KIFO CHA MUAMMAR GADDAFI NI KIFO CHA UHURU WA AFRIKA

Jumapili iliyopita yalitokea makosa katika safu yangu ya Tusemezane. Makala iliyotokea hapo juu ya Muammar Gaddafi, haikuwa yangu. Nafikiri ni kazi ya mhariri kuwaelezea wasomaji kilichotokea. Nilipokea simu na sms nyingi. Wengine wakinipongeza, wengine wakinilaumu na kunitukana. Kilichonisikitisha, pamoja na makosa ya uhariri, ni kwamba makala iliyowekwa kwenye safu yangu ilikuwa na mawazo na msimamo tofauti na wa kwangu juu ya maisha ya Muammar Gaddafi. Maana yake wale waliokuwa wananipongeza kwa makala nzuri, ni kwamba mimi si sitahiri hizo pongezi na wale walionitukana walinionea bure! Sikuweza kuwajibu wote; hivyo nina imani makala ya leo ni jibu. Huu ndio msimamo wangu juu ya kuawa kwa Muammar Gaddafi.

Afrika tulitawaliwa na tuliuzwa sokoni kama bidhaa nyinginezo. Utumwa na ukoloni ni historia mbaya katika historia ya dunia yetu. Hadi leo hii wakoloni, walishindwa kuomba msamaha kwa dhambi kubwa walizotutendea. Inajulikana wazi kwamba walitupatia uhuru shingo upande na kuendelea kututawala kwa njia mpya za utandawazi, soko huria na ukoloni mambo leo kama ilivyojitokeza juzi kwa Waziri Mkuu wa Uingereza kutamka wazi kwamba bila kuukubali ushoga hatutapata misaada!

Viongozi wa Afrika walioonyesha kuwa na mwanga wa kutaka uhuru kamili walizimwa. Mfano mzuri ni wa Patrice Lumumba. Hata akina Nkrumah, kupinduliwa kwao kulikuwa na msukumo wa hawa mabwana wakubwa. Wana ujanja wa kutumia misemo kama Demokrasi, haki za binadamu, kulinda maisha ya watu na upuuzi mwingine mwingi, huku wakiuma na kupuliza. Lengo lao ni kuwapumbaza  Waafrika, kuendelea kuwatawala na kuwafanya soko lao kubwa na sehemu ya kuchuma rasilimali nyingi kama vile mbao, madini, ardhi ya kulima chakula na kuzalisha nishati, sehemu za kupumzikia na mengine mengi.

Kilele cha hujuma za wakoloni kimejionyesha wazi kwa kifo cha Muammar Gaddafi, aliyekuwa rais wa Libya. Shutuma zote juu yake kwamba alikuwa dikteta, kwamba alikuwa anawaua watu wake, kwamba alikuwa akisaidia makundi ya kigaidi ni uongo mtupu. Gaddafi, alikataa kuwauzia mafuta Wazungu kwa dola, yeye alitaka awauzie kwa dhahabu. Walete dhahabu awapatie mafuta. Gaddafi, alikataa makampuni ya kigeni kuja Libya kuchimba mafuta. Alisimama imara na kusema wao wana makampuni yao ya kuchimba mafuta. Wazungu, waje wanunue mafuta na si kuja kuchimba mafuta Libya. Gaddafi, alitaka Afrika kuungana. Alitaka Afrika iwe na serikali moja, ili bara letu liwe na nguvu na kuweza kushindana na hawa wakoloni. Alikuwa tayari kutoa fedha ili kutekeleza mradi huu mkubwa na wenye manufaa makubwa kwa bara zima la Afrika. Wakoloni hawakuyataka mawazo yake haya na sasa wamehakikisha ameondoka na kufutika! Ni unyama ule ule wa Ukoloni na utumwa.

Kifo cha Gaddafi, kimewasikitisha wengi na hasa Waafrika ambao wanatambua mchango wake mkubwa. Kama alivyosema Waziri Membe, ni kichaa peke yake anayeweza kusimama na kusema kwamba Gaddafi, hakufanya kitu. Sote tunakumbuka alivyoligeuza jangwa kuwa kijani, sote tunajua jinsi ambavyo watu wake wasiokuwa na kazi walivyokuwa wakipata posho ya kujikimu, tunajua jinsi alivyowajengea wananchi wake makazi bora ya kuishi, sote tunajua jinsi alivyoigeuza Libya kuwa ni nchi yenye maendeleo makubwa ndani ya bara la Afrika. Ametoa michango mingi kwenye nchi mbali mbali za Afrika. Amekuwa akitoa fedha za kuuendesha mikutano ya Umoja wa Afrika. Ni mtu aliyewapenda watu wake wa Libya na ni mtu aliyelipenda bara letu la Afrika. Kifo cha kinyama kilichomfika ni aibu na laana kubwa kwa watu wa Libya kukubali kutumiwa na wakoloni kutekeleza adhima yao.

Kama kweli wakoloni walikuwa na nia njema, mbona nguvu zilizotumika Libya kumuondoa Gaddafi, hazitumiki mashariki ya kati? Mbona Syria, kuna maandamano ya kuikataa serikali iliyo madarakani kuondoka na watu wengi wamekufa, lakini hatujaona nguvu kubwa zikitumika kama zile zilizotumika Libya?

Wanataka mafuta ya Libya! Wanataka rasilimali za Afrika, wanataka soko la Afrika; wanataka Afrika isiungane na kuwa na nguvu ili waendelee kutugawanya na kututawala. Wanataka kuendeleza ukoloni na utumwa, wanataka kuzirudia sera za mababu zao zilizoliteketeza bara la Afrika.

Wapo watanzania wenzetu wanasema Gaddafi, alikuwa mbaya maana alishirikiana na Iddi Amin kuivamia nchi yetu. Ni kweli alifanya vibaya, hata yeye alijuta na kuomba msamaha. Hizo zilikuwa ni siasa. Hata sisi Tanzania wakati wa vita ya Biafra, pamoja na msimamo wa Tanzania wa kutaka umoja, tulisimama upande wa Biafra wa kutaka Nigeria igawanywe vipande  viwili. Mwalimu Nyerere, alikuwa na hoja nzuri na alijielezea vizuri. Msimamo wetu huo juu ya Biafra, haukutufanya tuonekane maadui wa Nigeria. Hata hivyo kwani ni Gaddafi peke yake alimsaidia Iddi Amin wakati wa vita ya Kagera?

Hakuna anayesema kwamba Gaddafi, alikuwa mtakatifu. Alikuwa na mapungufu yake kama binadamu wengine wote. Lakini kwa suala la kujenga taifa huru lenye maamuzi yake, kwa suala wa umoja wa Afrika, kwa suala  la rasilimali za Afrika kuwanufaisha Waafrika wenyewe, hakuwa na mfano wake. Kama tuna bishi tusubiri utawala mpya wa Libya ndo tutatambua kazi kubwa iliyofanywa na Gaddafi.

Kwamba alikuwa akieneza Uislamu, hilo si kosa maana kila muumini ana wajibu wa kuieneza dini yake. Miaka mingi Waislamu na Wakristu wameeneza dini zao ndani ya bara la Afrika, lakini ukweli usiopingika ni kwamba hadi leo hii bado kuna Waafrika wanaoamini bado dini zao za jadi. Hawakukubali kuingia kwenye Uislamu ama Ukristu. Kueneza na kupokelewa ni vitu viwili tofauti; watu wakikubali kupokea imani fulani, maana yake ni kwamba wameilewa na kuipenda; kama si kuwalazimisha watu kwa upanga kama ilivyofanywa miaka ya nyuma katika Bara letu la Afrika  na Amerika ya kusini, hakuna tatizo la mtu kuipokea imani anayoamini itaboresha utu wake na kumwongoza kuishi vyema na binadamu wenzake.

Kifo cha Gaddafi, kitufumbue macho. Ni lazima Waafrika kushikamana na kusema hapana! Ni lazima kukataa mbinu hizi za wakoloni kutaka kutuchagulia viongozi. Ni lazima kuwakataa hawa vibaraka wao na kuwa tayari kulilinda bara letu la Afrika, ili liwe salama kwa vizazi vijavyo. Ni bora kufa tukilitetea bara letu kuliko kuliacha likachukuliwa na hawa wakoloni wajanja wanaojifanya wanaipenda sana Afrika kumbe ni mbinu za kuhakikisha bara letu linabaki gizani na kuendelea kunyonywa. Uhuru wetu unakufa ni lazima tusimame kidete kuutetea.

Na,
Padri Privatus Karugendo

0 comments:

Post a Comment