ANGWANI WAKIHAMA NA SERIKALI IHAMIE DODOMA?

Wasomaji wangu nianze makala hii kwa kuwatakia Heri ya mwaka mpya. Tumshukuru Mungu kwa wema wake kutuvusha kuingia mwaka wa 2012. Ni kwa neema  na huruma yake na si kwa ubora wetu tumeendelea kuishi. Ninawashukuru wote pamoja na Mhariri wangu walionitumia matashi mema ya mwaka mpya kwa ujumbe mfupi wa simu ya kiganjani, niungame wazi kwamba sikushindwa  kujibu ujumbe kwa kila mmoja aliyenitumia bali naendeleza mgomo wangu niliouanza miaka miwili iliyopita wa kutotuma ujumbe mfupi wakati wa Christmas na mwaka mpya. Sababu yangu ya msingi ni kupinga utamaduni huu wa kuyatajirisha makampuni ya simu za viganjani wakati wa sikukuu. Ni wazi makampuni haya yanatunyonya kila siku, hivyo ni bora kupunguza mirija yao wakati wa sikukuu. Kama kutojibu ujumbe wenu kuliwakwaza,  mnisamehe. Naomba makala hii basi iwe jibu la ujumbe wenu wa matashi mema ya mwaka mpya.

Kama nilivyotaja hapo juu tumeruhusiwa kuendelea kuishi hapa duniani kwa neema na huruma ya Mungu na si kwa ubora wetu. Kuna watu bora zaidi yetu wameshindwa kuiona 2012. La msingi ni kwamba kwa vile tupo ni lazima tutoe mchango wetu wa kuifanya dunia hii kuwa bora zaidi kwa kila kiumbe. Ni imani yangu kwamba hatukuruhusiwa kuishi ili tuendelee kula kunywa tu bila kutoa mchango wowote ule. Hatukurusiwa kuendelea kuishi ili tuyatafute madaraka kwa gharama zozote zile ili tuwagandamize na kuwanyanyasa ndugu zetu wanyonge badala ya kuwaongoza na kuwaelekeza. Dunia ya leo ina changamoto nyingi, bila kujaliwa hekima na busara, tutaivuruga dunia yetu na tutalivuruga taifa letu. Badala ya kutumia nguvu zetu kutafuta mali, fedha na madaraka, ni muhimu kuelekeza nguvu zetu zote kutafuta hekima na busara.

Tanzania, tunauanza mwaka huu wa 2012 tukiwa na changamoto nyingi; kuna suala la katiba, bunge kuyumba, uporaji wa ardhi,  vurugu ndani vyama vya siasa, unyanyasaji wa kijinsia, vurugu kwenye vyuo vyetu vikuu, vurugu kwenye dini zetu, urais wa 2015 nafasi ni moja lakini mamia ya watu wanaitaka nafasi hii, uhaba wa chakula, mfumuko wa bei na kigugumizi cha kufanya maamuzi magumu na mengine mengi. Tumeshuhudia serikali ikitaka kutumia nguvu kubwa kuwahamisha watu wa Jangwani, wakati serikali hiyo hiyo inashindwa kutumia nguvu hizo kuhamia Dodoma. Mpango wa kuhamia Dodoma ni wa miaka mingi, lakini hadi leo hii Serikali imeshindwa kuhama kwa visingizio vinavyoelekea kufanana na vile vya watu wa Jangwani. Swali ni je, watu wa Jangwani wakihama na serikali ihamie Dodoma? Zile nguvu zitakazotumika kuhamisha watu wa Jangwani zitumike pia kuihamisha serikali kwenda Dodoma?

Tumeshuhudia Serikali ikitumia nguvu zake kuwakamata “Wachochezi” waandishi wa habari na wahariri na kushindwa kutumia nguvu hizo hizo kuwakamata wafanyabiashara wa mafuta wanaoificha nishati hiyo na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi hadi kufikia kule Musoma lita moja ya petroli kununuliwa shilingi elfu kumi! Kuna uchochezi zaidi ya huu wa kuificha nishati hii na kuwachonganisha wananchi na serikali yao? Usafiri unakuwa taabu na shughuli za uzalishaji zinakwama. Kwa maneno mengine watu hawa ni wahujumu uchumi. Serikali iko kimya na nguvu zake hazionekani kuwakamata na kuwaweka ndani hawa wahujumu uchumi.

