MAAMUZI MAGUMU NI PAMOJA NA KUDHIBITI UPORAJI WA ARDHI.

Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba sasa ardhi inaporwa kwa kisingizio cha uwekezaji. Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba uporaji huu wa ardhi ni ufisadi na wala si kitu kingine kile. Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba viongozi wetu ni miongoni mwa waporaji wakubwa wa ardhi. Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba uporaji wa ardhi ni ukoloni mpya. Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba uporaji wa ardhi utapelekea vijana kutopata ajira. Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba uporaji huu unaongozwa na mfumo dume. Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba watanzania sasa wameamua kujichulia sheria mkononi ili kuilinda ardhi yao. Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba uporaji wa ardhi umeshika kasi katika serikali ya awamu ya nne….

Baada ya kukaa kimya kwa muda mrefu, mheshimiwa Edward Lowassa, ameibukia Bungeni akiwalaumu viongozi kushindwa kuchukua maamuzi magumu katika maswala  ya kitaifa; hata mtoto mdogo aliweza kutambua kwamba Mheshimiwa Lowassa alikuwa akituma ujumbe wa moja kwa moja kwa ndugu yake Rais Jakaya Kikwete; bila shaka alimaanisha na maamuzi magumu ya kumfukuza yeye na wenzake kutoka kwenye chama cha  CCM na kufikishwa mbele ya sheria kujibu tuhuma zote zinazoelekezwa juu yake. Hotuba yake ilikuwa kwenye mfumo wa ushairi kitu kilichoonyesha kwamba Mheshimiwa Lowassa ni msanii na mwanasiasa wa kweli. Lakini pia kushangiliwa kwa kila neno alilolisema, ni dalili kwamba bado ana ushawishi mkubwa ndani ya Bunge, ndani ya chama chake cha CCM na kwenye jamii ya Tanzania? Ilikuwa ni kumshangilia kwa kumpongeza au kumtaka asiendelee kusema? Ina maana bado anakubalika kugombea kiti cha urais na kwenda kinyume na wasia wa Baba wa taifa? Swali hili ni la kujibiwa na kila Mtanzania mwenye uchungu na taifa letu.

Kwa mtindo wa Watanzania wanajua na dunia nzima inajua, Mheshimiwa Lowassa, alijitahidi kuyaorodhesha yale yote  yaliyotendwa na serikali wakati akiwa madarakani (Kama waziri Mkuu); kama vile ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma na uamuzi mgumu wa kuyasafirisha maji kutoka Ziwa Victoria hadi Shinyanga na labda baadaye hadi Dodoma. Kwa bahati mbaya au kwa makusudi alisahau kutaja kwamba ni lazima Serikali ifanye maamuzi magumu ya kudhibiti wimbi la uporaji wa ardhi; maana watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba Mheshimiwa Lowassa ni kati ya wanaotajwa kuongoza wimbi hili la uporaji wa ardhi.

Pamoja na usanii wake, hoja ya Mheshimiwa Lowassa ni nzito. Tanzania tunahitaji viongozi wa kuchukua maamuzi magumu; kulinda uhuru wetu, kulinda maliasili na hasa kulinda ardhi yetu; maamuzi magumu ya kuifanya Tanzania kuwa sehemu ya utandawazi na si kumezwa na utandawazi; kulinda lugha yetu, utamaduni wetu na umoja wetu. Kiongozi wa nchi ni lazima afanye maamuzi na wakati mwingine yasiyomfurahisha yeye na marafiki zake wa karibu lakini yana manufaa makubwa kwa taifa zima.

Swali la kujiuliza ni Je Mheshimiwa Lowassa, amechelewa kulitambua hili? Je yeye ni mtu wa kulieleza hili  Bungeni au ana nafasi ya karibu kulipenyeza kwa Rais wetu ambaye; Watanzania wanajua na dunia nzima inajua kwamba wao ni kitu kimoja? Au Mheshimiwa Lowassa, anataka kutudhihirishia kwamba yeye ni msanii wa kweli?

Sina maana ya kuubeza usanii au kukubaliana na wa wanaosema kwamba: “wasanii ni waundaji wa matatizo katika jamii”. Hoja yangu ni kwamba Mheshimiwa Lowassa ni msanii aliyeusomea usanii. Hivyo naongelea dhana nzima ya uigizaji.

Katika ufundishaji wa sanaa hasa za maonesho, nadharia mbali mbali hutumika. Konstantin Stanislavski (1863- 1938) ni mmoja wa wakongwe wa nadharia za uigizaji ambaye pia alikuwa mwanzilishi wa Moscow Art Theatre (1897) kundi la uigizaji linalofanya kazi hadi leo.  Yeye anaamini kabisa mbinu moja wapo ya kuigiza ni kufanya ‘emotional recal’ (kuvuta/kurudisha hisia) ambayo itapelekea mtu kuweza kuleta uhalisia.  Hapa tunakutana na wale mabingwa wa kutiririsha machozi. Baadhi yao huweza kuvuta hisia za mambo mabaya (sijui mazuri?) yaliyowaliza kama chanzo cha kumwaga uchozi kwenye jukwaa au kwenye filamu. Kutiririsha huku kwa machozi, ni zoezi la kisayansi linalotokana na mwitiko wa mwili. Mwitiko huu wa mwili ni katika kubana/kubanwa pumzi au kwa kutumia kemikali (kama zile za vitunguu) ili kufungua mirija ya machozi. Zote ni njia zinazotumika kutiririsha machozi. Huu ni mfano mmoja tu katika uigizaji. Kuna wengine wanaoona kuigiza ni ‘reality plus one’ yaani ukweli jumlisha moja. Na wengine wamekwenda mbali zaidi wakasema kuigiza ni zoezi la ‘protrayal of convincing emotions to be real while it is not’. Naam, naamini hili sasa ndio linalotumika zaidi. Na bila shaka ndo uigizaji wa Mheshimiwa Lowassa. Ni imani yangu kwamba wakati akiongea kuna wabunge waliotokwa na machozi na inawezekana na yeye machozi yalikuwa yakitoka!

Na sasa mimi naendelea kuchambua uigizaji kama kitendo cha kutoa ujumbe kwa kama ukweli ‘real’ wakati sio kweli yaani kuigiza kutoka kwenye mzizi wa neno ‘iga’. Nadharia hii ni ngumu sana kwani ni vigumu pia kujua ukweli unaanzia wapi na usio ukweli unaishia wapi. Maana hizi za kuigiza ndizo zinazosababisha watu kulinganisha usanii na uongo. Naomba kusisitiza, sanaa Si uongo labda unaweza kuwa uigizaji, ambacho ni kipengee kidogo sana katika sanaa.

Kwa mujibu wa kumbukumbu Mheshimiwa Edward Lowasa alipata shahada ya kwanza ya sanaa za maonesho (performing/theatre arts) katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hii ndio shahada ya ngoma, sindimba au ‘kukata viuno’ kama wengine walivyopenda kuikejeli. Baadaye shahada ya pili katika masomo ya Maendeleo (Development studies) toka chuo kikuu cha Bath nchini Uingereza. Mheshimiwa Lowassa ni kati ya wasanii wachache waliofundishwa na wahadhiri waandamizi ambao ni magwiji wa sanaa za maonesho nchini Tanzania na katika nyanja za kimataifa. Lowassa akiwa mwanafunzi aliigiza katika tamthiliya mbalimbali zilizochapishwa katika vitabu.

Ukitaka kufahamu kuwa Mhe. Lowassa ana shahada ya uigizaji, soma kwa makini utetezi wake alioutoa Bungeni wakati wa sakata la Richmond. Alisema, “Mheshimiwa Spika, lakini nimetafakari kwa makini sana jambo hili nikajiuliza hivi kulikoni mpaka watu wazima wenye uwezo wao, watu maarufu wenye heshima zao, mpaka wafike mahali waache jambo la msingi kama hilo kulikoni? Mimi nadhani there is a wish which I am going to grant, ni Uwaziri Mkuu. Nadhani tatizo ni Uwaziri Mkuu. Kwamba ionekane Waziri Mkuu ndio amefanya haya, tumuondolee heshima au tumwajibishe“.

Swali langu ni kuwa alijuaje kuwa watu wanauonea gere uwaziri mkuu kama hakuwa na lake jambo? Kwa waliosoma kitabu cha Mfalme Oedipus, wanakumbuka pale Oedipus alipogundua karaha ya kuwa “amezalia pale alipozaliwa“ aliamua kujiadhibu kwa kujitoboa macho ili asione. Pia alilalama sana. Alisema maneno yanayofanana na haya, “Nimefadhaika sana, nimedhalilishwa sana, nimeonewa sana katika hili...Mheshimiwa Spika, nimetafakari kwa niaba ya chama changu, kwa niaba ya Serikali yangu nimeamua kumwandikia Rais barua ya kumwomba niachie ngazi. Nafanya hivyo kwa moyo mweupe kabisa ili kuonyesha dhana ya uwajibikaji lakini kutokubaliana na utaratibu uliotumika kusema uongo ndani ya Bunge wa kumsingizia mtu“.  Kama umesoma kwa makini alisema kuwa ameamua ’kuachia ngazi’ na mdomo wake haukuwa radhi kutamka kuwa amejiuzulu, kwani anaamini atendelea kuwa nyuma ya pazia akiangalia na zaidi kuongoza igizo hili na mengine yatakayofuata.

Mhe. Lowassa alilalama kwa kusema, “Mheshimiwa Spika, wewe ni Mwanasheria unafahamu suala la Natural Justice. Kwamba Kamati Teule imesikiliza watu wengine wote pamoja na wanaoita minong'ono ya mitaani, wamesafiri mpaka Marekani kutafuta mashahidi, lakini mimi ambaye ni mmoja kati ya watuhumiwa mle hawakunihoji hata siku moja. Mheshimiwa Spika, nimesimama kueleza masikitiko yangu. Ofisi ya Bunge mpaka ofisini kwangu hata kama wangeniita ningekwenda kwa miguu kama hamna gari na nilikuwa tayari kufanya hivyo“.

Alihitimisha uzoefu wake wa kuigiza alisema, “nimpongeze Dk. Harrison Mkwakyembe, Mwenyekiti wa kamati Teule kwa kuwasilisha kwa mbwembwe nyingi sana taarifa yake, mbwembwe zilikuwa nzuri kweli“. Ni nani ambaye angeambiwa kuwa Mhe. Lowassa alikuwa anawaigizia wa Tanzania angekataa?

Na sasa amerudi na uigizaji mpya wa Watanzania wote wanajua na dunia nzima inajua. Ni wazi tunampongeza kwa hatua yake ya kuachia ngazi; maana hii ni hatua kubwa katika mchakato mzima wa kuchukua maamuzi magumu. Lakini Mheshimiwa huyu ametuhumiwa kwa mambo mengine mengi. Mfano hili la uporaji wa ardhi; ametuhumiwa kupora ardhi kule Arusha na jijini Dar-es-Salaam. Tumelalamikia kubadilisha sura ya Jiji la Dar-es-Salaam kwa kujenga majengo marefu bila mpangilio wowote, kuvunja majumba ya kihistoria, ukiuuliza wanasema Lowassa yuko nyuma ya mpango huu wa kujenga majengo marefu. Tunakumbuka vizuri sakata zima la jengo refu la Umoja wa vijana.

Tunataka kujua hatua anazozichukua Mheshimiwa Lowassa, kukisaidia chama chake cha CCM kufanya maamuzi magumu. Anamsaidia vipi rafiki yake wa karibu Mheshimiwa  Rais Dk.Jakaya Kikwete, kudhibiti uporaji wa ardhi na mengine mengi kama vile biashara ya madawa ya kulevya.

Wakati nikiandika makala hii kuna mtu amenipiga simu akinijulisha kwamba Mkoa mpya wa Katavi, mwekezaji kutoka nje ametengewa ardhi yenye ukubwa wa wilaya nzima na kupewa hati miliki ya mikaka 99! Kule Kilombero kuna mgogoro wa ardhi kati ya serikali na wananchi, baada ya kijiji kumegwa na kumilikishwa na mwekezaji. Kuna matatizo na migogoro ya ardhi kila sehemu ya taifa letu.

Vijiji vingi vya Tanzania havijapimwa. Wananchi hawana hati miliki ya mashamba yao; wakati wowote wanaweza kutolewa kwenye mashamba yao ili kuwapisha wawekezaji. Ndo maana tunasema tunahitaji viongozi wenye uwezo wa kufanya maamuzi magumu ya kulinda ardhi yetu na uhuru wetu.

Hata kama Mheshimiwa Lowassa, anafanya mchezo wa kuigiza ndani ya Bunge, hoja yake ni ya msingi: Ni bora kulaumiwa kwa kufanya maamuzi kuliko kulaumiwa kwa kutokufanya maamuzi. Na wakati mwingine kuchelewa kufanya maamuzi kwa maswala ya msingi kama hili la uporaji wa ardhi ni chimbuko la migogoro na wakati mwingine umwagaji damu.

Na,
Padri Privatus Karugendo.





0 comments:

Post a Comment