WAHARIRI WAMEISALITI MWANAHALISI Wahariri wa vyombo vya habari Tanzania wana umoja wao. Tumeshuhudia wakifanya mikutano yao kwenye mahoteli makubwa na wakati mwingine wakisafiri mikoani kufanya mikutano yao. Imani yetu ni kwamba umoja huu si wa kunywa chai, si wa kukutana na kupiga soga au kujadili mishiko bali pamoja na mambo mengine muhimu ya umoja huu ni sauti ya pamoja. Sauti ya kutetea haki, sauti ya kupinga kuonewa na wamiliki wa vyombo vya habari na kupinga uonevu wowote unaoweza kutoka serikalini na kuhakikisha vyombo vya habari ni jukwaa huru la majadiliano. Vyombo vya habari ni mhimili mkubwa katika jamii yetu, ukiachia mbali serikali, mahakama na Bunge. Hivyo wahariri wanaoviongoza vyombo hivi ni watu muhimu na wana ushawishi mkubwa katika jamii. Ni muhimu kabisa watu hawa kuwa na sauti ya pamoja ili mhimili huu muhimu uwe na nguvu za kutosha kutetea haki na kusimamia ukweli. Bila sauti ya pamoja, sauti ya uzalendo, vyombo vya habari vinaweza kuleta vurugu katika nchi au vinaweza kuleta ukombozi. Kuna mifano mingi ambayo imetolewa kila wakati kiasi cha kuyaumiza masikio ya watanzania. Si muhimu kuirudia mifano hii kwenye makala hii, labda yakitukuta ndo majuto yatakuwa mjukuu. Inashangaza kwamba sauti hii ya pamoja, sauti ya kutetea haki sauti ya kupinga kunyanyaswa na kuonewa haijasikika kulitetea gazeti la Mwanahalisi. Badala yake tunashuhudia chuki binafsi na wivu; tunashuhudia usaliti wa wazi wazi na labda kwa vile sasa hivi waandishi wa habari wanaingizwa serikalini na wengi wao kupandishwa hadi kuwa wakuu wa Wilaya, wanaamua kuusaliti umoja wao ili kesho na keshokutwa nao wapandishwe? Tulitegemea kuwaona wahariri wakitumia nguvu zao zote, magazeti yao, mikutano yao na hata maandamano ya amani kupinga kitendo cha Serikali kulifungia gazeti la Mwanahalisi. Nguvu zilizotumika kulifungia gazeti la Mwanahalisi, zinaweza kutumika kuyafungia magazeti mengine pia.Wahariri wamekaa kimya kana kwamba hakuna jambo kubwa lilitokea katika umoja wao. Inawezekana na wahariri hawa wanainyoshea kidole Mwanahalisi? Nao wanaamini Mwanahalisi ni gazeti la uchochezi? Kwamba Kubenea ni kichwa ngumu? Kwamba ameonywa na hakusikia? Kwamba sasa amekipata? Ina maana wahariri hawa wanashangilia msiba wa mwenzao? Bahati mbaya au nzuri wahariri wengi ni vijana. Na tujuavyo vijana mara nyingi wanakuwa msatari wa mbele kutetea haki na kutaka mabadiliko. Katika hali ya kawaida, bila kuzingatia itikadi yoyote ile kitendo cha kulifungia gazeti la Mwanahalisi, na kulifungia kwa kuandika habari iliyokuwa inafichua unyama aliofanyiwa Dkt Ulimboka, kingepigiwa kelele na wahariri hadi mbingu zikasikia. Inatia shaka kama wahariri hawa ni vijana wa kweli au ni vijana wa “kutengenezwa”? Ni vijana wanaosubiri kuelekezwa la kufanya na Baba? Ni vijana wanaoendelea kunyonya kidole hadi wanazeeka? Ni vijana wenye tabia ya kujipendekeza na kuhakikisha uwezo wao wa “kufikiri” wanauwekeza na kuufungia kwenye sanduku lisilofunguka milele? Kimya hiki cha wahariri kinashangaza sana. Inawezekana ni aina Fulani ya upambanaji? Ukimya unahesabika katika sauti ya pamoja, sauti ya kutetea haki? Au wakati umefika kuamini kwamba wahariri wetu wamefungwa midomo na serikali? Au ni wafanyakazi wa Serikali? Juzi hapa tumeshuhudia Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete, akiwaita wahariri na kuongea nao. La kushangaza, au labda kulikuwa na maelekezo? Hatukushuhudia hata mhariri mmoja kujitokeza kuuliza swali juu ya Mwanahalisi au kumweleza Rais wetu ukweli kwamba kulifungia gazeti katika nyakati hizi tulizomo ni kichekesho: Wahariri wangemwelezea Rais, kwamba kitendo cha kulifungia gazeti la Mwanahalisi, kilisaidia kuusambaza ujumbe uliokuwa kwenye gazeti hilo ambao serikali haikutaka wananchi waufahamu. Kitendo cha kulifungia gazeti hilo lilitafutwa na kurudufiwa na kusambazwa Tanzania nzima. Na wale wanaosoma mtandao, ambao wengi wao ni vijana, waliusambaza ujumbe huu kwenye mtandao na hadi leo hii ujumbe huu unazunguka. Wahariri wangemweleza Rais, ukweli kwamba hata akiamua kuvifungia vyombo vyote vya habari, watu watatumia mitandao ya kijamii, wataendelea kusoma habari hata kwa kutumia simu zao za mkononi. Hivyo kulifungia gazeti kwa vyovyote vile si nyenzo ya kuzuia uchochezi au kuzuia habari ya aina yoyote ile kusambaa. Wahariri wangemkumbusha Rais ahadi yake ya kutengeneza ajira milioni moja. Kulinfungia gazeti la Mwanahalisi ni kusitisha ajira za vijana waliokuwa wakilitegemea gazeti la Mwanahalisi na kwamba kitendo hiki ni cha kikatiri na hakivumiliki. Vijana wanajitafutia kazi ili waweze kuendesha maisha yao, juhudi zao zinazimwa na mtu mmoja mwenye madaraka makubwa bila kujadiliana na vyombo husika? Kuna baraza la habari Tanzania, mbona halikusishwa? Lakini la msingi zaidi wahariri hawa wangehoji juu ya kosa la Mwanahalisi. Suala la kukamatwa, kupigwa na kuteswa kinyama kwa Dkt Ulimboka, limekuwa na utata. Yanasemwa mengi na watu wengi wanahusishwa. Mwanahalisi wamefanya utafiti na kutaja jina la mtu ambaye ndiye alikuwa mtu wa mwisho kuwasiliana na Dkt Ulimboka. Mtu huyu kufuatana na namba yake ya simu alikuwa na mawasiliano ya mara kwa mara na Dkt Ulimboka na ushahidi unaonyesha anafanya kazi Ikulu. Hapa kosa la Mwanahaisi liko wapi? Ulimboka mwenye alisema aliyemkamata na kumpiga anamfahamu,ni mtu walikutana Ikulu na siku hiyo alimpigia simu mara nyingi. Walichokiandika Mwanahalisi, ndicho hicho alichokisema Ulimboka. Rais, hata angesema mara miamoja kwamba Serikali haiusiki, haitasaidia kama hamkani au kumkubali mtu huyo anayetajwa na Mwanahalisi. Tulitegemea wahariri kumkumbusha Rais, Ikulu kukana kwamba mtu huyo si mfanyakazi wake. Ili mtu huyo akamatwe na kuhojiwa juu ya suala zima la Ulimboka. Kwa njia moja ama nyingine Mwanahalisi iliwasaidia Polisi kufanya kazi yake ya upelelezi. Tulitegemea wahariri wamtake Rais, kueleza kwa kina na ufasaha utamaduni huu unaojengeka wa kuitumia mahakama kuzima sauti za watu. Au mahakama kutumiwa kuwanyanyasa wanyonge kama ilivyofanyika kwa mgomo wa madaktari na walimu. Au hata kwa suala zima la Ulimboka, kwamba sasa hivi suala hilo liko mahakamani na kulijadili ni kuingilia kesi iliyo mahakamani. Tulishuhudia mchezo wa kuigiza uliotumika kulifikisha suala la Dkt Ulimboka mahakani. Huyo mkenya aliyekamatwa wakati alipokwenda kuungama kanisani, na kufikishwa mahakamani kwa kosa la kumteka na kumtesa Dkt Ulimboka, hajasikika tena. Hiyo kesi yake itasikilizwa lini? Na je mbona sura yake haikuonyeshwa kwenye vyombo vya habari? Au ni kutaka kulinda usalama wake? Ina maana usalama wa huyu jambazi kutoka Kenya ni muhimu kuliko maisha ya watanzania? Hatukushuhudia wahariri wakiuliza maswali ya kumsaidia Rais wetu na watanzania. Tunataka tusitake tuna matatizo makubwa. Madaktari wanagoma, walimu wanagoma, watu wanatengeneza makampuni ya kuiba umeme, wanauza umeme miaka saba bila kukamatwa, Bunge linatunga sheria ambazo hata kabla ya kuanza kutumika zinaonekana zina kasoro, serikali inalipa mishahara hewa, magazeti yanafungiwa… kuna kasoro sehemu Fulani na kasoro hizi ni lazima zijadiliwe vinginevyo hatuwezi kufika mbali. Wahariri wa vyombo vyetu vya habari wana mchango mkubwa katika hili. Ndo maana wengi wetu tulitegemea kwa suala la Mwanahalisi, ambalo linaelekea kuzima uhuru wa majadiliano na uhuru wa kuibua yale yaliyojificha ambayo ni “adui” wa Umma, lingepigiwa kelele na wahariri wetu. Usaliti wao kwa Mwanahalisi ni mauti yetu na ni mauti yao pia! Na, Padri Privatus Karugendo.

1 comments:

Unknown said...

Habari am Bi, kiutamaduni na Tumaini, Taasisi mkopo halali na za kuaminika na mikopo
katika sheria na masharti wazi na ya kueleweka kwa 2% kiwango cha riba. kutoka
USD $ 12,000 kwa $ 8,000,000, Euro na paundi tu. Mimi kutoa mikopo ya biashara,
Mikopo binafsi, mikopo ya wanafunzi, gari mikopo na mikopo kwa kulipa bili. kama wewe
haja mkopo una kufanya ni kwa ajili ya wewe kuwasiliana nami moja kwa moja
Katika: (merithope6@gmail.com)
God Bless You.
dhati,
Bibi: sifa Hope
Barua pepe: (merithope6@gmail.com)

Kumbuka: majibu yote upelekwe kwa: (merithope6@gmail.com)

Post a Comment