MIAKA HAMSINI YA UHURU WETU NI HISTORIA YA WATANZANIA WOTE.

Tunaposherehekea miaka hamsini ya uhuru wetu ni wakati mzuri wa kuwakumbuka mashujaa waliopigania uhuru wa taifa letu na ni muhimu pia kuwakumbuka wale wote waliochangia maendeleo ya taifa letu mara baada ya uhuru hadi leo hii. Kumekuwepo na michango mingi ya watu binafsi, mashirika ya dini na mashirika yasiyokuwa kiserikali. Wote hao wamekuwa wakichangia kuijenga Tanzania yetu. Kwa maana hiyo basi historia hii ya miaka hamsini ya uhuru wetu ni mradi wa pamoja uliotekelezwa na watanzania wote na utaendelea kutekelezwa na watanzania wote miaka mingine hamsini na kuendelea.

Ingawa uhuru wetu ni mradi wa pamoja ni vyema kutambua mchango wa makundi mbali mbali. Katika makala hii na nyingine zitakazofuata nitajadili mchango wa harakati wa mashirika yanayotetea usawa wa jinsia na ukombozi wa wanawake kimapinduzi katika kipindi cha miaka hamsini ya uhuru wetu.

Mashirika haya yamefanya mambo mengi ya kutetea haki za binadamu, usawa wa jinsia na ukombozi wa mwanamke kama tutakavyoshuhudia kwenye makala hizi: Mfano kusaidia kuiweka sahihi historia ya taifa letu. Tumekuwa tukisikia majina ya wanaume bila kutajwa wanawake katika historia ya kupigania uhuru wa taifa letu lakini kwa kazi iliyofanywa na TGNP ( Mtandao wa Jinsia Tanzania) wa kutafsiri katika lugha ya Kiswahili utafiti wa Susan Geiger juu ya Wanawake wa TANU, na kuhakikisha kitabu hiki kinasambazwa na kusomwa na wengi, kumeleta mwanga mpya wa ukweli wa Wanawake kushiriki kikamilifu katika kupigania uhuru wa taifa letu. Huu ni mchango mkubwa wa TGNP ambao inawezekana hata na wao hawautambui maana daima tunaelekeza nguvu zetu kwa mambo makubwa ya dunia hii na kusahau maisha ya siku kwa siku yanayotuzunguka. Baada ya uhuru mfumo dume ulishika hatamu, historia ya wanawake waliopigania uhuru ikasahaulika na kufunikwa.

Marehemu Susan Geiger ni msomi mwanaharakati ambaye alifundisha masomo ya Kiafrika na yale ya Jinsia katika Chuo Kikuu cha Minnesota/Twin Cities, huko Marekani kwa muda wa miaka mingi. Alikuja Tanzania kwa mara ya kwanza akiwa mwalimu wa kujitolea katika miaka ya 1960. Baadaye aliendelea kurudi katika nyakati tofauti katika kipindi chote cha maisha yake.

Kazi yake kubwa ya utafiti ilikuwa juu ya historia ya uchifu wa Wachagga. Utafiti huo ndio uliokuwa chimbuko la kujipatia Shahada ya Udaktari wa Falsafa. Baada ya hapo alifanya utafiti mwingine wa makusanyo ya wanawake wanaharakati wapigania uhuru. Susan alikuwa mwanaharakati aliyejitolea kwa michango ya hali na mali hadi mwisho wa maisha yake. Alitoa mchango mkubwa kwa wanamtandao wa masuala ya jinsia hapa nchini ili waweze kuendeleza shughuli zao.

Utafiti wake juu ya Wanawake wa TANU, uliibua mengi yaliyokuwa yamefunikwa. Mbali na Bibi Titi Mohamed, mwanamke anayetajwa kwa mbali katika harakati za kupigania uhuru wa taifa letu, kuna majina ya wanawake wengi waliojulikana kama “Wanawake wa TANU” waliopigana kufa na kupona kulikomboa taifa letu. Kufuatana na ushuhuda wa Wanawake wa TANU, ni kwamba chama hiki kilisimikwa na Wanawake, kama alivyonukuliwa Bi Mashavu binti Kabonge kutoka Tabora:
Nikwambie ukweli, wanawake ndio walioleta TANU. Ukweli ni kwamba wanawake ndio waliofanya hivyo. Wanaume wengi waliogopa kufukuzwa kazi. Waliambiwa na waajiri wao kwamba yeyote atakayejiunga na TANU atafukuzwa mara moja…. Lakini wanawake walikuwa mashabiki wa nguvu wa TANu na wengine waliachika kwa sababu ya sushuli zao za siasa”

Mashavu binti Kabonge, ni kati ya wanaharakati wanawake wa Dar-es-Salaam, waliopigana kufa na kupona kuleta uhuru wa taifa letu, lakini hawatajwi wala kukumbukwa. Hivyo tunaposherehekea miaka hamsini ya uhuru wetu kwa vile TGNP imetusaidia kuyafufua baadhi ya majina ya wapigani uhuru hawa ni bora kuwakumbuka na kuwaenzi. Pia ni wakati kuendeleza mapambo ya mfumo dume ambao ni hatari kwa mambo mengi hadi kuifuta historia. Ni wazi majina ya wanawake hawa waliopigania uhuru wa taifa letu yamefunikwa na mfumo dume! Hakuna maelezo mengine!

Mbali na Mashavu binti Kabonge, kuna majina mengine mengi ya wanaharakati wanawake wa Dar-es-Salaam: Tatu Binti Mzee, pamoja na Bibi Titi Mohamed,Tatu Binti Mzee alikuwa mmoja wa wajumbe wanawake wa kwanza katika chombo muhimu cha maamuzi, yaani, kamati Kuu ya Chama.

Halima Hamisi, huyu naye ni mpambanaji wa kuleta uhuru, katika utafiti wa Susan, ananukuliwa akisema “ Tulitembea kwa miguu siku nzima bila chakula. Ukichukua chai nyumbani na ukijaliwa kupata karanga, unanunua. Wakati mwingine tuliweza kupata fedha za chakula kutoka ofisi ya TANU, lakini ilibidi  wapige hesabu kwa makini….”

Wanawake wengine wa Dar-es-Salaam, walioshiriki harakati za kuleta uhuru na majina yao yamefunikwa na historia ni: Salima Ferouz, Binti Kipara, Mwasaburi Ali, Fatuma Abdallah na wengine wengi ambao watafufuliwa na  tafiti nyingine zitakazofanyika kwa kuchochewa na hii ya Susan.

Katika utafiti wa Susan, Salima Ferouz, ananukuliwa akisema: “ Sisi wanawake tulikuwa na nguvu… tuliongoza njia kwa sababu ya uonevu wa watoto wetu na jinsi tulivyowekwa ndani… tulifanya kazi pamoja, tukajiunga na Kitengo cha wanawake na kutumikia TANU, tukichangisha fedha na kuwahamasisha wengine wengi wajiunge..”

Hata mikoani kulikuwa na wanawake walioshiriki harakati za ukombozi wa taifa letu. Kule Kilimanjaro kulikuwa na Halima Selengia Kinabo, Mwamvita Salim, Zainab Hatibu, Morio Kinabo, Violet Njiro, Elizabeth Gupta, Kanasia Tade Mtenga,Natujwa Daniel Mashamba na Lucy Lameck.

Hata kule Mwanza kulikuwa na wanaharakati wanawake waliopigania uhuru wa taifa letu, lakini historia haiwakumbuki  tena. Wanawake hao ni: Agnes Sahani, Aziza Lucas, Tunu Nyembo, Halima Ntungi, Mwajuma Msafiri, Pili Juma, Mwamvua Kibonge, Zuhura Mussa  na  Chausiku Mzee.

Ni wazi wako wanawake wengine wengi walioshiriki harakati za kuleta uhuru wa taifa letu, ni kazi ya Mashirika yanayotetea usawa wa jinsia na ukombozi wa mwanamke kwa kushirikiana na watanzania wanaopenda kuweka kumbukumbu sahihi kuendeleza utafiti na kuibua majina mengine ya wanaharakati wote walioshiriki kuleta uhuru wa taifa letu. Tusitake kusherehekea kwa kuimba, kunywa na kucheza bila kuiandika historia sahihi ya taifa letu.

Ni lazima tujiulize tumeteleza wapi? Kama  huko nyuma tuliweza kuendesha harambee ya kuchangia harakati za mapambano, shughuli zote zikaendelea bila misaada ya kutoka nje. Mapato yote ya nchi yakiwa mikononi mwa mkoloni. Inakuwaje sasa wakati tumeshika mapato ya nchi mikononi mwetu, tunaendelea kuomba misaada ya kujenga vyoo na vyandarua? Uwezo wa kujitegemea uliokuwa miongoni mwa wananchi wakati wa kupigania uhuru umekwenda wapi? Tulipigania uhuru wa kisiasa, ili  tupoteze uhuru wa kujitegemea na kujiamulia mambo yetu wenyewe? Ukipokea misaada, ni vigumu kukwepa masharti yake!

Makala hii ni mwanzo mzuri wa kuangalia mchango wa Mashirika yasiyo kuwa ya kiserikali yanayoshughulikia usawa wa jinsia na ukombozi wa mwanamke. Swali la kujiuliza ni je, kama Wanawake walikuwa mstari wa mbele wakati wa kupigania uhuru wetu, ilitokea nini wakawa mstari wa nyuma baada ya uhuru? Wanawake walichangisha fedha za kuendesha mapambano, walifanya kazi kwa nguvu kupata fedha, walipika maandazi na wengine walifanya kazi za kujidhalilisha ili wapate fedha za kukiendesha chama cha TANU. Mapambano ya kuleta uhuru hayakutegemea misaada kutoka nje. Uwezo mkubwa wa kujitegemea ulioongozwa na wanawake ulikwenda wapi baada ya uhuru kufikia hatua ya kutafuta fedha kutoka nje ili kuendesha “ Miradi” ya kuwakomboa wanawake wa taifa letu? Ni lazima kutafakari kwa kina wakati tukisherehekea miaka Hamsini ya taifa letu.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment