makubwa(maana huyu ndio mtoto pekee wa kiume aliyekuwa amebakia) alitangaza wazi mbele ya vyombo vya habari bila aibu kwamba mtoto wake alikufa kutokana na ugonjwa wa UKIMWI. Hapa pia mafundisho magumu ambayo roho yake haikuwa na uwezo wa kuyakwepa yalikuwa mbele ya macho yake:
“ Jihadharini na chachu ya Wafarisayo, yaani unafiki. Kila kilichofunikwa kitafunuliwa, na kila siri itajulikana. Kwa hiyo, kila mlichosema gizani, watu watakisikia katika mwanga, na kila mlichonong’ona, faraghani ,milango imefungwa ,kitatangazwa juu ya nyumba.” (Luka 12:1-3).
Hili limekuwa fundisho jingine kutoka kwa Mzee Mandela, la mafundisho magumu ambayo wengi wetu na hasa Barani Afrika, kusini mwa jangwa la Sahara, tumekuwa tukidhani ni ndoto. Tumezoea kusikia watu mashuhuri wakifa kutokana na shinikizo la damu, kisukari, ugonjwa wa muda mrefu na ugonjwa wa ghafla nk. Ni nadra kusikia mtu mashuhuri amekufa kwa UKIMWI. Ugonjwa huu, umezungukwa na unafiki mkubwa. Ndio maana ugonjwa huu umekuwa wa hatari katika nchi zetu hizi masikini. Ugonjwa unafichwa na unafiki unaendelea kutawala. Hawa watu mashuhuri wanaokufa kwa shinikizo la damu wanatoa mwanya wa wenzi wao kuendelea kusambaza virusi vya UKIMWI, hakuna anayeshughulika kuchukua tahadhari maana shinikizo la damu si ugonjwa wa kutisha kama UKIMWI!! Matokeo yake ni janga kama tunavyoendelea kushuhudia. Ni lazima tumpongeze Mzee Mandela, kwa ujasiri wake na tuendee kujifunza kutoka kwake.
Hadharani, karibu kila mtu anapiga vita tendo la ngono na matumizi ya kondomu. Tendo la ngono linachukuliwa na wengi kuwa ni kitu cha aibu na labda kitu kisichofaa kwa mwanadamu! Sirini, karibu kila mtu (aliyemzima) anachangamkia tendo la ngono! Baadhi ya wanaopiga vita matumizi ya kondomu hadharani, wanazitumia kondomu mafichoni, wanawapotosha watu wengine na kuwaacha waangamie huku wao wanayalinda maisha yao. Unafiki mkubwa!

Mzee Mandela, alipougua ugonjwa wa saratani ya kibofu cha mkojo, alitangaza wazi. Hakuficha ugonjwa wake. Alipatiwa matibabu, na sasa anaendelea kuishi! Hapa Tanzania, tumewapoteza watu wengi kwa ugonjwa huu kwa sababu ya aibu na unafiki! Pia watu wanakufa kwa kuficha magonjwa ya zinaa yanayotibika kwa sababu ya aibu na unafiki. Magonjwa yakigusa sehemu za siri, watu wanakuwa na aibu. Aibu hii inatokana na mawazo ya kulichukulia tendo la ngono kama la aibu. Ingawa kuna ukweli kwamba si magonjwa yote yanayozishambulia sehemu za siri yanasababishwa na tendo la ngono. Baadhi ya watu wakiugua sehemu za siri, wanataja kichwa, tumbo na mgongo. Madaktari wanatibu kichwa, tumbo na mgongo, kumbe mgonjwa ana saratani ya kibofu cha mkojo au magonjwa mengine ya zinaa. Inapotokea bahati ya kuugundua ugonjwa, mgonjwa anakuwa amezidiwa na kufa! Aibu na unafiki vinasababisha vifo visivyokuwa vya lazima katika taifa letu na katika nchi nyingine za Kiafrika.

Kama tunataka kupambana na UKIMWI tuachane na unafiki. Kila Mtanzania aachane na unafiki na kuwa wazi. Mtu akifa kwa UKIMWI, tuseme wazi kama alivyofanya Mzee Mandela, ili watu wote wanaomzunguka marehemu na kuwa kwenye mtiririko wa mkufu wa mahusiano yake waanze kuchukua tahadhari. Mpaka sasa hivi silaha pekee dhidi ya UKIMWI ni Kinga. Kuna kinga za aina tatu: Uaminifu, kuacha kabisa tendo la ngono na kutumia kondomu. Tukiacha unafiki kinga hizi zinaweza kusaidia kupunguza maambukizo ya UKIMWI. Bahati mbaya kwa upande wa Afrika kusini mwa jangwa la Sahara, kinga hizi tatu zimegubikwa na unafiki mkubwa.

Ripoti za mashirika yasiyokuwa ya kiserikali yanayoshughulika kutetea haki za wanawake, yanaonyesha ongezeko kubwa la ukosefu wa uaminifu katika ndoa. Kesi za kufumaniwa zinaongezeka, ubakaji na unyanyasaji wa kijinsia kwa watoto wadogo unaota mizizi, tabia za ushoga na usagaji zinaanza kujipenyeza, nyumba ndogo zinashika kasi ya kutisha na kuna ongezeko kubwa la watoto wa nje ya ndoa. Imegundulika pia kwamba hata wale wanaoendesha “porojo” za uaminifu kama kinga dhidi ya UKIMWI, wanaogelea katika dimbwi la nyumba ndogo na unyanyasaji wa kijinsia! Unafiki mkubwa!

Kuacha kabisa tendo la ngono, hii ni siri ya mtu na Mungu wake. Hakuna mwenye uwezo wa kuhakikisha jambo hili – labda kwa vile maendeleo yanashika kasi, kutagunduliwa mtambo wa kuwapima wale wasiofanya tendo hili hadi kufa kwao! Takwimu zinaonyesha kwamba hata watu wanaoaminika kuacha kabisa tendo la ngono wanakufa kwa ugonjwa wa UKIMWI. Kwa vile ugonjwa huu una njia nyingi za kuambukiza, tunabaki kujituliza (unafiki) kwamba “watakatifu wa Mungu” waliambukizwa ugonjwa huu kwa njia nyingine na wala si ngono. Kwa mantiki hii wenzi wao hawachukui tahadhari yoyote na wanaendelea kusambaza virusi.

Unafiki unaoyazunguka matumizi ya kondomu, unajulikana. Kuna wale wanaojitangaza kwamba wanatumia kondomu, lakini hawazitumii – ni unafiki wa kutafuta pesa na kuwafurahisha wahisani. Watu hawa ni hatari, wanatoa matumaini yasiyokuwepo! Kuna wale wanaotumia kondomu, siku za mwanzo za kukutana na wapenzi wao, wakizoeana kidogo, hata bila ya kupimwa, wanazitupilia kondomu mbali na kuendelea na tendo la ngono bila ya kinga kwa kisingizio cha kujenga uaminifu katika kuzoeana! Hawa pia ni hatari, maana wanaongozwa na unafiki. Kumzoea mtu, haina maana hawezi kuwa na virusi na ikizingatiwa kwamba mtu mmoja anaweza kuwa na watu zaidi ya kumi wa kuzoeana naye! Kuna wale wanaopiga vita matumizi ya kondomu, likini wao wanazitumia, hawa si hatari tu bali ni mashetani, maana wanajikinga na kuulinda uhai wao wakati jamii nzima inateketea. Kuna wale wanaoeneza uvumi kwamba virusi vya UKIMWI, vinawekwa kwenye kondomu, kwamba ni mbinu za Wazungu kuwamaliza Waafrika! Kama ni kutumaliza mbona Wazungu wana nafasi nyingi? Madawa tunayotumia yanatengenezwa na Wazungu, cocacola, inatengenezwa na Wazungu, vyakula mbali mbali vinatengenezwa na Wazungu hata na computer ninayoitumia kuandika makala hii inatengenezwa na Wazungu, wakitaka wanaweza kuweka vitu vya kumaliza uhai – kwa nini watumie kondomu, kumaliza maisha ya Waafrika? Wengine wanasema kondomu ni miradi ya watu, wanatengeneza pesa. Wataalam wengine wanasema virusi vinapenya kwenye kondomu. Ni mengi, mengine ya kweli na mengine ni unafiki mtupu!

Lengo la makala hii ni kuonyesha jinsi tulivyo na mambo mengi ya kujifunza kutoka kwa Mzee Mandela. Taifa letu la Tanzania halijawa na mwelekeo mzuri wa kupambana na ugonjwa huu wa UKIMWI. Bahati mbaya viongozi wetu wa dini na serikali ni woga. Hatujapata viongozi wa kuyashika na kuyaishi mafundisho magumu kama alivyofanya Mzee Mandela. Hatujapata viongozi wasioogopa macho na masikio ya watu, viongozi wasiojali kudhalilishwa na ikibidi kuupoteza uhai wao katika harakati za kutetea ukweli na kupingana na unafiki.

Tunapojifunza kutoka kwa Mzee Mandela, ni lazima tumwangalie yeye na historia yake. Si kwamba misimamo yake hii ya kuishi na kuyashika mafundisho magumu, ilimnyeshea kama mvua. Ni mtu aliyefanya maandalizi, ni mtu aliyeitafuta elimu akiwa na malengo katika maisha yake – hakusoma tu kwa vile kusoma ni lazima – hakusoma kuishinda mitihani, bali alisoma kwa vile alikuwa na lengo la kuikomboa nchi yake. Lengo hili lilijaa kwenye roho
yake. Hata ungeupiga na kuumiza mwili wake, usingeliligusa lengo lililokuwa kwenye roho yake. Alijiandaa kwa maamuzi magumu –alijua jinsi njia ya kulifikia lengo lake ni kupitia kwenye maamuzi magumu. Alijifunza na kujiandaa kulitanguliza taifa lake kwa kila kitu. Hakuangalia tumbo lake, cheo chake au biashara yake (mambo ya mwili) aliangalia uhai wa taifa zima(mambo ya kiroho) Ndiyo maana hata leo katika uzee wake bado anafanya maamuzi magumu ya kutangaza ugonjwa wa mtoto wake ili achangie kuliokoa taifa zima!

Tunapojiandaa kwa uchaguzi mkuu mwaka huu, tujiulize ni nani hapa Tanzania, ataweza kuyaweka mafundisho magumu mbele ya macho yake na kuamua kuyafuata. Ni nani atalitanguliza taifa kabla ya kulitanguliza tumbo lake, familia yake, kabila lake na dini yake? Ni nani atashinda uchaguzi akakaa meza moja na wapinzani wake bila kulipiza kisasi? Ni nani ataangalia uhai wa taifa na kuteua watendaji wa serikali bila kuangalia vyama vyao vya siasa, bila kuangalia mchango wao katika kampeni, bila kuangalia sura zao na dini zao akaongozwa kwa kuangalia uwezo na uaminifu wa mtu kwa taifa letu? Ni nani atapambana na ugonjwa wa UKIMWI, bila woga na bila kuogopa kupoteza “mapenzi” kwa viongozi wa dini? Ni nani atapambana na rushwa, umasikini na kuangalia maendeleo ya watanizaania wote. Ni nani mwenye maandalizi kama haya?

Na,
Padri, Privatus Karugendo.

TUKIBADILIKA YAWEZEKANA, VINGINEVYO....

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA RAI 2005.

TUKIBADILIKA YAWEZEKANA,VINGINEVYO….

Nimeguswa kwa namna ya pekee na makala ya “Mwandishi wetu” RAI 587 “Tukibadilika Yawezekana, vinginevyo….”. Bahati mbaya au ni makusudi mazima mwandishi hakutaja jina lake. Ingekuwa ni vyema kufikia mahali majadiliano kama haya yakazaa kitu kinachoonekana cha kuchangia maendeleo ya taifa letu. Ili jambo kama hilo litokee, ni lazima watu kufahamiana na kujadiliana na karibu, wakati mwingine kufahamiana kunaweza kusaidia kuondoa “Ndoto”!

Sikuguswa na makala hii kwa vile mwandishi anaunga mkono maoni yangu nimekuwa nikiguswa na makala zote zinazochangia juu ya maoni yangu, hata zile za kunitukana na wakati mwingine kunidhalilisha zimekuwa zikinisaidia kufikiri na kutafakari maana hayo ndiyo majadiliano na uhuru wa kila mtu kutoa maoni yake. Mchango wa “Mwandishi wetu” umenichonyota kwa vile anagusia kitu kinachoisumbua akili yangu na roho yangu. Ni imani yangu kwamba kitu hiki kinawasumbua pia na baadhi ya watanzania wengine: Kuijenga jamii inayoishi kwa kutenda Haki, Wema na Huruma. Mwandishi wa makala hii aliguswa na makala yangu ya “Mkia wa Shetani”. Niliandika makala hii baada ya kupata fundisho; niliwatetea vibaka, wakanifundisha kwa kunikwapulia wallet yangu Niliumia kuibiwa, lakini hadi leo hii siamini kwamba ni haki kuwachoma moto vibaka. Badala yake ninajiuliza: Ni kwa nini tuna vibaka katika jamii yetu, kwa nini tuna majambazi, wezi na walarushwa, kwa nini tumeshindwa kuijenga jamii inayoishi kwa kutenda haki, wema na huruma? Sina haja ya kuandika kwamba hadi leo vibaka wanachomwa moto, kupigwa hadi kufa na wananchi wanaendelea kujichukulia sheria mkononi. Si kwamba ninajifanya nabii, bila mabadiliko, hali ikiendelea jinsi ilivyo, kasi ya kuwachoma vibaka itaendelea. Jambo la kuogopesha ni kwamba dalili za kuacha kuwachoma vibaka wa kukwapua simu, vijisenti, saa na mikufu na kuanza kuwachoma vibaka wa uchumi wa taifa letu, vibaka wanaoiba mabilioni, zinaanza kujitokeza. Hii ni hatari maana vibaka wa uchumi wana uwezo wa kujilinda. Historia inatuonyesha kwamba wanyonge wanaoonewa wakishirikiana wanaweza kupambana vilivyo na vibaka wa uchumi Tukio kama hilo linajulikana kama vita ya wenyewe kwa wenyewe Si lazima kutoa mifano. Tuendelee kufanya mchezo, matukio mabaya(ya uzembe) ni mwalimu mzuri. Lengo la makala hii ni kutaka kushirikiana na “Mwandishi wetu” na wengine wanaojali kutafakari; “Tufanye nini ili tubadilike?”. Ni chombo gani au ni mfumo gani wa kutusaidia kuleta mabadiliko? Huwezi kuleta mabadiliko katika jamii bila ya kuwa na chombo au mfumo.

Je ni watu gani wa kutusaidia kuleta mabadiliko? Ni kweli kwamba watanzania wote ni lazima tubadilike! Ili mabadiliko ya kweli yatokee ni lazima kila mtu ajibadilishe yeye mwenyewe. Kosa kubwa linalojitokeza ni kwamba daima tunataka wengine wabadilike. Tunataka watu waache uzinzi, ujambazi, rushwa. Je ni kiasi gani kila mtu anahoji nafsi yake juu ya uzinzi anaoufanya yeye mwenyewe? Kama hili lingekuwa linatokea, basi uzinzi ungepungua. Je ni nani anaihoji nafsi yake kuhusu kutowatendea watu wengine haki, wema na huruma? Hili lingetokea basi ujambazi na rushwa vingepungua. Udhaifu wetu ni kwamba tunataka tutendewe haki, wema na huruma, hatuangalii ni kiasi gani sisi tunawajibika kwa wengine! Mtu wa kufikia hatua ya kuanza kuihoji nafsi yake ni lazima awe ameandaliwa, nia lazima awe ameelekezwa, ni lazima awe amepitia katika mfumo wa aina fulani, ni lazima awe anaishi kwa malengo, ni lazima awe anaguswa na maisha ya jamii nzima. Kwa vile mwanadamu ana tabia ya kusahau, mifumo inasaidia kumkumbusha!

Mtu ambaye ameonja adha ya kuomba chumvi kwa jirani, akipatana nafasi ya kuingia madarakani atahakikisha anashiriki kikamilifu kurekebisha mifumo ya uchumi ili watu wasipate adha ya kuomba chumvi kwa jirani. Mtu ambaye ameonja adha ya kugombana na mwenye nyumba kwa kushindwa kulipa pango, akifanikiwa kuingia madarakani atapigia debe mpango wa kujenga nyumba nafuu kwa wananchi. Mtu anayejua adha ya kushindwa kulipia matibabu, akifanikiwa kuingia madarakani atajitahidi kupiga kelele juu ya huduma bora za afya. Mtu anayejua adha ya taabu ya usafiri, akiingia madarakani atajitahidi kuboresha huduma ya usafiri nk. Lakini kwa vile mwanadamu anabaki ni mwanadamu, aliyeonja adha anaweza akajisahau akiingia kwenye neema, kama kuna mfumo mzuri, ni rahisi kumsuta na kumrekebisha mtu aliyeonja adha mbali mbali katika jamii kuliko yule anayeshuka kutoka mbingu nyingine!

Nimetoa mifano hii ili kuonyesha kwamba wakati tunalilia mabadiliko katika taifa letu, ni bora kujiuliza ni nani wa kutuletea mabadiliko, pamoja na kwamba tunahitaji mifumo na vyombo, na pamoja kwamba ni lazima kila Mtanzania abadilike, lakini kuna watu muhimu wa kuhimiza mabadiliko. Mtu asiyejua adha ya kuomba chumvi kwa jirani, asiyejua adha ya kufukuzwa kwenye nyumba ya kupanga, asiyejua adha ya usafiri, anayeugua mafua akakimbizwa kwenye hospitali za London na Afrika ya Kusini, asiyejua adha ya usafiri, anayesomesha watoto wake nje ya nchi, anaweza kuchangia mabadiliko gani katika nchi masikini kama ya Tanzania? Kuna msemo kwamba, Ndege wenye bawa moja huruka pamoja! Mabadiliko ya kweli ni ya ndege wanaoruka pamoja!

Viongozi wetu wa serikali, viongozi wetu wa dini, hawaguswi na adha zote nilizozitaja na ambazo sikuzitaja, wana mabawa tofauti na jamii! Wanaruka kivyao na jamii inaruka kivyake. Hali kama hii haiwezi kuleta mabadiliko!

Mwandishi wetu anasema: Utawala bora hauwezi kuwapo kama hakuna mtawala/kiongozi bora. Utawala bora ni ule tu unaojali haki za raia, maslahi ya raia au taifa na unaongoza watu kufikia matarajio yao, utawala bora ni kujikana na kujitoa kwa dhati utumike kwa wengine. Kwa kuyazingatia mawazo kama haya waasisi wa taifa letu waliamua kuanzisha chama cha siasa cha CCM. Kirefu chake: Chama Cha Mapinduzi. Kamusi ya Kiswahili sanifu inaelezea neno Mapinduzi: Mabadiliko ya haraka katika mfumo wa maisha ya jamii ambayo huwanufaisha watu walio wengi. Kwa mtu anayeona mbali anaweza kusema CCM, ni chama kilichokuwa kimelenga mabadiliko. Kililenga kujenga jamii yenye kutenda haki, wema na huruma. Ni chama kilichokuwa kimelenga kufuta mifumo ya kikoloni ya unyanyasaji ubaguzi, matabaka, kupunguza ufa kati ya walionacho na wasiokuwa nacho. Ni chama kilichokuwa kimelenga kuleta mapinduzi katika maendeleo ya taifa letu; mapinduzi katika huduma za kijamii, watu wapate maji, umeme, shule, hospitali, makazi bora, chakula cha kutosha na kuumiliki uchumi wa nchi yao. Sera ya ujamaa na kujitegemea ilikuwa inalenga kuleta mabadiliko ya kweli katika taifa letu. Hivyo tunapotafakari juu ya ni chombo gani cha kutusaidia kuleta mabadiliko katika nchi yetu kila mtu angekuwa anajibu kwa haraka hata bila ya kufikiria kwa, ni CCM. Kwa vile bado tunajiuliza ni chombo gani kitusaidie, ni wazi kwamba CCM, imeshindwa kutekeleza malengo yake. Badala ya kusema Chama Cha Mapinduzi, tunasikia Chukua Chako Mapema! Hali hii ya kutokielewa chama, imezaa matatizo mengi katika jamii yetu. Rushwa, imeongezeka na kuwa na mizizi kwa sababu ya Chukua Chako Mapema. Ni wanaCCM wachache, labda silimia mbili wanaofahamu maana ya neno “Mapinduzi”. Asilimia kubwa ni Chukua Chako Mapema. Malengo ya waasisi wa chama yametupiliwa mbali. Sera ya Ujamaa na kujitegemea, imefutwa! Walioifuta hawakuwa na uwezo wa kubuni mfumo mwingine. Wameliacha taifa kwenye “utupu” unaoendelea kuzaa matatizo juu ya matatizo. Ninalotaka kusema ni kwamba CCM,(Sina maana ya Chama Cha Mapinduzi, cha Mwalimu, ninaongelea kivuli tulichonacho leo hii) haiwezi kutusaidia kuleta mabadiliko.

Vyama vya upinzani ni vyama vya kuipinga CCM na wala si vyama vya kuleta mabadiliko. Vyama hivi vinatumia nguvu nyingi kupambana na CCM, badala ya kuutumia muda uliopo kuunda sera na mifumo ya kusaidia kuleta mabadiliko ya kweli katika taifa letu. Ni mapambano yaleyale ya Chukua Chako Mapema. Ingawa si haki kuvipima vyama vyote kwenye mizani ile ile, lakini ukweli unabaki pale pale kwamba hakuna chama chenye mfumo wa kuleta mapinduzi ya kweli. Mfumo wa kupunguza adha ya kuomba chumvi na wananchi kuumiliki uchumi wa taifa. Mfumo wa kujenga utaifa na uzalendo. Mfumo wa kufuatilia kila Mtanzania na kumbadilisha awe raia mwema wa kutenda haki, wema na huruma kwa ndugu zake.

Wale wote wanaotaka kuingia Ikulu. Hakuna hata mmoja mwenye mfumo wa kuleta mabadiliko ya kweli. Ni nani na mfumo wake unapatikana wapi ili tuujadili na kutoa maoni?. Mimi binafsi nisingemlaumu Mheshimiwa Frederick Sumaye, kwa kutumia pesa za serikali kuendesha kampeni ili chama chake kimpendekeze kugombea urais. Kama ana mfumo mzuri wa kuleta mabadiliko ya kweli katika taifa letu, ni ruhusa kutumia pesa zote hata kama zikiisha. Tatizo langu si kwa Sumaye, ni kwa wote hata wale wanaotumia pesa zao walizoziiba kutoka serikalini, wanataka kuupata urais ili kufanya nini? Wana mfumo gani wa kule mabadiliko ya kweli katika taifa letu? Si lazima kuwasikiliza, tunajua kusoma! Tusome wapi aina ya mfumo wao, mawazo yao na sera zao? Wana nini cha kutuelezea zaidi ya matumbo yao, mali walizonazo, wake zao na dogodogo, utukufu wao na mbwembwe zao? Ni nani kati yao anaijua adha ya kuomba chumvi kwa jirani au kulala njaa?

Dini zetu zimeshindwa kutuletea mabadiliko. Au labda niseme kwamba si lengo la dini hizi kuleta mabadiliko katika taifa letu. Tuchuke mfano wa kibaka. Huyu kibaka akifanikiwa kukwapua pesa bila ya kuonekana, atakwenda kanisani Jumapili au msikitini Ijumaa, kusali, atatoa sadaka, itakubaliwa na kubarikiwa na kiongozi wa Ibada. Kibaka, huyu ataungama na kuondolewa dhambi zake. Kwa vile hakuna mfumo wa kumfuatilia kibaya huyu, kujua matatizo yake, maisha yake, kipato chake nk., ataendelea kufanya kazi yake ya kuiba. Siku atakapokamatwa na kupigwa hadi kufa, ni wengi watakaoikosa huduma yake, kuanzia kwa kiongozi wa ibada hadi familia yake. Viongozi wetu wa dini wanaijua mishahara ya viongozi wetu wa serikali, mbona hawatusaidii kuhoji ufa uliopo kati ya viongozi wa serikali na wananchi, mbona hawahoji michango mizito inayotolewa na viongozi wa serikali kusaidia taasisi za kidini? Wanakaa kimya na kwa unafiki wanalaani rushwa!

Viongozi wa dini wameshindwa kubuni mfumo wa kufundisha elimu ya dini na maadili katika shule na vyuo. Huwezi kuleta mabadiliko ya kweli bila kuwafundisha na kuwaelekeza vijana. Haitoshi kuendesha mahojiano kwenye luninga, ni watanzania wangapi wenye uwezo wa kununua luninga? Haitoshi kuhubiri Jumapili na Ijumaa, ni waumini wangapi wanakwenda kwenye Ibada? Walio wengi wanautumia muda wa kenda kwenye Ibada kupamba na ugumu wa maisha. Viongozi wa dini hawaijui adha ya kuomba chumvi na kushinda njaa. Waumini wanaofanikiwa kuujua ukweli huu, wameanza kupuuzia kwenda kwenye Ibada, labda uwe msiba, ndoa au sherehe kubwa kama Iddi ,Christmas na Pasaka! Mfumo wa kufundisha elimu ya dini mashuleni na vyuoni ungesaidia.

Kuna NGO mbali mbali katika jamii yetu. Nyingine zinahudumia watoto yatima, nyingine watoto wa mitaani, nyingine zinatetea haki za akina mama, nyingine za kulinda mazingira nk, hakuna NGO, ya kuhimiza mabadiliko katika taifa letu. Sijasikia NGO, yenye malengo ya kuwaandaa watanzania kulipenda taifa lao, kutoa maisha yao katika kulijenga taifa lao, kutenda haki wema na huruma na kufundisha maadili mema. NGO, inayoweza kumfuatilia kibaka na si kumsaidia kujirekebisha tu bali kumsaidia kujitegemea. NGO, inayoweza kumsaidia changudoa kubadilisha maisha yake.

PCB, inasaidia kuwafichua wale wanaokula rushwa. Ingawa sina uhakika inasaidia kiasi gani na wale wanaofichuliwa wanachukuliwa hatua gani. La msingi si kuwafichua wala rushwa, ni kuwa na mfumo wa kuidhibiti rushwa. Mfumo wa kujenga jamii ya watu wanaowajibika. Bila hivyo, hata PCB, kinaweza kugeuka chombo cha wala rushwa.

Tunamuhitaji kiongozi anayeyaona haya. Kiongozi mwenye uwezo wa kubuni mfumo na kutengeneza chombo cha kuleta mabadiliko ya kweli katika taifa letu. Kiongozi ambaye hawezi kufungwa mikono na miguu na chama chake cha siasa, ambaye hawezi kunyamazishwa na nguvu za pesa, ambaye hawezi kutekwa na nguvu za viongozi wa dini, ambaye si mlevi wa madaraka na ambaye anajua kuutawala vizuri mwili wake, ambaye anasoma, kuandika na kufanya utafiti wa mara kwa mara, kiongozi mwanamapinduzi na mwenye kuchochea mabadiliko katika mawazo ya kila Mtanzania.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

NANI ADUI WA UMOJA WETU WA KITAIFA?

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005.

NANI ADUI WA UMOJA WETU WA KITAIFA?

Hakuna taifa linaloweza kusimama bila ya kuwa na umoja wa kitaifa. Tanzania imesimama imara hadi leo hii kwa sababu ya umoja wa kitaifa uliojengwa na waasisi wa taifa letu. Tunasifiwa kwa utulivu na amani. Sifa hizi ni za kweli na kilichotukifisha hapa tulipo ni umoja. Na hili halikunyesha tu kama mvua ni jambo liliofanyiwa kazi usiku na mchana. Waasisi wa taifa yetu walijitahidi kuujenga umoja katika taifa letu. Kuna mambo mengi yaliyowasaidia kuujenga umoja huu: Tulikuwa na chama kimoja cha siasa. Chama kilitunga sera na kutoa vision. Hivyo chama kilikuwa ni chombo kimojawapo cha kuujenga umoja wa taifa letu. Ingawa kulikuwa na watu wachache walioupinga mfumo wa chama kimoja, hawakuwa tishio la kuuvunja umoja wetu. Walikuwa wapinzani wenye kulenga kujenga umoja wa kitaifa.

Waasisi wa taifa letu hawakuzitanguliza dini zao, jambo la kuabudu lilibakia kuwa la mtu binafsi. Watanzania walikuwa na dini, lakini Tanzania, haikuwa na dini – haikutawaliwa kidini. Jambo hili lilionekana wazi katika katiba ya nchi yetu. Mwalimu Nyerere, alikuwa mcha Mungu na Mkatoliki hodari, lakini hakuthubutu kujenga nyumba ya ibada ndani ya Ikulu.

Ukabila ulipigwa vita na utawala wa machifu ulifutiliwa mbali. Lugha ya Kiswahili ilipewa kipaumbele na kuwa chombo cha kuwaunganisha watanzania wote. Nchi ambazo zinatumia lugha za kigeni kama lugha zao za kitaifa, hadi leo zinapata shida ya kujenga umoja wa kitaifa. Ni watu wachache wanaozimudu lugha hizi za kigeni, walio wengi wanaendelea na lugha zao za kikabila jambo ambalo linafanya mawasiliano kuwa magumu. Mfano nchini Uganda, taarifa ya habari ili iwafikie wananchi wote inatangazwa kwenye lugha zaidi ya sita!

Jeshi la kujenga taifa lilianzishwa kwa lengo la kuwakutanisha vijana waliomaliza kidato cha sita na vyuo wa Tanzania nzima. Kipindi chote cha mafunzo ya vijana hawa uzalendo na umoja wa kitaifa ni mambo yaliyosisitizwa. Mfumo huu ulipunguza kasi ya ukabila, kasi ya ukanda, majivuno na kiburi. Jeshi liliwatendea vijana wote sawa, bila ya kujali mtoto wa tajiri, kiongozi na mtoto wa masikini, wasichana wala wavulana.

Mfumo wa elimu wa kuwasambaza vijana kwenye shule mbali mbali za mikoa ya Tanzania, ulisaidia kuwakutanisha vijana na kujenga umoja wa kitaifa. Vijana kutoka Kagera, walipelekwa kusoma Mtwara, Moshi au Dar-es-Salaam. Wa Kigoma, walipelekwa Arusha, Kagera, Musoma au Dodoma nk.

Mwenge wa huru ulibuniwa kwa malengo ya kujenga umoja wa kitaifa. Mbio za kuuzungusha Tanzania nzima, zilichochea cheche za umoja wa kitaifa.

Mwaka 1995, Tanzania, ilijiingiza katika mfumo wa vyama vingi vya kisiasa. Tunayoyashuhudia sasa hivi hakuna chama kinachoonyesha sera ya kujenga umoja wa kitaifa. Wapinzani wa leo ni tofauti kabisa na wapinzani wa zamani wakati wa utawala wa chama kimoja. Wapinzani wa leo pamoja na chama tawala cha CCM, wanaangalia zaidi umoja wa vyama vyao kuliko umoja wa kitaifa, wanatanguliza kuingia Ikulu, ruzuku, mbwembwe za madaraka na ushindani wa chuki na utengano. Wakati wanasiasa wa zamani walikuwa na sera ya uhuru na umoja, wanasiasa wetu wa leo wana sera ya ukoloni mambo leo (Utandawazi, ubinafsishaji, soko huria) na utengano.

Katika awamu ya pili ya utawala wa taifa letu tumeshuhudia baadhi ya viongozi wa ngazi za juu serikalini kuanzisha mtindo wa kujenga nyumba za ibada katika ofisi za serikali. Uteuzi wa viongozi kufuatana na dini zao. Dini ilianza kutangulizwa. Waheshimiwa wengine walianza kubadilisha dini zao kwa siri. Malumbano kati ya Waislamu na Wakristu yalishika kasi. Magomvi yalizuika kati ya Waislamu na Wakristu.

Mfumo wa elimu umevurugika, shule nyingi za binafsi zimeanzishwa na kuchochea watoto wengi waziweze kuivuka mikoa yao. Watoto wa matajiri hawasomi tena na watoto wa masikini. Kiwango cha elimu kimeanza kutofautiana na kuleta hatari ya kuanza kuunda tabaka katika taifa letu. Tabaka ni adui mkubwa wa umoja na amani. Baadhi ya watoto wameanza kuvuka mipaka ya nchi na kusomea Uganda, Kenya na nchi nyingine jirani kama Zambia na Malawi. Hii haiwezi kusaidia kujenga umoja wa kitaifa. Maana watoto hawa itakuwa vigumu kulelewa katika misingi ya utamaduni wa Mtanzania.
Jeshi la kujenga taifa limefutwa na Mwenge wa uhuru kimekuwa chombo cha kampeni! Badala ya kueneza amani katika taifa letu, Mwenge, wa huru umegeuka na kuwa chombo cha kusambaza virusi vya UKIMWI. Mwaka jana Mwenge, huu ulipowashwa mjini, Bukoba, uliacha kumbukumbu ya watu kubakwa ndoa kuvunjika, watu kufa na vitendo vingine vya kusambaza virusi vya UKIMWI.

Mfumo uliokuwa umejengwa na waasisi wetu wa kuunda umoja wa kitaifa umeanza kupotea! Ni wajibu wa kila Mtanzania kujiuliza: Ni nani adui wa umoja wetu? Kama nilivyosema hapo juu, ni vigumu taifa lolote kusimama bila ya umoja. Kama tunataka taifa letu liendelee kusimama ni lazima tukazane kujenga umoja.

Tukigundua adui wa umoja wetu ni lazima tumpige vita kwa nguvu zetu zote. Kati ya mambo ambayo yanaonyesha dalili za kutishia uhai wa umoja wetu ni dini! Na hasa hizi dini mbili kubwa katika Taifa letu, Uisilamu na Ukristu. Kabla ya kuendelea na makala hii ngoja nitoe nukuu ya mteolojia mmoja wa Brazil,Leonard Boff. Mteolojia huyu aliyekuwa padri mtawa wa Kanisa katoliki, alipambana na mifumo ya kanisa iliyokuwa inafumbia macho unyanyasaji, ukiukwaji wa haki za binadamu, uvunjaji wa umoja wa kitaifa, hadi akalazimishwa na utawala wa kanisa katoliki kuacha huduma ya upadri. Mteolojia huyu aliishia kufundisha kwenye vyuo vikuu nchini Brazil na kuunda jumuiya ndogo ndogo za Kikristu.

“Kueneza Injili hakuna maana ya kueneza mifumo ya Ukristu.
Kueneza Injili maana yake ni kuishi pamoja kama dada na kaka, kushirikiana katika kazi, kuwajibika kwa upendo katika maisha ya watu wengine, kuheshimu utamaduni, mila na desturi za watu wengine, maana kila utamaduni umejaa ukweli wa milele.

Kueneza Injili maana yake ni: kuishi, kulia, kucheka, kufanya kazi na kujiingiza kikamilifu katika maisha ya watu wengine ili sote kwa pamoja tupate wokovu” (Kutoka kwenye Sinema ya “On the Way Together.” Tafsiri ni yangu.”

Pale niliposema “Kueneza Injili”, unaweza kuweka neno “Kueneza imani mpya kwa watu wengine”. Nikiangalia hali ya sasa hivi ya nchi yetu ninashawishika kukubaliana na maneno ya Leonard Boff.

Wakati tunajianda kwa uchaguzi mkuu mwaka huu. Majadiliano makali yanaendelea. Waislamu wanamtaka rais Mwislamu na Wakristu wanamtaka rais Mkristu. Maoni haya yanafunika hekima na busara yote. Si uwezo wa mtu na wala si mapenzi ya mtu katika taifa lake. Jambo muhimu ni dini! Haya si maoni ya kujenga umoja na wala haya si mawazo ya waasisi wa taifa letu.

Bahati nzuri tuliyo nayo ni kwamba hata mfumo wa vyama vingi umeanza chini ya uongozi wa waasisi wa taifa letu ndio maana hakuna vyama vya kisiasa vya kidini. Lakini tunakoelekea jambo hili litakuja tu! Kama tumeanza kujiuliza rais anatoka dini gani, utafika wakati waka kujiuliza rais anatoka kwenye chama cha dini gani. Kuna nchi ambazo zina vyama vya kidini. Ili uwe mwanachama ni lazima uwe mfuasi wa dini au dhehebu Fulani. Nchi hizi hazisifiki kwa umoja wa kitaifa. Mfano nchini Uganda, kuna chama ambacho ili uwe mwanachama ni lazima uwe Aglicana na kingine ni lazima uwe Mkatoliki na kingine Mwislamu au dini ya kujitegemea kama ya Joseph Konny.

Chimbuko la tatizo ni wale walioeneza imani hizi za kigeni katika nchi za Afrika. Badala ya kueneza imani walieneza mifumo ya dini zao. Na kila dini ilishikilia kuwa ndiyo yenye wokovu Na malengo hayakuwa ya kuishi kama dada na kaka, bali bwana na mtwana! Hakukuwa na ushirikiano katika kazi za kila siku wakati wa kueneza dini hizi za kigeni wala uwajibikaji wa wageni katika maisha ya watu wenyeji Historia inatueleza jinsi Ukristu na Uislamu zilivyoenea duniani kote kwa upanga, chuki na ubaguzi. Dini hizi zilifuta utamaduni, mila na desturi za watu wengine. Dini hizi hazikucheka na wanaocheka na wala hazikulia na wanaolia. Dini hizi hazikujiingiza kikamilifu katika maisha ya watu wengine ili watu wote wapate wokovu. Aliyezikumbatia dini hizi alipokelewa kwa mikono miwili, aliyezikataa alilaaniwa na wakati mwingine kuuawa!

Watanzania walio wengi wamejiingiza kwenye dini hizi mbili. Ni vigumu kuwaambia wazikimbie maana zinahatarisha umoja wa taifa letu. Ushauri wa pekee ni kuzilazimisha dini hizi zikakubali utamaduni wetu. Waasisi wa taifa letu walitujengea utamaduni wa umoja, utulivu na amani, hivyo ni lazima dini zetu ziheshimu utamaduni huu. Mtanzania Mwislamu ni Mtanzania, na ni lazima apate haki zote za Mtanzania. Aheshimiwe na watanzania wote kufuatana na karama zake alizonazo na mchango wake kwa taifa letu. Mtanzania Mkristu ni mtatanzania na ni lazima apate haki zote za Mtanzania, aheshimiwe na watanzania wote kufuatana na karama zake na mchango wake kwa taifa letu. Mtanzania anayefuata dini za jadi ni Mtanzania na ni lazima apate haki zote za Mtanzania, aheshimiwe na watanzania wote kufuatana na karama zake na mchango wake katika taifa letu.

Wale wanaoiona hatari iliyo mbele yetu ya kuuvuja umoja wetu, na hasa hatari ya dini za kigeni, ni lazima wafikirie kwa haraka jinsi ya kuunda chombo cha kujenga umoja wa kitaifa. Nilivyodokeza hapo juu vyama vya kisiasa tulivyonavyo kwa sasa haviwezi kujenga umoja wa kitaifa. Dini za kigeni ni adui mkubwa wa umoja wetu. Mifumo mingine imeharibiwa makusudi! Ni lazima sasa kuundwe chombo cha kujenga umoja wa kitaifa. Chombo ambacho hakitatawaliwa na vyama vya kisiasa, chombo ambacho hakitatawaliwa na dini, chombo ambacho hakitatawaliwa na matajiri, wawekezaji kutoka nje, ushawishi na nguvu kutoka nje ya nchi, ukabila wala ukanda .Chombo cha kujengwa na watanzania wenyewe na wala si chombo cha kujengwa na umoja wa mataifa au umoja wa nchi huru za Afrika. Chombo ambacho kitamfanya kila Mtanzania kumthamini Mtanzania mwenzake si kwa vile ni wa chama fulani, dini fulani au kabila fulani, bali kwa vile ni Mtanzania.

Kuna tetesi kwamba sasa hivi Wakristu wanaomba na kusali kwa nguvu zote ili Tanzania, isitawaliwe na rais Mwislamu. Na Waislamu wanasali kwa juhudi ili Tanzania, isitawaliwe tena na rais Mkristu! Kwa vile tumezoea kutawaliwa na unafiki, mambo haya hayasemwi na kuonyeshwa wazi – ni agenda za siri ambazo kila kikundi kinazitunza kwa uaminifu mkubwa. Mwelekeo huu si wa umoja na wala si wa kujenga amani.
Kazi kubwa ya rais ajaye mwaka huu ni kuunda chombo cha kujenga umoja wa kitaifa. Bila ya hivyo Tanzania, inaelekea kubaya.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

K.K.K.T WANAVUNJA AMANI

MAKALA HII ILITOKA KATIKA GAZETI LA RAI 2005.

K.K.K.T WANAVUNJA AMANI

Katika makala zangu nyingi kwenye ukurasa huu, nimekuwa napigia kelele huku nikijenga hoja juu ya kujenga jamii yenye maadili. Na wito wangu daima umekuwa ni kujenga maadili ya kitaifa ambamo utu, uadilifu na heshima vinapewa kipa umbele. Msingi wa maadili kitaifa katika taifa changa kama letu, ni kuwepo kwa dhamira na makusudi kwa viongozi wa ngazi zote kujiheshimu na kutanguliza maslahi ya taifa na ya watawaliwa. Yawezekana sana hii ni falsafa isiyovutia masikioni mwa wengi na kwa kweli katika hali tuliyo nayo hivi sasa, wengi wanaposikia hizi kelele zangu wanaweza kukimbilia kusema kuwa ni ndoto zisizowezekana. Uvivu wa kufikiri utaendelea kuwa sumu katika mustakabali wa taifa changa kama letu.
Daima nimekuwa nikisema kwamba ili kujenga taifa lenye maadili, lenye amani na mshikamano tunahitaji mfumo au chombo cha kutufikisha huko. Nimekuwa nikionyesha mashaka juu ya mifumo tuliyonayo kwa sana. Mawazo yangu ni kuunda mifumo mipya au kuboresha ile tuliyonayo. Mifumo ya dini tulizonazo kwa sasa hivi inaweza kuwa mizuri pale tu tutakapofanya jitihada ya kuiboresha. Mfano makanisa, yakiboreshwa yanaweza kutoa mchango mzuri.
Makanisa ni taasisi nyeti sana katika nchi yetu. Watu wengi wanayaheshimu sana kutumainia mema tu kutoka huko. Watawala wa dola wanatazamia makanisa yawe mfano wa uadilifu, uvumilivu na ukomavu wa fikra. Mambo ya makanisa daima hubakia huko huko makanisani, na waumini wakati wote hutoa utii usio na mipaka katika kuwaheshimu viongozi wa makanisa. Kwa maana nyingine, viongozi wa makanisa ni nguzo muhimu katika kuandaa kile ninachokipigania daima yaani, “maadili ya kitaifa”. Watu wamejenga imani ya kupindukia katika makanisa. Makanisa yakienda tenga, jamii nzima inakwenda tenge. Hivyo ni jukumu la viongozi wa makanisa kuwa waangalifu kwa kila jambo wanalotenda kufanyia uamuzi. Ni jambo la lazima viongozi wa makanisa kufanya maamuzi bila kutanguliza maslahi binafsi, bali kuliangalia kanisa zima na taifa letu la Tanzania.
Wiki iliyopita na hii tuliyomo, vichwa vya habari vya magazeti vimeripoti kila siku juu ya mgogoro wa KKKT. Niliwahi kuandika katika ukurasa huu juu ya mgogoro ule na wakati nilihoji juu ya nani ananufaika na mgogoro huu wa kanisa kubwa la KKKT? Sasa ni wazi hakuna anayenufaika na lakini pia ni wazi, ni nani anaumizwa na mgogoro huu. Watu wengi tunajiuliza hivi Mwenegoha ni nani hata maaskofu watwangane makonde mkutanoni? Mwenegoha ni nani hata maaskofu waanikwe aibu yao hadharani? Mwenegoha ni nani hadi mamilioni ya shilingi yateketee kwa vikao visivyoisha na watu waendeshe magari nchi nzima kufanya kampenini ya kumpinga mkuu wa kanisa hilo? Kinachonijia mawazoni kama mmoja wa wanaokerwa na mgogoro huu, ni kuwa tatizo sasa si la Mwenegoha ni la maaskofu wasiokuwa na msimamo; maaskofu wanaotanguliza maslahi yao na ya Mwenegoha; na maaskofu wasiopenda ukweli unaowahusu ujulikane. Matokeo ya kukosa msimamo kwa maaskofu, kumeleta ufa mkubwa katika imani ya watu dhidi ya viongozi wa dini. Hali hii inavunja AMANI na isiachwe kuendelea.
Kitendo cha Askofu kumshambulia mwenzake kwa ngumi kinavunja amani ya jamii. Askofu akipigana, waumini watafanya nini? Yeye ni kiongozi na ni mfano wa kuangalia! Hali hii haitakiwi kufanywa hata miongoni mwa wanasiasa au hata majambazi walio katika kundi la kukamilisha kazi zao. Kwa Askofu kuamua kutumia ngumi badala ya hoja au sala, ni kiwango kwa mwisho kabisa cha ustaarabu wa Askofu huyo. Nimewahi kuona Askofu mmoja katika nchi moja ya Ulaya aliyevuliwa uaskofu kwa kitendo cha kumsalimia mwana mama kisha akamfinya vidole vyake. Kitendo hicho ambacho kwa wengi hapa kingeonekana cha kawaida, kwa wenzetu wanaojali maadili na nafasi ya mtu, kilimwondolea hadhi na heshima ya kuendelea kuwa Askofu. Huyu Askofu aliyeamua kutumia ngumi badala ya hoja na sala, anaweza kujiona ni Askofu lakini ajue anaongoza miili ya waumini na siyo roho zao.
Ninajenga hoja ya KKKT kuvunja amani kwa sababu viongozi wa dini na hasa maaskofu, kwa wengi bado wanaonekana kama watemi na wafalme wenye himaya kasoro bendera. Kwa hiyo Askofu (Mkuu wa himaya) kumshambulia mwingine, ni kutangaza vita kati ya himaya mbili. Himaya ya yule aliyeshambuliwa ingekuwa na kila sababu kutamka kuwa “sababu, nia na uwezo” wanavyo kuhakikisha wanalinda utu na heshima ya himaya yao. Pengine ndiyo maana mtunza hazina wa Askofu wa aliyeshambuliwa aliamua kupoteza maisha yake na kudundwa magumi na Askofu mshambuliaji ili amlinde Askofu wake. Hali hii ya kulindana kwa magumi na kulazimisha maamuzi kwa magumi ni utamaduni mpya si tu ndani ya kanisa bali hata ndani ya jamii. Mwenegoha atakumbukwa kwa kuasisi na kuendeleza utamaduni huu wa magumi mikutanoni, japo unavunja amani.
Wasomaji na waumini tumefika mahali pa kujiuliza kuna nini kati ya Mwenegoha na maaskofu wa Kaskazini pamoja na yule wa Iringa? Kwanini inaonekana wale wanaopinga uamuzi wa Halmashauri kuu ni wa upande mmoja? Wanataka kujenga ukanda ambao ni adui mkubwa wa nchi yetu. Wanataka hata na wanasiasa waanze kuiga mfano huu wa kujigawa kufuatana na ukanda? Hii ni mbegu mbaya ambayo ni lazima ipingwe vita na kila mtaziania mwenye kulitakia mema taifa letu. Mgogoro huu usiangaliwe kwa upande mmoja wa kanisa (KKKT), uangaliwe kwa upana maana watanzania ni wale wale, walio makanisani ndiyo walio kwenye siasa na kwenye nyanja mbali mbali katika taifa letu.
Mwanzoni tulijiuliza kuna nini kati ya Mwenegoha na maaskofu saba? Matamko ya maaskofu saba tuliyasoma magazetini na sasa Mkuu wa kanisa kwa tamko lake wiki hii ametuthibitishia kuwa tuhuma za maaskofu saba dhidi ya Mwenegoha zimethibitishwa na tume iliyozichunguza. Halmashauri Kuu ikaamua kumfukuza kazi Mwenegoha. Kwa hiyo sasa tunajua kisa cha maaskofu saba na Mwenegoha. Bado tunajiuliza kuna nini kati ya Mwenegoha na Maaskofu wanaomuunga mkono? Haiwezekani maaskofu hawa kuamua kuasi maamuzi ya vikao halali na hata kutishia kuunda kanisa lao wenyewe na Mwenegoha bila sababu nzito! Hawa ni watu wazima sawa na wale saba ambao sasa tunaambiwa tuhuma zao zimethibitishwa. Siri ya mshikamano wa hawa maaskofu wa kaskazini na Mwenegoha inavunja amani ya nchi na ni vema ikajulikana kwa sababu mshikamano wao ni maumivu ya waumini na taifa letu.
Maaskofu hawa wanaovunja amani (kwa kuanzisha ngumi mkutanoni na sasa kuchochea kukaidi maamuzi waliyoyapitisha wao wenyewe), ni mfano wa halisi wa mgogoro wa kukosekana kwa maadili ya kijamii. Hata kama Mwenegoha ndiye kiini cha wao kuungana kukaidi maamuzi halali ya kanisa, lakini si Mwenegoha anayeupa uhalali ule mshikamano. Nikiwa mwanakanisa (si Mlutheri), kwangu mimi nauona ule mshikamano kama umejengwa juu ya kulinda uovu wa aina fulani. Ndani ya mshikamano wa namna hii atakuwemo mtu mmoja au wawili aliyeshikilia siri nyingi za kundi hilo ili lisisambaratike. Siku siri hizo zikiwa wazi, kundi litakombolewa na kuwa huru. Tutaanza kuwasikia wakizungumza mikutanoni bila kutumia ngumi na hatutasikia wakitumia magari kuzunguka nchi nzima baada ya vikao ili kufanya kampeni za kubadili maamuzi.
Niliwahi kusema pia makanisa yana miundo mbali mbali iliyo wazi na isiyo wazi. Mfano kanisa Katoliki, mambo mengi mazuri na mabaya yanabaki ndani. Kuna maaskofu wanatunza chuki zaidi ya miaka kumi, wengine wanavunja maadili, wengine wana ukabila, wengine ni walevi kupindukia nk., yanatunzwa kwa mfumo wao umeundwa kisiri na si wazi kama mfumo wa KKKT. Haya yanayovunja amani kutokea katika KKKT yanafanyika pia katika makanisa mengine ila tofauti yake ni kuwa huko hayatangazwi na haya ya KKKT yanatangazwa. Ndani ya makanisa mengine wapo watu kwa sababu ya umri, nafasi, na uzoefu wao ndani ya kanisa wanapata nafasi ya kujua madhaifu ya walio chini au juu yao. Wakati wa mgogoro kama huu, hupenda kutumia nafasi hiyo kuwanyima mateka wao nafasi ya kuwa na uhuru wa kufikiri na kuamua wapendavyo. Kwa nafasi ya uaskofu hii ni tabia ya maaskofu wastaafu wakiitumia vizuri kuwanyima uhuru maaskofu walio kazini. Ikiwa hii ndiyo dhana inayoendelea ndani ya KKKT nashauri maaskofu walio kazini waamue kuasi utumwa huu kwa maslahi ya kanisa na amani katika jamii.
Huko Zambia, kuna Askofu mmoja ambaye kabla hajawa Askofu mlevi na mvuta sigara kupindukia. Ulevi ule ukamfanya ambake mtoto wake wa kike na kufanya mapenzi naye! Aliyekuwa Askofu wakati huo akalitunza jambo hilo likaishia ndani ya nyumba ile na huyu mume (Askofu sasa) akaacha ulevi na sigara, lakini pia mke wake akaacha kujuana na mmewe. Yule Askofu mzee alipostaafu akahakikisha huyu mrithi hawi na uhuru wa kuamua kwa sababu ya dhambi ile. Licha ya kuwa dhambi ile sasa inajulikana, lakini Askofu wa sasa ameshindwa kabisa kujikomboa na hawezi kuamua lolote mpaka Askofu mzee atakapokufa. Askofu mzee anakiuka maadili ya kutubisha dhambi pale anapowaweka utumwani wale waliotubu kwake. Hili kama linatokea katika mgogoro wa KKKT ni kosa la maaskofu vijana na si la wazee au Mwenegoha anayejua madhambi ya hawa maaskofu. Wote tunajua kuwa maaskofu wanazo dhambi na washarika wako tayari kuwasamehe iwapo maaskofu wazee au watendaji kama Mwenegoha watazitaja hadharani. Kufunika dhambi kusivunje amani ya nchi na kudhalilishana kama ilivyotokea Mbagala.
Gazeti moja wiki iliyopita liripoti kuwa tume iligundua ubadhilifu wa fedha nyingi katika KKKT na jingine likaripoti kuwa Mkuu wa Kanisa alilazimika kuvunja ofisi ya Mwenegoha pale Mwenegoha alipokataa kufika katika makabidhiano. Mambo haya pia yanavunja amani. Watu wengi wanaamini kanisani ni mahali patakatifu, hakuna wizi, hakuna ubadhilifu, hakuna ufuska, hakuna kughushi na ukaidi. Itakuwa vema KKKT ili kurejesha imani ya waumini ichapishe ile ripoti ya uchunguzi ili kila mtaziania ajionee maana kanisa ni taasisi ya watu na inakusanya fedha (sadaka) kutoka watu. Aidha kitendo cha kuvunja ofisi ya kanisa kwa kutumia polisi kinaashiria kabisa kuwa Bw. Mwenegoha anazo sababu nyingine zaidi ya zile anazodai ni haki zake. Katika ofisi nyingi hata mtu akisimamishwa kazi kwa wiki moja anakabidhi ofisi. Mwenegoha amefukuzwa kazi na hakuenda mahakamani hadi ofisi zinavunjwa. Ukaidi wa namna hii katika ofisi ya umma ni kuvunja amani.
Mwisho KKKT inavunja amani pale ambapo inafumbia macho vitendo viovu viendelee ndani ya kanisa kwa muda mrefu bila kuvishughulikia. Ni wazi matendo maovu kama hayo yanayotajwa na vyombo vya habari kama ni ya kweli, yanaiweka hata serikali mahali pagumu maana serikali inayaheshimu mno makanisa. Lakini kwa sasa kwa kuwa ni wazi KKKT inavunja amani ni vema serikali ikalichukulia hili kwa uzito wake. Hufika wakati hata wale tuliowadhania wana hekima wakabainika wamefilisika. Nani alijua dayosisi za Kaskazini ambazo ndizo kitovu cha Ulutheri leo ziwe msitari wa mbele kutetea kinachoonekana wazi ni kinyume kabisa na sura ya kanisa? Sasa si tatizo tena la Mwenegoha, ni tatizo la maaskofu wanaomkumbatia Mwenegoha. Kwa manufaa ya taifa letu, ni vyema maaskofu hawa wakamaliza tatizo hili vinginevyo watapunguza nguvu za kanisa katika kulinda na kutetea amani katika taifa letu.
Na,
Padri Privatus Karugendo.