Tumeshuhudia serikali ikitumia nguvu zake kuyazuia maandamano ya wananchi wanaotaka kufikisha ujumbe wao kwa njia ya amani na wakati huo serikali hiyo hiyo inashindwa kuwakamata wafanyabiashara wanaopandisha bei ya sukari. Serikali ilitamka kwamba bei ya sukari isiwe juu ya shilingi elfu moja na mia saba. Nenda madukani leo hii uone bei ya sukari.

Wakati serikali inataka kutumia nguvu kuwahamisha watu wanyonge wa Jangwani, kila Mtanzania anashangaa serikali hiyo hiyo kushindwa kuwakamata watu walioingia Benki Kuu na kuiba. Ilipobainika kwamba kuna wezi, wao wakajitokeza na kukiri kwamba waliiba, na kwa dharau kubwa “ wakarudisha” fedha walizoziiba, haijulikani pamoja  na riba au walirudisha kiasi kile kile? Hawakukamatwa! Wako huru hadi leo hii. Serikali yenye nguvu, yenye Jeshi la polisi inashindwa kuwakamata wezi wanaojitangaza wazi, tena wezi wa mabilioni ya shilingi,  badala yake inawakamata waandishi wa habari na wanafunzi wanaofanya maandamano kudai mikopo ya elimu ya juu?

Hoja hapa ni kwamba tumeuanza mwaka na changamoto kubwa. Kwa vile ni nyingi, nijikite kwa suala hili la Jangwani. Nimemsikia Mkuu wa Mkoa wa Dar-es-Salaam, akisema kwamba “ Watu wa Jangwani wasipokubali kuhama kwenda Mabwepande, watatambua nguvu za serikali”. Maana yake ni kwamba wataitumia polisi kuwahamisha watu hawa. La kushangaza hawajaitumia polisi kuihamisha Serikali kutoka Dar-es-Salaam na kuhamia Dodoma! Hawajaitumia polisi kuwakamata wahujumu uchumi!

Siandiki makala hii kuwatetea watu wa Jangwani, najua wako pale kinyume na sheria pamoja na ukweli kwamba viwanja vyao vimepimwa na wana hati miliki, bali mimi naandika kushangaa jinsi Hekima na Busara kutotumika. Serikali ina makosa, ilivipima viwanja hivyo ikijua kwamba huo ni mkondo wa maji. Wananchi nao wana makosa kuvikubali viwanja hivyo wakijua kwamba ni mkondo wa maji. Maafa yametokea, nini kifanyike? Mungu, anaturuhusu kuendelea kuishi kutumia bunduki na virungu kuleta amani na maendeleo, au kutumia hekima, busara na majadiliano? Serikali imesikiliza hoja za watu wa Jangwani? Inajua sababu zinazowasukuma kutaka kuendelea kuishi pale pamoja na tishio la mafuriko? Tamko la Mkuu wa Mkoa la kutaka kuwahamisha watu wa Jangwani kwa nguvu linaonyesha wazi kwamba tunaishi dunia mbili tofauti. Kuna dunia ya wanyonge na dunia ya wakubwa. Mtu ambaye ana mshahara wake, ana posho zake, ana nyumba ya kifahari ambayo hata mafuriko yakiingia, maji yananyonywa haraka kwa mashine, ana gari la bei mbaya, manunuzi yake ni kwenye maduka makubwa na wakati mwingine nje ya nchi, akiugua hata mafua anakimbizwa India na Uingereza hawezi kuelewa na kuguswa na maisha ya watu wa Jangani.

Watu wa Jangwani ni wa hali ya chini, wanaishi Jangwani si kwa kutaka bali kwa kulazimishwa na hali ya maisha: wanaishi karibu na soko, wanaishi karibu na wateja. Wengi wao ni mamantilie, ni machinga, changu doa, ni waosha magari, ni mafundi wa magari na piki piki na kazi nyingine ndogo ndogo ambazo hazipatikani Mabwepande. Hawa tishio la maisha yao si mafuriko bali ni uwezo wa kuishi siku hadi nyingine. Kufikiri kwamba wanakataa kuhama kwa ujeuri, ni kuonyesha wazi kwamba hatufahamu mazingira yao na tunaishi dunia mbili tofauti.

Mtu wa Jangwani anauza mchicha wake Kariakoo, na kujipatia fedha za kusogeza maisha yake, anapika chakula na kuwauzia madreva wa daladala. Mtu wa Jangwani anapata kibarua kwenye majengo haya yanayojengwa usiku na mchana ndani ya Jiji la Dar-es-Salaam, mtu wa jangwani anapata kazi ya ulinzi, mtu wa Jangwani ni konda kwenye magari, mtu wa Jangwani anafanya kazi za nyumbani kwenye majumba ya matajiri, mtu wa Jangwani anafanya usafi barabarani, mtu wa Jangwani inaishi siku hadi nyingine kutegemea uwanja mkubwa wa matumaini unaomzunguka. Uwanja huu wa matumaini hawezi kuupata kule Mabwepande. Nguvu za serikali zikitumika kuwahamisha matokeo yake ni kuzitenganisha familia. Wanawake na watoto watakaa Mabwepande wakipata shida, wanaume na vijana watarudi Dar-es-Salaam kutafuta maisha kwenye uwanja mkubwa wa matumaini. Hili likitokea serikali haiwezi kukwepa lawama za kuwanyanyasa wanawake na watoto.

Hoja kwamba watu wa Jangwani wamejenga kwenye mkondo wa maji haina msingi kwa dunia yetu ya leo. Kule Holland, watu wanaishi baharini, si mkondo tu bali wanayafukuza maji na kutengeneza makazi ya watu. Serikali inayowajali watu wake itaubadilisha mkondo wa maji kuwa makazi bora kwa kutengeneza miundombinu. Hata Jangwani kama kungekuwa na miundombinu mafuriko yasingeonekana. Hata hivyo kwa nini wahame wa  Jangwani na wasihame wa Msasani, wa Sinza, wa Tandale na Tabata Kisiwani? Huku kote yalikuwa mafuriko, watu na mali zao walisombwa na maji. Kwa nini zoezi la kuhama linaelelekewa kwa  watu wanyonge wa Jangwani?

Je wakihama maeneo hayo yatabaki wazi au tutashuhudia maghorofa yakijengwa? Je haiwezekani hizi ni mbinu za wajanja wachache kutaka kuwahamisha watu wa Jangwani ili kuliacha eneo hilo wazi kwa wawekezaji ambao watakuja na utaalamu wa kisasa wa kutengeneza miundombinu na kuubadilisha mkondo wa maji kuwa makazi bora? Na hili likitokea Serikali haiwezi kukwepa lawama za kuwatelekeza watu wake na kuwakumbatia wawekezaji wa nje.

Busara si kuwahamisha watu, bali ni kutengeneza miundombinu na kuyajali maisha yao. Wakati serikali inataka kutumia nguvu kuwahamisha watu wa Jangwani kwa lengo la kuwaponyesha mafuriko, ikumbuke kwamba kule Mabwepande, watakufa kwa magonjwa, watakufa kwa njaa na wengine watauwa wakiiba, maana bila kazi ya kujipatia kipato na hasa kwa vijana watajiingiza kwenye ujambazi na mwisho wake ni kifo. Serikali inataka watu hawa wahamie Mabwepande ndani ya Juma moja kuanzia sasa. Je huko Mabwepande kuna hospitali? Kuna maji?  Kuna shule? Maana watoto wa Jangwani, walikuwa wakisoma shule za mjini. Wataweza kutoka Mabwepande, na msongamano na nauli kuja kusoma mjini?

Ni wazi kuna shinikizo la shule kufunguliwa, maana wahanga wa mafuriko wako kwenye shule.  Hata hivyo serikali ina maeneo mengi ambayo inaweza kuyatumia kuwatunzia watu hawa kwa muda mpaka pale mipango mizuri itakapo fanyika. Kuna lile jengo kubwa la Machinga, ambalo serikali ilijenga kwa fedha nyingi lakini machinga kwa sababu zao za msingi( machinga anamfuata mteja na si mteja kumfuata machinga) wamekataa kuhamia. Jengo hili linaweza kutumika kuwapatia makazi ya muda wahanga wa mafuriko, ili waendelee na shughuli zao na watoto wao wasome shule badala ya  kutumia nguvu kubwa kuwahamishia Mabwepande, zoezi ambalo matokeo yake hayawezi kuwa mazuri.

Tunapouanza mwaka huu wa 2012, pamoja na changamoto nyingi, tupige magoti mbele za Mwenyezi Mungu na kuomba atujalie hekima na busara, atujalie kipaji na uwezo wa kuishi kwa kufuata sheria za nchi, tuishi kwa kuwaheshimu binadamu wenzetu na kutambua haki zao za msingi; sote ni binadamu tunahitaji makazi bora, tunahitaji huduma bora, tunahitaji furaha na amani rohoni. Mungu atujalie uwezo wa kuongozwa na uzalendo na kulipenda taifa letu la Tanzania. Heri ya mwaka mpya wa 2012.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment