MADAKTARI WETU MSIGOME, IGA MFANO WA DAKTARI PRATHAP C REDDY WA INDIA. Kila mtu anayejali akisikia madaktari wanataka kugoma ni lazima awe na wasi wasi. Ni wazi kuna wale wasiojali na kulichukulia jambo hili kama la kawaida. Wale ambao wao na jamaa zao wana uwezo wa kwenda kutibiwa nje ya nchi au kutibiwa kwenye hospitali binafsi, mgomo wa madaktari ni msamiati. Lakini wale ambao wanategemea hospitali za serikali, mgomo ni tishio na kama kuna la kufanya wangelilifanya ili kuepusha mgomo huu. Kusikia kwenye vyombo vya habari haitishi zaidi ya kuguswa, ukapeleka mgonjwa wako hospitali akamaliza masaa bila huduma na wakati mwingine ukashuhudia roho ya ndugu yako inakatika mikononi mwamo kwa vile hakuna daktari wa kumshughulikia. Mgomo wa madaktari ni tishio la uhai. Sisi Tanzania tunakazana na kilimo kwanza, lakini nchi nyingine duniani zinakazania Uhai kwanza. India ni mfano mzuri, hawa wamewekeza kwenye afya na uhai. Wakati Tanzania tunawekeza kwenye vitu vingine kama magari ya kifahari na posho kubwa kwa viongozi wetu, nchi nyingine duniani zinawekeza kwenye Afya, kwenye uhai. Uhai ni kitu hadimu, ukitoweka hakuna wa kuurudisha! Wajibu wetu mkubwa ni kuhakikisha tunaulinda uhai, ni wajibu wa kila mtu hata madaktari wetu wakiwemo. Hivyo ninaandika makala hii kuwaomba madaktari wetu waachane na mgomo wambao kwa njia moja ama nyingine utahatarisha maisha ya uhai wa watanzania. Nawasihi sana watangulize uhai wa watanzania kabla ya kutanguliza maslahi binafsi Sina lengo la kusema kwamba madaktari wanakosea kudahi haki zao, na wala sipendi kuitetea serikali kwamba haina fedha za kutimiza ahadi zake kwa madatari. Naungana na madaktari wetu kuishingaa serikali inayofunika matatizo bila kuyatanzua, serikali inayoamini kwamba kila kitu kitakwisha kwa miujiza. Ninajua kabisa kwamba madatari wetu wanalipwa mshahara kidogo, wanafanya kazi nyingi na ngumu kwenye mazingira magumu. Madaktari wetu hawana vifaa vya kutosha kuyakoa maisha ya watanzania wengi. Ninajua jinsi madaktari wetu walivyo na moyo wa uvumilivu na wamekuwa wakiivumilia serikali na ahadi zake za uongo. Muda walioipatia serikali unatosha kwaruhusu kugoma. Ila wakigoma, watakaoumia si viongozi wanaokataa kutimiza ahadi zao, bali ni wananchi wa kawaida. Uhai wa watu wasiokuwa na hatia utapota na ukipotea hauwezi kurudi. Wakati naandika makala hii nimesikia taarifa ya kuchekesha kwamba mahakama ya Kazi imesitisha mgomo wa madaktari. Huku ni kutumia ubabe bila kufikiri. Sawa Mahakama imezuia mgomo wa wazi, lakini haina uwezo wa kuuzima mgomo baridi ambao ni mbaya zaidi. Madaktari watafika kazini kama kawaida, lakini hawatafanya kazi. Watashinda wanazunguka kutoka upande mmoja wa hospitali na kwenda mwingine. Sawa mahakama imeusitisha mgomo, lakini je Mahakama hiyo itashika bunduki ili kuhakikisha kila daktari anafanya kazi? Serikali itafurahi kutosikia dalili za mgomo, lakini je serikali ina uwezo wa mtu anayekataa kuwatibu wagonjwa kwa kisingizio cha ugonjwa? Kwa maoni yangu ni bora waachane na mpango wao wa kugoma. Waachane na kazi za serikali na kujiunga pamoja kuanzisha Hospitali nzuri ya binafsi. Hili ndilo jibu la matatizo yao na serikali ni lazima itafunza na kuanza kuwahudumia watakao baki kwa nguvu zote, vinginevyo hospitali za serikali zitafungwa. Leo serikali yetu inalipa fedha nyingi kuwapeleka viongozi na watu wengine kutibiwa India. Hivyo wadaktari wetu wakijiunga na kujenga hospitali nzuri yenye vifaa vya kisasa, fedha yote ya serikali inayokwenda India, itaelekezwa kwenye hospitali zao nzuri watazozianzisha. Ninawaomba madaktari wetu waige mfano wa Dakta Prathap C Reddy, wa India Aliyeanzisha mahospitali ya Appolo. Daktari huyu alisomea India na baadaye alienda kujiendeleza kusoma Uingereza na Marekani. Alifanya kazi huko kwa muda na baadaye kuamua kurudi India. Aliporudi India, jirani yake alikuwa mgonjwa na alihitaji matibabu nje ya India. Daktari Prathap, alijitahidi kumsaidia jirani kwa uwezo wake aliokuwa nao, lakini kwa vile alikuwa hana vifaa vya kisasa na fedha hazikupatikana kumpeleka jirani yake India kwa matibabu, jina yake huyo alikufa. Tukio hilo lilimsikitisha, maana yeye alikuwa na utaalamu wa kumtibu, lakini hakuwa na vifaa na hakuwa na fedha kumsaidia aende kutibiwa nchi za nje. Tukio hilo lilimsikitisha na kumsonenesha. Hicho ndicho kilimsukuma kuanzisha Hospitali za Appolo. Leo hii hospitali hizi zinasifika India na nje ya India, ni hospitali ambazo zinafanya kazi ya kuyaokoa maisha ya watu wa India na watu wa mataifa mengine. Daktari huyu mwanzilishi wa Appolo, aliwashawishi madaktari waliokuwa wakifanya kazi kwenye hospitali za serikali na kulipwa mshahara kidogo kuachana na kazi za serikali na kuunga naye kuanzisha hospitali nzuri zenye vifaa vya kisasa. Mbali na kuwashawishi madaktari wa ndani ya nchi, alitembea dunia nzima akiwashawishi madaktari wahindi waliokuwa wakifanya kazi Ulaya na Amerika ,kurudi nyumbani kuokoa maisha ya wahindi wenzao. Appolo ilianza mwaka wa 1983, ikiwa na vitanda 150. Leo hii ina vitanda zaidi ya elfu nane, na imewatibu wagonjwa zaidi milioni 26 kutoka nchi 120 na Tanzania ikiwemo. Appolo wana hospitali zaidi ya 53 India na nchi nyingine na Tanzania ikiwemo. Nilipokwenda India mwanzoni mwa mwezi huu, niliambiwa kuna Appolo hospital jijini Dar-es-salaam. Bado naisaka hospitali hii niipata nitawashauri madaktari wetu waende huko jijifunza namna ya kujiunga na kufanya kazi pamoja. Alichokifanya daktari huyu ni kuwakusanya madatari, kutafuta mikopo kutoka kwenye mabenki makubwa na kuanzisha hospitali nzuri yenye vifaa vya kisasa.Madaktari hawa sasa wana mishahara mizuri ambayo wasingeweza kuiipata kule serikalini. Wanatoa huduma nzuri kwa wagonjwa na maisha yao yameboreka. Hili ndilo ombi langu kwa madaktari wetu. Badala ya kuendeleza migomo na kuyaweka maisha ya watu hatarini, ni bora wakaachana na serikali. Wajiunge pamoja na kuanzisha hospitali ya binafsi nzuri na yenye vifaa vya kisasa. Kama mabenki yanawakopesha wafanyabishara wengine, kwanini isiwakopeshe madaktari wetu wanaotaka kujenga hospitali nzuri na yenye vifaa vya kisasa? Ninajua kuna hospitali ya namna hii iliyoanzishwa na madaktari Bingwa wa Muhimbili, ni wazi inajitahidi, lakini bado inasuasua kwa huduma na haina vifaa vya kisasa. Mbaya zaidi ni kwamba madaktari bingwa bado wanaendelea kufanya kazi Muhimbili, wakitoka huko wamechoka, wanakuwa hawana nguvu za kuwahudumia wagonjwa kwenye hospitali hiyo ya binafsi. Dawa pekee ni kuacha kazi serikalini na kujiuunga pamoja kuanzisha hospitali iliyotukuka. Nina imani serikali inayokataa kuwasiliza madaktari leo hii, serikali inayokaa kutoa fedha za kumaliza matatizo ya madaktari, itatoa fedha nyingi kuwalipia viongozi na watu mbali mbali watakaotibiwa kwenye hosptiali binafsi za madaktari wetu. Migomo ni mizuri kushinikiza kudai haki, lakini wakati mwingine si dawa ya matatizo yote. Dawa pekee ni madatari kuachana na serikali na kuanzisha hospitali nzuri ya binafsi. Tanzania tuna madaktari wazuri na wenye sifa za juu nje ya nchi. Ukienda Botswana, Namibia, na nchi nyingine za Ulaya na Amerika, utawakuta madaktari mabingwa kutoka Tanzania. Hawa wakipata mtu wa kuwashawishi na kuwahamasisha kurudi nyumbani,Tanzania tunaweza kuwa na hospitali nzuri ya Afrika ya mashariki na kati. Na, Padri Privatus Karugendo. +255754633122 pkarugendo @yahoo,com www.karugendo.net

0 comments:

Post a Comment