MWANDISHI ELIESHI LEMA

MWANDISHI ELIESHI LEMA.

Nimekuwa nikifanya uhakiki wa vitabu mbali mbali vya mwandishi Elieshi Lema. Mama huyu amejitokeza kuwa mwandisi mzuri wa vitabu vya watoto na watu wazima. Vitabu vyake ambavyo nimefanyia uhakiki hadi sasa hivi ni Parched Earth, Freshi na Maisha, kitabu cha kwanza hadi cha nne, Mkate Mtamu, Mwendo na Wanawake wa TANU. Wale waliofanikiwa kusoma uhakiki wangu, waliweza kutambua mchango wa mama huyu katika jamii yetu. Ubunifu wake wa kuandika hadithi za watoto kwa lengo la kufikisha ujumbe mzito kwa watoto ni jambo la kusifia.

Uchambuzi wangu na uchambuzi unaofanywa na watu wengine juu ya vitabu vya Elieshi Lema, au vitabu vya waandishi wengine unatoa mwanga wa kitabu, lakini wakati mwingine inakuwa vigumu kugusa kikamikilifu alicholenga kuandika mwandishi. Mara nyingi mahojiano na mwandishi wa kitabu yanasaidia kuongeza mwanga.

Mnamo mwaka 2000, Elieshi Lema, alifanya mahojiano na Mwalimu wa Kiswahili Irmi Hanak, kutoka Vienna Austria, juu ya vitabu vyake viwili: Safari ya Prospa na Mwendo. Mahojiano yalifanyika kwa lugha ya Kiswahili na kiingereza na baadaye kutafsiriwa kwa Kijerumani na Mwalimu Irmi Hanak.

Nilishafanya uhakiki wa Mwendo, kwenye safu hii ya Kisima cha Ujuzi. Na siku za hivi karibuni nitafanya uhakiki wa Safari ya Prospa. Kwa faida ya wasomaji nieleze kwa kifupi juu ya vitabu hivi viwili: “Safari ya Prospa” ni hadithi ya mtoto wa miaka kumi hivi anayeondoka
nyumbani ili kumtafuta mpwa wake Merisho aliyepotea. Anasafiri mpaka
Dar-es-Salaam akiwa peke yake. Anapata msaada kutoka kwa watoto mitaani,
hasa kwa msichana Sara anayemkuta njiani. Mwishoni wanafaulu kumpata
Merisho na kumrudisha kwa mama yake.

“Mwendo” ni hadithi ya msichana wa miaka kumi na minne. Felisia anaondolewa
shuleni na wazazi wake ili achezwe kufuatana na mila ya Kimakonde.
Walimu wa Felisia wanashindwa kufahamu. Felisia mwenyewe anahofu, kwa
vile alisikia hadithi ya kutisha ya wasichana waliotahiriwa.
Lakini Shangazi Helena Margareta ambaye ni mtu bila woga anaondoa wasiwasi
wake na kumsindikiza katika njia yake. Anaeleza wazi kwamba ni mila
yenye faida tu inayofaa kufuatwa na kuendelezwa. “Sitakubali kamwe mwili
wangu uguswe na mtu ye yote bila ya idhini yangu” ni ujumbe wake muhimu
kwa Felisia.
Mwishoni Helena Margareta anawakabili walimu wa shule wanaokataa Felisia
arudi darasani baada ya kutofika shuleni kwa miezi kadhaa.

Sasa tumsikilize Elieshi, mwenyewe anavyosema juu ya vitabu vyake. Nimeaandika habari hii kwa kusaidiwa na Internet na maongezi na Elieshi mwenyewe:
Swali: Irimi Hanak: Kitu gani ni muhimu zaidi katika kuandika vitabu kwa watoto au vijana?

Jibu: Elieshi Lema: Kuandika hadithi kwa watoto – kitu kimoja ambacho ni
muhimu sana – lazima uwapende watoto, na ukishawapenda, unawatazama na
ukiwatazama, unajaribu kuwaelewa ni kwa nini wanafanya hivi, ni nini
kinachowafurahisha, nini kinachowasikitisha, kwa hiyo unaweza ukajiingiza
katika nafsi yao na wewe mwenyewe ukawa mtoto.
Kwa hiyo ndivyo hivyo unaweza kuandika kitabu cha watoto, wakaonekana
kweli watoto walio ndani, na wahusika wako ukawachora kama watoto, na
siyo kama mtu mzima anayezungumza kuhusu watoto.

Swali: : Irimi Hanak: Kabla ya kuandika kitabu cha Safari ya Prospa, ulifanya utafiti mrefu. Ulichunguza nini hasa katika utafiti huo?

Jibu: Elieshi Lema: Vyote viwili nimefanya utafiti, “Mwendo” ndiyo nimefanya utafiti wa muda
mrefu zaidi. Utafiti wa “Safari ya Prospa” ulikuwa rahisi. Kwa sababu
nilitaka kufahamu anapitia wapi, na pale anapopitia, wana utamaduni wa
namna gani. Kwa sababu „Safari ya Prospa“, mtoto anatazama sana jamii,
anasikiliza, anauliza ni kwa nini. Kwa hiyo jamii inatathminiwa na mtoto.
Kwa hiyo ni lazima ufanye utafiti, ili ujue hiyo jamii ikoje, na mtoto
anapoona vitu vya namna hii, anafikiria nini, kwa mfano askari anauliza
maswali, anasema “Haya nitakwenda kufanya utafiti”, askari anachukua muda
wake.

Yeye mtoto (Prospa) anaona “A-a, mtoto amepotea, huyu atachukua muda
mrefu kiasi gani, mpaka apate mtoto.“ Kwa askari, kuna urasimu. Hatafanya
utafiti kwamba mtoto amepotea, huku aliko anaweza akaumia, sijui .. Aa,
urasimu, lazima njia fulani zifuatwe. Kwa hiyo unafanya utafiti wa vitu vyote
hivyo, halafu unajua ile jamii ikoje, na huyo mtoto anapokuja, anaitazama ile
jamii na kuitathmini, anatazama vitu gani. Huu ndiyo ulikuwa utafiti wa
“Safari ya Prospa”. Na kwa vile walifika mpaka Zanzibar, ilibidi nijue
Zanzibar ikoje, na watu wakoje, na ni vitu gani muhimu kwao, na hivyo mtoto
akienda, ataona vitu vya namna gani.

Swali: : Irimi Hanak: mimi kama msomaji nafikiri ule mtazamo wa mtoto ndiyo muhimu sana, unasema nini juu ya hili?
Jibu: Elieshi Lema: Ni muhimu kwa sababu mara nyingi, hatuna subira kwa watoto, hatuna subira
kabisa, tunasema “We mtoto acha utundu” Hatujajua, hatujamwuliza ni kwa
nini unafanya hivi. Au “Nieleza unajisikiaje.” No. Tunaingia tu, tunahukumu,
tunatoa ama ni adhabu au ni sifa au ni nini. Sasa watoto wanatuonaje,
wanatazama hiyo jamii, wanaona “Nyie watu wa ajabu kweli”
Nilitaka mtoto apotee, yule mtoto anapopotea, Prospa, kila anapopita,
anatathmini, anauliza, anafanya uamuzi, na kwa hiyo ule uamuzi
unamwendesha. Halafu Prospa anakutana na Sara. Sasa unajua mambo ya
jinsia pale, yanajitokeza yenyewe tu kwa mitazamo yao wenyewe, kwa
mitazamo yao wenyewe watoto. Na siyo kusema - Prospa hana uamuzi kamili
juu ya Sara kama mtoto wa kike... Lakini anauliza maswali ambayo Sara
anamjibu, na wakati wenzake wanapokuja kumwambia “Aa msichana hawezi
kufanya chochote, msichana yule atasema tu”, Prospa anasema “ Hata, no,
mimi sana namwamini, hawezi kusema“, unaona, ameshafanya utathmini
wake mwenyewe, kwa kutembea na Sara, na kumwona anavyofanya vitu,
anavyofanya uamuzi. Si kwamba ni rahisi, wanagombana wakati mwingine,
na Sara anamshinda kabisa, na „agh huyu mbona siwezi kumshika, siwezi
kumcontain“.

Huyu ni mtoto. Mtoto akifanya vitu, isiwe ni mimi mtu mzima nizungumze
kwa niaba ya mtoto. Mtoto anaonaje jamii, na kwa hiyo tafsiri yake ya jamii
inakuwaje? Mtoto anaonaje jinsia, na kwa hiyo tafsiri yake ya jinsia
inakuwaje? Na ni pande zote mbili, wa msichana na mvulana. Na kwa hiyo
kwa kusema kwamba watoto wenyewe hawajengi mawazo mabovu kuhusu
jinsia. Ni jamii ya watu wazima inayowafanya watoto wajenge yale mawazo
mabovu kuhusu jinsia. Siyo watoto wenyewe. Watoto wenyewe wana
heshima. Wanajiona kama watoto. Halafu jamii, watu wazima inapoleta yale
mawazo yao, mtoto wa kike ni hivi, mtoto wa kiume ni hivi, wanaanza kujua
“aha sehemu yangu ni hiyo, na sehemu yako ni hiyo”. Na kwa hiyo yale
mawazo tofauti, na ni watu wazima wanaosema hivi, wanaojua watu wazima
ni sahihi, kwa hiyo wanachukua yale mawazo.

Swali: : Irimi Hanak: Kwanini uliamua kuandika kuhusu mada ngumu kama ile ya watoto mitaani?

Jibu: Elieshi Lema: Kwanza ilikuwa rahisi zaidi kwa sababu hiyo ilikuwa tu sehemu ya kitabu,
siyo kitabu kizima. Mimi nilijiambia baada ya kutoa “Safari ya Prospa”, nilitaka
kwenda kumfuata Sara mitaani, kwa sababu Sara alibaki. Kwa sababu
Sara alikuwa mtoto wa mitaani. Na kila siku nasema nikipata nafasi, lazima
nirudi kwa Sara, ili nimchukue Sara pale kama mtoto wa mitaani. Lakini nahitaji
utafiti mrefu, mkubwa, kwa hiyo kidogo hiyo nafasi imekuwa bado sijaipata.
Lakini hapo sasa, ingekuwa niyachukue na mambo yale ya ukatili wa
wenyewe kwa wenyewe, ukatili wa watu wazima kwa watoto wa mitaani, na
shida wanayoipata, an wao wenyewe wanatazamaje.
Nisipofanya utafiti, itakuwa ni mawazo ya mtu mzima nayaweka kwa watoto.
Na yanaweza yapata mengine yakawa ukweli, na mengine yasiyo kweli. Na
hutaki kuandika kitu bila kujua ni kwa nini unaandika.

Kwanza, watoto wa mitaani, ni kitu kipya Tanzania. Na tulikuwa tunashangaza
kila mtu. Watoto wa mitaani walikuwa hawapo miaka kadhaa iliyopita. Na
ilipokuja sasa ikawa phenomenon. Watu wakawa eh – “watoto wa mitaani, ni
watoto wabaya, piga, ni wezi nyiye”. Halafu unafanya urafiki na watoto wa
mitaani, unaanza kujua kwamba kweli siyo wezi, siyo watoto wasio na heshima,
ni watoto wenye shida. Na kwa hiyo watoto hapa wanapokuja, kwanza
wanapokutana (na Sara na Prospa) wanavunja chupa wanasema “Wewe unakaa
kwenye ile kundi” ni kwamba kwanza wanahitaji uongozi ili waweze
kuishi mitaani. Wakajua kwamba hawa siyo watoto wa mitaani. Wakamwambia
usilale ovyoovyo utaumia, ni kama wamekuwa wazazi sasa kwa wale
watoto. Na wakawachukua, wakawaambia wewe uende huku na wewe uende
huku, kwa sababu wanaishi tofauti, na wakapata familia mpya, wakaishi nao.
Wakaongozwa, jinsi ya kuishi, unaenda wapi unapata chakula, unaishi vipi,
unsafisha magari unafanya hivi unafanya hivi, wakaishi. Na mimi nilifanya
makusudi kwamba kwa sababu ya kuelewa maisha ya mitaani na maisha ya
shida, yana tena ile tathmini ya jamii, inatoka vizuri sana hapo, na wanatathmini
jamii vizuri kabisa, na ukiangalia wamekuwa na stadi za kuishi, ambazo
zinazidi hata za watu wazima, kwa sababu wanapokutana na yule mjomba,
mjomba hana stadi za kuishi. Anaishi vizuri, ana gari nzuri anafanya biashara
nzuri, anaendesha gari na anaishi huku, mbali na dunia ya mtaani, hana stadi
za kuishi. Kwa hiyo anaposema ingia we peke yako, wanaingia wote, na wanajua
jinsi ya kuingia na jinsi ya kukaa, na jinsi watakavyofanya mambo. Na
ni katika hivyo mpaka wanakuja kugundua kwamba mtoto kweli amepotelea
wapi.

Swali: : Irimi Hanak: Kwa vipi ulipata kufahamu wa watu wanaoishi kama wahusika wako?

Jibu: Elieshi Lema: Kuna ule utafiti kwa vitendo. Unajua kama uko kwenye utafiti wa watoto
usiowajua. Kwa sababu mimi sijui, sijaishi, maisha ya mtoto mtaani, kwa
hiyo siwezi kuyajua, sasa njia wa kuyajua ni kufanya utafiti kwa vitendo na
kuyafuata. Unajua, anaishi wapi, unaenda, anakula nini, unajua, anafanya kitu
gani, kazi gani, na wakati mwingine unamwambia “We fanya, nioshe gari nikupe
pesa”, na kwa hiyo, wanakuwa rafiki na wanaanza kukuambia, “mimi
ninaishi mahali fulani, baba yangu alikuwa hivi, mama yangu alikuwa hivi”,
halafu unauliza maswali ilikuwaje, wanakuambia “mimi sipendi kukaa mitaani
basi, lakini nikienda nyumbani napigwa, kwa hiyo afadhali tuwe hapo.”
Baada ya kujua ndani kwao wanajisikiaje unaweza sasa ukafuatilia ukahisi,
ukajenga ile hisia na kusema ingekuwa mimi. Imenisaidia kuchora hawa wahusika
watoto wa mtaani kwa huo utafiti.

Swali: : Irimi Hanak: kitabu chako cha pili, “Mwendo” kinazungumzia jinsi ya wasichana wanavyokuwa watu wazima na pia tatizo la tohara kwa watoto wa kike. Kwa nini umechagua tena mada inayogusa matatizo tele ya jamii?

Jibu: Elieshi Lema: Kwa sababu hiyo ndiyo ilinigusa na tulikuwa tunaizungumzia sana hiyo, na
kwa muda mrefu. Watu wanazungumza female genital mutilation, halafu unaandika
makala kwenye gazeti, halafu watu wanafanya semina lakini hakuna
kinachotokea. Na kuna kitu kingine hapo - issue ya “Oh ni utamaduni wetu,
kufanya hivi na hivi” Kwa hivyo hicho kitu kikanigusa. Na mwaandishi kila
mara huandika vizuri wakati anapoandika kitu kilichomgusa yeye mwenyewe,
anasema “Ah, lazima niseme kitu hapo” Kweli ilikuwa ngumu, nilifanya utafiti
kwa miaka mitatu. Kwanza ilibidi nichague.

Nilichagua jamii ya Kimakonde kwanza, kwa sababu wao hawatahiri. Kwa
hiyo nilijua nitatumia hiyo jamii ambayo haitahiri kama kioo cha ile inayotahiri.
Hiyo ni moja. Halafu baada ya kuamua hivi, sasa ilibidi nifuatilie, wanapitia
katika rituals gani, wakati mtoto anapofika huo. Kwa hiyo ilibidi nifanye
utafiti. Mimi siyo Mmakonde. Ilibidi niwatafute Wamakonde, niwafahamu,
niwaeleze nilitaka kufanya nini, nizungumze na watu, waweze kuzungumza
na watu wengine ambao wanafanya vitu hivyo katika zile rituals, ili niweze
kuona zinafanywaje. Nikaongea na wanawake wa Kimakonde wengi, nikaenda
Mtwara, nikazungumza na wasichana, nikaenda Lindi, kwenye shina la
Wamakonde.
Kila nilipokuwa nikiandika “Mwendo” nilifika mahali nikajikuta aa siwezi
kuendelea kwa sababu sijui kwa hiyo nina haja, naenda tena kwenye utafiti,
kuulizia hiki kinakwendaje. Kwa hiyo kweli kilinipa shida, kile kitabu kimenipa
shida sana, lakini nafurahi kama kimetokea, kama wasomaji wakisoma,
wanaona kile kitu nilichotaka kusema kimetoka. Mwanamke Helena Margareta,
yule mama nampenda sana, kwa sababu ilibidi nimtumie yeye kuonyesha
kwamba kuna myth na kuna ukweli wa maisha, na kwamba rituals tunazitengeneza
wenyewe. Na kwamba tunaweza tukazibadilisha wenyewe. Kwa hiyo
ile kitu ya “Ni utamaduni wetu, kwa nini tusitahiri wasichana”, hiyo siyo valid,
kwa hiyo Helena Margareta – kwangu kumchora Helena Margareta ilikuwa
rahisi kwa sababu ni mtu mzima, anazungumza ninachojua mimi, lakini
wale wasichana na wale wavulana pia, wanavyopita na wanapokuwa na kuona
ulimwengu wa watu wazima - ngumu.

Swali: : Irimi Hanak: Uliwahi kuwakuta watu kama Helena Margareta?

Jibu: Elieshi Lema;
Hakuna mtu niliyekutana naye ambaye ni Helena Margareta. Hakuna kabisa.
Kwanza, watu unaoongea nao wanaamini kwamba hicho wanachofanya ni
sawasawa. Lakini Helena Margareta nilimpenda kwa sababu mimi niliweza
kutumia akili yangu ya mtu mzima zaidi katika kumchora. Umefahamu? Kwa
hiyo nilimpenda, alikuwa anasema vitu ambavyo mimi kama mtu mzima niliweza
kupenda.
Nimekuta mama Felisia, ni typical, hao nimewakuta, ambao walisema: “Aa,
mtoto wa kike lazima achezwe, asipochezwa tunamkataa”, hao wapo, hao nimekutana
nao.
Helena Margareta ni vipande, nimesikia, labda ni wanaume nusu, labda ni
wanawake nusu, labda ni robo kidogo tu sehemu fulani. Na Helena Margareta
amechorwa zaidi kwa kusikia mtoto wa kike mdogo aliyekuwa amechezwa,
alivyokua anazungumza.
Unajua unaweza ukasikiliza mtoto mdogo anavyozungumza ana mawazo safi
kabisa, hayaendani na tabia ya wale watoto wengine ambao unawachora. Kwa
hiyo unawaleta kwenye - nani - ya watu wazima. Ni kitu nimechora kutokana
na watu wengi, na mtazamo hasa ile ya Margareta anatokana na mtazamo wa
mwandishi. Nampenda kwa sababu ndiye ametoa ile changamoto, anakuja
kwa mwalimu anasema:
“Aa. Hiyo ni harakati. Na mimi nilipokuwa katika harakati ya ukombozi
Msumbiji, niliambiwa kwanza kabla ya hujabadilisha kitu lazima uamini, ili
ukibadilisha unabadilisha kitu ambacho unaamini kwamba kile kingine kitakachokuwa
ndicho”. Hasa huo ni mtazamo wangu ambao kwamba tukisema
tu: “Aa, hatutabadilisha kitu”. yatakuwa mabadiliko superficial.
Kwa hiyo nilimpenda Helena Margareta, alinipa hiyo fursa ya kusema unaotaka
wewe kama mwandishi useme. Alifungua dirisha, nikaweza kupata
mambo ya kuweza kumchora na kuwa hivyo alivyokuwa. Lakini kwa kweli
wanawake wengi ni kama mama yake Felisia.

Swali: : Irimi Hanak: Reception ya kitabu hiki ikoje, wasomaji watanzania wanaonaje?

Jibu: Elieshi Lema: Hivi vitabu vilinunuliwa na “Mradi wa Vitabu vya Watoto Tanzania” na vilisambazwa
shuleni. Kila mara naambiwa watoto wanakipenda. Kitabu hiki,
watoto wa kike waliamua wavulana hawatasoma. Vilikuwa vinafichwa, yaani
akishapata mmoja, hataki kukitoa, anasoma, anampa mwingine, anasoma,
anampa mwingine anasoma, anampa mwingine. Watoto wenyewe, ambao
ndiyo haswa niliwaandikia, walikipenda, wameona kwamba kuna kitu nimesema
ambacho nilitaka niseme. Mimi ndiyo hiyo ilinifurahisha kuliko vyote.
“Safari ya Prospa” vilevile. Safari ya Prospa inapendwa sana.
Shida moja hapa Tanzania ni uwezo wa kununua vitabu. Hiki kitabu tunakiuza
elfu mbili mia tano, ni ghali kwa jamii ya kawaida ya Tanzania. Kwa hiyo
kusambaza kwake kwa watoto wengi ni kwamba lazima kuwe na mpango
maluum ya kuvinunua na kuvisambaza. Hapo vitafikia watoto wengi zaidi.
Hiyo ni moja. Pili, usambazaji wa vitabu hapa ni mgumu, kwa sababu nchi hii
ni kubwa. Hatuna wasambazaji wa vitabu wenye uwezo wa kifedha na organisation
wa kuweza kusambaza vitabu mpaka huku vijijini. Na vikifika huku
vijijini, kama ni wasambazaji wa kuuza, havitanunuliwa, kwa sababu bei yake
ni juu, bei ya hiki kitabu itashindana na bei ya unga, bei ya sukari. Kwa hiyo
sitegemei mkulima aache kununua unga anunue “Mwendo“”
Ukiniuliza ni watu wangapi wanaonunua “Mwendo” mimi sijui.
Na hapa utamaduni huo wa “reading session” haupo. Tuseme tukimaliza
kutengeneza ofisi yetu, tutakuwa tukifanya readings kila mara. Lakini mara
nyingine hakuna mahali maalum ya kufanyia readings. Kwa hiyo lazima sisi
tuanzishe tukimaliza ofisi.

Watu wazima waliokisoma hiki kitabu, wamefurahi, wakarudi wakanunulia
watoto wao kama zawadi, nampa mwanangu zawadi, soma. Ilikuwa vizuri.
Halafu hiki kitabu, tulikilaunch kwenye telvisheni, kwa hiyo kilijulikana, kwa
mara moja kilijulikana sana. Lakini wengine waliuliza kwa nini, watu wengine
walioona kwenye televisheni walishangaa: “Aa, kwa nini ameandika, kwa
nini Mchagga aliandika kuhusu Wamakonde” kwa hiyo kwanza hawana utamaduni
wa vitabu, pili hawatazami maswala, wanatazama kwa nini Mchagga
aliandika kuhusu Wamakonde.”
Kwa hiyo matatizo ni mengi, kama tunataka kuanza utamaduni kama huu.

Swali: : Irimi Hanak: Ukiandika katika lugha ya Kiswahili, unawaandikia wasomaji gani?

Jibu: Elieshi Lema: Mwandishi wa Tanzania ambako Kiswahili kinaongeka, watu wanaongea
Kiswahili zaidi ya asilimia tisini na tisa, huna uchaguzi mkubwa sana, kama
unawaandikia Watanzania. Inakubidi kama una swala linalokuchokoza na ni
la jamii ya Watanzania na unataka kuwaandikia jamii ya Watanzania, lazima
unandike kwa Kiswahili. Kiingereza watu wengi hawaongei. Kwa hiyo hii
ilinibidi niandike kwa Kiswahili. Lakini pia nimeandika vitu vingine kwa
Kiingereza, na hata hivyo, nimeandika kwa Kiingereza nikijua kama kweli
ikibidi Watanzania wasome nitafsiri kwa Kiswahili.

Swali: : Irimi Hanak: Lakini kama ungeandika kwa kiingereza, watu wengi zaidi duniani wangeweza kusoma vitabu vyako. Na pengine ungeuza vitabu vingi zaidi.

Jibu: Elieshi Lema: Mimi nahusika kama mwandishi, jukuma langu la kwanza ni kuwaambia vijana
wanaokuwa kitu fulani, kwamba mnao uwezo ndani mwenu ya kuamua
kiasi fulani ya maisha yako yaende vipi. Hiyo ilikuwa ni lazima, ilinikera kwa
hiyo ilinibidi nijaribu kuambia. Na hao vijana wataelewa Kiswahili. Na walipata
ujumbe: Aa, kumbe naweza nikakataa. Naweza nikakataa mwili wangu
usiguswe na mtu mwingine. Yaani ni kitu muhimu mno, ilibidi niandike kwa
Kiswahili kwanza. Level ya pili ndiyo hiyo kama publisher. Wakaja kuniambia
“Unajua Elieshi, nitafsiri kitabu chako kwa Kiingereza”, nikasema ni sawa,
lakini kile kitu nilichotaka kusema ningekisema kwa lugha ya Kiswahili
tu. Kwa hiyo lazima niwe mwandishi kwanza, halafu niwe mchapishaji baadaye.
Hiyo nyingine ambayo niliandikia ambao ni ya watu wazima ni Kiingereza.
Kwa sababu maswala yanayohusu watu wazima yameshajadiliwa na yanajulikana,
yapo.

Hiki kitabu kipya ni riwaya pia, ni hadithi ya msichana aliyekulia kijijini. Anafanya
hivyo hivyo, anatathmini jamii pia. Na huyo ni msichana, amezaliwa
katika nyumba ya single mother, ach, kama kuna tathmini ya jamii ya patriarchy,
unafanywa hapo. Vyote vile vidogovidogo nilikuwa nilijaribu kuzungumzia
huku vidogo tu, huku ni mtoto, kwa hiyo huwezi kuzungumza mambo
makubwa (Anaonyesha kitabu cha “Mwendo”). Lakini hapa (anaonyesha kitabu
kipya), hapa kila kitu anatathmini, kila kitu anauliza maswali ni kwa nini
kiwe hivi, na kweli njia yangu ni hii. Kwa hiyo ambacho kinanikera ambacho
bado kinaendelea, labda kimepata culmination hapo. Kitabu hiki kitatokea
hivi karibuni. ( kitabu hiki kimeshaoka, na nimekifanyia uhakiki – ni kitabu chenye ujumbe mzito)
Hii nimeandika kwa Kiingereza inaweza ikasomwa na watu wengi zaidi. Lakini
pia ni ukweli wameshakuja watu kama wawili hivi, wanataka kutafsiri
“Safari ya Prospa” kwa Kiingereza. Hiki ndiyo kipya zaidi hawajaja watu wa
kutafsiri. Ila sidhani kama mimi ni mtafsiri, sitaweza kutafsiri mimi mwenyewe.
Nilipenda mtu mwingine atafsiri halafu nikione utafsiri ukoje. Mimi
ningepewa uchaguzi ni kipi kianze, naona hiki (“Mwendo”) kwanza kipate
tafsiri, kwa vile kinazungumza mambo makubwa, makubwa hata kwa kitabu
cha mtoto.
Unajua, pia sitaki ile cut-throat thing. Mtu kama akiona kuna maswala muhimu
akatafsiri, ndivyo ningependa. Hili ni swala muhimu na ni lazima tulishughulikie
katika mtazamo fulani. Hiyo sympathetic approach, bila hiyo inaweza
ikatokea ukasema “aa kaa huko, kwa nini unanijua, huwezi kunisemea
miye, kaa huko.” Sasa sisi tunasema kaa huku, wale wanasema “mm, una shida
gani” hakuna kitakachofanyika. Unajua hizo ni levels, kuna international
levels, kuna national levels, halafu unakuta level ya kabila kwa kabila, kwa
hiyo kila siku hatuwezi kusema “Mm, wewe mbaya, wewe ovyo, wewe akili
yako mbovu” hatuwezi kusema, lazima tuingie ndani, tufanye utafiti tujue,
wanaangaliaje hiki kitu, ni kwa nini wanafanya hivi vitu, maana yake ni nini.
Uzuri wa Helena Margareta, ameshaanalyze ritual na kusema: kuna maana
yake, kuna vizuri, kuna vibaya, vibaya, achana naye, vizuri enda navyo. Kwa
sababu ritual ni identity ya watu, huwezi kuifuta identity kwa kusema sipendi
hiyo ritual. Unaangalia hiyo ritual na unasema: Ni nini katika hiki kinachosaidia
hawa watu kukuwa, to grow, kwa sababu tunakuwa katika mazingira.

Swali: : Irimi Hanak: Tungeweza kusema kwamba kitabu cha Mwendo kina ajenda ya feminism?

Jibu: Elieshi Lema: Ni kweli. Definitely there is a lot of feminism in everything I write. Lakini
Feminism siyo kitu cha Ulaya. Jina la feminism ndiyo linalotoka Ulaya. Lakini
concept ni ya dunia nzima. Wanawake ni watu na wana mtazamo. Basi.
Wanawake wanaishi katika jamii ya wanawake na wanaume. Na wana
mtazamo wa maisha. Ambao ni tofauti na wa wanaume, kwa sababu wao ni
wanawake. Sasa hiyo ni feminism. Siyo lazima iwe na neno feminism, lakini
the essence ndiyo hiyo. Kwa hiyo mimi hata ukiniambia Western feminism
inasema nini, mimi bado sijui sana, najua kidogo tu.

Wengine wanafikiri feminism ni kitu kinachotoka Ulaya. Feminism iko hapa
hapa! Mahali popote anapoishi mwanamke katika jamii, na wanawake wengine
na wanaume, lazima kutakuwa na feminism. Kwa sababu ni mtazamo wao.
Ni ile kusema: sisi tunataka hivi, sisi tunaona hivi, iendelee hivi. Dunia yangu
naitazama hivi naitafsiri hivyo.
Lakini feminism – huwezi kuwa mwanamke katika jamii, uwe na mwamko,
usiwe feminist. Ni jina tu tunaliogopa. ... Mimi sijiiti feminist. Sina haja ya
kujiita feminist. Hata siku moja. Ninajiita tu mwanandishi ambaye anatazama
maswala ya wanawake, na ambaye anachunguza, kila siku naingia ndani,
nauliza maswala.
Irimi Hanak: Ningependa kukushukuru kwa mazungumzo yetu.

Jibu: Elieshi Lema: Nakushukuru pia kwa sababu mara nyingi waandishi wa Kiafrika hatupati
sympathi kutoka Ulaya, ile ya hata kujua wanazungumzia maswala gani, matatizo
yao ni nini, waandishi wanafikaje pale wanapofika. Kuwa mwandishi
wa Kiafrika, ni vigumu in the sense kwamba unafanya vitu vingi mno. Hatuna
ile starehe ya kuwa mwandishi peke yake. Unakuwa mwandishi, unakuwa
mama, unakuwa mchapishaji, unakuwa unafanya kazi na vikundi, unafanya
vitu vingi, kwa hivyo kufanya utafiti tu wa kitu hiki kinachukua miaka mitatu
ambayo mahali pengine ni miezi sita au even miezi mitatu kwa sababu inafanywa
tu. Kwa hiyo kweli na mimi nafurahi umechukua ile jukumu ya kupeleka
ujumbe wa mwandishi mdogo katika jamii yako.

Na,
Padri Privatus Karugendo.

0 comments:

Post a Comment