MAASKOFU KUPIGANA NI ISHARA YA NINI?

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005.

MAASKOFU KUPIGANA NI ISHARA YA NINI?

Tarehe 16 mwezi huu gazeti hili liliandika habari za kusikitisha na kushangaza:
“Maaskofu watatu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) wiki hii walipigana makonde na kurushiana viti wakati Halmashauri ya KKKT ilipoketi kujadili ripoti ya tume iliyoundwa kuchunguza tuhuma dhidi ya aliyekuwa Katibu mkuu wa kanisa hilo, Amani Mwenegoha. Habari kutoka ndani ya kikao hicho zinasema kwamba katika tukio lililofanyika kwenye ukumbi wa Mbagala Spiritual Centre, Dar es salaam, ugomvi huo ulianzishwa na Askofu wa Dayosisi ya Arusha, Thomas Laizer, aliyenyanyuka na kumrukia Askofu mwenzie, Dk Benson Bagonza wa Dayosisi ya Karagwe”. (Tanzania Daima Jumapili Januari 16, 2005)

Kupigana ni kitendo cha kishenzi. Hata kama Askofu Laiser, alikuwa na sababu za msingi dhidi ya Askofu Bagonza, angezijibu kwa hoja na wala si kipigo. Kumpiga mtu ni kumdhalilisha! Hata katiba yetu ya nchi inapinga kitendo hiki. Haki za Binadamu zinapinga kitendo hiki. Ustaarabu na kuelimika kunapinga matendo ya kishenzi kama kupigana. Katika nchi zilizoendelea, kitendo cha Askofu Laiser, ni sababu tosha ya yeye mwenyewe kuwajibika na kuacha cheo cha Uaskofu!

Askofu ni mtu wa aina gani:
“Mtu akitaka kuwa askofu katika Kanisa, huyo anatamani kazi nzuri. Basi, kiongozi wa kanisa anapaswa awe mtu asiye na lawama; anapaswa awe na mke mmoja tu, awe mwenye kiasi, nidhamu na utaratibu, ni lazima awe mkarimu na anayeweza kufundisha, asiwe mlevi au mtu wa matata, bali awe mpole, apendaye amani……….. Anapaswa awe mwenye sifa njema kati ya watu walio nje ya kanisa, ili asije akalaumiwa na kuanguka katika mtego wa Shetani.” (Timoteo 3:2 – 7 ).

Kitendo cha kumpiga Askofu mwenzake, Askofu Laizer, anaondolewa sifa zote zilizotajwa hapo juu. Watu walio nje ya kanisa wanamlaumu na kumkusanya Askofu Laizer, kwenye kundi la watu washenzi, maana kupigana ni kitendo cha kishenzi. Anayepigana anakuwa ameanguka kwenye mtego wa Shetani!

Kupigana si kitendo cha Ukristu. Tunaambiwa katika maandiko matakatifu:
“Mmesikia kwamba ilisemwa: Jicho kwa jicho, jino kwa jino. Lakini mimi nawaambieni, usimlipize kisasi mtu mbaya. Mtu akikupiga kofi shavu la kulia, mgeuzie pia shavu la Pili. Mtu akikupeleka mahakamani kutaka kukuchukulia shati lako, mwache achukue pia koti lako. Na mtu akikulazimisha kuubeba mzigo wake kilomita moja, ubebe kilomita mbili….” (Matayo 5:38 – 41).

Haya ni miongoni mwa mafundisho magumu ya Bwana Yesu Kristo. Ndio maana si watu wote ni Wakristu na si watu wote ni maaskofu. Hata na wale wanaojiita Wakristu, Yesu mwenyewe akirudi leo hii watajificha au yeye mwenyewe atawakana! Tunashuhudia wale wanaojiita Wakristu wakipelekana mahakamani. Majambazi, walarushwa na wenye tabia ya kunyanyasa ndugu zao, ni miongoni mwa wale wanaojiita Wakristu. Hakuna Mkristu anayepigwa shavu la kushoto akageuza na la kulia! Sote ni binadamu na kila mtu ana udhaifu wake. Kwa Mkristu aliyeikubali imani hii, akishindwa kuitekeleza ni lazima kuwajibika. Zipo njia nyingi za kuwajibika, kwa Wakristu walio wengi tendo la kuungama dhambi ni njia mojawapo ya kuwajibika. Lakini haitoshi kutubu, ni lazima kuwepo na ishara ya wazi. Enzi za zamani na leo hii kwa wale ambao wana mtazamo wa kizamani, ishara ya wazi ni kama kufanya kazi za mikono, kama kulima mashamba ya kanisa, kusomba mawe na matofali ya ujenzi wa majumba ya kanisa au mchango wa pesa au wengine kuitesa miili yao kwa kupigwa na kujipiga wao wenyewe na kuichoma miili yao kwa vitu vikali.

Askofu ni mfano wa kuonyesha njia ya kuishi imani ya Kikristu. Anaposhindwa, kama alivyoshindwa Askofu Laiser, ishara ya wazi ya kutubu si kulima kwenye mashamba ya kanisa, kusomba mawe na matofali ya ujenzi wa nyumba za kanisa, au kutoa pesa, ni kujiuzulu kazi ya uaskofu na kuwaachia nafasi wengine wenye uwezo kuhimili mapigo ya dunia hii ya utandawazi.

Ukiuchunguza ule unaoitwa mgogoro wa KKKT, utagundua kwamba kanisa hili sasa hivi linawahitaji maaskofu wa kuhimili mapigo ya dunia ya leo. Mgogoro huu ni magomvi kati ya maaskofu vijana, wasomi na maaskofu wazee ambao walichaguliwa kushika nafasi zao si kwa usomi bali kwa uzoefu. Maaskofu vijana na wasomi wanatumia hoja za kisomi, wazee wanatumia uzoefu na vitisho vya heshima ya uzee na madaraka, ikishindikana hiyo basi ni kiboko maana kwa Mwafrika, mtoto ni lazima achapwe pale anapoonyesha ukaidi. Hayo ndio yalitokea kwa Askofu Laizer mzee na Askofu Benson Bagonza, ambaye ni kijana.

Maaskofu Vijana, hawakubali kuwekwa mfukoni. Wengi wao wamesoma Amerika na Ulaya. Njia za kutafuta wahisani wanazifahamu, lugha ya kuongea nao wanaifahamu, utaalamu wa kuandika miradi wanaujua. Hivyo wanajua njia za kuingiza pesa katika diosisi zao bila ya kumtegemea Katibu mkuu wa KKKT. Maaskofu vijana wanapingana na ukabila, ukanda na lugha ya huyu ni mwenzetu. Wanaiona KKKT, kama kitu kimoja na mtu apewe madaraka kufuatana na sifa zake, si kwa vile ni mtoto wa fulani au mtu wa kabila fulani. Wanapinga kuanzisha diosisi za kikabila, hasa zenye kabila moja.

Bahati mbaya inayowakumba Maaskofu Wazee wa KKKT, ni kwamba mfumo wa KKKT, ni wa kidemokrasia. Hauna chombo chenye nguvu na madaraka kama ROMA, kwa upande wa Wakatoliki. Vatican, inajua kuwadhibiti Maaskofu vijana na wenye mawazo ya kisasa. ROMA, ina mfumo wa kimafia wa kuwafutilia vijana wakati wanasoma. Kama mtu ana mawazo ya kisasa hawezi kupata uaskofu katika kanisa katoliki. Na mfumo wa Kikatoliki, hauruhusu mtu asiyekuwa Askofu, kuingia kwenye mikutano ya maaskofu. Hivyo wakipigana kwenye mikutano yao, siri zinabaki ndani. Si kwamba mambo yao yanakwenda vizuri kuliko ya KKKT, labda yao ni mbaya zaidi, lakini kwa vile wanakutana peke yao, kuta ndizo mashahidi! Na kuta hazina uwezo wa kuandika na kutoa habari kwenye vyombo vya habari! Habari zao zinaweza kuvuja akijitokeza Askofu mkorofi, lakini pia kuna njia za kumtorosha na kumficha kifungoni kule ROMA!

Kitendo cha Askofu Laizer, ni lazima kiwe changamoto kwake yeye na kwa kanisa nzima. Atawezaje kusimama na kufundisha kuvumiliana, kuchukuliana na kuheshimiana. Atawezaje kutoa ushauri katika serikali yetu ambayo sasa hivi inahitaji majadiliano na si ngumi na kurushiana viti? Atawezaje kukemea maovu katika jamii yetu ya Kitanzania. Atawezaje kuwakemea majambazi yanayovamia watu na kuwapiga? Atawezaje kuwakemea wanaume wanaowapiga ovyo watoto wao na wake zao? Atapata wapi nguvu za kufanya kazi zake za kiuchungaji?

Kanisa lianze kufikiria kwa makini kuwapandisha wanawake katika daraja la Uaskofu. KKKT, ina wachungaji wanawake, lakini bado haijakubali kuwa na maaskofu wanawake. Mawazo kwamba Yesu, alimchagua Petro na mitume kuliongoza kanisa hauna utetezi wowote kwenye Agano Jipya. Chenye utetezi ni hiki:
“Mmejengwa juu ya msingi uliowekwa na mitume na manabii, naye Kristo mwenyewe ndiye jiwe kuu la msingi. Yeye ndiye mwenye kulitegemeza jengo lote na kulikuza hata liwe hekalu takatifu kwa ajili ya Bwana. Katika kuungana naye, ninyi pia mnajengwa pamoja na wote wengine, muwe makao ya Mungu kwa njia ya Roho wake.” (Waefeso 2:20 – 22)

Utetezi huu unaonyesha jinsi mtu yeyote yule anayekubali kuungana na Kristo na kusimama juu ya msingi uliojengwa na mitume na manabii anaweza kuliongoza kanisa. Sharti hili haliangalii jinsia! Mawazo ya jinsia yameingizwa na wahuni, wapenda madaraka walioivuruga historia nzima ya kanisa.

Pamoja na huruka ya wanaume ya kupenda madaraka, unyanyasaji, uhuni, ujambazi, ukatili, kutokuwa na huruma, kulipiza kisasi na kupenda vita, wana tabia ya woga. Kristu, alipokamatwa hadi kufa msalabani alikuwa amezungukwa na wanawake peke yao. Inashangaza jinsi Kristu, angefanya uamuzi wa kuacha kanisa lake mikononi mwa watu wenye woga kama wanaume, wakati alijua magumu yaliyokuwa yakilikabili kanisa lake.

Ushuhuda wa Matayo:
“ Na pale walikuwako wanawake wengi wakitazama kwa mbali. Hao ndio wale waliomfuata Yesu kutoka Galilaya wakimtumikia. Miongoni mwao walikuwa Maria Magdalena. Maria mama yao Yakobo na Yosefu, pamoja na mama wa wana wa Zebedayo” (Matayo 27:55 – 56).

Kufuatana na Matayo, hakuna mwanaume aliyekaribia msalaba wa Yesu. Imani ya Kikristu, inasimama juu ya fumbo la msalaba, kufa na kufufuka. Wanaume waliyakimbia matukio haya, iweje waachiwe jukumu la kuyasimamia na kuyaeneza?

Ushuhuda wa Marko na Luka, unafanana na wa Matayo. Wote wanakubaliana kwamba msalabani walikuwepo wafuasi wanawake. Wanaume walikuwa wanaogopa. Wote walimkana Kristu kama Petro. Ushuhuda wa Yohana, ni tofauti kidogo, lakini ni msaada mkubwa maana unafumbua fumbo ambalo limewasumbua watu siku nyingi. Kama Yesu, alimwacha mama yake mikononi mwa wanawake basi na kanisa aliliacha mikononi mwa wanawake. Hakuna popote katika Agano la kale panapoonyesha kwamba Yesu, alikuwa karibu sana na mtume mwanaume, hakuna! Mtu, anayeonyeshwa kuwa karibu naye ni Maria Magdalena. Huyu ndiye aliyeshuhudia ufufuko! Kama tunasema imani ya Kikristu, imesimama juu ya fumbo la msalaba, kufa na kufufuka, shuhuda mkubwa ni Maria Magdalena. Alimsindikiza Yesu, katika maisha yake yote ya taabu na raha, ni mtu pekee aliyeonyesha kumjali hadi kusafisha miguu yake na kuipangusa kwa nywele zake, alimsindikiza hadi Msalabani na kushuhudia ufufuko wake.

“Karibu na msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mama yake na dada ya mama yake, Maria mke wa Kleopa, na Maria Magdalena. Yesu alipomwona mama yake, na karibu naye amesimama yule mwanafunzi aliyempenda, akamwambia mama yake: “Mama! Tazama, huyo ndiye mwanao” Halafu akamwambia yule mwanafunzi: “Tazama, huyo ndiye mama yako”. Na tangu saa ile huyo mwanafunzi alimchukua akae nyumbani kwake.” Yohana 19:25 – 27)

Haiwezekani huyu mwanafunzi aliyependwa na Yesu, awe mwanaume. Haikuandikwa popote na wala hakuna tukio katika Agano Jipya, la kuuonyesha uhusiano wa karibu kati ya Yesu na mtume mwanaume. Hata hivyo hakuna injili inayoonyesha kwamba wanaume waliukaribia msalaba. Hata hivyo waliokuwa na nyumba na mali na kumtunza Yesu, ni wanawake! Luka, anashuhudia jambo hili:
“Pia wanawake kadhaa waliokuwa wamepagawa na pepo, au wagonjwa ambao Yesu, alikuwa amewaponya, waliandamana naye. Hao ndio akina Maria (aitwaye Magdalena), ambaye alitolewa pepo wabaya saba; Yohana, mke wa Kuza, mfanyakazi mkuu wa Herode; Susana na wengine kadhaa. Hao wanawake walikuwa wakiwatumikia kwa mali yao wenyewe.” (Luka 8:2 – 3)

Hakuna mtu mwingine anayetajwa kumtunza Yesu na watu wake, isipokuwa wanawake. Mitume wanaume walikuwa wavuvi na walalahoi. Hawakuwa na uwezo wa mali kumtuza mama ya Yesu na kulitunza kanisa la mwanzo. Kanisa la mwanzo liliishi na kutunzwa kwenye nyumba za wanawake. Ushuhuda wa Paulo:
“Salamu zangu ziwafikie Priska na Akula, wafanyakazi wenzangu katika utumishi wa Kristo Yesu. Wao walihatarisha maisha yao kwa ajili yangu. Wanastahili shukrani; si tu kutoka kwangu bali pia kutoka kwa makanisa yote ya watu wa mataifa mengine. Salamu zangu pia kwa kanisa linalokutana nyumbani kwao.” (1 Wakorinto 16:19)

“Salamu zetu kwa ndugu zetu wa Laodikea; msalimuni dada Nimfa pamoja na jumuiya yote ya waamini inayokutana nyumbani kwake” (Wakolosai 4:15)

“Mimi Paulo, mfungwa kwa ajili ya Kristo Yesu, na ndugu Timoteo, tunakuandikia wewe Felemoni, mfanyakazi mwenzetu na kanisa linalokutana nyumbani kwako, wewe dada Afia, na askari mwenzetu Arkupo.” (Barua ya Paulo kwa Filemoni 1:1 – 2)

Ipo mifano mingi inayoonyesha jinsi kanisa la kwanza lilivyokuwa mikononi mwa wanawake na jinsi wanawake walivyokuwa viongozi bora na imara. Hata historia ya kanisa ina mifano mingi ingawa kwa vile historia hii imeandikwa na wanaume, mifano ya matendo ya wanawake imepuuzwa na kutupwa pembeni!

Maaskofu kupigana ni ishara tosha kwamba wanaume sasa wanaelekea kushindwa kuliongoza kanisa. Ili imani ya watu isipotee, ni wakati mzuri wa kulikabidhi kanisa mikononi mwa wanawake.

Na
Padri Privatus Karugendo.

ULEMAVU WA FIKRA

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA TANZANIA DAIMA JUMAPILI 2005


ULEMAVU WA FIKRA

Nimemsikia Mzee Mengi, akiongelea ulemavu wa fikra kwenye matukio mawili tofauti. Kama si taifa letu kushambuliwa na ulemavu wa fikra. Maoni ya Mzee Mengi, yangezua mjadala mkali. Watu wangejiuliza ana maana gani anaposema ulemavu wa fikra. Mara ya kwanza nilimsikia Mzee Mengi, akiongelea ulemavu wa Fikra, wakati akiongea na walemavu. Aliwaambia wasifikirie kwamba kwa vile wana ulemavu wa viungo vya mwili, basi wao ndio walemavu; au kufikiri kwamba wao si watu muhimu katika taifa; au kujisikia unyonge na kukata tamaa, hata watu wenye viungo kamili vya mwili wanaweza kuwa walemavu na hasa ulemavu wa fikra Kwa maoni ya Mzee Mengi, mtu mwenye viungo kamili vya mwili, lakini ana ulemavu wa fikra, anaweza kuwa mnyonge na mtu asiyefaa katika jamii kuliko mtu mwenye ulemavu wa viungo!

Jana nimemsikia tena Mzee Mengi, akiongelea ulemavu wa fikra wakati akitoa hoja za kususia mkutano wa Mawasiliano. Yeye pamoja na wamiliki wa vyombo vya mawasiliano Tanzania, walisusia mkutano wa kupendekeza masharti mapya ya kutoa leseni za vyombo vya mawasiliano.

Mzee Mengi, alilalamika, kwamba watu wenye ulemavu wa fikra, waliwaacha wataalam wa mawasiliano hapa nchini na kutafuta wataalam kutoka nchi za nje Zimetumika pesa nyingi, ambavyo wataalam wangepatikana hapa kwa malipo nafuu. Kosa kama hili linafanyika kila wakati kwenye wizara nyingine. Madaktari Muhimbili, kwenye kitengo cha mifupa (MOI), walimfukuza mzungu aliyekuwa akifanya kazi ambazo watanzania wengi wangeweza kuzifanya kwa malipo nafuu. Makampuni yetu yanatupwa nje, na kazi yanapewa makampuni kutoka nje ya nchi yetu.

Inawezekana wengine wakasema kwamba watanzania hajui kufanya kazi, wanashindwa kuwajibika, wanashindwa kufanya kazi kwa uaminifu, wanafanya kazi kwa upendeleo wa kuwaajiri ndugu zao. Huo ndio ulemavu wa fikra, anaouzungumzia Mzee Mengi. Mtu mwenye fikra pevu, angejitahidi kuunda mifumo ya kutoa dosari, kabla ya kukimbilia kuwatafuta wataalam nje ya nchi. Kufunika tatizo, zi kulimaliza tatizo! Ulemavu wa fikra ndio unasababisha tuendelee kufunika matatizo!

Maoni ya Mzee Mengi, yamenifanya nitafakari mambo mawili: Kwanza nilitafakari juu ya kitabu “ Why God Won’t Go Away”. Kitabu hiki ni matokeo ya utafiti uliofanywa na Andrew Newberg,Eugene D’aquili na Vince Rause, juu ya Sayansi ya Ubongo na Biolojia ya Kuamini. Wazo kuu katika utafiti wao ni: Je, Mungu anautengeneza Ubongo au Ubongo unamtengeneza Mungu? Kitu wanachokigundua ni kwamba Ubongo ndicho chombo cha pekee katika mwili wa mwanadamu kinachotengeneza kumbukumbu na kuzitunza. Ubongo unamsukuma mwanadamu kuwa na woga na kujiuliza maswali mengi ambayo majibu yake yanamfanya mwanadamu kuishi tofauti na wanyama wengine. Mwanadamu hujiuliza: Kwanini tulizaliwa kama mwisho wetu ni kufa? Kunatokea nini tukifa? Nafasi yetu ni ipi katika ulimwengu mzima? Kwanini kuna mateso? Ni nani anayatuma mateso? Ni nani anautunza na kuulinda ulimwengu? Ulimwengu utaendelea kuwepo hadi lini? Tunawezaje kuendelea kuishi kwenye ulimwengu usioaminika bila kuwa na woga? Majibu ya maswali haya ni lazima yamwelekeze mwanadamu kwa Mungu. Majibu ya maswali haya ndio chimbuko la dini zote za dunia hii. Mtu asiyejiuliza maswali kama haya, hapana shaka ataishi kama mnyama mwingine wa porini! Huu ni mjadala mrefu na ni utafiti wa kisayansi, ni vigumu kuujadili kwenye makala hii. Unahitaji makala inayojitegemea, Mungu, akiniwezesha, nitauendeleza siku za usoni! La msingi katika mfano huu ni kutaka kuonyesha jinsi maneno ya Mzee Mengi, yalivyonifanya kutafakari mambo mazito.

Baada ya kutafakari kitabu cha “Why God Won’t Go Away”, nilitafakari maneno ya Bwana Yesu: “ Ndiyo maana ninasema nao kwa mifano, kwa sababu wanatazama lakini hawaoni, wanasikiliza lakini hawasikii, wala hawaelewi..” (Matayo13:13).

Kama anavyosema Mzee Mengi, kwamba walemavu si wale tu walio na upungufu katika viungo vya mwili, bali pia na wale wenye ulemavu wa fikra. Maana kama mtu ana macho lakini hawezi kuona, ana masikio lakini hawezi kusikia, ana pua, laikini hawezi kunusa, huyu anakuwa ni kilema. Ni wangapi wanauona umasikini wa taifa letu? Ni wangapi wanayaona magonjwa yanayotishia uhai wetu? Ni wangapi wanaosikia kelele za “Mvua za kwanza ni za kupandia”, “Tumia chandarua kujikinga na malaria”, “UKIMWI unaua”, “Usitumie pesa kuuza uhuru wako wa kuchagua, chagua kiongozi bora”, “Rushwa ni adui wa Haki, usitoe wala kupokea rushwa”. Maana yake ni kwamba kilema wa hivi ambaye ana macho lakini hawezi kuona, ana masikio lakini hawezi kusikia na ana pua lakini hawezi kunusa, Ubongo wake unakuwa umedumazwa na kupunguziwa nguvu za kutengeneza kumbukumbu na kuzitunza. Anakuwa anaelekea kwenye hali sawa na mnyama wa porini. Mara nyingi matendo yake yanakuwa ya kinyama. Ubongo ukishindwa kutengeneza kumbukumbu na kuzitunza, wema, haki na huruma, hutoweka. Mauaji ya Wayahudi milioni 6, mauaji ya Watutsi ya mwaka 1994,magomvi kati ya Waisraeli na Wapalestina, chuki kati ya Wahutu na Watutsi ni vielelezo vizuri. Ulemavu huu ni mbaya zaidi. Mtu, ambaye ana mguu mmoja, lakini ubongo wake unafanya kazi vizuri, anakuwa na manufaa makubwa katika jamii kuliko mtu ambaye ana viungo vyote vya mwili lakini ubongo wake umedumazwa.

Yesu alielezea vizuri hali kama hii:
“ Kwao yanatimia yale aliyosema nabii Isaya: ‘Kusikia mtasikia, lakini hamtaelewa; Maana akili za watu hawa zimepumbaa, wameziba masikio yao, wamefunga macho yao. La sivyo, wangeona kwa macho yao, wangesikia kwa masikio yao, wangeelewa kwa akili zao, na kunigeukia, asema Bwana nami ningewaponya”( Matayo 13:14-15).

Ulemavu wa fikra unaweza kusababishwa na mambo mengi. Mtu anaweza kuzaliwa akiwa na ulemavu wa fikra. Inawezekana ubongo ukawa na kilema cha kutoweza kutengeneza kumbukumbu na kuzitunza vizuri. Wapo watu wanazaliwa wakiwa pungwani, vichaa na wendawazimu Lakini pia kuna ulemavu wa fikra wa kujitakia au kulazimishwa. Wale wanaotumia madawa ya kulevya na ulevi wa kupindukia, wanaulazimisha ubongo kushindwa kutengeneza kumbukumbu na kuzitunza. Lakini pia kumtawala mtu kimawazo kunaweza kusababisha ulemavu wa fikra. Utumwa na ukoloni ni kati ya vitu vilivyosababisha ulemavu wa fikra. Athari hii inajitokeza katika nchi karibu zote zilizotawaliwa na kuonja adha ya utumwa. Mfano Utumwa na Ukoloni, ulisababisha baadhi ya watu kukataa mila zao, rangi ya ngozi zao, lugha zao nk.

Mtu anayeichubua ngozi yake, anakuwa na ulemavu wa fikra. Mtu anayebadilisha nywele zake na wakati mwingine kulazimika kuvaa nywele za bandia ili afanane na mzungu, anakuwa na ulemavu wa fikra. Mtu anayebadilisha jina lake la kienyeji na kujipachika jina la Wazungu au Waarabu, anakuwa na ulemavu wa fikra. Mtu anayeshabikia bidhaa kutoka nje ya nchi na kuzorotesha uchumi wa nchi yake, anakuwa na ulemavu wa fikra n.k.

Kama anavyosema Yesu: “Maana akili za watu hawa zimepumbaa….”. Ni ukweli, Wazungu walipumbaza akili zetu hadi Ubongo ukatengeneza kumbukumbu na kuzitunza kwamba Mwafrika hawezi kitu. Wazungu walituzabishia ulemavu wa fikra. Ndo maana hadi leo hii bado tunatafuta wataalam kutoka nje, kama anavyolalamika Mzee Mengi, juu ya swala zima la mawasiliano.

Tuchukulie mfano wa jamii za kwanza kuishi hapa Tanzania. Jamii zilizoanza kushuhudia kifo. Mwanaukoo anakufa. Mwili wake unawekwa mbele ya ukoo mzima, na kila mtu anashangaa ni kitu gani kimetokea. Kila mtu anajitahidi kuugusa mwili wa marehemu na kuhisi hauna uhai tena. Mtu aliyekuwa akitembea, akicheka na kufanya kazi sasa, amelala mbele yao bila kujitingisha, mwili wake hauna joto tena, hawezi kuzungumza wala kucheka. Kiongozi wa ukoo anaagiza ukokwe moto mkubwa, wanaukoo wanauzunguka moto huo wakiwa na mwili wa mwanaukoo mwenzao asiyeweza kusimama. Kila mtu anatafakari juu ya tukio hilo. Ni kitu gani kimetoweka kwenye mwili wa ndugu yao, je kitu hicho kitakuwa kimekwenda wapi. Jinsi muda unavyopita kasi ya moto mkubwa inaanza kupunguka. Kuni zilizokuwa rundo zinaanza kuungua na kuwa majivu. Kadri moto unavyopungua ndivyo moshi unavyokazana kupaa juu mawinguni. Moto unatoweka na moshi unaishia mawingu. Kiongozi wa ukoo anaanza kutafakari juu ya kuni, moto, moshi na majivu. Ubongo wake unaanza kutengeneza kumbukumbu na kuleta fikra pevu, jinsi kuni, moto na moshi vinavyopotea na kubakiza majivu, ndivyo mwili wa rafiki na mwanaukoo aliye lala mbele yao ulivyopoteza kicheko, sauti, kusimama na kubaki mwili usiokuwa na uhai. Jinsi moshi unavyoishia mawinguni, ndivyo uhai wa rafiki yao unavyoishi mawinguni pia! Fikra hii ya kiongozi inasambazwa kwa wanaukoo wote. Kwa njia hii ukoo wote unamgeukia Mungu na…. Yasemavyo maandiko: “La sivyo, wangeona kwa macho yao, wangesikia kwa masikio yao, wangeelewa kwa akili zao, na kunigeukia, asema Bwana nami ningewaponya”

Mtu ambaye hana ulemavu wa fikra. Mtu ambaye ubongo wake unafanya kazi sawa awa ni lazima ajifunze kutokana na matukio. Kama mfano nilioutoa wa watu wa jamii za mwanzo walivyokumbana na kifo bila kujua kifo ni nini, lakini kwa kuagalia kuni zikiteketea kwa moto na moshi ukipaa juu mawinguni walianza kutafakari na kutengeneza fikra pevu ambayo iliendelea vizazi na vizazi.

Mtu ambaye ana ulemavu wa fikra, hawezi kutafakari. Atakazana kulimbikiza pesa ambazo hazitamnufaisha yeye wala familia yake. Ni nani ananufaika na pesa za Mobutu au Sani Abacha? Pamoja na mifano hii ya wazi, bado kuna watu hapa Tanzania, wanaendelea kulimbikiza pesa. Watu wanakufa kwa njaa, watoto hawawezi kwenda shule, Watu wanakufa kwa magonjwa yanayotibika, Wafungwa wananyimwa haki ya kukutana na wake/waume zao kwa kisingizio kwamba serikali haina pesa, wakati kuna watu wachache wamelimbikiza pesa ambayo ingeweza kumaliza matatizo yote hayo!
Mtu mwenye fikra pevu, anaangalia uhai wake na uhai wa taifa zima. Mzee Mengi, anasema kuna mbinu za makusudi au za bahati mbaya za kuua uwezo wa wamiliki wa vyombo wa mawasiliano hapa nchini. Kipaumbele wanapewa watu kutoka nje ya nchi. Kama hii ni kweli, wale wanaotengeneza mbinu hizi wanaupenda uhai wao na uhai wa watanzania wote? Watu hawa wana fikra pevu au ni walemavu wa fikra?

Leo imetokea kwa vyombo vya mawasiliano. Kesho ni Shelaton, Royal Palm….(jina jipya ni lipi?), hivyo hivyo wanakuja wanachuma na kuondoka. Sisi tunabaki na marehemu wetu tukiwa na maswali kibao: Mbona hapumui, mbona acheki, mbona hawezi kutembea, ni kitu gani hiki kinatokea. Tukiishia hapo ndio mwisho wetu!

Ningependa kuunga mkono mawazo ya Mzee Mengi, kwamba walemavu, wasikate tamaa wala kujiona ni watu wasiokuwa na muhimu. Ulemavu wa kuchukia ni ule wa fikra.

Hivyo tunapojiandaa kuwachagua viongozi wetu, tusiwapime kwa ubora wa viungo vyao, ubora wa pua, miguu urefu, ufupi, uzuri wa sura, ubora wa kuongea lugha za kigeni, ubora wa kuvaa suti za kigeni! Tuwapime kwa ubora wa fikra zao. Kiongozi ambaye ubongo wake hauwezi kutengeneza kumbukumbu na kuzitunza, kiongozi ambaye anaitizama maiti bila kutafakari, kiongozi anayeziangalia kuni zikiteketea na moshi ukiishia mawinguni bila kutafakari, kiongozi anayeona yanayotokea kwa majira zetu akaendelea kuishi bila kutafakari, kiongozi anayeishi kwa kunywa, kula na kulala hawezi kuitawala Bongoland! Mlemavu wa viungo vya mwili anaweza kuwa kiongozi mzuri, lakini mlemavu wa fikra ni moto wa kuotea mbali!

Na,
Padri Privatus Karugendo.

UJASIRI WA SUMAYE NI PESA

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA RAI 2005

UJASIRI WA SUMAYE NI PESA.

Ninaandika makala hii kwa wale wote wanaohoji ujasiri wa Sumaye, wa kutangaza kwamba anataka kugombea kiti cha Urais, ninawaandikia wale wanaofikiri Sumaye, amechanganyikiwa kuonyesha nia ya kutaka kuingia kwenye viatu vya Mkapa. Ninaandika makala hii nikicheka ingawa moyo wangu unanilazimisha kulia. Ninacheka kicheko cha huzuni na kujilaumu, kicheko ambacho ni dalili za kuonyesha ushujaa wa kijinga na ubwege! Ingawa ninacheka, wewe unacheka, nyinyi pia mnacheka, sote tunacheka, na wao kule wanacheka, ukweli ni kwamba, utalia wewe Tanzania! Utalia ukiwa umeshikilia kitanzi chako mikononi. Kamba uliyoitengeneza wewe mwenyewe kwa mikono yako mitukufu, ewe Tanzania, itayamaliza maisha yako, furaha yako, utulivu wako, amani yako na mshikamano wako. Dhambi uliyoilea wewe mwenyewe ewe Tanzania, mtukufu, ikutafune wewe na vizazi vyako. Mwalimu Nyerere, aliomba na Mungu, akamsikiliza, hayupo kushuhudia jinsi dhambi zetu zinavyotutafuna. Ningejua, huja baadaye. Ni heri ungesikiliza ewe Tanzania!

Jesse Kwayu na wenzako, nitumie maneno gani ili macho yenu yapate kufumbuka na masikio yenu kusikia? Maneno yangu niyapambe kwa vito gani ili myapokee na kuyakubali Tumrundishe nabii Isaya, aliyesema:
" Kusikia mtasikia, lakini hamtaelewa kutazama mtatazama, lakini hamtaona. Maana akili za watu hawa zimepumbaa, wameziba masikio yao, wamefunga macho yao. La sivyo, wangeona kwa macho yao, wangesikia kwa masikio yao, wangeelewa kwa akili zao, na kunigeukia, asema Bwana nami ningewaponya."
Haya ni maneno ya zamani, lakini leo yanatunyea kama mvua ya mawe. Mvua isiyokuwa na huruma, mvua isiyojali mafuriko, mvua ya kuleta maafa! Aisifuye mfua imemnyea! Ole wake mtu huyo atakayekulazimisha kuifuta historia yako kwa kamba uliyoitengeneza wewe mwenyewe, ewe Tanzania. Heri mtu huyo asingezaliwa!

Jesse na wenzako, ujasiri wa Sumaye ni pesa! Ana pesa! Pesa adui wa haki, pesa yenye uwezo wa kupindisha ukweli kuwa uwongo, pesa inayowanyamazisha mashujaa, wasomi na wacha Mungu! Pesa yenye nguvu za kuvunja undugu na kupandikiza chuki, kuvunja ndoa na kusambaratisha familia. Pesa chanzo cha rushwa, ujambazi, ufisadi na kuyapotosha maadili mema katika Taifa letu. Hicho ndicho kitanzi tulichokisuka kwa mikono yetu wenyewe. Na sasa kimegeuka kuwa hukumu ya maisha yetu. Tungemsikia Mwalimu, tungetambua kwamba pesa si msingi wa maendeleo, bali ni matokeo. Sisi tumetanguliza pesa! Wahaya wana msemo: " Ekilalema amaela onage". Tafsiri ya kubabaisha: Jambo litakaloshindwa nguvu ya pesa, achana nalo! Asilimia kubwa ya watanzania ni walalahoi, hawana pesa, hawana ajira! Hata wale wenye ajira, mishahara yao ndio hiyo chini ya dola mia kwa mwezi. Matumizi, juu ya dola miatano kwa mwezi. Wakimwagiwa pesa za uchaguzi wote wataimba CCM juu, Sumaye, apite!

Pesa zikimwagwa vizuri vyombo vyote vya habari na waandishi wa habari wataimba CCM juu, Sumaye, apite! Ni vigumu masikini mlalahoi kuhimili nguvu za pesa. Ni nani mwenye ubavu wa kukataa pesa na kutenda haki? Utakataa pesa wakati mtoto anataka kwenda shule, wakati mwenye nyumba anakufukuza kwa kushindwa kulipa pango, wakati huna pesa ya kulipia matibabu? Mtu hujawahi kushika 100,000 mikononi mwako, zikutembelee hizo kwa sharti la kumpitisha mbunge na rais, kwa nini usiimbe CCM juu, Sumaye, apite?

CCM, ina pesa na vyombo vyote vya dola. Ikitaka kumpitisha Sumaye, hata ukienda Bagamoyo, ukeshe makanisani na misikitini ni kazi bure! Kama "mwenye CCM" anamtaka Sumaye, wajumbe wa mkutano mkuu watanunuliwa kwa pesa, au hata sasa hivi ninapoandika makala hii wamekwisha nunuliwa. Wanajiandalia kitanzi chao wanyewe!

Mbali na Sumaye, kuwa na pesa zake binafsi, za chama na za serikali wale anaotaka kuwalinda wana pesa za kutosha. Na kwa vile bado wanataka kuchuma ni lazima wafanye chini juu ili mtu wao asimame. Sumaye, analionyesha hili wazi katika mahojiano aliyofanya hivi karibuni na gazeti moja la hapa nchini:
" Tumefanya kazi kubwa pamoja na rais, kwa miaka tisa sasa, najiuliza, hivi akija mwingine asiyetaka kuyaendeleza haya mafanikio, si wawekezaji watakata tamaa? Siku hizi kuna mashindano makubwa katika masuala ya uchumi kila nchi inavutia wawekezaji, sasa kukiwa na kiongozi asiyetaka kuendeleza haya mazuri, wawekezaji wataondoka. Lakini wawekezaji wakitambua kuwa nafasi imeshikwa na kiongozi aliyekuwa karibu na aliyeongoza mabadiliko hayo, watakuwa na uhakika wa kuwekeza zaidi".

Hiyo ndiyo sera yake, kuhakikisha usalama wa wawekezaji. Kuangalia usalama wa IPTL, ambayo inaliingizia taifa hasara kubwa. Si kulinda usalama wa raia, bali usalama wa wawekezaji! Cheka kama una cheka, na lia kama moyo wako unakusukuma kulia, ukweli ndio huo, wawekezaji kwanza!

Sumaye, ana wasiwasi kwamba kama si yeye kuingia Ikulu, watakuja wengine wasiopenda "maendeleo" na kuvunjilia mbali yale mazuri yaliyofanywa na serikali ya awamu ya tatu. Ni mtu gani anaweza kuharibu mambo mazuri? Kichaa anaweza kufanya hivyo. Lakini kama wananchi wana akili timamu, watamkatalia mwenda wazimu huyo. Akija mtu akakataa kuendelea na mikataba mibovu, akakataa hasara ya IPTL, akafichua madhambi ya wale walioliingiza taifa katika hasara kubwa kwa kukubali matapeli wa IPTL, mtu huyo atakuwa hayapendi maendeleo?

Sumaye, anaamini kwamba:
" Mimi ni sehemu ya mafanikio yote ya kiuchumi na kijamii ambayo nchi yetu imeyapata. Akija mwingine, asipoyaendeleza haya, nchi itarudi nyuma, nchi itaporomoka."

Wakati Jese na wenzake wanamlaumu Sumaye, kwa mikataba mibovu ya uwekezaji, mikataba ya TTCL, IPTL na NBC, yeye anaamini bila kuiongoza Tanzania, nchi itaporomoka! Huo ni ujasiri wa pesa. Bila kiburi cha pesa, asingeweza kusema hayo. Anajua kwa pesa atawanunua watu wote. Pesa, itafunika madhambi yake yote.

Bahati mbaya hatuna tena mtu mwenye busara kama mwalimu wa kuweka mambo sawa. Pesa itatuchagulia rais, wabunge na madiwani. Haya tuliyataka kwenyewe. Tulikuwa na nafasi ya kuwapigia kura za kutokuwa na imani viongozi wote waliokuwa na kashfa mbali mbali. Tulikuwa na wakati mzuri wa kumkataa Sumaye, alipoponda milioni 500 za taifa kwa ziara binafsi na pale alipojikanyaga na Kibaigwa, mara shamba si langu, mara nina hisa na mara ni shamba la mke wangu. Dalili zilijionyesha tukachagua kuwa vipofu! Tulikaa kimya kwa woga ili kuenzi amani na utulivu. Ya nini kulalamika? Tumeyavulia, tuyaoge!

Sasa si wakati wa kulalamika. Tumechelewa kwa hilo. Kama unasema hatujachelewa, sema usikike, tenda tukuone! Simama na kusema hapana, kataa kununuliwa, kataa kuchaguliwa rais, tumia haki yako ya kura kumchagua rais kufuatana na sifa zake za "Utanzania", sifa tulizoachiwa na waasisi wa taifa letu. Huu si wa kati wa kuhoji ujasiri wa wale wanaotaka kuingia Ikulu, wakati wamezungukwa na kashifa za rushwa na kutumia vibaya peza za umma. Tuliyataka wenyewe. Tulizembea, sasa matokeo yake ndio hayo. Kilichobaki ni kujililia sisi na vizazi vyetu.

Sasa hivi ni wakati wa kuwapamba marais wetu watarajiwa. Ni wakati kumpamba Sumaye. Yeye ni mnyenyekevu. Walio karibu naye wanaungama wazi kwamba mheshimiwa ana unyenyekevu wa hali ya juu. Hii ni sifa muhimu sana kwa nchi inayotaka kutunza amani na utulivu bila kuzingatia mambo mengine kama uchumi na utawala bora. Watu waendelee kuongelea kwenye umasikini huku wakiimba wimbo unaochefua wa amani na utulivu ni nguzo za taifa letu.

Sumaye, ni mvumilivu. Amejaliwa kipaji na mwenyezi Mungu, kuwa mvumilivu. Amevumilia maadui zake, hata na wale waliokuwa wakimpaka matope. Yeye mwenyewe anasema:
"Wapo wanaoamua kuwachafua wengine ili kutimiza malengo yao ya kisiasa, huu si ustaarabu. Unapotumia mbinu hiyo, maana yake mwenzako anakuzidi nguvu, kwani kama hakuzidi, ni kwa nini umchafulie?...Mimi siwezi kumhujumu mtu na wala sitamchafua mtu".
Hawezi kulipiza kisasi. Amekuwa kwenye nafasi ya juu serikalini. Alikuwa kiranja wa mawaziri, hatujasikia akijilipiza kisasi. Katika nchi kama Tanzania, inayotanguliza amani na utulivu na mshikamano, huyu ndiye anayefaa. Atashughulika na amani na mshikamano na kuwaachia wawekezaji wasombe kila kitu. Apite Sumaye! CCM, juu!

Sumaye, ana uzoefu wa muda mrefu katika siasa. Taifa kama Tanzania, linalotanguliza amani, utulivu na mshikamano, linahitaji rais mwenye uzoefu wa muda mrefu katika siasa. Elimu si jambo muhimu, hata Iddi Amin, aliitawala Uganda na kuiacha historia nyuma yake, yeye Sumaye anasisitiza jambo hili katika mahojiano aliyofanya na gazeti mojawapo siku za hivi karibuni:
" Sidhani kama suala la elimu ndicho kigezo kilichopo. Ni watu wanaonisema. Hata katika chama chetu tunasema mgombea awe na elimu ya chuo kikuu au inayolingana nayo. Sasa kama ni suala la elimu, mimi ninayo inayolingana na hiyo, kinachotakiwa zaidi ni uzoefu wa uongozi.. nimekuwa kwenye siasa kwa muda mrefu, nadhani hayo ndiyo muhimu".

Kama tungekuwa na mfumo mzuri wa demokrasia, tungemuuliza Mheshimiwa Sumaye, miaka yote katika siasa imezaa nini. Haitoshi kukaa miaka mingi katika siasa. Jambo la muhimu ni umefanya nini katika siasa. Kuna watu wanakaa muda mfupi katika siasa, lakini kwa vile walikuwa na vision na kusimamamia maoni yao katika jamii, wanakumbukwa kwa miaka mingi, wanaandika historia isiyofutika. Kennedy, hakuitawala Amerika kwa miaka mingi, lakini hadi leo hii anakumbukwa. Kwa vile sisi tunaongozwa na pesa, basi Sumaye, anaweza kusema lolote, na kupata kura! Si kwa sifa zake, bali kwa pesa zake! Cheka kama unataka na lia ukijisikia kulia, ukweli ndio huo!

Sumaye ni mtiifu. Tumeambiwa amemtii kwa kiwango kikubwa rais Mkapa. Huyu ndiye rais tunayemtaka. Alivyo mtiifu, ndivyo atakavyotaka wengine wamtii. Viongozi wakimtii, wakifuata kila anachokisema " Ndiyo mzee", nchi itakuwa na amani na utulivu.


Sumaye, ni rafiki wa karibu wa rais Mkapa. Huyu atamtunza vizuri rais wetu mstaafu. Hatupendi mpendwa wetu apate yale yaliyompata Kaunda na Chiluba. Tungependa mzee wetu akapumzike vizuri kule Lushoto kwenye hewa safi bila kusumbuliwa na malalamiko ya walalahoi.

Sumaye, ni mcha Mungu Tunakutana naye kanisani. Amekuwa mwaminifu kuhudhuria sherehe zote za kidini. Ziwe za Wakristu au Waislamu. Imani yake ni imara. Hatujamsikia kuhama kanisa lake la KKKT na kujiunga na makanisa mengine. Hatujamsikia akihama dini yake ya Ukristu na kuingia Uislamu au kutembelea Bagamoyo!

Sumaye ni kijana, ukimlinganisha na "Babu". Kuna msemo ya kihaya: "Abafu, bakilana okunuka", Tafsiri ya harakaraka: Maiti huzidiana kwa harufu mbaya.
Ingawa kampeni za Sumaye na "Babu" ni za kutumia nguvu ya pesa, pesa za "Babu" zinanuka zaidi, kuna mashaka kama zinaweza kuleta amani na utulivu.

Sumaye ana sifa nyingi! Labda Jesse na wenzake wanafikiri ninaandika haya nikilia na machozi yakidondoka. Si kweli! Ninaandika nikicheka. Ninafanana na mtu anayejinyonga kwa kamba aliyoitengeneza yeye mwenyewe. Ni lazima mtu huyu afe akicheka. Hata shujaa Mkwawa, alikufa akicheka. Kicheko cha huzuni na kujilaumu, dalili za kuonyesha ushujaa wa kijinga na ubwege! Maisha ni kitu muhimu, ukishayapoteza ni mwisho. Hekima ni kuyalinda maisha na wala si kuyapoteza!

Huu si wakati wa kulia. Hata tukilia haitasaidia kitu. Ni wakati wa kucheka kicheko cha huzuni na kujilaumu. Ni wakati wa kujinyonga kwa kamba tuliyoitengeneza sisi wenyewe.

Huu ni wakati wa kufikiria jinsi ya kubadilisha mfumo wa siasa katika Taifa letu. Ni wakati wa kukaa chini na kuandika katiba mpya ya taifa letu, ili tuachane na katiba iliyojaa viraka. Ni wakati wa kubuni mbinu za kuendesha uchaguzi wa haki. Uchaguzi utakaowaingiza watu madarakani kwa kufuata sifa na uwezo wao na wala si kwa kutumia pesa.

Nina imani akina Jesse Kwayu, wameupata ujumbe wangu. Ujasiri wa Sumaye, ni pesa. Kama kuna mtu au kikundi cha watu chenye uwezo wa kumpokonya Sumaye, ujasiri wa pesa, kuipokonya CCM, ujasiri wa pesa na kuwapokonya wawekezaji ujasiri wa pesa, na kama kuna mtu au kikundi cha watu chenye uwezo wa kuipokonya CCM, uwezo wa kutumia vyombo vya dola wakati wa uchaguzi mkuu,tunaweza kujadiliana juu ya ni nani ataingia kwenye viatu vya rais Mkapa. Kinyume na hapo hakuna mjadala. Mwenye nguvu mpishe! Mnyonge ni mnyonge daima hadi pale anapofumbua macho na kusema hapana!
Na,
Padri Privatus Karugendo.

YU WAPI DESMOND TUTU WETU TANZANIA?

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA RAI 2005

YU WAPI 'DESMOND TUTU' WETU TANZANIA?


RAI toleo Na 587,Paulo Mapunda, aliandika makala yenyekichwa cha habari: Yu wapi Desmond Tutu wetu Tanzania.Makala hii ilifanana kwa karibu na makala ya PrinceBagenda, kwenye toleo hilo hilo yenye kichwa chahabari: Ushirikina wa ushindi wa kishindo. PauloMapunda, anahoji:" Najaribu kutumia rejea mbalimbali kuwashtua kutokausingizini viongozi wetu wa dini ili tuweze kuwapatakina Desmond Tutu wa Tanzania...... Yu wapi DesmondTutu wetu, mtu anayeweza kuzinduka toka usingiziniakafumbua macho kuangalia, kutazama na kusikilizasauti za watu walio nyikani watesekao kwanjaa, magonjwa yanayotibika na yasiyotibika uporaji wamamilioni ya walipa kodi, ujambazi, ukosefu wa ajira,akakemea juu ya ongezeko la ufa kati ya matajiri(watawala) na masikini (watawaliwa)" (RAI 587).Kwa Mtanzania aliye makini, kilio cha Paulo Mapunda,hakitofautiani na cha Prince Bagenda, pale anaposemahivi: "Kama mtu akitamka kwamba Chama Cha Mapinduzikimeshinda kwa haki katika chaguzi hizi, basi kwa ninitusiamini kwamba hayo ni matayarisho ya vurugu kubwazitakazojitokeza mwaka huu wa Uchaguzi Mkuu 2005? Nayote haya yanatokea wakati viongozi wetu wa diniwanabuni wakorofi na wenye kutaka kuleta vurugu kwenyeuchaguzi Mkuu, wakati tayari kuna chama kinajulikanana kimekwisha kuanzisha vurugu, lakini viongozi wetuwa dini wanakionea haya?" (RAI 587).Kabla ya kuwaangalia Paulo Mapunda na Prince Bagenda,kwa jicho moja, kuna machache ya kuweka sawa. Nikianzana Mapunda, badala ya kuhoji: Yu wapi Desmond Tutuwetu Tanzania, angelihoji: Yu wapi Askofu wetu waAnglikana Tanzania. Kwa haraka inaweza kuonekanahakuna tofauti. Desmond Tutu, ni Askofu, hivyo inatoshakusema yuko wapi Desmond Tutu, kila mtu akafahamu nijuu ya maaskofu wote! Labda wengine wangependaMapunda, anahoji hivi: Yu wapi Askofu wetu wa Tanzania?Au mbona maaskofu wetu hawajitokezi kukemea maovukatika taifa letu? Kwa mchambuzi makini kuna tofautikubwa. Kanisa la Anglikana, lina historia ya kutoaviongozi shupavu, jasiri na wanaojisimamia, viongoziwanaotanguliza taifa lao na kuyaweka mbele maslahi yaraia katika taifa husika. Maaskofu wasiotangulizamaslahi yao binafsi ambao wako tayari kutoa maisha yaokwa manufaa ya wengine. Askofu Desmond Tutu, ni kutokakatika kanisa la Anglikana. Aliyoyafanya na ambayoanayafanya Afrika ya Kusini, tuliyasikia na badotunayasikia. Askofu wa Uganda, aliyesimama na kupingautawala wa Iddi Amin, alikuwa ni wa kanisa laAnglikana. Wakati maaskofu wa makanisa menginewaliendelea kumkumbatia Iddi Amin, na kumtukuza iliayapendelee makanisa yao, Askofu wa Anglikana,alikataa kuendelea kukumbatia uovu, alisimama bilawoga na kumpinga Iddi Amin, alimwambia aache kuuawatu, atawale kwa kufuata katiba na sheria, alipotezamaisha yake mikononi mwa Iddi Amin, wakati akiteteahaki za raia wa nchi yake ya Uganda. Tumesikia jinsimaaskofu Waanglikana wa Amerika, walivyompatiaUaskofu, mchungaji Shoga. Hili ni tukio liliopigiwakelele na dunia nzima. Lakini, maaskofu waKianglikana, hawakuyumba kwa vile walikuwa wanaangaliaumuhimu wa Askofu Shoga, katika kutoa huduma kwa raiawa nchi yake. Ipo mifano mingi inayoonyesha msimamousio yumba wa viongozi wa kanisa la Anglikana. Kwaninisisi Tanzania, hatuna Askofu wa Anglikana, aliyeshupavu ka wenzake? Baadaye tutaona ni kwa niniviongozi hawa wa kanisa la Anglikana wanakuwa namsimamo imara.Kwa upande wa Prince Bagenda, jambo la kuweka sawakabla ya kuendelea na mjadala ni pale anaposema:" Nakumbuka maneno ya Mhashamu Kilaini aliyotoa baadaya mauaji ya waandamanaji Pemba, Januari 27 2001.Askofu Kilaini alisema kwamba polisi wasiwaue raialakini vilevile raia wasiwachokoze polisi. Hivyokatika mantiki ya Askofu Kilaini, suala la polisikuwaua raia waliokuwa wakiandamana linalinganishwa namatatizo ya raia kuwachokoza polisi. Na pale raiawanapowachokoza polisi adhabu yao yaweza kuwa kifokutokana na mashambulizi ya polisi....).Sina hakika Prince Bagenda, anamfahamu Askofu Kilaini,kwa kiasi gani. Kama ni kweli aliyatamka hayoyaliyonukuliwa na Bagenda, basi hayakuwa maoni yaAskofu Kilaini, bali kivuli chake. Askofu Kilaini nimsomi wa hali ya juu, ni mtu anayeheshimu haki zabinadamu, utawala wa katiba na sheria, ni mtu mwema namzalendo. Wale wanaomfahamu kwa karibu wanajua jinsianavyokuwa akipigana na nafsi yake wakati akiendeshamajadiliano ya mambo mbalimbali katika luninga. Aminiusiamini anayeonekana kwenye luninga, anakuwa siAskofu Kilaini, bali kivuli chake. Mfano paleanapolinganisha ugonjwa wa UKIMWI, na ugonjwa wakisukari. Kwamba kama mgonjwa wa kisukari anakatazwakutumia sukari, basi na mgonjwa wa UKIMWI, akatazwetendo la ngono. Huyo si Askofu Kilaini, bali kivulicha Askofu Kilaini. Askofu Kilaini, ni kati yamaaskofu wachache wanaofahamu kwamba kazi ya Serikalisi kuwaua raia wake ambao wakati huohuo ni waumini wadini na madhehebu mbalimbali, anajua jinsi ilivyomuhimu kwa viongozi wa dini kulinda na kutetea uhai.Yeye Askofu Kilaini, kama Kilaini, hawezi kutoamatamshi yanayopingana na uhai. Ni mtu makini, mtu wawatu na mtu wa Mungu! Kivuli chake kinawezakuteteleka, lakini si Kilaini! Hoja hapa ni kutakakumfahamisha Bagenda, kwamba hatuwezi kupambana navivuli! Mapambano ni lazima yaelekezwe kwa kituchenyewe kinachozalisha kivuli! Ni kitu gani hicho?Tutakigusia wakati tukiwajadili na kuwaangalia Bagendana Mapunda, kwa jicho moja.Bagenda na Mapunda, wanapiga vita ukimya wa viongoziwetu wa dini hapa Tanzania. Mapunda anasema: "Viongozi wetu wa vikundi vya kijamii na hasa hasadini mara zote wamekuwa kimya dhidi ya maamuzi mabaya,yasiyo na visheni yafanywayo na Serikali hii ya awamuya tatu...". Kwa maneno mengine lakini kwa kutaka kuelezea kitukilekile Bagenda, anasema: "Kuna unafiki mkubwa unafanywa na wakuu wa dini namadhehebu ambao wana nafasi ya kujua lakini wanatumiahisia na mazoea. wanaona fahari kuwa upande wa wenyemadaraka na kuwaombea, bila kutaka kujua waumini waowako katika hali gani?".Unaweza kuuitaunafiki, ukimya, woga, ufahari, kujipendekeza, utumwa, ulemavuwa fikra nk. lakini hali hii ya viongozi wa dini zetuinaelezeka. Dini kubwa tulizonazo hapa Tanzania,Uislamu na Ukristu ni dini za kigeni. Zililetwa nakupandikizwa. Kwa bahati mbaya mizizi yake haikushikavizuri! Zilibaki kuwa dini za kigeni hadi leohii Zinatawaliwa na kupokea maelekezo kutoka nje.Zinaendeshwa kwa misaada na pesa za kutokanje. Viongozi kama maaskofu wanateuliwa kutoka nje nasi kwa kuzingatia matakwa na mahitaji ya nchi husika,bali kwa kuzingatia maslahi ya dini husika yenye makaomakuu nje ya nchi Uzalendo wa mtu na mapenzi yake kwawatu wake na nchi yake si kitu kinachotiliwa maanani.Kwa kutaka au kutotaka viongozi hawa wanakuwavibaraka. Hali hii inawafanya kuonekana kama vivuli.Wanasema na kusimamia yale wanayotumwa. Ukiliwekakanisa la Kianglikana pembeni, Ukristu na Uislamuzimebaki ni dini za kigeni. Anglikana, walifanikiwakujizingarisha. Ndio maana tunasikia the church ofUganda,The province of Tanganyika, The Church ofKenya, the church of England, nk. Kanisa la Anglikana,linakuwa na uhuru wa kuamua mambo yake katika nchi.Viongozi wake wanachaguliwa kulingana na mazingira yanchi. Hii inatoa mwanya kwa watu wenye uzalendo nauchungu wa nchi kujipenyeza na kufikia madarakamakubwa katika kanisa hilo na kuweza kuitumia nafasihiyo kutetea maslahi ya raia. Kwa njia hii alipatikanaAskofu Mkuu Desmond Tutu na yule Askofu wa Uganda,aliyepoteza maisha yake mikononi mwa Iddi Amin. Ndeomaana inashangaza Tanzania, kushindwa kumpata DesmondTutu, wetu, Askofu shupavu wa kanisa la Anglikana laTanzania.Ili hoja yangu ilieleweke vizuri, nitoe mfano wakanisa katoliki ambalo ninalifahamu vizuri. Kwa Askofuwa kanisa katoliki, kanisa ni kubwa kuliko Tanzania.Analiangalia kanisa lote kabla ya kuiangaliaTanzania. Hawezi kujiingiza kwenye kitu chochote chenyekuleta matata bila kusikiliza kwanza viongozi wakekule ROMA, wanasema nini. Mfano mzuri ni nchi za LatinAmerika, ambazo karibu wakazi wake wote ni Wakatoliki.Nchi hizi zimekuwa zikitawaliwa kwa mabavu, uchumiwote wa nchi uko mikononi mwa watawala, ardhi nzuriiko mikononi mwa watawala na washirika wao, wakatiraia wanaongelea kwenye umasikini unaonuka! Kanisalimekuwa upande wa hawa watawala wa mabavu, maanaMaaskofu wanachaguliwa kutoka ROMA, Vatican, imekuwana uhusiano wa karibu na wakati mwingine kuwa na hisa katikamakampuni makubwa ambayo mara nyingi yanaunga mkonoutawala wa mabavu katika nchi za dunia ya tatuinayozijumuisha nchi za Latin Amerika. Mapadre namaaskofu, walioamua kuwa upande wa wanyonge,walitengwa na kanisa na kupachikwa jina la waasi.Baadhi yao wamejiunga na makundi ya wapiganaji wamsituni.Askofu wa Kanisa Katoliki, anaweza akahamishwa kutokaTanzania na kwenda kufanya kazi nchini Ghana, India auRoma, na kufa na kuzikwa huko. Kanisa, ni kubwa kulikonchi zao. Uzalendo wao ni wa kanisa zima! Maaskofuwetu hawajui adha ya umasikini, wana majumba mazuri,wana magari mazuri, wanakula chakula cha kila aina,wakiugua wanapelekwa Ulaya. Hawaguswi na adha yarushwa. Kwa vile kanisa ni kubwa kuliko nchi kama vileTanzania, matatizo ya nchi moja yanafunikwa na neemakutoka nchi nyingine na mara nyingi kutoka nchi zadunia ya kwanza. Mazingira wanamoishi ni vigumukuamsha moyo wa uzalendo kiasi cha kusimama nakutetea haki za raia. Mazingira wanamoishi hayawezikuwaruhusu kuangalia, kutazama na kusikiliza sauti zawatu walio nyikani watesekao kwa njaa magonjwayanayotibika na yasiyotibika, uporaji wa mamilioni yawalipa kodi, ujambazi ukosefu wa ajira, na kukemea juuya ongezeko la ufa kati ya matajiri na masikini kamaambavyo Mapunda, anapendekeza. Ndio maana viongozi wetuwa dini wanafanya yale anayoyalalamikia Bagenda: "Mara nyingi tumeona viongozi wakuu waliomo ndani yaSerikali na chama tawala, wengine ambao wanadaiwa kuwawala rushwa, ndio wanaoongoza harambee za kuchangishamamilioni kwa ajili ya shughuli za kanisani namisikiti". Haya yanatokea kwa sababu viongozi wa dini hawaguswina maisha ya hapa Tanzania. Wanaishi kwenye mfumomkubwa zaidi ya Tanzania. wanaishi kwenye mfumounaoweza kuwaruhusu kupata kitu chochote au hudumayoyote kutoka nje.Ni vigumu kumtegemea mtu asiyeishi maisha ya watuasimame na kuwatetea! Viongozi wetu wa dini ni wagenikatika nchi yao. Hawana uchungu, kwa vile hawaguswi nakitu! Wanaweza kuvumilia serikali zote ilimradiwaruhusiwe kufanya mambo yao bila kuingiliwa.Waruhusiwe kuingiza magari bila kutozwa ushuru,wafanye biashara bila kulipa kodi, wamiliki ardhi kubwana wakati mwingine wawe juu ya sheria!Nimetoa mfano wa kanisa katoliki. Lakini hataukiangalia yale yanayoendelea kule KKKT utasemayanafanywa na watu wenye uchungu na nchi? Ni naniasiyeona kwamba maaskofu wa KKKT, wanatangulizamaslahi binafsi? Wanavunja amani na kuivuruga imani yawatu wanaowaongoza. Wanataka kila Tarafa iwe naDiosisi, kila kabila liwe na Diosisi yake. Wanatakakuigawa Tanzania, katika kanda. Mambo yakienda vibayatukianza kuchinjana wengi wao watakimbilia Amerika naGermany. Utapeli ulioufanya na Askofu Mgwamba, wa KKKTDar, angelikuwa mtu wa kawaida angekuwa anasota kuleKeko. Sasa yeye Bwana Askofu anapeta kule Marekani!Kama tunataka dini zetu zisaidie kuchangia katikamaendeleo na ustawi wa taifa letu ni lazima tufanyejitihada za kuzilazimisha kujizingarisha. Tuwe naviongozi wetu wa dini wanaoweza kufanya maamuzi kwakujitegemea bila kusikiliza maamuzi kutoka nje ya nchi.Tuwe na viongozi wanaoishi na kuguswa na maisha yawatu wa kawaida, wanaoguswa na maendeleo ya Taifa lao.Bila hivyo ni ndoto kumpata Desmond Tutu wetu waTanzania na ni upuuzi kutegemea mchango wa maanakutoka kwa viongozi wetu wa dini katika siasa za Taifaletu.Dini zetu kubwa Uislamu na Ukristu, zikiendelea kuwani dini za kigeni, tutaendelea kushuhudia vivuli. Kamanilivyodokeza hapo juu, ni vigumu kupambana na vivulina ni makosa kuvilaumu vivuli, maana kivuli si kituhalisi! Ingawa pia kivuli si kitu cha kupuuzia, kwavile kinatoa picha ya kitu halisi, kwa vile kinawezakuchangia kuwadumaza watu na kuwaletea ulemavu wafikra, kuna ulazima wa kufuatilia chanzo chake. Nilazima kupambana na kitu halisi kinachozalisha kivuli!Tukifika hatua hii tutakuwa tumepiga hatua ya kuelekeamwanzo mpya!

Na,

Padri Privatus Karugendo.

KUJICHUKULIA SHERIA MKONONI

MAKALA HII ILITOKA KWENYE GAZETI LA RAI -2004

KWANINI WATANZANIA WAMEAMUA KUJICHUKULIA SHERIA MIKONONI?

Zamani, wengine watahoji zamani ya lini? Sina maana zamani ya mwaka 2000, kwa wengine ni zamani!, Sina maana zamani ya miaka ya tisini au thamanini katikati, ninamaanisha zamani ya miaka ya 50,60,70 na 80 mwanzoni, kulikuwepo na wahalifu wa aina mbali mbali: majambazi, wezi, vibaka, wahaini nk. Walikamatwa, walifikishwa polisi, polisi walifanya kazi yao kwa uaminifu na uzalendo na wahalifu walifikishwa mahakamani na sheria ilichukua mkondo wake kwa msingi wa haki. Wahalifu walipatiwa haki yao ya kikatiba ya kusikilizwa na kujitetea. Mwamwindi, alinyongwa baada ya kesi yake kusikilizwa kwa muda wa kutosha na baada ya jitihada za serikali za kuhakikisha kama Mwamwindi, alikuwa na akili timamu wakati wa kitendo cha mauaji aliyoyafanya ya aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Iringa. Baada ya mauaji hayo ya kwanza na ya aina yake hapa Tanzania, ya kiongozi wa ngazi ya juu katika serikali, Mwamwindi, alijisalimisha mwenyewe na kuubeba kwenye gari mwili wa marehemu hadi kwenye kituo cha polisi. Polisi, hawakujichukulia sheria mkononi, kwa kumpiga risasi Mwamwindi, hapohapo. Alikuwa amefanya kosa kubwa la mauaji ya kiongozi wa serikali. Aliwekwa ndani na kesi yake iliendelea na kutangazwa kwenye vyombo vya habari. Hakukuwepo na siri hadi kila mtu aliamini kwamba haki ilitendeka!

Wale waliotaka kuipindua serikali ya Kambarage, na njama zao kugundulika dakika za mwisho, kesi yao iliendelea kwa miaka mingi na kutaganzwa kwenye vyombo vya habari. Karibu wahaini wote waliachiwa huru.

Zamani hizo wahalifu waliopatikana na makosa, walipatiwa adhabu ya vifungo. Baadhi yao kifungo ilikuwa ni nafasi ya ukarabati, elimu na toba. Wengi walijifunza mambo mbali mbali kama ufundi, kilimo, ufugaji na lugha mbali mbali. Baada ya kifungo majambazi, wezi na vibaka waligeuka na kuwa raia wema na kuendelea kutoka mchango wao katika kulijenga taifa letu la Tanzania.

Ipo mifano mingi inayoonyesha kwamba zamani kila raia alikuwa na haki sawa mbele ya sheria kama inavyosema katiba ya jamhuri ya muungano wa Tanzania:
Ibara 13(1) “Watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria.
13(3) “ Haki za raia, wajibu na maslahi ya kila mtu na jumuiya ya watu yatalindwa na kuamriwa na mahakama na vyombo vinginevyo vya mamlaka ya nchi vilivyowekwa na sheria au kwa mujibu wa sheria.”
13(6) “Kwa madhumuni ya kuhakikisha usawa mbele ya sheria, mamlaka ya nchi itaweka taratibu zinazofaa au zinazozingatia misingi kwamba :-
(6) a) “ Wakati haki na wajibu wa mtu yeyote vinahitaji kufanyiwa uamuzi wa mahakama au chombo kinginecho kinachohusika, basi mtu huyo atakuwa na haki ya kupewa fursa ya kusikilizwa kwa ukamilifu, na pia haki ya kukata rufani au kupata nafuu nyingine ya kisheria kutokana na maamuzi ya mahakama au chombo kinginecho kinachohusika;
(6) d) “ Kwa ajili ya kuhifadhi haki ya usawa wa binadamu, heshima ya mtu itatunzwa katika shughuli zote zinazohusu upelelezi na uendeshaji wa mambo ya jinai na katika shughuli nyinginezo ambazo mtu anakuwa chini ya ulinzi bila uhuru, au katika kuhakikisha utekelezaji wa adhabu;
(6) e) “ Ni marufuku kwa mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu zinazomtweza au kumdhalilisha.”

Leo hii majambazi, wezi na vibaka wanahukumiwa kifo bila kufikishwa polisi au mahakamani. Wananchi wenye hasira wanajichukulia sheria mkononi. Mtu asiyekupenda, mwenye chuki binafsi nawe, akikunyoshea kidole na kusema wewe ni mwizi, katikati ya jiji la Dar-es-Salaam, Mwanza au miji mingineyo ya hapa nchini, atakuwa anakutakia kifo; utavikwa tairi shingoni, utamwagiwa petroli na kuchomwa moto! Matukio kama haya ni mengi kiasi cha mtu kuwa na maswali mengi juu ya umuhimu wa kuwa na katiba. Watu, ambao wengi wao ni vijana wa kulijenga taifa hili wanapoteza maisha yao kwa kukwapua saa, mikufu ya dhahabu, pesa, simu nk.

Hakuna mtu anayeunga mkono matendo ya ujambazi, vibaka na wezi. Haya ni matendo yanayovunja amani na utulivu katika jamii. Jambo muhimu la kujiuliza ni je, jambazi, kibaka au mwizi hana haki ya kujieleza mbele ya sheria kama inavyotajwa kwenye katiba ya nchi yetu? Je, jamii yetu haina la kujifunza kutokana na matendo haya? Je, jamii haina la kuwafundisha na kuwakarabati majambazi, vibaka na wezi? Je, jambo la msingi ni kuwaua watu hawa au ni kutafuta chanzo cha matendo yao kiovu na kutafuta mbinu za kuyaponya? Vibaka na majambazi wana mangapi ya kuilaumu na kuishutumu jamii yetu? Wana kero ngapi ndani ya roho zao? Ni mangapi yamewazunguka na kuwalazimisha kutenda yale ambayo wasingependa kuyatenda? Je, wanaiba ili kuwapeleka watoto shule? Wanaiba ili kupata pesa za kulipia matibabu? Wanaiba ili kupata pesa za kununua viwanja na kujenga nyumba za kuishi? wanaiba ili wanunue nguo, chakula na kuishi maisha bora? Je, wanaiba ili watoe sadaka na zaka kwenye dini zao - maana pesa zafanana, ziwe za wizi au zile zilizopatikana kwa njia za halali – viongozi wa dini wanapokea tu bila kuhoji – kwao la msingi ni pesa! Wanaiba kwa vile hawana kazi? Au wanaiba kwa vile karibu watanzania wote ni wezi – kama si majambazi wa kuvamia, basi wanaiba na kupora mali ya taifa! Je, bila ya kuwapatia majambazi, vibaka na wezi nafasi ya kuwasikiliza tunawezaje kugundua chanzo? Mbona kadri majambazi, vibaka na wezi wanavyouawa na wananchi wenye hasira ndivyo ujambazi na matendo mengine ya uovu yanavyoongezeka kwa kasi ya kutisha? Je, si kweli kwamba majambazi, vibaka na wezi wanakuwa na watu wengi nyuma yao? Je, si ukweli kwamba matendo haya ya uovu yanaongozwa na vigogo? Vigogo hawa, si wanaendelea kuishi na kuyafurahia maisha wakati watu wanyonge wanakamatwa na kuchomwa moto?

Je, kama uchumi wa nchi unakuwa mikononi mwa watu wachache, tunawezaje kuthibiti ujambazi? Wananchi wanasema majambazi, vibaka na wezi ni kero kubwa katika jamii ya leo. Tofauti na zamani ambapo vibaka na majambazi walikuwa wanashughulikiwa na sheria, siku hizi wakikamatwa baada ya siku mbili au tatu wanakuwa tena mitaani wakienelea na vitendo vyao viovu. Rushwa na hongo inatumika kuwaachia. Hivyo wananchi wanaona njia pekee ya kumaliza kero hii ni kifo. Serikali yetu inayaona haya yakitendeka, badala ya kuyakemea na kuielimisha jamii juu ya kuifuata katiba, utawala wa kisheria, elimu ya uraia na kuheshimu haki za binadamu, inashikwa na kigugumizi. Viongozi wetu kama vile waheshimiwa wabunge wanaogopa kuwakemea wananchi wanaojichukulia sheria mkononi ili wasinyimwe kura. Wanatanguliza maslahi binafsi, bila kutanguliza maslahi na heshima ya taifa letu.

Jambo tunalolisahau wote ni kwamba Tanzania, kuna kero nyingi. Je, kila kero wananchi wakiamua kujichukulia sheria mkononi mwao, ni nani atakuwa salama? Waheshimiwa Wabunge hawatakuwa salama, viongozi wa serikali hawatakuwa salama, viongozi wa kidini hawatakuwa salama, matajiri hawatakuwa salama na sisi sote hatutakuwa salama! Mifano ni mingi. Rwanda, Maaskofu walichinjwa, mapadre, masista, viongozi wa dini mbalimbali, viongozi wa serikali, matajiri na kila mnyarwanda hawakupona. Ni hatari wananchi wakiamua kujichukulia sheria mkononi. Ni bora kuthibiti mapema hali hii inapojitokeza katika jamii.

Msemo wa Waswahili wa: “ Usipoziba ufa utajenga ukuta” utufikirishe. Ilianza kero ya vibaka. Wananchi walichoka na kuamua kujichulia sheria mkononi. Sasa hivi imekuwa ni desturi ambayo ni kazi ngumu kuizuia! Akikamatwa kibaka anavikwa tairi shingoni, anamwagiwa petroli na kuchomwa moto! Ikafuata kero ya majambazi. Wananchi walichoka na kuamua kujichukulia sheria mkononi. Ukisikiliza taarifa ya habari, utasikia jinsi wananchi wanavyowazingira majambazi na kuwaua. Baada ya hapo utasikia pongezi za polisi! Leo hii ni kero ya wavuvi wanaovua kwa kutumia sumu. Mikoa ya Kagera, Mara na Mwanza, inashuhudia mauaji ya kimyakimya ya wavuvi wanaovua kwa kutumia sumu. Iwe ni kusingiziwa au ni kweli unavua kwa sumu, hukumu ni kifo! Inatisha!

Ni tendo baya, la kiovu na la hatari kuvua kwa kutumia sumu. Ni hatari kwa viumbe vya majini, ni hatari kwa maisha ya watu wanaokula samaki na kuyatumia maji ya ziwa Victoria na pia ni hatari kwa soko la nje la samaki. Hakuna ubishi juu ya haya. Swali la kujiuliza ni je mauaji haya yamekomesha kabisa uvuvi haramu wa kuvua kwa kutumia sumu? Mbona kuna habari kwamba sato karibu wote wanaosambazwa nchi nzima ni sumu tupu? Je, watu hawa wanapouawa bila yakufikishwa mbele ya sheria ukweli kwamba miradi hii ya uvuvi wa kutumia sumu inaendeshwa na vigogo ambao wengine ni viongozi wa ngazi ya juu serikalini utajulikana vipi? Ukweli huu wanao hawa vibarua na wanyonge wanaouawa kinyama na kimyakimya. Mauaji haya yanatisha na kutoa picha kwamba sasa hivi Tanzania, haifuati utawala wa kisheria na kuziheshimu haki za binadamu. Ingawa mauaji haya yanatokea kwenye mikoa yote inayolizunguka ziwa Victoria, inashangaza zaidi na kusikitisha mauaji haya yakitokea kwenye jimbo la uchaguzi la Waziri wa Ulinzi, Mheshimiwa Mzee Dr.Sarungi. Nchi zilizoendelea, hili lisingekuwa jambo la kujadiliwa. Waziri, angejiuzulu haraka. Mauaji ya kinyama, ya kimyakimya, yasiyofuata sheria na kuheshimu haki za binadamu, kutokea kwenye jimbo la uchaguzi la Waziri wa Ulinzi ni aibu na kashifa kubwa. Hii ni sababu tosha ya kulifanya jambo hili kuagaliwa kwa makini.

Katika kijiji cha Kyomwami, kata ya Komuge, tarafa ya Suba, wilaya ya Tarime, mauaji ya wavuvi wanaovua kwa kutumia sumu yanaendelea kimyakimya. Hakuna anayeguswa na mauaji haya, isipokuwa jamaa wa karibu sana na marehemu. Miezi kama miwili iliyopita Bwana Paul Tunduye George, wa kijiji cha Kyomwami, aliuawa kwa kushutumiwa kuvua kwa kutumia sumu. Hakuna aliyekamatwa kufuatana na kifo cha Bwana Paul, hadi pale kaka yake Bwana Damiana George, alipowasili kutoka Holland, anakoishi na kufanya kazi mwanzoni mwa mwezi huu. Bahati nzuri alipata ushirikiano mzuri wa polisi makao makuu Dar-es-Salaam na Mara. Baadhi ya watu walikamatwa na kuhojiwa katika kijiji cha Kyomwami. Juhudi za Damian George, za kutaka waliofanya mauaji ya mdogo wake wakamatwe na kufikishwa mbele ya sheria hazikupokelewa vizuri na wanakijiji wa Kyomwami na vijiji vya jirani kama Kinesi,Komuge na tarafa yote ya Suba hadi makao makuu ya wilaya ya Tarime.

Nilipotembelea kijiji cha Kyomwami, tarehe 8.11.2004, nilikuta malalamiko kijijini kwamba Damian George, alikuwa analeta usumbufu kijijini. Hata jamaa zake wa karibu hawakutaka aendelee kufuatilia swala la kifo cha mdogo wake. Mipango ilikuwa ikifanyika ili Damian George, akamatwe na kuwekwa ndani kwa usumbufu aliousababisha wa kuwaleta mapolisi kijijini na kuwasumbua watu. Wakati Damian George, aliamini ni haki yake kikatiba kutetea haki ya watu waonyonge wanaopoteza maisha yao kimyakimya, wananchi walimnyoshea kidole na kumtuhumu kuwa yeye ni adui wa umma!

Wananchi hawataki mtu anayevua kwa kutumia sumu kufikishwa mbele ya sheria. Wanasema mbele ya sheria hakuna haki! Kwamba mbele ya sheria mwenye pesa ndio anapatiwa haki yake. Inaaminika wavuvi wana pesa! Ukiwapeleka mbele ya sheria huwezi kuwashinda! Dawa ni kuwaua kimyakimya. Siku nilipokitembelea kijiji cha Kyomwami, mvuvi mwingine alikuwa ameuawa na hakuna aliyekuwa anajishughulisha kujua chanzo cha kifo chake. Maiti ilikuwa haijazikwa baada ya siku mbili, walikuwa wakisubiri polisi kutoka Tarime! Hakuna aliyeonyesha kusikitika maana walijua kwamba ni hao hao wavuvi wanaovua kwa kutumia sumu na hukumu yao ni kifo tu!

Hakuna ubishi kwamba uvuvi wa sumu ni wa hatari na ni kero kubwa. Swali ni je, kila kero wananchi wakiamua kujichukulia sheria mikononi mwao tutafika wapi? Je, hawa wavuvi wakipewa nafasi ya kujitetea mbele ya sheria si wanaweza kufichua madhambi makubwa yanayozunguka biashara ya uvuvi wa samaki: uonevu wa matajiri, wizi wa mitumbwi, wizi wa nyavu, matambiko(ya binadamu),dhuluma ya viwanda vya samaki, ukwepaji ushuru, wamiliki waviwanda wanaodai ni watanzania kumbe ni hewa tupu hadi kufikia mzunguko unaomgusa kila mtu katika jamii awe ni kiongozi wa serikali, kiongozi wa jadi, kiongozi wa dini nk.! Mwisho wa mwisho kila mtu anaweza kujikuta anahusika!

Na je, kero nyingine ambazo hazijulikani vizuri kwa wananchi, siku zikijulikana itakuwaje? Mfano mmoja. Kata ya Komuge, ina soko kubwa la Nyamaguku. Ni soko linalofanyika kila siku ya Jumanne. Nilikwenda kwenye soko hilo kununua mbuzi, nikakutana na mambo ya kustaajabisha. Mtu anayeuza mbuzi analipa ushuru wa soko na mtu anayenunua mbuzi analipa ushuru wa soko! Ni hivyo hivyo kwa Ng’ombe, kuku na wanyama wengine. Soko lenyewe halina choo, vibanda vilivyojengewa na huduma nyingine za kuhalalisha malipo ya ushuru wa soko. Nilipotaka kujua ushuru huo ulikuwa ni wa kitu gani. Niliambiwa ushuru huo ni kati ya vyanzo vya mapato ya halmashauri ya wilaya ya Tarime! Tunatangaziwa kwamba ushuru mdogo uliokuwa kero kwa wananchi umeondolewa, Wilaya ya Tarime Mbuzi, Ng’ombe, Kuku na wanyama wengine wanatozwa ushuru mara mbili – kwa maana ya anayeuza na anayenunua! Je, siku wananchi wa Komuge, wakifunuliwa juu ya kero hii wajichukulie sheria mkononi na kufanya kama yale wanayowafanyia wavuvi wanaovua kwa kutumia sumu?

Ni imani yangu na imani ya watu waliostaarabika kwamba hakuna mtu anayetamani kuwa jambazi, kibaka au kutenda maovu katika jamii kama vile kuvua kwa kutumia sumu na kuwatoza watu ushuru usioruhusiwa. Kuna mambo mengi yanayochangia hali hii: Siasa mbovu, uchumi mbovu, maadili mabaya, dini za kitapeli, uchoyo wa viongozi wa serikali, dini na jadi, ufa mkubwa kati ya walionacho na wasiokuwanacho.

Ni bora kukaa chini tukatafuta chanzo cha matatizo katika jamii yetu na kutafuta njia za kuyaondoa kuliko kuwaachia wananchi kujichukulia sheria mkononi. Tunaendelea kuwapoteza vijana wenye nguvu ambao kama wangekarabatiwa, kurekebishwa, kuelimishwa, kuelekezwa na kuwezeshwa wangebadilika na kuwa raia wema wa kulijenga taifa letu. Tujifunze kuifuata na kuiheshimu katiba ya nchi yetu. Anayekiuka katiba awajibishwe. Hivyo ndivyo wanavyoishi watu waliostaarabika na kuishi kwa kuziheshimu haki za binadamu.

Na,
Padri Privatus Karugendo.